Kusitawisha Kiasi cha Kikristo
1. Ni maneno gani yanayoonyesha kwamba watu fulani wa ulimwengu wamethamini ubora wa kiasi?
KIASI ni sifa ya wema ambayo wakati mmoja ilithaminiwa na wenye hekima wa ulimwengu huu. Hivyo tunaambiwa: “Mtu mwenye kiasi anashindwa mara chache sana kupata upendeleo wa wale anaoongea nao, kwa sababu hakuna mtu anayeona kijicho juu ya mtu asiyeelekea kusema mambo mazuri juu yake mwenyewe.” Na imesemwa hivi pia: “Kiasi ni nuru inayong’aa; kinatayarisha akili ipokee maarifa, na kutayarisha moyo upokee ukweli.” Mtu asiye na kiasi ataelekea kutokutaka kukubali kwamba mambo yako namna yalivyo hasa, aelekee kuyafanya yaonekane kuwa vingine.
2. Watu fulani wanaojulikana sana wameonyeshaje kiasi?
2 Halafu tena, watu fulani wanaojulikana kwa sababu ya vitu walivyovumbua wameonyesha kiasi. Hivyo wakati mmoja Albert Einstein alisema kwamba “inaonekana wazi kuwa kuna roho fulani katika sheria za Ulimwengu Mzima—roho fulani yenye nguvu nyingi sana sana kuliko zile za mwanadamu, ambayo sisi tukielekeana nayo lazima tujisikie kuwa wanyenyekevu kwa sababu uwezo wetu ni wa kiasi.” Naye Bwana-mheshimiwa Isaac Newton, anayefikiriwa na wengi kuwa ndiye mwanasayansi anayewashinda wanasayansi wa nyakati zote, alisema hivi wakati mmoja: “Ikiwa nimeona mbali kuliko wengine, nimefanya hivyo kwa sababu ya kutegemea wenye kunipita mimi.” Ni wazi kuna madaktari fulani wapasuaji wenye akili hiyo ya kiasi ambao wamepasua Mashahidi wa Yehova. Baada ya kupata mafanikio katika upasuaji mbalimbali wenye kutatiza sana bila kutia damu mishipani, wamewaambia wagonjwa wao walio Mashahidi kwamba sifa inamwendea Mungu, wala si wapasuaji hao wenyewe.
Mifano ya Kiasi
3. (a) Ni nini kitakachotusaidia tusitawishe kiasi? (b) Inaweza kusemwaje juu ya Musa na kiasi?
3 Ni nini kitakachotusaidia katika kusitawisha ile sifa ya kupendeza sana na inayohitajiwa sana ya kiasi? Ni wazi kwamba kufuata mambo yote ambayo yamesemwa katika makala iliyotangulia juu ya kimbelembele na kiasi kutatusaidia tusitawishe kiasi. Msaada mwingine katika kusitawisha kiasi ni kufikiria namna Yehova alivyowatumia watumishi wake wenye kiasi kwa njia hodari sana. Mungu angewezaje kutumia watu wenye kujitafutia sifa walioelekeza fikira za watu juu yao wenyewe badala ya kuzielekeza kwa Mfanyi wao! Ni kweli kwamba ni Wakati mmoja tu Musa alipofanya hivyo akiwa chini ya mkazo mkubwa na kwa sababu ya kuvurugwa sana na watu. Lakini loo, alipata hasara kubwa kama nini! Lakini jambo la kwamba Musa alikuwa mwenye kiasi kweli kweli linaweza kuonwa kutokana na woga aliokuwa nao hapo mwanzoni juu ya kumwendea Farao. Tena, Maandiko yanasema kwamba “huyo Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.”—Hesabu 12:3; Kutoka 4:10-17.
4. Elihu na Yusufu walionyeshaje kiasi kinachofaa?
4 Mfano mwingine mwema wa kiasi ni kijana Elihu. Yeye alingoja kwa subira mpaka waliokuwa wazee kuliko yeye, yaani, Ayubu na wenzi wake watatu, wakamaliza kusema kabla yeye hajaanza kunena. Elihu hakuwa na majivuno ya kujiona kuwa bora bali alielekeza sifa yote kwa Mfanyi wake. (Ayubu 32:4-11, 21, 22; 36:9) Yusufu, mwana wa Yakobo mzee wa ukoo, alionyesha kiasi kinachofaa pia wakati alipoletwa mbele ya Farao mwenye cheo kikubwa sana na kuulizwa kama angeweza kufasiri ndoto ya maliki (mfalme) huyo. Yusufu alimpa Yehova sifa kwa kuzifasiri ndoto.—Mwanzo 40:8; linganisha Danieli 2:26-30.
5. Kwa sababu gani kiasi cha Gideoni kilikuwa jambo la maana kwa Yehova Mungu?
5 Fikiria, pia, kisa cha Gideoni. Alipokuwa akipokea agizo la mgawo wake, yeye alisema kwa kiasi kwamba mbari ya watu wao ilikuwa ndiyo ndogo zaidi ya zote katika Manase na yeye mwenyewe alikuwa ndiye mdogo kuliko watu wote katika nyumba ya baba yake. Kwa hiyo Gideoni ndiye aliyefaa kabisa kutumiwa na Yehova katika kuwashinda Wamidiani kwa sababu Mungu alikuwa ameamua kabisa kujipatia mwenyewe sifa kwa ushindi ambao ungepatikana. Ni mtu mwenye kiasi kweli kweli tu ambaye angeweza kutumikia vizuri katika hali hiyo.—Waamuzi 6:14-16; 7:2-7.
6. (a) Kwa sababu gani Yehova alipendezwa na ombi la Mfalme Sulemani kijana? (b) Ni mtumishi gani mwingine wa Yehova aliyekuwa kijana ambaye alionyesha kiasi kinachofaa, na katika jambo gani? (c) Nia iliyoonyeshwa na kijana Elihu, Sulemani na Yeremia inaweza kuwa na matokeo gani juu ya mashahidi vijana wa Yehova au walio na ujuzi mchache kwa kulinganishwa na wengine?
6 Kijana Sulemani pia alionyesha kiasi alipofanywa mfalme hapo kwanza. Alipoulizwa na Mungu katika ndoto angependa kupata nini, Sulemani alijibu hivi kwa kiasi: “Nami ni mtoto mdogo tu. . . . Nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi [walio wagumu, NW]?” Yehova alipendezwa sana na kiasi cha Sulemani mpaka Yeye akampa mali nyingi sana na utukufu, zaidi ya kumpa hekima. (1 Wafalme 3:4-14) Kwa sababu ya kiasi cha Sulemani, Yehova alimfanya akawa ndiye mtawala mwenye hekima kupita watawala wote wa kibinadamu. Yeremia alionyesha kiasi cha namna iyo hiyo kwa habari ya ujana wake alipoitwa awe nabii wa Yehova. (Yeremia 1:6-8) Je! wewe ni shahidi wa Yehova aliye na ujana au hali ya kutokuwa na ujuzi kwa kulinganishwa na wengine? Ikiwa ndivyo, kwa uhakika utajithibitisha kuwa mwenye hekima kama utaonyesha kiasi kinachokupasa, kama kijana Elihu, Sulemani na Yeremia.
7. Ni kwa njia gani maneno ya Paulo kwenye 1 Wakotintho 2:1-5 ni mfano mwema wa kiasi kwa watangazaji wa Ufalme?
7 Kinachostahili kuangaliwa pia ni kiasi cha mtume Paulo. Ingawa yeye alikuwa amekuwa Farisayo mwenye elimu ya juu sana na baadaye alitumiwa kwa njia hodari na Yehova Mungu, Paulo hakujionyesha-onyesha juu ya vile alivyokuwa na hali bora za namna nyingi. Ni kama vile yeye mwenyewe alivyosema: “Basi, ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima. Maana naliazimu nisijue neno lo lote kwenu ila Yesu Kristo, naye [ametundikwa mtini]. Nami nalikuwako kwenu katika hali ya udhaifu na hofu na matetemeko mengi. Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za [roho] na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.” (1 Wakorintho 2:1-5) Wengine wa Mashahidi wa Yehova wametoka kati ya watu wenye elimu ya juu sana. Lakini, kama Paulo, wao wanaonyesha kiasi katika kuzitangaza habari njema, wakifuata kwa hekima mfano mwema wa mtume.
8. Yesu alikuwaje ndiye mfano ulio mwema na mkubwa zaidi wa kuwa na kiasi?
8 Bila shaka, mfano ulio mkubwa na mwema zaidi wa kiasi si mwingine ila Yesu Kristo. Pana tofauti kubwa kama nini kati ya Mwana wa Mungu na yule ambaye baadaye alikuwa Shetani Ibilisi! Hakuna hata wakati mmoja Kristo ametafuta usawa na Yehova Mungu kwa kukosa kiasi. (Mathayo 4:8-10; Wafilipi 2:5-8) Basi, Yesu anaridhika kabisa kuwa msaidizi na mnenaji wa Baba yake. (Mithali 8:30; Yohana 1:1) Alipokuwa duniani alisema mara nyingi kwamba cheo chake kilikuwa kidogo kuliko cha Mungu. (Yohana 5:19, 30; 7:28; 8:28, 42) Alikataa kupewa sifa ya kibinafsi, akaelekeza fikira za watu kwa Yehova. (Marko 10:18) Na wakati Yesu alipokuwa katika jaribu lililo kubwa kupita yote, nia yake ilikuwa kwamba: “Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki kiniepuke; walakini si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.” (Mathayo 26:39) Pasipo shaka, Yesu alituwekea mfano mwema katika kuwa na kiasi. Basi, kwa uhakika inawapasa viumbe wote wa Mungu wa kiroho na wanadamu wote wawe wenye kiasi.
Kuwa na Kiasi Ni Jambo la Akili
9. Kulingana na 1 Wakorintho 4:6, 7, kwa sababu gani ni jambo la akili watumishi wa Mungu wawe na kiasi?
9 Ni jambo linalolingana na akili nzuri kwamba sisi tuwe wenye kiasi. Kwanza, je! sisi sote si watu wasio wakamilifu? Hakuna anayeweza kukana jambo hilo! (1 Wafalme 8:46) Sisi sote tunafanya makosa. Ujuzi wetu ni mchache na kwa vyo vyote maarifa yetu yana mipaka. Zaidi ya hilo, sisi tumepokea kila kitu tulicho nacho. Hivyo mtume Paulo alihimiza waamini wenzake wasiyapite mambo yaliyoandikwa “ili,” kama yeye alivyosema, “mmoja wenu asijivune kwa ajili ya huyu, kinyume cha mwenziwe. Maana ni nani anayekupambanua na mwingine? nawe una nini usichokipokea? Lakini iwapo ulipokea, wajisifia nini kana kwamba hukupokea?” (1 Wakorintho 4:6, 7) Kwa wazi, sehemu kubwa ya namna sisi tulivyo inategemea urithi tuliopata kutokana na chembe zinazoamua tabia ya mtu, inategemea mazingira yetu na hasa majaliwa kutoka kwa Mungu.
10. Mafanikio katika utumishi mtakatifu yanategemea nini, na kutambua uhakika huo kunapasa kuwa na matokeo gani juu yetu?
10 Tena, je! si jambo la hakika kwamba hata tupate mafanikio ya namna gani katika utumishi mtakatifu wetu, kila jambo linategemea baraka ya Yehova? Kwa mfano: Hata mkulima afanye bidii namna gani, hali ya hewa ni jambo la maana sana katika ukuzi wa mazao. Na mtunga zaburi alitoa maoni hayo kwa kufaa: “[Yehova] asipoijenga nyumba, waijengao wafanya kazi bure. [Yehova] asipoulinda mji yeye aulindaye akesha bure.” Akionyesha jambo ilo hilo juu ya kazi ya wahudumu (maminista) Wakristo, mtume Paulo aliandika hivi: “Mini nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.” (Zaburi 127:1; 1 Wakorintho 3:6, 7) Ndiyo, tukilifikiria jambo hilo, tutalazimika kukubali kwamba kiasi kinatupasa sisi sote, hata tuwe tuna majaliwa ya kuweza kufanya nini, tuwe tumetimiza mambo gani au tuwe tuna mali nyingi namna gani.
Misaada Katika Kusitawisha Kiasi
11. Kupenda Yehova Mungu kutatusaidiaje tuwe na kiasi?
11 Upendo ni kati ya sifa zitakazotusaidia tuwe wenye kiasi, yaani, upendo usio wa kichoyo. Ikiwa tunathamini yote ambayo Yehova Mungu amefanya, anaendelea kufanya na bado atafanya kwa ajili yetu, tutampenda yeye kweli kweli kwa moyo wetu wote, nafsi yote, akili na nguvu zote. (Marko 12:30) Halafu sisi hatutajisifu juu yetu wenyewe. Ingawaje, majisifu ndicho kinyume cha kiasi. Bali, sisi tutasema na kutenda nyakati zote tukiwa na kiasi kinachofaa ili tuelekeze fikira za watu kwa Yehova Mungu wala si kwetu wenyewe, kuacha utukufu na utukuzo wote umwendee yeye. Ndipo tutakapokuwa tukitii shauri hili: “Mtu mwenye hekima asijisifu juu ya hekima yake wala juu ya uthabiti wa ushujaa wake; mtu tajiri asijisifu juu ya mali zake; lakini ikiwa mtu ye yote angependa kujisifu, ajisifu juu ya jambo hili, kwamba yeye ananifahamu na ananijua. Kwa maana mimi [Yehova], naonyesha upendo usioshindwa, mimi nafanya haki na yanayofaa juu ya dunia; kwa maana juu ya hayo mimi nimeweka moyo wangu. Hilo ndilo neno lenyewe la [Yehova].”—Yeremia 9:23, 24, The New English Bible.
12. Uhusiano mwema pamoja na Mungu unaweza kutusaidiaje tuwe wenye kiasi?
12 Kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kutatusaidia pia tuwe wenye kiasi nyakati zote. Tunatazamiwa tuwe wenye kiasi katika kutembea pamoja na Mungu wetu. (Mika 6:8, NW) Kwa kadiri ile ile ambayo sisi tunamhesabia Muumba, ukuu wake, adhama yake na sifa zake kuwa halisi, ni kwa kadiri iyo hiyo tutajiendesha wenyewe kwa kiasi kinachofaa. Inatupasa tuwe na nia ile ile ya akilini aliyokuwa nayo Musa, ambaye “aliendelea kuwa thabiti kama kwamba anamwona Yule asiyeweza kuonekana.” (Waebrania 11:27, NW) Ni kama kwamba sisi ni watoto wadogo wanaoshika mkono wa Baba yetu wa kimbingu. Tukijilisha Neno la Yehova kwa ukawaida na ‘kudumu katika kusali,’ ndiyo ‘kuomba bila kukoma,’ tutasaidika tuwe na uhusiano mzuri huo wa kindani pamoja na Mungu.—Warumi 12:12; 1 Wathesalonike 5:17.
13. Ni kwa njia gani tamaa yetu ya kumwiga Yesu Kristo inaweza kutusaidia tuwe wenye kiasi?
13 Upendo na uthamini kwa yote ambayo Bwana wetu, Yesu Kristo, ametufanyia na kujua maana ya kufuata hatua zake kwa ukaribu ni mambo ambayo yatatusaidia pia tuwe wenye kiasi. Lo! Yesu alituwekea sisi mfano mwema kama nini, usio wa kichoyo na mkamilifu! Kwa kadiri tutakavyochukua kwa uzito wajibu wetu wa kufuata hatua zake kwa ukaribu, tutasaidika tuwe wenye kiasi. Namna gani hivyo? Kwa sababu tutathamini tunashindwa kwa mbali sana kufuata mfano wake. Huenda tukajisikia tukijifurahia wenyewe tunapojilinganisha na wengine. Lakini je! sisi tuna msingi wa kujifurahia sana tunapowekwa kando ya Yesu Kristo kwa kulinganishwa? Badala ya kuwa hivyo, imetupasa tujisikie kama vile mtume Paulo alivyojisikia—tukumbuke kwa masikitiko mengi kwamba tunashindwa kufanya lile tunalotaka hasa na kwamba mara nyingi sana tunafanya lile ambalo kwa kweli tusingetaka kulifanya. Hakuna Mkristo anayejua sana kwamba anapungukiwa kwa mbali sana kuwa mfuataji wa mfano wa Yesu Kristo atakayejisikia akitaka kujivuna ndani yake mwenyewe.—Warumi 7:15-25.
14. Kwa sababu gani upendo wa kidugu unaweza kutusaidia tuwe wenye kiasi?
14 Vivyo hivyo, kupenda mashahidi wenzetu wa Yehova na washiriki wa jamaa yetu wenyewe kutatusaidia tuwe wenye kiasi. Ni kama vile wimbo mmoja wa Ufalme unavyosema: “Laona mema pendo. Lajenga ndugu pendo.” Ndiyo, upendo utatufanya tuthamini sifa njema zilizo katika wengine. Lakini kufanya hivyo kunaweza kutusaidiaje tuwe wenye kiasi? Ni kwamba, ukosefu wa kiasi unaudhi wengine, unawafanya wajisikie wamekosa starehe (wana wasiwasi). Kwa kuwa hatutaki kuwaudhi wale tunaowapenda, upendo wa kweli wa kidugu utatufanya tuwe wenye kiasi. Ukosefu wa kiasi unachochea mashindano, ushindani mkali, au unafanya wengine wajisikie hawafai kitu wakilinganishwa nasi. Lakini upendo “haujigambi, haujitutumui kwa kiburi.” Bali, ni wenye kiasi.—1 Wakorintho 13:4, NW.
15. Kujiweza kunaweza kutusaidiaje tuwe wenye kiasi?
15 Kujiweza, tunda la roho takatifu ya Mungu, kunatusaidia pia kusitawisha kiasi. (Wagalatia 5:22, 23, NW) Je! kweli kuna uhusiano kati ya mambo hayo mawili? Ndivyo hakika. Mara nyingi mtu anaelekea kusema au kutenda jambo la kujitukuza au la kujisifu-sifu kupita kiasi, nyakati nyingine sababu ikiwa ni kwamba tu anatenda kwa kusisimuka haraka bila kwanza kufikiri vizuri. Mara tu baada ya yeye kusema au kutenda hivyo, huenda akajua kosa lake. Hiyo ni kwa sababu moyo wa kibinadamu ni wenye ujanja, wenye hila, mdanganyifu. (Yeremia 17:9, The Jerusalem Bible; NE) Lakini kutumia kujiweza, kungoja kidogo, kufikiri, kuwaza hasa maneno au vitendo vyetu vitakuwa na matokeo gani juu ya wengine, kutatusaidia tuonyeshe kiasi kinachofaa. Kwa mfano, tusipofikiri vya kutosha, huenda tukawa na melekeo ya kuchukua kipande kilicho kizuri au kikubwa zaidi cha nyama, mkate au tunda wakati vinapopitishwa mbele yetu au vinapozungushwa tukiwa kwenye chakula cha jioni. Lakini kujiweza na kutangulia kufikiri ni mambo yatakayotuwezesha tupinge msisimuko huo. Ndivyo pia kwa habari ya kuketi juu ya kiti kilicho bora zaidi kwenye karamu. Kama Yesu alivyoonyesha, huenda tukaambiwa tuondoke tukaketi mahali pa cheo kidogo zaidi. Lakini, tukitumia fikira na kiasi kidogo tutaepuka kufanya kosa lenye kutuaibisha katika mambo ya namna hiyo.—Luka 14:8-11.
16. Kwa sababu gani kuwa na imani katika Yehova kunaweza kutusaidia tuwe wenye kiasi?
16 Tunda jingine la roho litakalotusaidia kusitawisha kiasi ni kuwa na imani katika Yehova, ambayo inatokana na uhusiano mzuri pamoja na yeye. Hali ya mwanadamu mwenye dhambi ina maelekeo ya kuchochea ndani ya mtu woga wa kupoteza mambo mazuri ya maisha, yawe ni ya kimwili, ya kiakili, ya kimoyo au ya kiroho. Lakini kuwa na imani katika Yehova kutatuepusha tusijisukume mbele kwa kimbelembele au kwa kukosa kiasi. Bali, tutaacha mambo mikononi mwa Yehova. Ikiwa tuna kiasi, tutaweza kungoja mpaka Mungu anyoshe mambo au ahakikishe kwamba tunapewa cheo cha kutambuliwa au tunasogezwa mbele. Kabla Daudi hajawa mfalme, yeye alionyesha kiasi hicho. Angaliweza kujitwalia mambo mikononi mwake mwenyewe, kwa maana alikuwa amepakwa mafuta awe mfalme. Daudi angaliweza kuwa mtawala wa Israeli moja kwa moja kwa kumwua Mfalme Sauli, lakini hapana, Daudi alimngojea Yehova kwa kiasi ndiye ampe uufalme huo, na Yehova alifanya hivyo, katika wakati Wake mwenyewe.—1 Samweli 24:2-6; 26:10, 11.
17. Ni katika njia gani mbalimbali huruma ya kujitia katika hali za wengine inaweza kutusaidia tuwe wenye kiasi?
17 Msaada mwingine wa kuwa na kiasi ni kuwa na huruma ya kujitia katika hali za wengine. Kwa mfano, ukosefu wa kiasi huenda ukafanya mzee wa kundi awe akipitisha wakati mara nyingi anaposhughulika na migawo yake katika mikutano ya kundi. Lakini kama yeye ana huruma ya kujitia katika hali za wengine, ataweza kujisikia namna wanavyojisikia wazee wenzake wanaohangaikia kupata wakati unaozitosha sehemu zao katika programu. Mzee mwenye kiasi atawafikiria pia ndugu na dada zake wa kiroho, ambao hawafurahi wakati mkutano unapopita saa zilizowekwa bila sababu nzuri. Kwa kweli, huruma ya namna hiyo itafanya mtu awe na kiasi katika uhusiano wa namna zote, si katika kundi la Kikristo tu. Huruma hiyo ilimfanya mtume Paulo akawa ‘kama Myahudi kwa Wayahudi, kama aliye chini ya sheria kwa wale walio chini ya sheria, kama mnyonge kwa wanyonge,’ na hivyo hivyo—akafanya yote hayo kwa ajili ya habari njema. Hiyo ilimaanisha kuwa mwenye kiasi, kuonyesha wasikilizaji wake kwamba hakujifikiria mwenyewe kuwa bora kuliko wao.—1 Wakorintho 9:19-23.
18. Ni mambo gani mema yanayoweza kusemwa juu ya kiasi cha Kikristo?
18 Kwa kweli, kiasi cha Kikristo kina mema mengi ya kupendekeza kwamba kinafaa. Loo, ni upotevu mwingi kama nini umetokea muda wote wa historia kwa sababu ya ukosefu wa kiasi! Kwa kweli kuonyesha kiasi ni jambo la akili kwa Mkristo. Kunaleta uhusiano mwema pamoja na Mungu, mashahidi wenzetu wa Yehova, jamaa yetu wenyewe na pamoja na wengine. Kiasi hata kitatusaidia sisi binafsi, kwa maana kitafanya turidhike na kutuzuia tusivurugike akili kwa kukata tamaa. Kwa hekima, Neno la Mungu linatusaidia sana tuwe wenye kiasi. Basi sisi na tuonyeshe uthibitisho wa kwamba tuna hekima ya kweli kwa kusitawisha na kuonyesha kiasi cha Kikristo.—Kutoka w1/15/84.
Wewe Ungejibuje?
◻ Vijana fulani walioandikwa katika Biblia wameonyeshaje kiasi?
◻ Yesu Kristo alikuwa namna gani mfano mkubwa ulio mwema zaidi ya yote wa kuwa na kiasi?
◻ Ni kwa njia gani mbalimbali kupenda Yehova na kuwa na uhusiano mzuri naye kunaweza kutusaidia tusitawishe kiasi?
◻ Tamaa yetu ya kufuata mfano wa Yesu Kristo inaweza kutusaidiaje tuonyeshe kiasi?
◻ Kwa sababu gani upendo wa kidugu unaweza kutusaidia tuwe wenye kiasi sisi waabudu wa Yehova?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Elihu aliepuka kwa kiasi hali ya kujiona kuwa anawapita wengine, akaelekeza sifa yote kwa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 17]
Kujilisha kwa ukawaida Neno la Mungu na ‘kuomba bila kukoma’ ni mambo yatakayotusaidia tusitawishe kiasi