Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rr sura 12 kur. 129-136
  • “Nitawafanya Kuwa Taifa Moja”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Nitawafanya Kuwa Taifa Moja”
  • Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Vitakuwa Kijiti Kimoja Mkononi Mwangu”
  • Yehova ‘Aliwakusanyaje Pamoja’?
  • “Mtumishi Wangu Daudi Atakuwa Mfalme Wao”
  • Yehova Atafanya Waabudu Wake Wawe “Kijiti Kimoja”
  • “Watakuwa Watu Wangu”
  • “Mahali Pangu Patakatifu [Patakuwa] Kati Yao Milele”
  • “Uwalinde kwa Sababu ya Yule Mwovu”
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • “Mtakuwa Hai”
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
  • Kuunganishwa kwa Vijiti Viwili
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
  • Umoja Katika Ibada Chini ya Mfalme-Mchungaji Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
rr sura 12 kur. 129-136
Ezekieli akiwa na vijiti viwili mbele ya Wayahudi waliokuwa uhamishoni.

SURA YA 12

“Nitawafanya Kuwa Taifa Moja”

EZEKIELI 37:22

WAZO KUU: Ahadi ya Yehova ya kuwakusanya pamoja watu wake; unabii wa vijiti viwili

1, 2. (a) Kwa nini huenda wahamishwa walikuwa na wasiwasi? (b) Kwa nini wataona jambo lisilotarajiwa? (c) Tutazungumzia maswali gani?

KUPITIA mwongozo wa Mungu, Ezekieli amewatolea wahamishwa huko Babiloni unabii mwingi kwa kutumia ishara. Unabii wa kwanza ambao Ezekieli aliigiza ulikuwa na ujumbe wa hukumu, hata unabii wa pili, wa tatu, na unabii mwingine pia. (Eze. 3:24-26; 4:1-7; 5:1; 12:3-6) Kwa kweli, unabii wote ambao Ezekieli aliigiza ulikuwa na ujumbe wa hukumu kali dhidi ya Wayahudi.

2 Hebu wazia jinsi wahamishwa hao wanavyoogopa Ezekieli anaposimama tena mbele yao, tayari kuigiza unabii mwingine. Wanajiuliza, ‘Sasa tutapokea ujumbe gani unaoogopesha?’ Lakini anafanya jambo wasilotarajia. Unabii ambao Ezekieli anaanza kuigiza sasa ni tofauti kabisa. Hauhusu hukumu inayoogopesha, bali ni ujumbe wa tumaini jangavu. (Eze. 37:23) Ezekieli anawatangazia wahamishwa ujumbe gani? Unamaanisha nini? Unawahusuje watumishi wa Mungu leo? Acheni tuone.

“Vitakuwa Kijiti Kimoja Mkononi Mwangu”

Vijiti viwili vya unabii wa Ezekieli.

SANDUKU LA KUFUNDISHIA LA 12A: Kuunganishwa kwa Vijiti Viwili

3. (a) Kijiti “kwa ajili ya Yuda” kiliwakilisha nini? (b) Kwa nini “kijiti cha Efraimu” kiliwakilisha ufalme wenye makabila kumi?

3 Yehova alimwagiza Ezekieli achukue vijiti viwili na aandike juu ya kimoja “kwa ajili ya Yuda” na kingine “kwa ajili ya Yosefu, kijiti cha Efraimu.” (Soma Ezekieli 37:15, 16.) Vijiti hivyo viwili vilimaanisha nini? Kijiti ambacho kilikuwa “kwa ajili ya Yuda” kiliwakilisha ufalme wenye makabila mawili ya Yuda na Benjamini. Wafalme wa ukoo wa Yuda walitawala makabila hayo mawili; ukuhani ulihusianishwa pia na makabila hayo, kwa sababu makuhani walitumikia katika hekalu huko Yerusalemu. (2 Nya. 11:13, 14; 34:30) Hivyo, ufalme wa Yuda ulikuwa na wafalme wa ukoo wa Daudi na pia makuhani Walawi. “Kijiti cha Efraimu” kiliwakilisha ufalme wa Israeli wenye makabila kumi. Kijiti hicho kilihusianaje na Efraimu? Mfalme wa kwanza wa ufalme wenye makabila kumi alikuwa Yeroboamu, kutoka kabila la Efraimu. Baadaye, Efraimu likawa kabila kuu katika Israeli. (Kum. 33:17; 1 Fal. 11:26) Ona kwamba ufalme wa Israeli wenye makabila kumi haukuwa na wafalme wa ukoo wa Daudi wala makuhani Walawi.

4. Jambo ambalo Ezekieli anafanya akitumia vijiti viwili linamaanisha nini? (Tazama picha mwanzoni mwa sura hii.)

4 Ezekieli aliagizwa aviunganishe vijiti hivyo pamoja “ili viwe kijiti kimoja tu.” Wahamishwa walipokuwa wakimtazama Ezekieli, walimuuliza: “Je, hutatuambia mambo haya yanamaanisha nini?” Alijibu kwamba mambo aliyoigiza yalionyesha jambo ambalo Yehova angefanya. Yehova alisema hivi kuhusu vile vijiti viwili: “Nitavifanya viwe kijiti kimoja, navyo vitakuwa kijiti kimoja mkononi mwangu.”—Eze. 37:17-19.

5. Ni nini maana ya jambo ambalo Ezekieli aliigiza? (Tazama sanduku “Kuunganishwa kwa Vijiti Viwili.”)

5 Kisha, Yehova akafafanua maana ya kuunganishwa kwa vijiti viwili. (Soma Ezekieli 37:21, 22.) Wahamishwa kutoka ufalme wenye makabila mawili wa Yuda na wahamishwa kutoka ufalme wenye makabila kumi wa Israeli (Efraimu) wangerudi katika nchi ya Israeli, ambako wangekuwa “taifa moja.”—Yer. 30:1-3; 31:2-9; 33:7.

6. Ni unabii gani unaopatana ulio katika Ezekieli sura ya 37?

6 Ezekieli sura ya 37 ina unabii kuhusu kurudishwa ambao ni wenye upatano! Yehova atathibitika kuwa Mungu anayerudisha uhai (mstari wa 1-14) na pia umoja (mstari wa 15-28). Ujumbe unaogusa moyo ulio katika unabii huo ni huu: Mtu aliyekufa anaweza kufufuliwa, na pia mgawanyiko unaweza kwisha.

Yehova ‘Aliwakusanyaje Pamoja’?

7. Simulizi lililo kwenye 1 Mambo ya Nyakati 9:2, 3 linathibitishaje kwamba “kwa Mungu mambo yote yanawezekana”?

7 Kwa maoni ya wanadamu, kukombolewa na kuunganishwa kwa wahamishwa kulionekana kuwa jambo lisilowezekana kabisa.a Hata hivyo, “kwa Mungu mambo yote yanawezekana.” (Mt. 19:26) Yehova alitimiza unabii aliotoa. Utekwa wa Babiloni ulikwisha mwaka wa 537 K.W.K., kisha, watu kutoka falme zote mbili wakafika Yerusalemu ili kurudisha ibada safi. Maandiko yaliyoongozwa na roho yanathibitisha jambo hilo: “Baadhi ya wazao wa Yuda, wa Benjamini, wa Efraimu, na wa Manase [waliishi] Yerusalemu.” (1 Nya. 9:2, 3; Ezra 6:17) Kwa kweli, kama Yehova alivyotabiri, watu kutoka ufalme wenye makabila kumi ya Israeli waliungana na watu kutoka ufalme wa Yuda wenye makabila mawili.

8. (a) Isaya alitabiri kuhusu nini? (b) Ni mambo gani mawili muhimu yanayopatikana katika Ezekieli 37:21?

8 Miaka 200 hivi mapema, nabii Isaya alitabiri kuhusu jambo ambalo lingewapata Israeli na Yuda baada ya utekwa. Alitabiri kwamba Yehova angeanza kukusanya pamoja “watu wa Israeli waliotawanywa” nao “watu wa Yuda waliotawanywa [angewakusanya] pamoja kutoka katika pembe nne za dunia,” hata “kutoka Ashuru.” (Isa. 11:12, 13, 16) Na kwa kweli, kama Yehova alivyotabiri, aliwachukua “Waisraeli kutoka katika mataifa.” (Eze. 37:21) Ona mambo mawili muhimu: Kufikia hapa, Yehova hawaiti tena wahamishwa hao “Yuda” na “Efraimu” bali “Waisraeli”—kundi moja. Isitoshe, Waisraeli walifafanuliwa kuwa wanatoka, si katika taifa moja, Babiloni, bali kutoka kwa mataifa mbalimbali, yaani, “kutoka kila upande.”

9. Yehova aliwasaidiaje wahamishwa waliorudi wawe na umoja?

9 Baada ya wahamishwa kurudi Israeli, Yehova aliwasaidiaje kuungana? Aliwapatia Waisraeli wachungaji wa kiroho, kama vile Zerubabeli, Kuhani Mkuu Yoshua, Ezra, na Nehemia. Mungu pia aliwaweka manabii Hagai, Zekaria, na Malaki. Wanaume hao wote waaminifu walijitahidi kulitia moyo taifa hilo lifuate maagizo ya Mungu. (Neh. 8:2, 3) Isitoshe, Yehova alililinda taifa la Israeli kwa kuharibu njama zilizopangwa na maadui wa watu wa Mungu.—Esta 9:24, 25; Zek. 4:6.

Ezra na wanaume wengine wakiwafundisha watu sheria za Yehova.

Yehova aliweka wachungaji wa kiroho ili kuwasaidia watu wake wawe na umoja (Tazama fungu la 9)

10. Hatimaye Shetani alifaulu kufanya nini?

10 Hata hivyo, licha ya maandalizi yote yenye upendo ya Yehova, Waisraeli wengi hawakushikamana na ibada safi. Matendo yao yaliandikwa katika vitabu vya Biblia vilivyoandikwa baada ya wahamishwa kurudi. (Ezra 9:1-3; Neh. 13:1, 2, 15) Kwa kweli, karne moja baada ya kurudi, Waisraeli walikuwa wameacha kabisa ibada safi hivi kwamba Yehova aliwahimiza hivi: “Nirudieni.” (Mal. 3:7) Yesu alipokuja duniani, dini ya Wayahudi ilikuwa imegawanyika katika madhehebu mbalimbali ambayo yaliongozwa na wachungaji wasio waaminifu. (Mt. 16:6; Marko 7:5-8) Shetani alikuwa amefaulu kuzuia jitihada za kuleta umoja kamili. Hata hivyo, bado unabii wa Yehova kuhusu kuunganishwa, ungetimia. Jinsi gani?

“Mtumishi Wangu Daudi Atakuwa Mfalme Wao”

11. (a) Yehova alifunua nini kuhusu unabii wake wa kuunganishwa? (b) Shetani alijaribu kufanya nini tena baada ya kufukuzwa mbinguni?

11 Soma Ezekieli 37:24. Yehova alifunua kwamba unabii wake kuhusu kuunganishwa ungetimizwa kikamili kuhusiana na watu wake baada ya ‘mtumishi wake Daudi,’ yaani, Yesu kuwa Mfalme, jambo lililotokea mwaka wa 1914.b (2 Sam. 7:16; Luka 1:32) Wakati huo, nafasi ya Israeli wa asili ilikuwa imechukuliwa na Israeli wa kiroho, watiwa mafuta. (Yer. 31:33; Gal. 3:29) Baada ya Shetani kutupwa kutoka mbinguni, alianza tena kuvuruga umoja wa watu wa Mungu. (Ufu. 12:7-10) Kwa mfano, baada ya Ndugu Russell kufa mwaka wa 1916, Shetani alitumia waasi imani kuleta mgawanyiko kati ya watiwa mafuta. Hata hivyo, baada ya muda waasi imani hao walijitenga na tengenezo. Shetani pia alifaulu kufanya ndugu waliokuwa wakiongoza wakati huo wafungwe gerezani, lakini hata hilo halikuwaangamiza watu wa Yehova. Ndugu watiwa mafuta walioendelea kuwa waaminifu kwa Yehova walidumisha umoja wao.

12. Kwa nini jitihada za Shetani za kuharibu umoja wa Israeli wa kiroho hazijafaulu?

12 Kwa hiyo, kinyume na jambo lililopata Israeli wa asili, Israeli wa kiroho walishinda mbinu za Shetani za kuleta mgawanyiko. Kwa nini jitihada za Shetani hazijafaulu? Kwa sababu watiwa mafuta wamejitahidi kabisa kufuata viwango vya Yehova. Matokeo ni kwamba Mfalme wao, Yesu Kristo, amekuwa akiwalinda, anapoendelea kumshinda Shetani.—Ufu. 6:2.

Yehova Atafanya Waabudu Wake Wawe “Kijiti Kimoja”

13. Tunajifunza ukweli gani muhimu kutokana na unabii wa kuunganishwa kwa vijiti viwili?

13 Unabii kuhusu kuunganishwa kwa vijiti viwili una maana gani katika nyakati zetu? Kumbuka kwamba kusudi la unabii huo ni kufafanua jinsi ambavyo vikundi viwili vingeunganishwa. Zaidi ya yote, unabii huo unakazia kwamba umoja huo unaletwa na Yehova. Basi, unabii huo wa kuunganishwa kwa vijiti viwili unakazia kweli gani muhimu kuhusu ibada safi? Kwa ufupi: Yehova mwenyewe atafanya watu wake wawe “kijiti kimoja.”—Eze. 37:19.

14. Unabii wa kuunganishwa kwa vijiti umetimizwaje kwa njia kubwa zaidi tangu 1919?

14 Unabii wa kuunganishwa kwa vijiti viwili ulianza kutimizwa kwa njia kubwa zaidi tangu mwaka wa 1919, baada ya watu wa Mungu kusafishwa kiroho na kuanza kuingia katika paradiso ya kiroho. Wakati huo, wengi kati ya wale waliounganishwa walikuwa na tumaini la kuwa wafalme na makuhani mbinguni. (Ufu. 20:6) Kwa njia ya mfano, watiwa mafuta hao walikuwa kama kijiti “kwa ajili ya Yuda”—taifa lililokuwa na wafalme wa ukoo wa Daudi na makuhani Walawi. Hata hivyo, kadiri muda ulivyopita, watu wengi zaidi walio na tumaini la kuishi duniani walijiunga na Wayahudi hao wa kiroho. Watu hao walikuwa kama “kijiti cha Efraimu”—taifa ambalo halikuwa na wafalme wa ukoo wa Daudi na makuhani Walawi. Vikundi hivyo viwili vinatumikia kwa umoja kama watu wa Yehova chini ya Mfalme mmoja, Yesu Kristo.—Eze. 37:24.

“Watakuwa Watu Wangu”

15. Unabii wa Ezekieli 37:26, 27 unatimizwaje leo?

15 Unabii wa Ezekieli unaonyesha kwamba watu wengi wangechochewa kujiunga na watiwa mafuta katika ibada safi. Yehova alisema hivi kuhusu watu wake: “Nitafanya . . . wawe wengi” na “hema langu litakuwa juu yao.” (Eze. 37:26, 27; maelezo ya chini.) Maneno hayo yanatukumbusha unabii ambao mtume Yohana alipokea miaka 700 hivi baada ya wakati wa Ezekieli, kwamba “Yule anayeketi kwenye kiti cha ufalme atatandaza hema lake” juu ya “umati mkubwa.” (Ufu. 7:9, 15) Leo, watiwa mafuta na umati mkubwa wanakaa wakiwa taifa moja, watu wa Mungu, chini ya ulinzi wa hema lake.

16. Zekaria alitoa unabii gani kuhusu kuunganishwa kwa Israeli wa kiroho pamoja na watu walio na tumaini la kuishi duniani?

16 Kuunganishwa kwa Wayahudi wa kiroho na watu walio na tumaini la kuishi duniani kulitabiriwa pia na Zekaria, mmoja wa wahamishwa waliorudi. Alisema kwamba ‘watu kumi kutoka katika mataifa wangeshika kwa nguvu joho la Myahudi’ na kusema: “Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yupo pamoja nanyi.” (Zek 8:23) Neno “Myahudi” halimaanishi mtu mmoja, bali ni kikundi cha watu, kama inavyoonyeshwa na maneno “pamoja nanyi.” Leo wanawakilishwa na watiwa mafuta waliobaki au Wayahudi wa kiroho. (Rom. 2:28, 29) “Watu kumi” wanawakilisha wale walio na tumaini la kuishi duniani. ‘Wanawashika kwa nguvu’ watiwa mafuta na kwenda “pamoja” nao. (Isa. 2:2, 3; Mt. 25:40) Maneno ‘kushika kwa nguvu’ na “kwenda pamoja nanyi” yanaonyesha kuunganishwa kikamili kwa vikundi hivi viwili.

17. Yesu alifafanuaje umoja tunaofurahia leo?

17 Huenda Yesu alikuwa akifikiria unabii wa Ezekieli wa kuunganishwa alipojifafanua kuwa mchungaji ambaye chini ya mwongozo wake kondoo (watiwa mafuta) na “kondoo wengine” (wale walio na tumaini la kuishi duniani) wangekuwa “kundi moja.” (Yoh. 10:16; Eze. 34:23; 37:24, 25) Maneno hayo ya Yesu na yale ya manabii wa zamani yanafafanua vizuri umoja wa kiroho tunaofurahia leo, bila kuzingatia tumaini tulilo nalo la wakati ujao! Ingawa dini za uwongo zimegawanyika katika vikundi vingi sana, tunafurahia muujiza wa kuwa na umoja.

Kutaniko la watu wa Mungu, kutia ndani ndugu mtiwa mafuta, wanasikiliza wakati msichana mdogo akitoa maelezo katika mkutano.

Leo, watiwa mafuta na “kondoo wengine” wanamwabudu Yehova kwa umoja wakiwa “kundi moja” (Tazama fungu la 17)

“Mahali Pangu Patakatifu [Patakuwa] Kati Yao Milele”

18. Kama inavyoonyeshwa katika Ezekieli 37:28, kwa nini ni muhimu kwa watu wa Mungu kutokuwa “sehemu ya ulimwengu”?

18 Maneno ya mwisho ya unabii wa Ezekieli kuhusu kuunganishwa yanakazia jambo linalohakikisha kwamba umoja wetu hautavunjwa kamwe. (Soma Ezekieli 37:28.) Watu wa Yehova wameungana kwa sababu mahali pake patakatifu, au ibada safi, iko “kati yao.” Na mahali pake patakatifu pataendelea kuwa kati yao ikiwa wataendelea kujitakasa, na kujitenga na ulimwengu wa Shetani. (1 Kor. 6:11; Ufu. 7:14) Yesu alikazia umuhimu wa kujitenga na ulimwengu. Katika sala inayotoka moyoni kwa ajili ya wanafunzi wake, alisema: “Baba Mtakatifu, walinde . . . ili wawe kitu kimoja . . . Wao si sehemu ya ulimwengu . . . Watakase kupitia ile kweli.” (Yoh 17:11, 16, 17) Ona jinsi Yesu alivyohusianisha kuwa “kitu kimoja” na kutokuwa “sehemu ya ulimwengu.”

19. (a) Tunathibitishaje kwamba sisi ni “waigaji wa Mungu”? (b) Katika jioni ya mwisho kabla ya kifo chake, Yesu alikazia ukweli gani muhimu kuhusu umoja?

19 Ni katika andiko hilo tu ambapo Yesu alimwita Mungu “Baba Mtakatifu.” Yehova ni mtakatifu na mnyoofu kabisa. Yehova aliwaamuru hivi Waisraeli wa kale: “Lazima muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.” (Law. 11:45) Tukiwa “waigaji wa Mungu,” tungependa kutii amri hiyo katika mwenendo wetu wote. (Efe. 5:1; 1 Pet. 1:14, 15) Inapohusu wanadamu, neno “takatifu” linamaanisha “kuwekwa kando.” Kwa hiyo, jioni ya mwisho kabla ya kifo chake, Yesu alikazia kwamba wanafunzi wake wangedumisha umoja ikiwa wangeendelea kujitenga na ulimwengu huu wenye migawanyiko.

“Uwalinde kwa Sababu ya Yule Mwovu”

20, 21. (a) Ni nini kinachofanya tutegemee zaidi ulinzi wa Yehova? (b) Umeazimia kufanya nini?

20 Umoja wa kipekee unaoonekana wazi kati ya Mashahidi wa Yehova leo ulimwenguni pote unathibitisha kwamba Yehova alijibu ombi hili la Yesu: “Uwalinde kwa sababu ya yule mwovu.” (Soma Yohana 17:14, 15.) Kwa kweli, tunategemea zaidi ulinzi wa Yehova tunapoona jinsi ambavyo Shetani ameshindwa kuharibu umoja wa watu wa Mungu. Katika unabii wa Ezekieli, Yehova alisema kwamba vijiti viwili vingekuwa kijiti kimoja mkononi mwake. Basi, Yehova amewaunganisha kimuujiza watu wake chini ya ulinzi wa mkono wake—ambapo Shetani hawezi kuwafikia.

21 Basi, tunapaswa kuazimia kufanya nini? Kuendelea kujitahidi kutimiza jukumu letu la kuchangia umoja wenye thamani tunaofurahia sasa. Ni kwa njia gani muhimu kila mmoja wetu anaweza kufanya hivyo? Kwa kushiriki kwa ukawaida kwenye ibada safi katika hekalu la Yehova la kiroho. Mambo yanayohusika katika ibada hiyo yatazungumziwa katika sura zinazofuata.

a Karne mbili hivi kabla Ezekieli hajapokea unabii huu, wakaaji wa ufalme wenye makabila kumi (“kijiti cha Efraimu”) walipelekwa uhamishoni na Waashuru.—2 Fal. 17:23.

b Unabii huu unazungumziwa kwa undani katika Sura ya 8 ya kitabu hiki.

SEHEMU YAKO KATIKA IBADA SAFI

  1. Unabii wa vijiti viwili unakazia ukweli gani muhimu kuhusu ibada safi? (Eze. 37:19)

  2. Kwa nini tunasema kwamba unabii huo kuhusu kuunganishwa ungetimizwa kwa njia kubwa zaidi baada ya 1914? (Eze. 37:24)

  3. Wewe binafsi unaweza kufanya nini ili kuchangia umoja wenye thamani tunaofurahia leo? (1 Pet. 1:14, 15)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki