Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 6/15 kur. 8-14
  • Kiasi cha Kikristo Ni Uthibitisho wa Hekima

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kiasi cha Kikristo Ni Uthibitisho wa Hekima
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Pana Tofauti Kati ya Kiasi na Unyenyekevu
  • Ole Mwingi Ulioletwa na Ukosefu wa Kiasi
  • Kuwa na Kiasi cha Kikristo Ni Jambo la Hekima Kweli Kweli!
  • Kusitawisha Kiasi cha Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Kwa Nini Sifa ya Kiasi Bado Ni Muhimu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • Unaweza Kudumisha Sifa ya Kiasi Unapojaribiwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • Kiasi Sifa Inayokuza Amani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 6/15 kur. 8-14

Kiasi cha Kikristo Ni Uthibitisho wa Hekima

“Kupitia fadhili zisizostahilika nilizopewa naambia kila mmoja aliye huko kati yenu asijifikirie makuu kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali afikiri kwa kusudi la kuwa na akili timamu, kila mmoja kama vile Mungu amemgawia kipimo cha imani.”​—warumi 12:3, NW.

1. Ni mambo gani ya hakika yanayoonyesha kwamba kiasi hakithaminiwi leo?

LEO ni watu wachache sana wanaothamini kuwa na kiasi na kukionyesha! Hiki ni kizazi cha mashindano yenye uchungu mkali. Makabila ya watu, mataifa, mbari, mashirika na watu mmoja mmoja wa ulimwengu wanataka kuwa bora zaidi ya watu wengine wote, kuwa juu ya watu wote. Hakuna anayetaka kuwa na kiasi. Roho hiyo hata imeingia katika jamaa, kama inavyoweza kuonwa kutokana na uasi wa vijana na kule kujikaza kwa wanawake wawe huru bila kusimamiwa na wanaume.

2. Kwa sababu gani ni lazima Mashahidi wa Yehova waepuke kuwa na nia kama ile ya ulimwengu juu ya kiasi?

2 Lakini njia ya ulimwengu haipasi kuwa ndiyo njia ya Wakristo wa kweli. Hapana, Mashahidi wa Yehova wanakubali wajibu walio nao wa kufuata ule mfano mzuri kabisa wa kuwa na kiasi ambao hakujapata kuwa na mwingine wa kulingana nao katika ulimwengu huu, yaani, Yesu Kristo, Mwana wa Mungu. Yanayoonyesha Yesu alikuwa na kiasi ni maneno haya aliyoyasema: “Mwana hawezi kufanya hata jambo moja kwa kujielekeza yeye mwenyewe.” “Mbona unaniita mwema? Hakuna aliye mwema ila mmoja, naye ndiye Mungu.” (Yohana 5:19, NW; Luka 18:19, UV) Ndiyo, ni lazima watu wote wanaotaka kufuata hatua za Yesu Kristo kwa ukaribu waonyeshe kiasi. Zaidi ya hilo, wote watakaofanya hivyo hawatapata hasara, bali wataona kwamba mwendo wa kuwa na kiasi cha Kikristo unathawabisha na ni uthibitisho wa hekima kweli kweli.

3. Kwa ujumla neno kiasi linatumiwa katika njia gani?

3 Neno “kiasi” linaweza kuwa na maana ya “udogo katika ukubwa, wingi, wastani, au kadiri.” Au linaweza kumaanisha kitu kilicho safi, chenye “ukosefu wa ushenzi, upujufu, au adabu mbaya.” Halafu tena, huenda likaonyesha “kujua kwa mtu hali za kupungukiwa kwake,” au “ukosefu wa kuwa na unyeti au ubatili.”a Akiwa chini ya uongozi wa kimungu, mtume Paulo alihimiza waamini wenzake waonyeshe kiasi, kwa maana aliandika hivi: “Kupitia fadhili zisizostahilika nilizopewa naambia kila mmoja aliye huko kati yenu asijifikirie makuu kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali afikiri kwa kusudi la kuwa na akili timamu, kila mmoja kama vile Mungu amemgawia kipimo cha imani,” (Warumi 12:3, NW) Ndiyo, ni lazima tujifikirie wenyewe kidogo. Lakini ni lazima tuepuke kujifikiria mengi kupita kiasi, kujiona kwamba majaliwa tuliyozaliwa nayo ya kufanya mambo au uwezo tuliojitafutia wa kufanya mambo ni bora mno.

Pana Tofauti Kati ya Kiasi na Unyenyekevu

4. (a) Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “-enye kiasi” linapatikana wapi katika Maandiko? (b) Ni lazima tukate maneno kwa kusema nini juu ya maana ya neno hilo kwenye Mithali 11:2?

4 Katika tafsiri nyingi za Biblia, kiasi kinafikiriwa kwa njia isiyofaa kuwa ni neno moja na unyenyekevu. Neno la Kiebrania lililotafsiriwa “-enye kiasi” linapatikana kwenye Mithali 11:2 na Mika 6:8 (tafsiri ya New World). Lina maana gani? Linaweza kumaanisha kujiona kuwa mdogo, kuwa na adabu, kuwa safi katika tabia au kuwa na utakato wa kibinafsi. Lakini, linaweza pia kumaanisha kujua kwa mtu hali zake za kupungukiwa. Kwenye Mika 6:8 neno hilo la Kiebrania linaweza kuwa na yo yote ya maana hizo, kiasi au unyenyekevu, kwa maana hapo tunahimizwa vyepesi tu ‘twende kwa unyenyekevu na Mungu wetu.’ (UV) Lakini hivyo sivyo ilivyo kuhusu Mithali 11:2 (NW), panaposema hivi: “Je! kimbelembele kimekuja? Ndipo utovu wa heshima utakuja; lakini hekima i pamoja na wenye kiasi.” Hapo kiasi kinatofautishwa na kimbelembele. Hapo kinyume cha kimbelembele kinaonyesha kuwa ni kiasi katika maana ya kutokujihesabia mengi mno, kujua kwa mtu hali za kupungukiwa kwake.

5, 6. Tofauti iliyopo kati ya unyenyekevu na kiasi inaweza kuonyeshwaje kwa habari ya Yehova Mungu?

5 Pana tofauti kati ya kuwa mnyenyekevu na kuwa mwenye kiasi. Kwa mfano, mtunga zaburi Daudi alisema hivi juu ya Yehova Mungu: “Unyenyekevu wako umenikuza.” (Zaburi 18:35) Kwa kweli, Daudi alikuja kuwa mfalme mkuu katika Israeli kwa sababu Yehova alikuwa na nia ya kujinyenyekeza, au kujishusha mwenyewe, aweze kumjali yeye. Hivyo tunasoma hivi pia juu ya Yehova: “Ni nani aliye kama Yehova Mungu wetu, huyo ambaye anafanya kao lake huko juu? Yeye anajishusha ili atazame mbingu na dunia.” (Zaburi 113:5, 6, NW) Hakuna shaka​—Muumba ametukuka juu sana hivi kwamba analazimika kujishusha ili aweze kuona mambo ya mbinguni na ya duniani.

6 Lakini je! tunaweza kumsema Yehova kuwa mwenye kiasi katika maana ya kwamba yeye anatambua hali zake za kupungukiwa? Ni wazi kwamba hatuwezi! Tungewezaje kumsema Mungu kuwa ana hali za kupungukiwa, na yeye hana mipaka katika hekima na uwezo wake, tena hana kikosa kabisa kabisa na ni mkamilifu katika haki kisha ndiye mfananishwa mwenyewe wa sifa ya upendo? Hakuna hata kidogo mtu anayeweza kulinganishwa naye kwa kufaa.​—Isaya 40:12-31.

7. (a) Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba huenda mwanadamu akawa ni mnyenyekevu lakini awe anakosa kiasi? (b) Jambo hilo linaweza kuonekanaje katika kisa cha mtume Petro?

7 Kwa upande ule mwingine, inawezekana wanadamu wawe ni wanyenyekevu na bado wawe wana ukosefu wa kiasi. Huenda wakawa ni wanyenyekevu, wenye kujishusha katika maono ya moyoni, na bado wawe hawatumii uwezo wa kufikiri ili watambue hali zao za kupungukiwa. Kwa mfano, ni jambo la uhakika kwamba mtume Petro alikuwa mwanamume mnyenyekevu. Wakati alipomwona Yesu akifanya mwujiza ulioonyesha uwezo wa kuwatolea mwongozo hata viumbe walio hai katika bahari, Petro alijiweka chini miguuni pa Yesu, akisema: “Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana.” (Luka 5:8) Tena tunasoma kwamba Yesu na hata mtume Paulo walimkaripia Petro. Lakini hakuna wakati wo wote tunapohisi kwamba Petro aliudhika kwa sababu ya makaripio hayo. (Mathayo 16:21-23; Wagalatia 2:11-14; 2 Petro 3:15,16) Bila shaka, Petro alikuwa mtume mnyenyekevu, mwenye unyenyekevu wa akili. Lakini je! yeye kweli alikuwa mwenye kiasi katika maana ya kutambua hali za kupungukiwa kwake? Si nyakati zote. Kama angalitambua, yeye asingalisisitiza kwamba hata kama mitume wale wengine wote wangemkimbia Bwana wao kwa kumwacha, yeye asingefanya hivyo​—kumbe akaja kushindwa vibaya sana, akimkana Yesu mara tatu!—Marko 14:29, 30, 66-72.

Ole Mwingi Ulioletwa na Ukosefu wa Kiasi

8. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba matata yote yaliyo katika ulimwengu mzima yalianzishwa na ukosefu wa kiasi?

8 Si kwamba ukosefu wa kiasi ulimletea ole mtume Petro tu, bali inaweza pia kusemwa kwamba ole wote ulio katika ulimwengu​—ndiyo, katika ulimwengu mzima​—ulianzishwa na ukosefu wa kiasi. Namna gani hivyo? Ni kwa sababu ya ukosefu wa kiasi kiumbe mmoja wa kimalaika alikuja kuwa Shetani Ibilisi. Alishindwa kutambua hali za kupungukiwa kwake akiwa mtu aliyeumbwa. Kwa sababu ya kutokuridhika na cheo ambacho Yehova alikuwa amemgawia, yeye alitaka usawa na Mungu. Baadaye, nia hiyo ya kiburi ilionyeshwa wakati Ibilisi alipojitolea kumpa Yesu falme zote za ulimwengu kama angemfanyia kitendo kimoja tu cha ibada. Lakini kama Yesu alivyomkumbusha Mshawishi huyo, ibada inamstahili Yehova Mungu peke yake. Ukosefu wa kiasi upande wa Shetani, ambao ulikuwa na ungali ndio kisababishi cha kimbelembele, umemletea utovu wa heshima na mwishowe utamletea uharibifu.​—Mathayo 4:8-10; Waebrania 2:14.

9. Ni katika mambo gani Hawa alionyesha ukosefu wa kiasi?

9 Vivyo hivyo, ukosefu wa kiasi ndio uliommaliza Hawa, yule “mama yao wote walio hai.” (Mwanzo 3:20) Wazo la kuwa kama Mungu, la kujijulia mema na mabaya yeye mwenyewe, lilimvutia. Kwa sababu gani? Kwa sababu alishindwa kutumia kiasi. Kama angaliendelea kuwa na kiasi, angaliweza kumwambia Mshawishi jambo kama hili: ‘Sababu gani nitake kuwa kama Mungu? Mimi naridhika kabisa na mpango wa Mungu wa kwamba niwe msaidiaji wa Adamu mkamilifu. Zaidi ya hilo, afadhali nimwombe Adamu maoni yake juu ya jambo hili, kwa kuwa yeye ndiye aliyenieleza juu ya ile amri ya kutokula tunda hili.’ Lakini hakufanya hivyo. Hawa alijiondoa katika hali ya kuwa na kiasi, kuhusiana na Mfanyi wake na mume wake. Na ukosefu wa kiasi ulimpotezea Hawa uhai wake kisha ukamwongoza mume wake afuate mwendo wa kujiua mwenyewe. Kwa hiyo je! kiasi ni cha maana? Ndivyo, ni cha maana kwa kadiri hiyo!—Mwanzo 3:1-19.

10. Kwa sababu gani sisi sote tunaona ni vigumu kuwa wenye kiasi kweli kweli?

10 Inaelekea sisi sote tulirithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza maelekeo fulani ya kuonyesha ukosefu wa kiasi. Ni kama vile Mungu alivyosema baada ya Gharika, “maelekeo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya kutoka ujana wake na kuendelea.” (Mwanzo 8:21, NW) Kwa hiyo, wakati Mfalme Daudi alipojikuta katika dhambi mbaya sana bila kutazamia, angeweza kumsihi sana Mungu akisema: “Tazama, niliumbwa katika hali ya uovu; na katika makosa mama yangu alinichukua mimba.” (Zaburi 51:5, ZSB) Na hiyo ndiyo sababu Yehova Mungu angeweza kusema hivi kupitia Yeremia nabii wake: “Moyo ni mudanganyifu kuliko vyote, una ugonjwa hatari; nani anayeweza kuujua?”​—Yeremia 17:9, ZSB.

11. Ni hali gani zilizopo ulimwenguni pote zinazoweza kusemwa zimetokezwa na ukosefu wa kiasi?

11 Matata mengi sana yaliyo katika ulimwengu yameletwa na ukosefu wa kiasi! Yanapata makabila yote, watu wa mataifa yote, mbari zote na hata washiriki wa jamaa. Mataifa yanayopendelea utawala wa kiujamaa na yale yasiyoupendelea, yote pamoja hayana nia ya kukubali yana hali za kupungukiwa. Kila upande unataka uwe juu ya ule mwingine. Watu wa kabila moja wanajiona kuwa bora kuliko wale wa kabila jingine. Kwa kweli, inasemwa kwamba mara nyingi ugomvi kati ya makabila fulani ya Kiafrika unatokea kwa sababu tu kila kabila linang’ang’ania kuthibitisha kwamba hilo ndilo bora kuliko mengine.

12. (a) Ni madhara gani yanayotokana na ukosefu wa kiasi upande wa waume fulani? (b) Ni nini kinachotokezwa na ukosefu wa kiasi upande wa wanawake wengi?

12 Namna gani juu ya ukosefu wa kiasi ndani ya jamaa? Katika visa vingi, waume na hata wake wameleta hali ya kutokupatana kwa sababu ya ukosefu wao wa kiasi. Kwa sababu ya waume kuwa wanawapita wake zao kwa nguvu za kimwili na za kiuchumi, mara nyingi wanaelekea kuwa wagandamizaji, na hapo jamaa inapatwa na huzuni nyingi. Bila shaka hilo ni moja la mambo yanayofanya wanawake wawe na chama cha kutaka kujikomboa utumwani, huku wakipinga maringo ya wanaume ya kujidai kuwa wakubwa. Lakini namna gani wanawake, na hasa wale ambao wameolewa? Mara nyingi wale walio na ukosefu wa kiasi wamepata mavuno ya huzuni nyingi, kutia ndani jamaa zilizogawanyika. (Wagalatia 6:7, 8) Wanawake wa namna hiyo wamelipuuza takwa la msingi la Kimaandiko linalosema ‘wawatii waume zao kama kumtii Bwana.’ (Waefeso 5:21-23, 33; 1 Wakorintho 11:3, 7-10) Kati ya wanawake wa ulimwengu, wao pia wana ukosefu mkubwa na ulioenea sana wa kutokuwa na kiasi katika usafi wa tabia. Kwa sababu ya kupiga madaha wakionyesha marembo yao ya kimwili kwa njia yao ya kusema, kuvaa na kujiendesha wenyewe, ni lazima wanawake hao washiriki lawama la wingi uliopo wa ngono za ovyo-ovyo, ukosefu wa kuaminika katika mambo ya ndoa na kuwapo kwa jamaa zilizogawanyika.

13. Ukosefu wa kiasi umezaa tunda gani kati ya vijana wa leo?

13 Ingawa kuna mifano myema ya kiasi kati ya vijana wa kisasa, wengine wana ukosefu mkubwa ajabu. Kwa sababu ya kushindwa kuonyesha sifa hiyo, vijana wengi wanafanya harara ya kutosubiri wazee wao au wanalaumu-laumu makosa yanayofanywa na kizazi cha wazee-wazee. Hata hivyo, wengine wa vijana hao wanaonyesha hekima gani juu ya kuzoea matumizi ya dawa za kulevya, kuwa walevi, kuendesha motokaa vibaya sana au kuhusika katika mtindo wa maisha ya kukosa maadili? Kama vijana hao wangalikuwa ni wenye kiasi, wangalisikiliza wazee wao na kufaidika na mashauri mema wanayopewa na watu hao wenye ujuzi.

Kuwa na Kiasi cha Kikristo Ni Jambo la Hekima Kweli Kweli!

14. Kwa sababu gani kiasi ni jambo linalofaa sana katika uhusiano wetu na Yehova Mungu?

14 Kuonyesha kiasi cha Kikristo ni mwendo wa hekima kweli kweli. Kwanza kabisa, kufanya hivyo kunafanya mtu awe na uhusiano mwema na Yehova. Kwa kweli, Mungu anatoa takwa la kwamba tuwe wenye kiasi katika kutembea naye. (Mika 6:8, NW) Tena, kiasi ni jambo linalotufaa sana tunapofikiria pengo kubwa lililo kati yetu na Mfanyi wetu aliye mweza yote na wa umilele. Ala, kwake yeye mataifa ni kama kivumbi kidogo tu juu ya mizani na kama kitone kimoja kinachoanguka kutoka ndani ya ndoo! (Isaya 40:15) Kiasi kitatufanya tuogope kumchukiza Yehova Mungu, na kwa uhakika huo ndio “mwanzo wa hekima.”​—Zaburi 111:10.

15. Kiasi kinaweza kusaidiaje ndugu Mkristo?

15 Kiasi kinaendeleza uhusiano mwema pia pamoja na mashahidi wenzetu wa Yehova. Kitazuia ndugu Mkristo asijisukume kwa kimbelembele apate mapendeleo ya utumishi. Kiasi kitamzuia atambue hali za kupungukiwa kwake, ukosefu wake wa maarifa na ujuzi katika mambo fulani kwa kulinganishwa na wengine. Pia kitamfanya ahangaikie kufanyia sifa zake za kiroho maendeleo badala ya kuhangaikia kupata cheo cha mtumishi wa huduma au mzee. Akiendelea kutumia kwa ukamili kila nafasi ya kuongeza maarifa na kuwa mwenye msaada kwa waamini wenzake, huenda akaja kushangaa kuona amependekezwa na kuwekwa kwenye cheo cha madaraka katika kundi. Kwa kweli hivyo ndivyo imekuwa katika visa vingi.

16. Kwa sababu gani kuonyesha kiasi ndio mwendo wa hekima upande wa wanawake Wakristo?

16 Kiasi ndio mwendo wa hekima kwa akina dada pia katika kundi. Ndivyo ilivyo katika mambo mengine pia, si katika lile jambo la kuwa na usafi wa tabia tu ingawa ni la maana sana. (1 Timotheo 2:9, 10; Tito 2:3-5) Kwa kutambua hali za kupungukiwa kwake na daraka alilogawiwa katika kundi, mwanamke Mkristo aliye na hekima atatumia kiasi kuongoza usemi wake. Atajizuia asiwe kidomodomo na asiwe akilaumu-laumu njia ambayo wazee waliowekwa wanatumia kushughulikia mambo.​—Linganisha Yuda 8, 9, 16.

17, 18. (a) Kwa sababu gani inawapasa vijana waonyeshe kiasi kuwaelekea wazazi wao? (b) Hapa ni mfano gani wa Kimaandiko unaotolewa kuonyesha kwamba ni jambo la hekima kutii shauri la watu wazee?

17 Vivyo hivyo, kiasi kwa upande wa vijana ni uthibitisho wa hekima. Vijana wanajifanya wapendwa na wengine wakati wanapojiendesha wenyewe kwa kiasi. Kwa kufaa Neno la Mungu linawapa amri ya kuheshimu baba na mama zao na kuwatii katika “mambo yote.” (Wakolosai 3:20; Waefeso 6:1-3) Ili mtu aweze kufanya hivyo na kuepuka kuwa na fikira ya kwamba vijana ni wenye hekima kuliko wazazi wao, anahitaji kuwa na kiasi. Na je! wewe huna deni la kupigia wazazi wako asante? Wao ndio walikuleta ulimwenguni. Kuanzia wakati huo mpaka sasa, wazazi wako wamekupa chakula, mavazi, makao, elimu, tafrija na mafundisho ya kiroho. Basi, je! kuwa na heshima peke yake hakutoshi kukusukuma uwaonyeshe kiasi?

18 Kuwatumaini wazazi wako kwa kuwaambia mambo yako binafsi ukiwa na kiasi na kukubali mashauri yao ndio mwendo wa hekima. Kwa sababu ya ujuzi wao, hakika wao wana hekima nyingi kuliko wewe. Ulimwengu umejawa na msukosuko, si kwa sababu ya ukosefu wa maarifa bali kwa sababu ya ukosefu wa hekima iliyo sawa. “Wamelikataa neno la [Yehova]; wana akili gani ndani yao?” (Yeremia 8:9) Hata katika lile jambo la kibinafsi sana la kuchagua mwenzi wako wa maisha, utakuwa mwenye hekima ikiwa utakuwa na kiasi uheshimu uamuzi wa wazazi wako kama inavyofaa, kwa kuwa wao wanakupenda na wangependa kuona ukifaidika kabisa. Wao wanaweza kukupa mawazo bora sana kuliko vijana wa rika lako. Ni kweli kwamba huenda mawazo hayo yakawa si ya kusifu-sifu uchaguzi wako kwa njia isiyo na unyofu, lakini yatakuwa ndiyo yanayokufaa zaidi. Biblia inafunua kwamba Mfalme Rehoboamu wa Israeli wa kale alipoteza sehemu kubwa ya ufalme wake kwa sababu ya ukosefu wa kiasi. Alikataa mashauri ya wanaume wazee waliokuwa wamekuwa washauri wa baba yake kisha akachagua kufuata mashauri yenye kumsifu-sifu bila unyofu ya vijana wa rika lake, wale waliokua pamoja naye katika ujana wao. Wao walikuwa watu wasio na ujuzi wala busara ya kuona mambo ya mbele, sawasawa na yeye mwenyewe.​—1 Wafalme 12:1-24.

19. Kiasi kinaweza kutusaidia sana namna gani katika utendaji wetu wa kutoa ushuhuda?

19 Kiasi cha Kikristo kitatusaidia sana pia tunapotoa ushuhuda juu ya jina la Yehova Mungu na Ufalme wake, iwe ni kwa njia rasmi au vivi hivi tu. Tukisema tukiwa na hali ya kujisikia tunajua sana, huenda tukavutia wasikilizaji fulani lakini tuudhi wengine wengi wasitake kusikiliza. Nyakati zote, inatupasa tuelekeze fikira kwa Yehova Mungu na Neno lake, si kwetu wenyewe. Wazo hili lenye msaada linaonyesha wazi sana jambo hilo: “Mtakaseni Kristo kama Bwana katika mioyo yenu, mkiwa tayari sikuzote kujitetea mbele ya kila mtu anayetaka kwenu sababu ya tumaini lililomo ndani yenu, lakini mkifanya hivyo pamoja na upole na heshima nyingi.” (1 Petro 3:15, NW) Kiasi kitafanya liwe jambo jepesi zaidi kuonyesha tabia ya upole na kuonyesha heshima yenye kina kirefu.

20. (a) Kufikia hapa, tumejifunza nini juu ya kiasi na ukosefu wa kuwa nacho? (b) Ni ulizo gani linalobaki?

20 Tunaweza kuona wazi kutokana na mambo yaliyotangulia kutajwa kwamba madhara makubwa yamepata wanadamu kwa sababu ya ukosefu wa kiasi. Tumeona pia kwamba pasipo shaka kiasi ndicho mwendo wa hekima. Mambo hayo yatusaidie tusitawishe kiasi. Lakini ni msaada gani zaidi tunaoweza kupata ili tusitawishe kiasi cha Kikristo?

[Maelezo ya Chini]

a Webster’s Third New International Dictionary.

Wewe Unaweza Kukumbuka?

◻ Kwa sababu gani ni lazima Mashahidi wa Yehova waepuke kuwa na nia ya ulimwengu juu ya kiasi?

◻ Mtu anaweza kuwa mnyenyekevu namna gani lakini asiwe ni mwenye kiasi?

◻ Kwa sababu gani sisi sote tunaona ni vigumu kuwa wenye kiasi kweli kweli?

◻ Kwa sababu gani ni jambo linalofaa sana tuwe wenye kiasi katika uhusiano wetu pamoja na Yehova?

◻ Kiasi kinaweza kutusaidiaje katika kazi yetu ya kutoa ushuhuda?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yesu alifanya kwa kiasi alivyoelekezwa na Baba yake wa kimbingu afanye

[Picha katika ukurasa wa 11]

Kiasi cha Kikristo kinaleta uhusiano mzuri pamoja na Mungu na mashahidi wenzetu wa Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki