Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 8/1 kur. 14-18
  • Umoja Katika Ibada Chini ya Mfalme-Mchungaji Wetu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Umoja Katika Ibada Chini ya Mfalme-Mchungaji Wetu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Umoja Katika Ibada
  • Kumtambua Mfalme
  • “Agano la Amani” la Yehova
  • “Nitawafanya Kuwa Taifa Moja”
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
  • “Watalazimika Kujua Kwamba Mimi Ni Yehova”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Kitabu Cha Biblia Namba 28—Ezekieli
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • “Nitamweka Mchungaji Mmoja”
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 8/1 kur. 14-18

Umoja Katika Ibada Chini ya Mfalme-Mchungaji Wetu

“Bwana [Yehova] asema hivi; Tazama, nitawatwaa wana wa Israeli . . . , na mfalme mmoja atakuwa mfalme wao Wote.”​—EZEKIELI 37:21, 22.

1, 2. (a) Vile vijiti viwili vya Ezekieli 37:16 vinafananisha nini? (b) Ni nini kilichovipata “vijiti” hivyo viwili?

TUNASEMA, umoja wa Ufalme. Na jambo hilo linapatana kabisa na ile sehemu ya mwisho-mwisho ya sura ya 37 ya unabii wa Ezekieli. Hapo, katika mstari wa 16, Yehova anamwambia Ezekieli achukue vijiti viwili. Juu ya kimoja ataandika, “Kwa Yuda, na kwa wana wa Israeli wenzake.” Juu ya kile kingine lazima aandike, “Kwa Yusufu, kijiti cha Efraimu, na kwa nyumba yote ya Israeli wenzake.” Vijiti hivyo vinawakilisha nini?

2 Vinasimamia zile sehemu mbili za ufalme wa Israeli, ambao uligawanyika ukawa Yuda huko kusini na Efraimu kule kaskazini. Kila moja ya sehemu hizo ilikwenda katika hali ya kuwa mateka kwa zamu​—ufalme wa kaskazini katika mwaka wa 740 K.W.K. na ufalme wa kusini katika mwaka wa 607 K.W.K. Lakini mwaka wa 537 K.W.K. mabaki kutoka makabila yote 12 ya Israeli yalirudi Yerusalemu, yasimamishe tena huko ibada ya Yehova yenye umoja. Jambo hilo linaonyeshwaje katika unabii wa Ezekieli?

3. Kama ilivyoonyeshwa na Ezekieli 37:19, ni nini lazima kiwepo kati ya watu wa Mungu waliorudishwa?

3 Sikiliza maneno ambayo Yehova anamwambia Ezekieli, kwenye mstari wa 19:

“Waambie, Bwana [Yehova] asema hivi; Tazama, nitakitwaa kijiti cha Yusufu, kilicho mkononi mwa Efraimu, na kabila za Israeli wenzake, nami nitawaweka pamoja nacho, yaani, pamoja na kijiti cha Yuda, na kuvifanya kuwa kijiti kimoja; navyo vitakuwa kimoja mkononi mwangu.”

Aha, lazima umoja uwepo kati ya watu wa Yehova waliorudishwa!

Umoja Katika Ibada

4. Unabii wa Ezekieli 37:21 ulitimizwaje (a) mwaka 537 K.W.K.? (b) katika nyakati za kisasa?

4 Watu wa Mungu hawangekuwa wamegawanywa kuwa mataifa mawili tena, ushikamanifu wao ukiwa umegawanywa kati ya falme za kaskazini na kusini, bali kwa kweli wangekuwa “taifa moja katika nchi.” Ezekieli anawaambia maneno ya kuwafariji, kama alivyoamuru Yehova:

“Ukawaambie, Bwana [Yehova] asema hivi; Tazama, nitawatwaa wana wa Israeli toka kati ya mataifa walikokwenda, nami nitawakusanya pande zote, na kuwaleta katika nchi yao wenyewe .. . na mfalme mmoja atakuwa mfalme wao wote.” (Ezekieli 37:21, 22)

Kama ambavyo maneno hayo yalivyotimizwa kuelekea baki la Israeli lenye umoja waliporudi kutoka utumwani mwaka wa 537 K.W.K., ndivyo ambavyo baki lililorudishwa la Mashahidi wapakwa mafuta wa kisasa limepata furaha ya kuwa na umoja katika nchi yao ya kiparadiso ya fanaka ya kiroho. -Ona pia Ezekieli 36:33-36.

5. Watu wa Mungu wamesafishwaje uchafu?

5 Wakati uo huo, watu wa Mungu wamesafishwa uchafu wote wa kiroho unaosababishwa na milki ya ulimwengu ya Shetani ya dini ya uongo, “Babeli Mkuu.” (Ufunuo 17:5; 18:2, 4) Kukombolewa kwao katika mafundisho ya dini ya uongo na mazoea yake ndio utimizo mkubwa wa kisasa wa unabii uliohusu kwa njia ndogo Israeli wa kale wakati wa kurudishwa kutoka utumwani katika Babuloni wa halisi:

“Wala hawatajitia uchafu tena kwa vinyago vyao, wala kwa vitu vyao vichukizavyo, wala kwa makosa yao mojawapo; lakini nitawaokoa, na kuwatoa katika makao yao yote, ambayo wamefanya dhambi ndani yake, nami nitawatakasa; basi watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao.”​—Ezekieli 37:23.

6. (a) Kwa sababu gani Israeli wa kiroho anafurahia sasa ukaribu na Mungu wake? (b) Ni lazima tufuate umoja gani, hata ikiwa mtu fulani anaiacha kweli?

6 Ibada ya sanamu yenye kuchukiza ya dini za Jumuiya ya Wakristo na upagani imewekwa kando na watu wa Yehova waliorudishwa. Hawaabudu viumbe tena wala kufuata desturi za dini ya kilimwengu, kama vile kuadhimisha “sikukuu” zenye kumvunjia Mungu heshima. Ibada yao haijagawanywa kwa miungu mitatu katika mmoja, uitwao mungu mkuu wa Utatu ulio fumbo, bali ni wenye umoja wakiwa watu pekee wanaomwabudu Mungu mmoja, Yehova. Kwa umoja wanamsifu Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu, na hilo linawafungamanisha pamoja katika umoja usiojulikana na watu wengine wo wote duniani! (Isaya 52:8) Hata ikiwa aliyekuwa mshiriki anasitawisha dhamiri mbaya, aache jumla ya kweli zinazotolewa na Yehova, sisi tunasimama tukiwa wenye umoja pamoja na tengenezo la Mungu katika kazi yalo na katika ukaribu wenye thamani pamoja na Mungu wetu.​—Mithali 3:32; Waebrania 10:22, 23.

Kumtambua Mfalme

7. Kuongezea ibada ya kweli, ni nguvu gani nyingine yenye kuleta umoja wanayoahidiwa watu wa Mungu?

7 Wakati Israeli wa kale aliporudishwa kwenye “nchi” yake, ibada ya kweli ilikuwa nguvu yenye kuleta umoja kati yao. Lakini ufalme huo haukurudishwa. Basi, ni kwa sababu gani Yehova katika Ezekieli sura ya 37, mistari ya 22 na 24, anazungumza juu ya “mfalme” mwenye kuwatawala? Mistari 24 na 25 inasema hivi:

“Na mtumishi wangu, Daudi, atakuwa mfalme juu yao, nao wote watakuwa na mchungaji mmoja; nao wataenenda katika hukumu zangu, na kuzishika amri zangu, na kuzitenda. Nao watakaa katika nchi niliyompa Yakobo, mtumishi wangu, walimokaa baba zenu; nao watakaa humo, wao na watoto wao, na watoto wa watoto wao, milele; na Daudi, mtumishi wangu, atakuwa mkuu wao wa milele.”

8. (a) Kwa sababu gani lazima mistari hii iwe inahusu Israeli wa kiroho? (b) Tunajuaje wakati wa utimizo huo?

8 Sehemu hiyo ya unabii huo haijapata kutimizwa kamwe juu ya Israeli wa kimwili, wala haitatimizwa kamwe juu yake. Basi matumizi ya unabii huo lazima yawe yanahusu Israeli wa kiroho. Lakini wakati gani? Ni wakati gani mfalme mwenye “haki” ya kutawala alipokalia tena kiti cha kifalme cha Daudi? Hilo lilitukia yalipomalizika ‘majira ya mataifa’ katika mwaka wa kisasa wa 1914. Majira ya Mataifa yalipokwisha, ‘ufalme wa dunia ukawa ufalme wa Bwana’ Yehova ambaye “atamiliki hata milele na milele,” na pia wa “Kristo wake,” Yeye ambaye alifananishwa na Daudi.​—Ezekieli 21:26, 27; Luka 21:24; Ufunuo 11:15.

9. Ni mambo gani mawili ambayo yamekuwa yenye kuleta umoja leo?

9 Kwa hiyo leo, si kwamba tu Mashahidi wa Yehova wameunganishwa kwa umoja na ibada ya kweli​—ibada hiyo ikiwa ni ya maana sana​—bali pia sisi tumeunganishwa kwa umoja kwa kukusanywa chini ya Mfalme wetu aliye “mkuu”! Ibada yetu na Ufalme pia ni mambo yaliyo ya kweli kwetu. Na yote mawili yanatuunganisha katika udugu wetu wa ulimwenguni pote.

10. (a) Tunamwonaje Mfalme-Mchungaji wetu? (b) Tunatekelezaje ‘hukumu za Yehova’?

10 Sisi tunampenda Mfalme wetu kwa upendo mkubwa! Kwetu sote yeye ni “mchungaji mmoja”​—Mchungaji mwenye fadhili, anayetuongoza kwenye maji ya uzima wa milele. Anatujua kila mmoja wetu kwa jina na anapendezwa na kutuita atuongoze kwenye malisho ya kiroho yenye utamu mwingi. Lakini kama vile kondoo wa zizi moja, ni lazima sisi tukae tukiwa na umoja, ‘kuenenda katika hukumu za Yehova.’ Ni lazima tujiweke tofauti tusifuate sehemu tatu za tengenezo la Shetani: siasa zake zilizopotoka, biashara yake ya pupa na dini yake ya kuabudu sanamu. Kwa umoja kama ule wa Yesu na wanafunzi wake wa kwanza, tunaonyesha kwamba sisi “si sehemu ya ulimwengu” (NW). Na hiyo inatia pia, kuepuka uasherati wa ulimwenguni. (Yohana 17:14, 16, 20, 21; 18:36) Hakupasi kamwe kuwa na migawanyiko kati yetu, tunapoendelea kushika sheria za Yehova na “kuzitenda.”

11. Njia yetu ya maisha inatofautianaje na ile ya wanadini wa kilimwengu?

11 Njia hiyo ya maisha inatofautiana sana na ile ya wanadini wa kilimwengu! Kwa kawaida, mambo yote ni sawa tu kwao. Wao wanairuhusu jamii ya watu yenye kuendekeza mabaya pamoja na ufisadi wayo. Mara nyingi wanakuwa na viwango vyenye kutofautiana kuhusu sehemu mbalimbali za ulimwengu. Kwa mfano, katika nchi zenye utajiri mwingi, ni kama wanafuata mpango wa mume mmoja kuwa na mke mmoja tu; katika kizio kingine wanakubali katika ushirika watu walio na desturi ya kuwa na wake wengi sana na ambao wangali wanashikilia desturi hiyo. (Linganisha Mathayo 19:4-6; 1 Timotheo 3:2, 12.) Lakini sisi tulio na umoja chini ya Kristo, Mfalme-Mchungaji, tunafuata sheria na kanuni za Biblia katika kila sehemu ya ulimwengu. Na wakati mataifa yanapoenda vitani, sisi tunakataa kuua ndugu zetu wa taifa jingine, kwa maana katika maneno ya Isaya inasemwa hivi juu yetu: “Wala hawatajifunza vita tena kamwe.”​—Isaya 2:3, 4.

12. Sisi tunaonyeshaje tuna umoja, “kama kundi la kondoo kati ya malisho”?

12 Umoja huo wa Mashahidi wa Yehova unafananishwa vizuri pia na andiko lililo kwenye Mika 2:12, ambapo Yehova anasema: “Nitawaweka pamoja kama kondoo . . . ; kama kundi la kondoo kati ya malisho yao; watafanya mvumo kwa wingi wa watu.” Hilo ni jambo tunaloona kwenye makusanyiko ya watu wa Yehova: Maelfu wakisikiliza kwa makini, kwa unyamavu, wakiwa na hamu nyingi wasipitwe na neno lo lote tunapoendelea kulisha chini ya uchungaji wa Yehova na wa Mfalme-Mchungaji wake. Watu wa kutoka nchi za Mashariki, weusi, weupe​—mabaki wapakwa mafuta na “kondoo wengine”​—wote wako kwenye umoja katika kundi hili la kondoo. Mikusanyiko yetu, makusanyiko yetu, mikutano ya kundi yetu, inatoa ushahidi usioweza kutolewa ubishi unaoonyesha kwamba umoja wa Ufalme umeonekana kweli kweli leo!

13. Kundi limekuwaje lenye “mvumo kwa wingi wa watu”?

13 Lakini namna gani maneno ya Mika, “Watafanya mvumo kwa wingi wa watu”? Tunaona nini kabla na baada ya mikutano na makusanyiko yetu? Si kingine ila mvumo wa kelele za ushirika wenye furaha, katika mazungumzo yetu tunapokuwa tukielezana tena furaha ya ushirika wetu wa Kikristo na kusema juu ya utumishi wetu kwa Mungu. Na kundi la ulimwenguni pote linakuwa lenye “mvumo,” pia, kwa maana ya kwamba wakati wote linaongezeka; makundi mapya yanapoendelea kuundwa, wimbo wenye upatano wa kusifu Yehova unazidi kuwa na kishindo duniani pote.​—Zaburi 96:1-3.

14. Toa mfano wa jinsi ulimwengu unavyouona umoja wetu.

14 Umoja huo wenye furaha, kama ule wa kondoo katika zizi, unaonwa na ulimwengu. Kwa mfano, wakati wa “Umoja wa Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya ya 1983 ya Mashahidi wa Yehova, polisi katika Taegu, Korea, walituma maafisa 30 kwenye jumba la kusanyiko siku ya kwanza, lakini walipouona utaratibu mzuri na jinsi Mashahidi walivyokuwa wakiongoza wenye motokaa nje, waliwatuma maafisa wawili tu katika siku tatu zilizobaki. Katika Taejon, msimamizi wa jumba alisema: “Inaonekana ninyi watu mnaongozwa kwa roho kutoka mbinguni​—we! ni ajabu.” Alitia chumvi kidogo, lakini aliyotaka kusema yalieleweka! Katika Rangoon, Burma, mmoja katika baraza la Jumba la Gandhi alieleza hivi: “Kama tu ulimwengu wote ungekuwa na sosaiti kama yenu, hakungekuwako matatizo katika ulimwengu.”

“Agano la Amani” la Yehova

15. Ni amani gani yenye kutamanika inayoelezwa katika Ezekieli 37:26?

15 Amani ya kweli ina wale ambao Mfalme-Mchungaji wetu, Kristo Yesu, anawaongoza malishoni. Ni amani inayoambatana na umoja, na umoja huo hakika ni jambo la kweli ambalo limeletwa na Ufalme kati ya Mashahidi wa Yehova katika dunia yote leo. Yehova anaeleza jambo hilo vizuri sana katika maneno aliyomwambia Ezekieli kwenye sura ya 37 mstari wa 26:

“Tena nitafanya agano la amani pamoja nao; litakuwa agano la milele pamoja nao; nami nitawaweka na kuwazidisha, na patakatifu pangu nitapaweka katikati yao milele.”

Amani pamoja na Mungu! Amani inayoweza kuwa ya milele, asante kwa ile dhabihu yenye upendo ambayo Mfalme-Mchungaji wetu alitoa alipokuwa hapa duniani!

16. Ni nini kimefanya “kondoo” waongezeke?

16 Na kwa kuwa sasa Israeli wa kiroho wamezidishwa wakafikia hesabu kamili ya 144,000, mkutano mkubwa wa “kondoo wengine” wanajiunga nao katika ibada takatifu kwenye patakatifu pa Yehova. Hakuna mwisho wa kuwazidisha “kondoo”​—tayari wamekwisha kuwa mamilioni! Watangazaji hao wa Ufalme wanaenda nyumba kwa nyumba wakiwa na umoja kuzunguka ulimwengu. Ibada hiyo ya waziwazi ni halisi na ina kusudi kwetu, maana inatutambulisha sisi kuwa lile kundi moja la watu katika dunia yote ambao wanapendezwa na kutukuza jina la Yehova na katika kutangaza Ufalme wake wa amani! Sisi tuna furaha kweli kweli kushiriki katika agano lake la amani!

17. (a) Yehova anatoa kitia-moyo gani katika Ezekieli 37:27, 28? (b) Tunajuaje ulinzi wa uangalifu wa Yehova si juu ya Israeli wa kiroho peke yake?

17 Kwenye Ezekieli 37 mistari 27 na 28 tunasoma maneno ya Yehova ya kumalizia ya kulitia moyo kundi lake lenye umoja:

“Tena maskani yangu itakuwa pamoja nao; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Na mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova], mimi niwatakasaye Israeli, patakatifu pangu patakapokuwa katikati yao milele.”

Sisi tunafurahi sana kwamba ulinzi wa Yehova umetandazwa juu yetu kama hema! Wala ulinzi huo wa uangalifu wenye upendo hawapewi Israeli wa kiroho peke yao, kwa maana tunasoma kuhusu “mkutano mkubwa” kwamba “yeye aketiye katika kiti cha enzi atatanda hema yake juu yao.” Wao hawapigwi tena na joto lo lote la kuchukizwa kwa Yehova.​—Ufunuo 7:9-17.

18. (a) Yehova ‘anatakasaje Israeli’? (b) “Mkutano mkubwa” unapataje pia kuwa na msimamo wa haki mbele za Mungu?

18 Sisi ni wenye furaha, pia, kwamba Yehova anakaa katikati ya Israeli wa kiroho akiweka patakatifu pake katikati yao “milele”! Kama vile makao hayo ya ibada yake yalivyo matakatifu, ndivyo pia wale wanaokuja kuabudu hapo wanapaswa kuwa watakatifu, waliotakaswa, waliotengwa kwa ajili ya utumishi wa Mungu wao. Wakristo wapakwa mafuta wanasemwa kuwa ‘wameoshwa, wakatakaswa, wakahesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika roho ya Mungu wetu.’ (1 Wakorintho 6:11) Na kama andiko hilo lililotajwa hapo juu la Ufunuo 7:9-17 linavyoonyesha, “mkutano mkubwa” wenye matumaini ya kidunia pia “wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” ili wamtolee Mungu “ibada takatifu mchana na usiku katika hekalu lake” (NW). Ni ushuhuda mkubwa kama nini unaoletwa na utumishi huo wa umoja duniani pote!

19. (a) Mataifa yatalazimishwaje kukubali maneno ya Ezekieli 38:23? (b) Mpaka wakati huo ufike, ni lazima tuazimie kufanya nini?

19 Lakini, furaha yetu iliyo kubwa zaidi tunaposonga mbele katika umoja wa Ufalme itakuwa kuifikia ile siku ya kuondolewa malawama juu ya Yehova. Hapo ndipo jina lake tukufu litakaposafishwa kwa kuondolewa mashutumu yote maovu ambayo yamelundikwa juu yalo. Mataifa watalazimika kushuhudia kwa macho ukombozi wa watu wenye jina la Yehova. Lakini jambo la maana zaidi ni lile ambalo Bwana wetu mwenyewe Mwenye Enzi Kuu anatangaza: “Nao watajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova].” (Ezekieli 38:23) Acheni sisi tushike sana umoja wa Ufalme tulio nao, ambao sasa umeonekana, tuushike mpaka jina tukufu la Yehova litakapotakaswa kweli kweli katika ulimwengu wote!—Kutoka w3/1/84

Unabii wa Ezekieli 37:15-28 umetimizwaje kuhusiana na:

Kufanya watu wa Yehovah kuwa ”kijiti kimoja”?

Kuweka ‘mfalme na mchungaji mmoja’?

“Agano la amani” la Mungu pamoja na watu wake?

Hema la Mungu “juu yao”?

[Picha katika ukurasa wa 17]

“Agano la amani” la Yehova limefanywa pamoja na watu wake wenye umoja sasa na linatoa uhakikisho wa kuwa fanaka itaendelea mpaka kuingia Paradiso ya dunia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki