Endeleeni Kupiga Kelele kwa Sauti Moja ya Furaha
“Pigeni kelele za furaha, imbeni pamoja.”—ISAYA 52:9.
1. Kwa sababu gani sasa Mashahidi wa Yehova wanapiga kelele “pamoja”?
PAMOJA! Maana yake ni kukubaliana kwa ukamili ili kuwa na upatani ulio sawasawa. Mashahidi wa Yehova wanatumikia kwa sauti moja kwa sababu wana akili ya Kristo, nao wameungana katika kulitukuza jina la Yehova. Kwa sababu ya baraka ya Yehova kuwa juu yao, hata nchi ya mfano ambamo wanakaa inapiga kelele, kila sehemu yake ikilia kwa shangwe. Yote hayo yanapatana na maneno aliyosema mtume Paulo katika sala: “Na Mungu mwenye saburi na faraja awajalie kunia mamoja ninyi kwa ninyi, kwa mfano wa Kristo Yesu; ili kwa moyo mmoja na kwa kinywa kimoja mpate kumtukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.”—Warumi 15:5, 6; Yohana 17:4, 6, 20, 21.
2. (a) Kulingana na 1 Wakorintho 1:10 na Waefeso 4:4-6, kwa sababu gani walinzi wanaona “jicho kwa jicho”? (b) Ni akina nani pia wanaojiunga katika ile kelele ya furaha, na kwa njia gani?
2 “Kumtukuza Mungu!” Hivyo ndivyo “walinzi” wa Yehova waliounganishwa vizuri wanavyofanya leo. Hivyo wanatimiza unabii huu: “Wanapaza sauti zao, wanaimba pamoja; maana wataona jicho kwa jicho, jinsi [Yehova] arejeavyo [akusanyavyo kurudisha, NW] Sayuni.” (Isaya 52:8) Wanaona “jicho kwa jicho,” kwa sababu wao ‘wameungana kwa kufaa katika akili ile ile moja na katika njia ile ile moja ya kuwaza.’ (1 Wakorintho 1:10, NW; ona pia Waefeso 4:4-6.) Na sasa, wakati “mkutano mkubwa sana” unapojiunga kupiga ile ‘kelele ya furaha,’ mlio huo wa duniani pote unainuka na kuwa sauti nene.—Ufunuo 7:9, 10,15.
3. Tengenezo la Yehova duniani limeonyeshaje furaha inayoonyeshwa na majeshi ya kimbingu?
3 Tengenezo la kimbingu la Mungu, kutia ndani “elfu kumi za elfu kumi” za malaika watakatifu, linainua “sauti” yalo katika kumpa sifa Yehova akiwa ndiye Muumba mkuu, na kumpa “Mwana-Kondoo,” Yesu Kristo. (Ufunuo 5:11, 12; 4:11, NW) Vivyo hivyo, watu wa Mungu waliopo duniani leo wamepangwa wakiwa tengenezo kwa ajili ya utumishi mtakatifu. Hata nchi ya mfano ambamo wanakaa ‘inapiga kelele.’ Nabii anasema hivi: “pigeni kelele za furaha, imbeni pamoja, enyi mahali pa Yerusalemu palipokuwa ukiwa; kwa kuwa [Yehova] amewafariji watu wake, ameukomboa Yerusalemu.” (Isaya 52:9) Yehova ameleta “watu wake,” wajumbe wa kidunia wa “Yerusalemu wa juu,” tengenezo lake la kimbingu, wakatoka katika hali ya ukiwa waliyopatwa nayo wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, na ‘kupiga kelele za furaha’ kwa sauti moja yenye kupatana kabisa kumetokeza mpanuko wa duniani pote unaoendelea mpaka leo hii!—Wagalatia 4:26, 27; Isaya 52:8.
4. Ni kwa njia gani Yehova amekwisha ‘kuweka wazi mkono wake mtakatifu,’ na jambo hilo linatupa sisi uhakika wa nini juu ya wakati ujao?
4 Ndipo unabii unaposema: “[Yehova] ameweka wazi mkono wake mtakatifu machoni pa mataifa yote; na ncha zote za dunia zitauona wokovu wa Mungu wetu.” Kwa kweli Yehova alichukua hatua ya kuokoa watu wake katika kipindi cha mwanzo-mwanzo wa “siku za mwisho” za wakati huo, na hivi karibuni, kwenye Har–Magedoni, yeye ‘ataweka wazi mkono wake mtakatifu’ kwa mara nyingine, awaletee wokovu watu wake waliofanywa tengenezo. Wakati huo, ‘mataifa mengi yatalazimika kujua kwamba yeye ni Yehova.’—Isaya 52:10; 12:2, UV; Ezekieli 38:23, NW.
5, 6. (a) Kwa sababu gani kazi ya Mungu inapasa kutimizwa kwa uharaka? (b) Tengenezo limechukuaje hatua ya kutoa ushuhuda wenye kuenezwa zaidi?
5 Siku ya Yehova ya kufikiliza hukumu iko karibu sana! “Inafanya haraka sana.” (Sefania 1:14) Kwa sasa, ni lazima “habari njema za jambo zuri zaidi” zitangazwe huko na huko katika sehemu zote za dunia. (Isaya 52:7, NW) Ili kuitimiza kazi hiyo, tengenezo la Yehova linatumia hesabu kadha ya mashirika halali kisheria, kama Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, Biblia na Trakti ya Pennsylvania, nayo yanasimamia kazi ya makundi ya Mashahidi wa Yehova katika matawi karibu 94 duniani kote. Wakati wa miaka mitano iliyopita, kumekuwa na mpanuko mkubwa wa sehemu za uchapaji na majengo mengine kwenye matawi hayo, na kwa hiyo Sosaiti iko katika hali nzuri kuliko zamani ya kuweza ‘kutangaza amani na wokovu’ kwa njia nzuri zaidi.
6 Wakati wa mwaka uliopita, ongezeo kubwa lilijengwa kwenye kiwanda cha Sosaiti katika Mashamba ya Sosaiti, Mkoa wa New York, ambako Makao ya Betheli pia yanaendelea kupanuliwa. Mashine kubwa sana ya ofseti ya kuchapia magazeti imekwisha kusimamishwa, nayo inaweza kuchapa magazeti yasiyopungua 400,000 kwa siku moja. Nyingi za mashine za zamani za Sosaiti za namna ya M.A.N., ambazo zilikuwa na mabamba ya kugandamiza maandishi moja kwa moja kwenye karatasi, zimebomolewa kisha zikatengenezwa upya ziwe mashine zenye mabamba mawili ya ofseti. Sasa hizo ndizo zinazotumiwa katika matawi ya Sosaiti ulimwenguni pote, na pia katika Brooklyn na kwenye Mashamba ya Sosaiti. Mpanuko unaendelea duniani pote. Kwa mfano, tawi lililo katika Ujeremani sasa linatumia mashine yalo ya pili ya ofseti yenye mwendo wa kasi inayochapa kwa mabamba ya rotari. Nalo tawi la Japani linakaribia kuanza uchapaji kwa kutumia mashine yalo ya tatu inayotumia mabamba ya rotari, nayo inaweza kutokeza magazeti 60,000 kwa saa moja.
Magazeti Yasogezwe Mbele!
7. Kulikuwa na maendeleo gani katika kupata maandikisho mwaka wa 1983?
7 Kwa sababu gani mpanuko wote huo unafanywa katika uchapaji wa kitheokrasi? Ni kwa sababu ya utendaji wa juhudi wa ninyi nyote ndugu mlio shambani. Wakati wa mwaka uliopita mlipata jumla ya kupendeza sana ya maandikisho mapya 1,756,153 ya magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 28 juu ya mwaka uliotangulia.
8. Kutambua ubora wa magazeti yetu kumeletaje matokeo?
8 Mwangalizi wa mzunguko katika United States (Amerika) aliandika kwamba ile habari iliyosema juu ya utendaji wa magazeti, ambayo ilichapishwa katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Aprili 1983, “ilituletea sisi sote matokeo makubwa.” Alisema lilikuwa jambo la kawaida kwa kikundi kilichokuwa katika gari moja kurudi kutoka kwenye utumishi kikiwa kimepata maandikisho manne au matano. Shahidi mmoja wa kike aliye painia aliweza kuyashinda maoni mabaya aliyokuwa nayo hapo zamani na akapata maandikisho tisa katika muda wa juma moja. Tawi la Japani liliripoti kwamba maandikisho mapya ya Mei na Juni yalijumlika kuwa 70,115—kulinganisha na yale 49,016 ya shughuli iliyotangulia ya miezi miwili—ingawa bei ya andikisho la mwaka mzima ilikuwa yen 1,800 (kama Kshs. 97.50)! Lakini ubora wa kiroho wa magazeti yetu hauwezi kupimwa kulingana na bei ya pesa, wala ya fedha wala ya dhahabu. (Mithali 8:10, 11) Na tuendelee kuonyesha juhudi katika kutoa maandikisho mwaka wa 1984!
9. Ongezeko la ugawaji wa magazeti linaweza kufikiwaje?
9 Lakini, namna gani juu ya ugawaji wetu wa ujumla wa magazeti wakati wa mwaka wa 1983? Ulikuwa mzuri, lakini hiyo ndiyo ile sehemu moja ya utumishi wetu ambayo haikuongezeka. Tunaweza kufanya nini turekebishe hali hiyo? Kwa mara nyingine, kuthamini sana sana mambo yaliyo katika magazeti yetu kunapasa kutuchochee tuyachukue na kuyatoa katika kila pindi, hasa katika Siku ya Magazeti tuliyopanga kila juma. Tunasema Siku ya Magazeti ya “kila juma,” kwa maana wengi sana kati ya ndugu zetu duniani pote wanafurahia sana ushiriki huo wa kawaida. Matawi yaliyotenganishwa na umbali mkubwa kama Kenya na Hong Kong yamepeleka ombi la kwamba maneno yanayosema Jumamosi ya pili na ya nne kwa utendaji wa magazeti yaondolewe katika kalenda ya Sosaiti, kwa kuwa yangeweza kufanya ugawaji wa magazeti katika maeneo yao upungue uwe nusu ya vile ulivyo. Kwa vyo vyote, kila mtu ashiriki utumishi huo wenye furaha katika Jumamosi ya pili na ya nne, lakini ingefaa sasa tusonge mbele tufikie mradi wa mbele zaidi wa kufanya utumishi wa magazeti kila Jumamosi—nyumba kwa nyumba, katika barabara na masoko na kwa wale watu tunaowapelekea magazeti kwa ukawaida!—Mhubiri 11:1.
10. Gazeti moja lililetea msomaji wa Awake! faida gani?
10 Mara nyingi sana ni gazeti moja tu linalochochea kupendezwa kwa mtu, na matokeo ya mwisho yanakuwa kwamba “kondoo” mwingine anaongezwa kwenye “zizi” la “mchungaji mwema.” (Yohana 10:14, 16) Jambo lililoonwa linalofuata ni mfano wa kuonyesha hivyo:
Siku moja mhubiri wa Ufalme katika Maurishasi alikuwa akipita karibu na nyumba ya mlevi asiyebadilika wakati mwanamume huyo alipomwita aende alipo. “Bwana-mheshimiwa, mimi nimeacha kunywa,” akasema kwa furaha. Kwa kuwa katika Reunion watu wengi wanaenda hospitali ili nguvu za pombe zikaondolewe katika miili yao, Shahidi alimwuliza, “Ulienda hospitali ipi?” Mwanamume huyo akajibu, “Sikwenda hospitali; nilisoma Awake! [Julai 8,1982, juu ya ulevi] halafu nikaacha kunywa.” Wakati wa kuandikwa kwa gazeti hili (katika Kiingereza), Shahidi huyo alikuwa amekuwa akiongoza jamaa hiyo katika funzo la Biblia kwa kutumia kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichochapishwa na Sosaiti. Gazeti moja liliweza kutimiza hayo!
Jambo hilo linatuingiza katika habari nyingine:
Mafunzo ya Nyumbani ya Biblia Yanaongezeka!
11. Kitabu Kuishi Milele kimekuwa na matokeo ya kadiri gani katika shamba la ulimwengu?
11 Katika Juni 1982, Sosaiti ilitoa kile kitabu cha mafunzo kinachoitwa Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani (kwa Kiingereza). Kufikia katikati ya mwezi Septemba wa 1983, nakala 14,663,229 za kitabu hicho zilikuwa zimekwisha kuchapwa katika viwanda vya Sosaiti duniani pote. Sasa kinapatikana katika lugha 55. Kitabu hicho kimekuwa na matokeo gani katika shamba la ulimwengu! Makubwa ajabu! Tawi la Sosaiti katika Puerto Rico linaandika hivi juu ya shamba la wenye kusema Kispania huko:
‘Sisi tulipokea vitabu 30,000 vya Kuishi Milele mwezi Agosti, lakini baada ya muda mfupi vikamalizika, kisha katika mwezi Oktoba tukapokea vingine 30,000. Mwezi Februari wa mwaka 1983 ulipofika vilikuwa vimeshuka vikawa “0,” lakini katika miezi Machi na Juni tulipokea jumla ya 40,000 vingine. Kwa mara nyingine imeshuka vikawa karibu 10,000, lakini tunatazamia kupokea vitabu vingine 35,000 karibuni.’
12. (a) Hali ya kuthamini kitabu hicho imeonyeshwaje? (b) Kwa kuangalia orodha iliyo katika kurasa 12-15, je! unaona nchi ambako mafunzo ya Biblia yanazidi hesabu ya wahubiri?
12 Katika Lapland mwanamume mmoja mzee-mzee, ambaye mwenyewe si Shahidi, aliliandikia hivi tawi la Sosaiti katika Finland:
“Mimi nimesoma hesabu kubwa ya vitabu vya kidini. Lakini, nafikiri kwamba kitabu chenu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani ni kimoja cha vilivyo vizuri zaidi ambavyo nimesoma. Ningependa mnipelekee nakala 11 za kitabu hicho niwape rafiki zangu.”
Bila shaka kitabu hicho kilishiriki kuleta ongezeko kubwa katika mafunzo ya nyumbani ya Biblia wakati wa mwaka wa utumishi wa 1983. Duniani pote, mafunzo 1,797,112 yalikuwa yakiongozwa kila mwezi kwa watu walioanza kupendezwa majuzi—ongezeko la asilimia 13.3 juu ya mafunzo 1,586,293 katika mwaka wa 1982.
13. Kitabu Kuishi Milele kinaweza kuwasaidiaje wale ambao si Mashahidi wenye kutenda?
13 Je! wewe unataka kujifunza namna ya kushughulika na matatizo ya maisha? Basi wafikie Mashahidi wa Yehova kwenye moja la Majumba ya Ufalme yao kisha uombe funzo la Biblia katika kitabu hicho cha Kuishi Milele. Je! wewe umepata kupendezwa kwa muda fulani na unabii wa Biblia kama unavyoelezwa na Mashahidi wa Yehova, lakini kwa sasa wewe si Shahidi mtendaji? Wewe pia unapaswa kujifunza kitabu hicho pamoja na mmoja wa Mashahidi.
14. Mashahidi wote watendaji wanaweza kutumia vizuri kitabu Kuishi Milele kwa njia gani?
14 Je! wewe ni Shahidi ambaye mpaka sasa haongozi funzo la Biblia kwa mtu aliyeanza kupendezwa majuzi? Basi sababu gani usiamshe kupendezwa kwa mtu fulani katika kitabu hicho—kupitia ziara za nyumba kwa nyumba au ushuhuda wa vivi hivi—kisha upendekeze mkisome kitabu hicho pamoja? Ni jambo jepesi sana kufanya hivyo kwa kuyasoma tu mafungu na kuyazungumza kwa msaada wa maulizo na picha zilizomo. Kama vile Yesu mwenyewe alivyosema, wakati tunapokubali nira ya uanafunzi wa Kikristo ‘tunapata raha nafsini mwetu,’ na furaha tuliyo nayo inaongezeka wakati sisi binafsi tunapokuwa na ushiriki katika kusaidia wengine wawe wanafunzi. (Mathayo 11:29, 30; 28:19) Na mafunzo ya namna hiyo yatatufungulia njia tuje kutumia baadaye zile habari za mafunzo yanayoitia imani nguvu zilizo katika kitabu chetu kipya cha mfukoni, United in Worship of the Only True God.
15. Broshua Furahia Maisha imekuwa na matokeo gani makubwa?
15 Wakati wa mwaka uliopita, ile broshua yenye picha ya kurasa 32 inayoitwa Furahia Milele Maisha Duniani! imekuwa chombo kingine chenye nguvu katika mpango wa Mashahidi wa Yehova wa kufundisha duniani pote. Nchi ile kubwa ya Kiafrika, Zaire, ambako kilele kipya cha wahubiri 28,126 ni ongezeko la asilimia 14 juu ya wastani ya mwaka wa 1982, inatoa ripoti hii:
Broshua ile ya Furahia Milele Maisha Duniani! katika lugha mbalimbali za kwetu imekuwa na matokeo makubwa katika kazi ya kuhubiri. Wengi wamesema kwamba hicho ndicho kitu kinachofaa kabisa eneo lao ambako watu hawajui kusoma au usomaji wao si mzuri. Makundi yanagawa upesi sana akiba zao. Kanisa la Kiprotestanti katika Isiro liliomba vifaa hivyo kutoka kundi la huko ili wavitumie katika shule ya Jumapili ya kufunzia watoto. Padri Mkatoliki katika Medje aliendesha motokaa yake ya Land-Rover mwendo wa maili nyingi akijaribu kupata vifaa hivyo kwa matumizi ya shule ya kwao. Ni jambo la kawaida kuona wasafiri wakiwa wameshika nakala yao ya broshua hii.
16. (a) Broshua hiyo imekuwa na ugawaji wa kadiri gani? (b) Kupatana na Mhubiri 11:6, watoto wadogo wanaweza kutumiaje broshua hiyo’
16 Viwanda vya Sosaiti vinavyotayarisha kichapo hicho sasa vimekwisha kuchapa nakala zaidi ya 17,000,000 katika lugha 111, na watu wa duniani pote wanakitaka sasa kwa wingi sana kuliko wakati mwingine wo wote Watoto wengi wameona kwamba broshua hiyo ni msaada mkubwa katika kupanda mbegu za kweli katika rafiki zao wa shuleni, na hiyo imefanya mafunzo ya Biblia yakaanzwa kwa rafiki hao.—Mhubiri 11:6.
17. Ni mambo gani yaliyoonwa yanayoonyesha ubora wa kufundisha wa broshua hiyo na picha zake?
17 Nchi moja ambako kazi yetu ni marufuku ilileta ripoti hii:
Ulikuwa ni muda mfupi tu baada ya dada Shahidi mwenye kutumia broshua ya Furahia Maisha kufundisha watoto watatu wadogo kumaliza kuzungumza habari ya sanamu. Baada ya funzo watoto walitoka mahali walipokuwa wakaingia upesi ndani ya chumba kingine. Walitokeza tena baada ya muda mfupi, mikono yao ikiwa imejaa vitu vilivyotengenezwa kwa mbao, misalaba na vitu vingine vya namna mbalimbali. Wakaviweka mezani mbele ya Shahidi yule. Yeye akashangaa akauliza ni vya kazi gani. Msichana aliyekuwa na umri mkubwa zaidi akajibu, “Sasa hivi tu tumejifunza kwamba ni lazima tutupilie mbali sanamu na mifano kulingana na inavyosema Biblia.”
Nchi ya Ivory Coast ilileta habari hii:
Mke wa mwangalizi wa mzunguko anaripoti kwamba yeye anaweza kutumia broshua hiyo kushughulika na habari za namna mbalimbali, kama vile kuwa na wake wengi, kufanya mapenzi na mtu ye yote upendaye, hali ya kupashana habari na roho waovu na sala, kwa kuonyesha tu chache kati ya zile picha zilizochorwa vizuri ambazo zinaonyesha mambo waziwazi kabisa. Ndiyo, kama yeye anavyosema, “Picha moja inalingana na maneno elfu moja.”
“Jitengeni, Jitengeni”
18. Inawapasa watu wa Yehova ‘wajitenge’ na kitu gani hasa?
18 Katika dunia yote, si katika Afrika tu, ni lazima wote wale wanaomwabudu Mungu yule wa kweli, Yehova, waiepuke dini ya uongo ya Kibabuloni na njia zisizofuata maadili ambazo dini hiyo ama inazalisha au inaruhusu ziwepo. Nabii wa Mungu anasema hivi: “Jitengeni, jitengeni, tokeni huko, msiguse kitu cho chote kichafu; tokeni katikati yake, endeleeni kuwa safi, ninyi ambao mnachukua vyombo vya Yehova.”—Isaya 52:11, NW.
19. Imetupasa tutende namna gani waasi-imani wakijaribu kutuvuta tuache utumishi mtakatifu wetu?
19 Tangu mwaka wa 1919, watu wa Yehova wametakaswa wakawa bila uongo wa namna nyingi wa dini za Jumuiya ya Wakristo. Hata hivyo, mara kwa mara, huenda mtu fulani akarudia ibada ya sanamu na kutengwa na ushirika wa kundi. Huenda akajaribu kuwavuta wale wanaochukua “vyombo vya Yehova,” yaani, yale maandalizi yenye thamani kubwa ambayo Mungu anatayarisha kwa ajili ya utumishi mtakatifu katika utendaji wa nyumba kwa nyumba, wa magazeti, wa mafunzo ya Biblia na utendaji mwingine wa Kikristo. Lakini Mashahidi washikamanifu hata ‘hawagusi’ uasi-imani huo.—2 Wakorintho 6:17; 2 Yohana 9-11.
20. Neno la Mungu linasema nini juu ya uchafu wa kukosa maadili, na sisi tunaweza kuuepukaje?
20 Lakini, leo kuna uchafu mwingine unaochukua majeruhi walio wengi mara nyingi kuliko uasi-imani, nao ndio uchafu wa kutokufuata maadili. Tunahitaji kuwa macho tujikinge na mikazo ya ulimwengu ya kuingia katika ufisadi! Mtume Paulo anaonya kwamba “waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti,” halafu kwenye orodha ya maovu anaongeza pia “uchafu, ufisadi [mwenendo mpotovu, NW].” (1 Wakorintho 6:9, 10; Wagalatia 5:19-21) Wafisadi hawana nafasi katika paradiso ya kiroho ambayo Yehova ameanzisha kati ya watu wake leo, wala hawatakuwa na nafasi katika Ufalme wala katika dunia-Paradiso, ambayo sasa imekaribia sana. Acheni watu wote safi wa Yehova washikilie mahali pao katika paradiso ya kiroho kwa kufuata shauri lililotolewa waziwazi kabisa na Paulo: “Ukimbieni uasherati,” “ikimbieni ibada ya sanamu.”—1 Wakorintho 6:18, NW; 10:14, UV.
21. (a) Kupatana na Isaya 52:12, imetupasa tuwe na uhakika gani sasa? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna ‘miguu mizuri’ ya kupendeza?
21 Wakati wapakwa mafuta wa Yehova walipokombolewa kutoka utumwa wa dini ya Kibabuloni, wao waliona nguvu za maneno haya yaliyonenwa na nabii wa Mungu: “Hamtatoka kwa haraka, wala hamtakwenda kwa kukimbia kwa sababu [Yehova] atawatangulia; na Mungu wa Israeli atawafuata nyuma; awalinde.” (Isaya 52:12) Leo, “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Bwana unafurahia sana pia ukombozi huo. Wahubiri wote washikamanifu walio 2,501-722 wa ule Ufalme wana uhakika kamili kwamba Yehova ataendelea kuwatangulia, na kwamba atakuwa ndiye mlinzi wao huko nyuma, moja kwa moja mpaka lile pigano la kukata maneno, Har–Magedoni, na hata baada ya hapo. (Ufunuo 16:13-16) Basi, ninyi mashahidi wa yule Mungu wa kweli, Yehova, “pigeni kelele, imbeni pamoja” kwa sauti moja ya shangwe! Acheni ‘miguu mizuri’ yenu iwapeleke upesi sana katika kutangaza habari njema za kitu kizuri zaidi, kwa maana “Mungu wenu anamiliki!’—Isaya 52:7-9.—Kutoka w1/1/84
Ni majibu gani ambayo wewe ungetoa kwa maulizo yanayofuata?
◻ Yehova amewatayarishaje watu wake ‘kupiga kelele’ kwa sauti moja ya furaha?
◻ Ni kwa njia gani za maoni yanayofaa tunaweza kuonyesha tunayathamani magazeti yetu?
◻ Sisi sote tunaweza kutumia vichapo vya mafunzo vya karibuni kwa njia gani yenye matokeo mazuri?
◻ Inatupasa tuwe na itikio la namna gani kwa shauri na kitia-moyo cha Isaya 52:11, 12?
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
Katika mwezi Juni, Korea iliripoti kilele kipya cha maandikisho 6,656, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 110 juu ya hesabu ile nyingine iliyotangulia ya mwezi wa Juni. Wahubiri wa Ufalme katika Greenland walipata maandikisho mapya 510 mwaka uliopita, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 71 juu ya mwaka wa 1982
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
Sasa gazeti Amkeni! linachapwa baada ya kila miezi mitatu katika lugha zaidi—Kiarabu. Kibikoti, Kikroashia, Kifiji, Kiebrania, lugha ya Hiri Motu, Kiiselandi, Kikuyu, Kirusi, Kishona, Kisinhali, Kituruki na Kiurdu, na pia katika lugha nyingine za nchi za Mashariki Ingawa watu hawawezi kufanya maandikisho nakala moja moja zinaweza kupatikana kupitia makundi Chapa hizo za pekee zimepokewa kwa shauku nyingi sana
[Sanduku katika ukurasa wa 21]
Jamaa moja ilihama Ufaransa ikaenda kwenye kisiwa cha Moorea katika Polinesia ya Kifaransa ili kusaidia kundi dogo la huko. Baada ya miezi kadha, sasa wanaripoti mapainia 4, wahubiri 5 na mafunzo ya nyumbani ya Biblia 51. Inasemwa kwamba kwenye kisiwa cha Raiatea, kilicho karibu, kila jamaa imekwisha kujifunza pamoja na Mashahidi wa Yehova. Ulimwenguni pote, “mavuno ni mengi.”—Mathayo 9:37.