Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 7/1 kur. 9-13
  • Waabudu Walioungana wa Mungu wa Kweli Mmoja Tu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Waabudu Walioungana wa Mungu wa Kweli Mmoja Tu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Ndiwe Mungu Peke Yako”
  • Mambo Yenye Nguvu za Kuunganisha
  • Kuwa Upande wa Ibada ya Kweli kwa Uthabiti
  • Umoja wa Ibada Katika Nyakati Zetu Unamaanisha Nini?
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Umoja Unatambulisha Ibada ya Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Familia ya Yehova Hufurahia Muungano Wenye Thamani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Dumisheni Muungano Katika Siku Hizi za Mwisho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 7/1 kur. 9-13

Waabudu Walioungana wa Mungu wa Kweli Mmoja Tu

‘Wewe, [Yehova],... ndiwe Mungu peke yako.”​—ZABURI 86:9, 10.

1. (a) Yehova ameanzisha utendaji wa kitu gani ili alete umoja wa ibada? (b) Ni nini kilichotokea mara tu baada ya kuanzishwa kwa “usimamizi” huo?

UMOJA wa kuabudu​—lo! ni jambo la kuvutia namna gani! Lakini walio wengi kati ya wanadamu hawajawa na umoja huo hata siku moja. Hata hivyo, umoja wa kuabudu si ndoto tu. Ni kusudi la Mungu. Karne kumi na tisa zilizopita Yehova alianzisha utendaji wa “usimamizi” fulani, lengo lao likiwa ni kupata umoja​—umoja ambao mtu angeona katika jamaa yenye mwungano mwingi sana, yenye upendo. Baada ya muda mfupi umoja uliotokezwa na “usimamizi” huo ukafanya Wayahudi Wakristo waabudu pamoja na Wasamaria kwa ushirika wenye upendo; halafu Mataifa wasiotahiriwa wakakaribishwa waingie ndani ya kundi. Jambo la maana zaidi ni kwamba wote waliingizwa katika umoja pamoja na Yehova Mungu kwa kutegemea imani yao katika ubora wenye kulipia dhambi wa dhabihu ya Yesu. Wakapata kufurahia pamoja naye uhusiano wa wana na Baba mwenye upendo.

2. (a) “Usimamizi” huo ni nini, nao ulianza kufanya kazi wakati gani? (b) Ni nini maana ya kukusanywa kwa “vitu vilivyomo mbinguni”?

2 Andiko la Waefeso 1:9, 10 (NW) linavuta fikira kwenye “usimamizi” huo, likisema: “Ni kulingana na furaha yake njema aliyokusudia ndani yake mwenyewe kwa ajili ya usimamizi [au, njia fulani ya kusimamia mambo ya jamaa] katika utimilifu wa nyakati zilizowekwa [tangu Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. na kuendelea], yaani, kuvikusanya tena vitu vyote pamoja katika Kristo, vitu vilivyomo mbinguni na [baadaye] vitu vilivyomo duniani.” Mkusanyo wa “vitu vilivyomo mbinguni,” yaani, watu mmoja mmoja ambao wangekuwa pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa kimbingu ulifanywa kwanza kati ya Wayahudi, halafu kati ya Wasamaria kisha kati ya Mataifa.

3. Kukusanywa kwa “vitu vilivyomo duniani” kumetokeza nini?

3 Katika siku zetu, hasa tangu mwaka wa 1935 W.K., tunaona “vitu vilivyomo duniani” vikikusanywa, yaani, watu ambao wangependelewa kuishi katika dunia-Paradiso. Tayari mamilioni ya watu wameitikia sehemu hii ya pili ya “usimamizi” wenye upendo wa Mungu. Wanatoka katika mataifa yote na vikundi vya lugha zote. Umoja wanaopata si wa kukusanyika kimwili tu kati ya watu wanaoendelea kushikilia imani zao na mazoea yao ya zamani. Badala ya hivyo, kama ilivyotabiriwa kwenye Isaya 2:3, wao wanajifunza njia za Yehova ili waweze ‘kwenda katika mapito yake.’

4. (a) Ni kwa kadiri gani umoja wa ibada utapatikana, na Biblia inaelezaje jambo hilo? (b) Baada ya jaribu la mwisho, wanadamu waliokamilishwa watafurahia uhusiano gani na Yehova?

4 Lakini, tunachoona leo si kipimo kamili cha umoja ambao utafikiwa. Kusudi la Mungu linahakikisha kwamba viumbe vyote vyenye akili vitaunganishwa katika ibada ya kweli. Mtume Yohana alipewa maono ya mapema juu ya hali nzuri sana ambayo itakuwako mwishoni mwa Utawala wa Kristo wa Mileani, naye anayasimulia kwenye Ufunuo 5:13, akisema: “Kila kiumbe kilichoko mbinguni na juu ya nchi na chini ya nchi [na] juu ya bahari, na vitu vyote vilivyomo ndani yake, nalivisikia, vikisema, Baraka na heshima na utukufu na uweza una yeye aketiye juu ya kiti cha enzi [yaani, Yehova], na yeye Mwana-Kondoo [Yesu Kristo], hata milele na milele.” Hapo Yohana aliona kila mtu akiwa ameungana na wengine chini ya Yesu Kristo katika kumwabudu Yehova. Baada ya hapo, jaribu la mwisho likiisha kupita na wote wenye kuasi wakati huo wawe wameangamizwa, Yehova atawachukua wanadamu wote waliokamilishwa ambao wamekuwa washikamanifu awafanye wawe wanaye wa kulelewa kupitia Kristo. Watafanywa wawe sehemu ya jamaa ya Mungu ya ulimwengu mzima iliyoungana, na kwa wote Yehova atakuwa milele Mungu wa pekee, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Mzima na Baba yao mwenye upendo. Hilo ni taraja lenye kuchangamsha moyo kama nini! Je! wewe una tamaa yenye shauku ya kutaka kutiwa ndani ya jamaa hiyo yenye furaha ya waabudu?​—Warumi 8:20, 21.

“Ndiwe Mungu Peke Yako”

5, 6. Katika Zaburi 86, Daudi aliandika nini juu ya Yule tunayempa ibada yetu?

5 Uchunguzi wa Zaburi 86 unaweza kutusaidia tufahamu tunayohitaji kufanya ili tushiriki katika baraka hiyo. Daudi, mwandikaji wa hiyo zaburi iliyoongozwa na Mungu, alikuwa tayari amekwisha kuwa na kumbukumbu la kujitolea sana mambo ya ibada ya kweli. Lakini alitambua kwamba yeye binafsi alihitaji kuzidi kufanya maendeleo kiroho, na jambo hilo linaonyeshwa katika aliyoandika.

6 Katika mistari 8-10 anakaza fikira juu ya Yule aliyekuwa akimwabudu, kwa kusema: “Katikati ya miungu hakuna kama Wewe, [Yehova], wala matendo mfano wa matendo yako. Mataifa yote uliowafanya watakuja; watakusujudia Wewe, [Yehova], watalitukuza jina lako; kwa kuwa ndiwe uliye mkuu, wewe ndiwe mfanya miujiza, ndiwe Mungu peke yako.”

7. Kwa sababu gani ni jambo la maana sana kutambua kwamba Yehova peke yake ndiye Mungu?

7 Katika siku za Daudi, kama ilivyo leo, mataifa yalikuwa na miungu mingi. Lakini akiwa na hali ya kweli ya kuthamini Daudi alimwambia Yehova: “Ndiwe Mungu peke yako.” Yesu aliukazia ukweli uo huo. Katika usiku wa mwisho kabla ya kufa kwake alimpelekea Baba yake sala, akamtaja kuwa “Mungu wa pekee wa kweli.” (Yohana 17:3) Lakini, Jumuiya ya Wakristo inaabudu Utatu, mamilioni ya watu wanainamia sanamu mbalimbali; wengine wamefanya watu mashuhuri wawe ndio miungu yao, wakafanya fedha, wao binafsi na ngono iwe ndiyo mungu wao. Kwa hiyo, namna gani wewe? Je! wewe binafsi unaushiriki usadikishi wa kwamba ‘hakuna aliye kama Yehova,’ kwamba yeye ndiye “Mungu wa pekee wa kweli”?

8. Kama inavyoonyeshwa kwenye Zaburi 86:11, ni nini kinachotakwa kwa wote wanaotaka kuabudu Yehova?

8 Kwa kuutazama wakati ujao katika siku zake, Daudi aliona njozi ya watu wa mataifa yote wakija kutumikia Yehova. Bila shaka Daudi alitambua kwamba wakati watu hao wangekuja kuabudu Yehova, wangekuwa na mengi ya kujifunza. Ingewalazimu kufanya mabadiliko katika maisha yao. Lakini Daudi aliangalia mambo inavyofaa, akakiri kwamba hata yeye alihitaji maagizo na kwamba marekebisho zaidi yangetakwa upande wake mwenyewe. Katika Zaburi 86:11 yeye alisema: “Ee [Yehova], unifundishe njia yako; nitakwenda katika kweli yako; moyo wangu na ufurahi kulicha jina lako.” Je! hata sisi tuna tamaa ya namna hiyo?

9. Kwa sababu gani sisi ni kundi la watu walioungana, na tuna daraka gani katika jambo hilo?

9 Umoja ambao tayari upo kati ya Mashahidi wa Yehova unatokeza wazi kweli kweli, Hiyo ni kwa sababu, tukiwa kikundi kwa ujumla, sisi tunajisikia kwa moyo mweupe kama Daudi​—tunatafuta mwelekezo wa Yehova na kutenda kupatana nao. Inatupasa pia tutake kushiriki kuongezea umoja huo sisi binafsi kwa nia yetu na mwenendo wetu. Tena, tunaweza kulinda umoja wetu na kusaidia wengine waushiriki kwa kujitahidi tusitawishe ndani ya walioanza kupendezwa hivi majuzi hali ya kuthamini mambo mbali-mbali yanayotuunganisha sisi.

Mambo Yenye Nguvu za Kuunganisha

10. Ni nini jambo la kwanza kati ya yale yanayotuunganisha?

10 La kwanza ni uhakika wa kwamba sisi sote tunamwabudu Yehova na kukiri ana haki ya kuweka kiwango juu ya mema na mabaya. (Ufunuo 14:6, 7; Mwanzo 2:16, 17) Jambo hilo limekuwa na matokeo mazuri sana juu ya watu wa Yehova ulimwenguni pote! Kama Biblia inavyosema, Yehova ndiye “aliye juu, aliyetukuka, akaaye milele; ambaye jina lake ni Mtakatifu.” (Isaya 57:15) Tunapomwabudu na kujipatanisha na viwango vyake, jambo hilo linainua hali yetu. Na kwa kuwa viwango hivyo vinahusika katika sehemu zote za dunia, tumevutwa tukakaribiana pamoja tukiwa kundi la watu wenye umoja kwa sababu ya kuvifuata.

11. Tunaweza kuwasaidiaje wale walio wapya zaidi waushiriki umoja huo?

11 Lakini nyakati fulani watu mmoja mmoja ambao wamekuwa wakishirikiana nasi wanaingia katika mwenendo mbaya ulio mzito. Kwa sababu gani? Wanapoulizwa habari za uhusiano wao na Mungu, wengine wamesema, ‘Mimi sikumchukua Mungu kuwa ni mtu halisi kwa maoni yangu.’ Kwa hiyo hawakuchukua hata matakwa yake kwa uzito. Je! tunaweza kuwasaidia wale tunaojifunza nao ili kwa maoni yao Yehova awe ni mtu halisi? Inatupasa tutie mkazo waone kwamba ibada ya kweli si shauri la kukubali mafundisho fulani tu ya kidini, kwenda kwenye Jumba la Ufalme tu na labda kutumia saa chache katika utumishi wa shambani mara kwa mara. Wale wanaotaka kumtumikia Yehova wanahitaji kuwa na uhusiano wa kukaribiana kibinafsi naye. Wanapaswa kujifunza kumpelekea sala kwa ukawaida na kibinafsi, kutafuta mwelekezo wake katika kila jambo wanalotenda. (Wafilipi 4:6; Mithali 3:5, 6) Halafu wataanza kushiriki katika ule umoja wa ajabu tunaofurahia.

12, 13. (a) Jambo la pili lililoonyeshwa hapa linatuunganishaje? (b) Ili mtu afaidike kwa ukamili kutokana na jambo hilo, inampasa afanye nini?

12 Jambo la pili ni hili: Sisi tumeungana kwa sababu, hata tuwe tuko wapi katika ulimwengu, tuna Neno la Mungu, Biblia, kutuongoza. Tunaikubali Biblia kuwa imeongozwa na Mungu, na moja la mambo yaliyovuta wengi wetu kwenye Mashahidi wa Yehova ni uhakika wa kwamba Mashahidi wanafuata Biblia kweli kweli, bila kwenda kando.​—2 Timotheo 3:16, 17.

13 Huenda wale tunaojifunza nao wakakubaliana nasi wakati tunaposema kwamba Biblia ni Neno la Mungu. Lakini ni kiasi gani cha Biblia ambacho wao wamesoma? Lingekuwa jambo lenye faida kutia kila mmoja moyo aisome yote, na wanapofanya hivyo waone namna Biblia inavyopasa kuongoza maamuzi wanayofanya katika maisha ya kila siku. Yesu aliyajua mapenzi ya Baba yake vizuri sana na yakawa yamekazika sana katika akili na moyo wake kwa kiasi cha kwamba angeweza kusema, “Nafanya sikuzote yale yampendezayo.” (Yohana 8:29) Hakika huo ni mradi mzuri sana ambao sisi sote tunapaswa kuwa nao!

14. Kwa sababu gani jambo la tatu lililotajwa hapa ni la maana sana, na tunaweza kufanya nini tusitawishe hali ya kuthamini jambo hilo katika wale walio wapya zaidi?

14 Jambo la tatu linalotuunganisha ni kwamba sisi sote tunafaidika kutokana na mpango ule ule mmoja wa kulishwa kiroho. Tunamkubali “mtumwa mwaminifu mwenye akili” kuwa ndiye wakili ambaye Yehova anatumia kutoa chakula cha kiroho kwa wakati wake. (Mathayo 24:45-47) Hakuna shaka katika akili yetu kwamba “mtumwa” huyu ni warithi wa Ufalme wa kimbingu waliopakwa mafuta ambao wanapatikana leo kati ya Mashahidi wa Yehova. Sisi tunathamini yale ambayo “mtumwa” huyo na Baraza Linaloongoza lake anafanya kutimiza mahitaji yetu ya kiroho. Nasi tunamshukuru Mungu kwa wingi wa misaada mizuri ya kiroho tuliyo nayo. (Isaya 65:13, 14) Je! sisi tunatumia wakati wa kutosha kukazia hali ya kuthamini mpango huo katika watu walioanza kushirikiana na kundi hivi majuzi pia?

15, 16. (a) Sisi tunategemea nani kuwa ndiye Kiongozi wetu? (b) Kuthamini daraka la Yesu katika ibada yetu kunakuwa na matokeo gani juu ya nia tunayokuwa nayo kati ya mtu na mwenzake?

15 Jambo la nne lenye kuunganisha, ambalo ni la maana kweli kweli, ni kwamba Yesu Kristo, wala si mwanadamu ye yote, ndiye Kiongozi wetu na ndiye ambaye kupitia kwake sisi sote tunamfikia Yehova katika ibada. Wakati wa juma la mwisho la maisha yake akiwa binadamu, Yesu alikazia umaana wa jambo hilo. Kwenye Mathayo 23:8,10 yeye alisema: “Ninyi msiitwe . . . viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo.” Leo, hata mtu awe yuko wapi katika ulimwengu, akiuliza mmoja wa Mashahidi wa Yehova, ‘Kiongozi wenu ni nani?’ atapewa jibu lile lile moja: ‘Kiongozi ni Bwana Yesu Kristo.’

16 Ni kupitia Yesu tu kwamba sisi tunaweza kumfikia Yehova katika ibada yenye kukubaliwa. Kwa sababu gani? Kwa sababu sisi sote tulizaliwa katika dhambi, chini ya laana ya kifo. Hakuna wo wote kati yetu walio tofauti na wale wengine katika upande huo. Njia ya pekee ambavyo wo wote kati yetu walikubaliwa kuwa watumishi wa Mungu ilitegemea kuamini kwetu ile dhabihu ya Yesu Kristo, na ni kupitia yeye tu kwamba ye yote kati yetu anaweza sasa kumfikia Yehova katika sala. Kuthamini jambo hilo kwa moyo ni jambo la maana kabisa katika ibada ya kweli.​—Warumi 3:23; Yohana 14:6.

17. Nia yetu kuelekea Ufalme wa Mungu imetutofautishaje na Jumuiya ya Wakristo lakini ikatuvuta pamoja tukiwa Mashahidi wa Yehova?

17 Jambo la tano linalotuvuta tuwe pamoja ni kwamba hata kama tunaishi wapi, sisi tunategemea Ufalme wa Mungu kuwa ndilo tumaini la pekee kwa wanadamu. (Mathayo 6:9, 10; Danieli 2:44) Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo hawakufanya hivyo Basi, wao wanahusika katika siasa na vita vya ulimwengu. Tofauti kabisa na wao, Mashahidi wa Yehova katika nchi zote wamethamini kwa moyo uhakika wa kwamba Yesu Kristo alisema wanafunzi wake wangekuwa “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:15 16, NW) Kupatana na Neno la Mungu, sisi tumefua panga zetu zikawa majembe na mikuki yetu ikawa miundu. Hatuinui silaha za kimwili kupigana na wanadamu wenzetu, wala hatujifunzi tena vita. (Mika 4:3) Tunasadiki kwa uthabiti kwamba utatuzi wa pekee kwa matatizo ya wanadamu ni Ufalme wa Mungu. Kwa sababu hiyo, hata tuwe tunaishi wapi sisi tumeungana pamoja na Mashahidi wenzetu wa ulimwenguni pote katika udugu wa kweli wa mataifa yote.

18. Tunda la roho ya Mungu linatuunganishaje? Toa mifano.

18 Jambo la sita linalofanya tuwe na umoja ni matunda ambayo roho takatifu inatokeza katika maisha ya waabudu wa Yehova. Nayo ni matunda yenye kuvutia sana​—namna ya matunda yanayofanya tufurahi sana kuwa pamoja! Hata kama kuna pande ambazo sisi tunahitaji kufanyia maendeleo kibinafsi, iko kweli kama Yesu alivyosema: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”​—Yohana 13:35; Wagalatia 5:22, 23.

19. Sisi tunakuwa tumeungana na nani kwa kushiriki katika huduma ya Kikristo?

19 Kuongezea yote yaliyotangulia ni jambo hili la saba: Sisi sote tulio Mashahidi wa Yehova tuna daraka la kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Hilo ni daraka linalopasa kutimizwa, lakini ni pendeleo pia, Kama mtume Paulo alivyoeleza, kwa kushiriki katika huduma ya Kikristo tunaweza kuwa wenzi wafanya kazi pamoja na Mungu. Ingawa huenda mmoja wetu akapanda, na mwingine akamwagia maji, Yehova Ndiye anayefanyiza ukuzi unaotokeza wanafunzi wapya.​—Mathayo 24:14; 1 Wakorintho 3:6-9.

Kuwa Upande wa Ibada ya Kweli kwa Uthabiti

20. (a) Kwa sababu gani wengine ambao huenda wakawa wanakuja kwenye Jumba la Ufalme hawafurahii kwa ukamili baraka za ibada hiyo yenye mwungano? (b) Kwa sababu gani wanapaswa kufanya haraka wachukue msimamo wenye mwelekeo mzuri upande wa Yehova sasa?

20 Wakati wale walioanza kushirikiana nasi majuzi wanapozikubali kibinafsi kweli zinazotuvuta sisi pamoja na kutenda kupatana nazo, wao pia wanaweza kuona furaha inayotokana na kushiriki katika ibada yenye mwungano ya yule Mungu wa kweli mmoja tu. Lakini, watu wengine wanatosheka kuwa na maarifa ya kuijua kweli kijuu-juu tu. Wanajifunza habari fulani juu ya baraka zitakazoletwa na Ufalme wa Mungu, lakini hawauachi ukweli utie mizizi katika moyo wao. Wanafurahia kuwa pamoja nasi, lakini wao hawataki kusema kwamba watafanya mambo kulingana na njia ya Yehova wakati wote. Katika mambo fulani wako kama watu fulani siku za nabii Eliya, wale ambao Eliya aliwaambia hivi kwa mkazo mwingi: “Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? [Yehova] akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! mfuateni yeye.” (1 Wafalme 18:21) Wakati wa Yehova uliowekwa utakapofika wa kuangamiza mfumo mbovu wa sasa wa mambo, yeye hatakawia. Yeye hataahirisha wakati huo wala kubadili viwango vyake ili awape nafasi wale wanaojaribu bado kushikamana na ulimwengu, wale ambao wana moyo nusunusu tu juu ya kujifunza na kuyatenda mapenzi ya Mungu. Basi, ni jambo la maana sana tuwatie moyo wote wanaoonyesha kupendezwa na ukweli wachukue hatua yenye mwelekeo mzuri sasa ili wathibitishe uhusiano wa kweli na wenye kudumu pamoja na Yehova!

21. Inatupasa tusaidie wanafunzi wetu wa Biblia wafanye maendeleo gani ya kiroho?

21 Tamaa yetu si kujifunza kweli za msingi tu pamoja na wale wanaofanya maendeleo wakabatizwe, bali ni kuwasaidia wasonge mbele wakapate ukomavu wa Kikristo. Kufanya hivyo kunatia ndani kusitawisha hamu ya kutaka chakula kigumu cha kiroho. Wanahitaji kujifunza namna ya kukifurahia, kupata nguvu kutokana nacho na kufahamu namna kinavyoweza kuwasaidia wafanye maamuzi yanayofaa ya kibinafsi.​—Waebrania 5:12-14.

22. Kwa sababu gani huduma yetu ni pendeleo kubwa kweli kweli?

22 Sisi tuna pendeleo kubwa kama nini kufaidika na kutenda kupatana na mpango wa Yehova wa kuunganisha watu wa mataifa yote pamoja na yeye mwenyewe kupitia Yesu Kristo! Mungu wa kweli aliye mmoja tu ametupa sisi pendeleo zuri ajabu la kuwa mashahidi wenye kuleta utukufu kwa jina lake takatifu, Yehova. Mwana wake mwenyewe mpendwa, ambaye sasa anatawala akiwa Mfalme, alikuwa na hata sasa ndiye mfano wetu wa kufuata katika ibada inayotuwezesha tufurahie uhusiano wenye uchangamfu na wa kindani pamoja na Yehova na kuwa na umoja sisi kwa sisi. Kwa hiyo acheni tushiriki kwa ukamili katika kutukuza jina la Yehova na kusaidia wengine wafahamu namna wao pia wanaweza kufurahia baraka zinazopatikana na wale tu walioungana katika kumwabudu Mungu wa kweli mmoja tu.

Kwa Njia ya Kurudia

◻ Ni kwa kadiri gani umoja wa ibada utapatikana, na jambo hilo linaweza kukufaidi wewe namna gani?

◻ Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunakubaliana na mawazo ya kusisimuka yaliyoandikwa kwenye Zaburi 86:11?

◻ Ni nini mengine ya mambo yenye nguvu yanayotuunganisha?

◻ Baada ya wanafunzi kujifunza kweli za msingi za Biblia, inatupasa sisi tuwasaidie wafanye maendeleo gani zaidi?

[Picha katika ukurasa wa 11]

‘Wewe Yehova, ndiwe Mungu peke yako’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki