1914 ni Mwaka Uliotiwa Alama—Kwa Sababu Gani?
WEWE ulikuwa wapi katika mwaka wa 1914? Je! wewe ungejibu: ‘Sikuwa nimezaliwa’? Lakini watu milioni chache leo wangali wanaweza kukumbuka mwaka huo wa 1914.
Katika mwaka wa 1914 Maria alikuwa akimaliza mwaka wake wa mwisho katika shule ya sekondari, akiwa anajifunza Kijeremani na kutazamia kazi yenye kuthawabisha maishani akiwa mwalimu wa shule. Wakati wa kiangazi hicho, kabla hajaenda tena chuoni, alikuwa nje kwenye makonde ya shamba la babaye upande wa kaskazini-mashariki mwa pwani ya United States. Alikuwa akiwaondoa wadudu kwenye nyanya zilizokuwa zikiiva, wakati katika umbali wa nusu ya ulimwengu, katika Sarajevo, risasi ya mwuaji ilikatisha uhai wa mkuu mmoja wa Austria. Hilo likaanzisha mlipuko mkubwa wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Habari za vita hiyo zilipomfikia Maria, yeye alidhani hivi: ‘Yametimia! Waliyokuwa wakisema Wanafunzi wa Biblia yametimia barabara; 1914 utakuwa mwaka uliotiwa alama!’
Si Maria peke yake aliyeyaona matukio ya ulimwengu kwa njia hiyo. Katika Agosti 30, 1914, kichwa kikubwa chenye kuvuta fikira “Mwisho wa Falme Zote katika 1914” kiling’aa kwenye ukurasa wa 4 wa kisehemu cha gazeti cha Jumapili cha The World, gazeti mashuhuri la New York. “Kuanza kwa vita vibaya sana katika Ulaya kumetimiza unabii usio wa kawaida,” ikasema makala hiyo kuu. “Kwa robo karne iliyopita, kupitia wahubiri na kupitia vichapo, ‘Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote [Mashahidi wa Yehova],’ ambao wanajulikana zaidi kuwa ‘Millenial Dawners,’ wamekuwa wakitangazia ulimwengu kwamba Siku ya Ghadhabu iliyotabiriwa katika Biblia ingefika mwaka 1914. ‘Jihadharini na 1914!’ kimekuwa ndicho kilio cha mamia ya waevanjeli wenye kusafiri ambao, wakiwakilisha imani hii ya ajabu, wameizunguka nchi yote wakieleza waziwazi fundisho la kwamba ‘Ufalme wa Mungu umekaribia.’ “
Uwe ulikuwa hai katika mwaka huo au la, 1914 wapasa kumaanisha zaidi kwako kuliko tu kuwa karatasi ya kalenda iliyojiviringa na kuchakaa au kuwa kichwa kikubwa tu kwenye ukurasa wa gazeti lililokunjamana. Huo ni mwaka wenye maana unaohusu uhai wako leo.
Sababu Gani Mwaka 1914 ni Mwaka Uliotiwa Alama?
Mashahidi wa Yehova walijuaje miaka zaidi ya 30 kimbele kwamba 1914 ingekuwa tarehe ya maana kwa utawala wa kimungu? Ingawa wakati huo Mashahidi hawakuelewa maana kamili ya matukio ambayo yalikaribia kutokea, gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la kule-e-e nyuma katika Desemba 1879 lilitaja mwaka 1914 kuwa tarehe tofauti kuhusiana na unabii wa Biblia. Na toleo la Machi 1880 la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) lilikamatanisha utawala wa Ufalme wa Mungu na kumalizika kwa ambacho Yesu alitaja kuwa “nyakati zilizowekwa za mataifa,” au “nyakati za Mataifa.” (Luka 21:24, NW; Authorized Version) Gazeti hilo la Mnara wa Mlinzi lilisema: “‘Nyakati za Mataifa’ zinamalizika mwaka 1914, na ufalme wa kimbingu hautatawala mpaka wakati huo.”
Ni nini maana ya usemi ‘Nyakati za Mataifa,’ au “nyakati zilizowekwa za mataifa”? Na zinakamatanaje na Ufalme wa Mungu? Ili kujibu maulizo hayo, ebu tuyaangalie kindani maneno ya Yesu. Yeye alisema: “Yerusalemu utakanyagwa na mataifa, mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa zitakapotimizwa.”—Luka 21:24, NW.
“Yerusalemu” unamaanisha nini? Ni Ufalme wa Mungu. Twajuaje? Israeli wa kale walikuwa watu wateule wa Mungu tangu mwaka 1513 K.W.K. mpaka karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu. (Kutoka 19:6; Mathayo 23:37, 38) Yehova aliwafanya tengenezo chini ya serikali halisi ya kitheokrasi, au utawala wa Mungu. Yerusalemu ukawa mji mkuu. Ni huko nasaba ya wafalme waliopakwa mafuta na kutokana na Daudi waliketi juu ya ‘kiti cha enzi cha Yehova.’ Walitawala wakiwa wafalme kwa ajili ya Yehova. (1 Mambo ya Nyakati 29:23; 2 Mambo ya Nyakati 9:8) Kitabu Cyclopaedia kilichoandikwa na M’Clintock na Strong kinasema: “Yerusalemu ulikuwa umefanywa kuwa makao ya utawala ya mfalme wa Israeli yote; na Hekalu, ambalo mara nyingi liliitwa ‘nyumba ya Yehova,’ wakati uo huo liliwakilisha makao ya Mfalme wa wafalme, kiongozi mkuu kupita wote wa taifa hilo la kitheokrasi.”
Ni wakati gani na ni jinsi gani Yerusalemu ulikanyagwa na Mataifa? Kukanyagwa huko kulianza mwaka 607 K.W.K. Jinsi gani? Kwa mwisho wa ghafula wa mfuatano wa watawala wa Kidaudi. Mfalme Sedekia alinyang’anywa kiti cha ufalme chake na mji wa Yerusalemu ukaharibiwa na majeshi ya Wababuloni wenye kuvamia wakiwa chini ya Nebukadreza. Biblia katika Ezekieli 21:26,27 ilitabiri mkatisho huo katika mfuatano wa wafalme wa Kidaudi kwa kusema: “Ivue taji [kofia ya kifalme, NW] . . . hiki nacho hakitakuwa tena, hata atakapokuja yeye ambaye ni haki yake; nami nitampa.” Utawala wa Mungu ungezuiwa mpaka “nyakati zilizowekwa za mataifa” zifikie mwisho. Kwa hiyo, Nyakati za Mataifa zilikuwa kipindi ambacho mataifa yalitawala pasipo Yehova Mungu kuwa na serikali ya kuwakilisha utawala wake duniani.
Nyakati za mataifa zilipofikia mwisho, Yehova angempa Yule “ambaye ni haki yake,” Yesu Kristo uwezo wa kutawala. Kwa hiyo, mwaka 1914 ungekuwa wakati ambao Kristo alianza kutawala akiwa Mfalme katika Ufalme wa kimbingu wa Mungu, na kwa kuwa utawala wake unaendelea mpaka siku hii, wewe unahusika.
Tarehe za Biblia ziliangaliwaje kuonyesha mwaka wa 1914 umetiwa alama? Toleo la Juni 1880 la gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) linaeleza: “Kipindi kirefu cha miaka 2520 na matukio machungu chini ya utawala wa wale wanyama, (serikali za kibinadamu, Dan. 7.) kinafananishwa waziwazi katika Dan. 4 na zile ‘nyakati saba’ za Nebukadreza na matukio machungu yaliyompata kati ya wanyama.” Basi ni lazima turudi kwenye ndoto ile yenye kusumbua ya mfalme Mbabuloni ili tuone mfuatano wayo wa tarehe mpaka mwaka 1914.
Ramani ya Kiunabii
Yehova, kupitia manabii wake, sikuzote amewapa watu wake ramani ya kiunabii ya kufuata. “Hakika Bwana [Yehova] hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake,” ndivyo linavyosema andiko la Amosi 3:7. Kwa mfano, Nuhu alikuwa mjumbe wa pekee wa Mungu miaka zaidi ya 4,000 iliyopita. Yehova alimpa Nuhu onyo la kiunabii la uharibifu wa maji ambao ungekuja juu ya ulimwengu huo mbovu. (Mwanzo 6:3; 7:4) Kilichotokea wakati huo kilikuwa pia kielelezo cha uharibifu wa wakati ujao wa wasiomcha Mungu wakati wa “kuwapo kwa Mwana wa mtu” Yesu Kristo, kusikoonekana. (Mathayo 24:37-39, NW) Kwa hiyo halipasi kuonekana kuwa jambo geni kwamba mambo ambayo Danieli alionyesha kuhusu utawala wa ulimwengu wa Nebukadreza—kuanguka kwake na kurudi kwake kwenye uwezo—yalikuwa pia mfano wa kadiri ndogo wa mabadiliko katika utawala wa ulimwengu wa kitheokrasi kupitia Mfalme mpakwa mafuta wa Mungu.
Tunaona nini tunapochunguza kielelezo cha kiunabii cha Danieli 4:10-17? Mti mkubwa sana wenye kufika mbinguni unawakilisha utawala wa kimungu. Mti huo ulikatwa wakati Ufalme wa Mungu wa Yuda pamoja na mji mkuu wake katika Yerusalemu ulianguka mwaka 607 K.W.K. Baada ya “nyakati saba” za utawala wa kinyama wa mataifa kumalizika, pingu mbili za chuma zenye kuzuia ziliondolewa, na utawala wa kimungu ukarudishwa wakati Yesu Kristo alipoanza kutawala akiwa Mfalme katika serikali ya kimbingu ya Mungu mwaka wa 1914.
Kila Siku Kuhesabiwa Mwaka
Tunajuaje kwamba zile “nyakati saba” ni miaka 2,520? Hesabu inafanywa katika njia inayofanana na ile iliyotumiwa na msimamizi wa kwanza wa Sosaiti, C. T. Russell, mwaka wa 1877 na kuandikwa katika kitabu ambacho alitunga pamoja na mwingine chenye kichwa The Three Worlds. Hesabu hiyo inafanywa hivi: Katika Ufunuo sura ya 12, mistari 6 na 14, tunajifunza kwamba siku 1,260 zinalingana na “wakati [yaani, wakati 1] na nyakati [yaani, nyakati 2] na nusu ya wakati,” au jumla ya nyakati 3 1/2. Kwa hiyo “wakati” ungelingana na siku 360. “Nyakati saba” zingekuwa ni 360 kuzidishwa na 7, au siku 2,520. Halafu tukihesabu kila siku moja kuwa mwaka mmoja, kulingana na kanuni ya Biblia, zile “nyakati saba” zinalingana na miaka 2,520. (Hesabu 14:34; Ezekieli 4:6) Basi, kipindi cha “nyakati saba,” Nyakati za Mataifa, ni kuanza 607 K.W.K. mpaka 1914 W.K.
Kuna sababu gani za kusadiki kwamba mti wa ndoto ya kiunabii ya Nebukadreza unafika mpaka katika karne yetu ya 20 na kutimizwa katika Ufalme wa Mungu? Sababu moja ni hii: Sehemu kubwa ya kitabu cha Danieli inahusu unabii mbalimbali unaotimizwa katika utawala wa ulimwengu na Ufalme wa Mungu baada ya wakati wa kuishi kwa Danieli. Kwa mfano, soma, Danieli sura ya 2. Inaonyesha sanamu yenye vyuma vingi mbalimbali inayofananisha mamlaka za ulimwengu zenye kufuatana ambazo zinasagwa-sagwa. Zinasagwa-sagwa na nini? Na Ufalme wa Mungu! (Danieli 2:44) Au soma Danieli sura ya 7 ambapo mfulizo wa serikali za ulimwengu unaonekana kama wanyama-mwitu wanaotoka baharini na mwishowe zikiondolewa na mahali pake kuchukuliwa na utawala mmoja. Utawala gani? Ufalme wa Mungu! (Danieli 7:14) Au soma Danieli sura za 11 na 12. Katika sura hizo mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wanajaribiana katika pigano la ni nani atakuwa mkuu zaidi ulimwenguni mpaka wanaposhindwa mkononi mwa Mwana-Mfalme Mikaeli. (Danieli 12:1) Mikaeli huyo ni nani? Yesu Kristo, mtawala katika Ufalme wa Mungu!
Kwa hiyo mwaka wa 1914 ulitiwa alama kwa kusudi zuri sana. Ulikuwa ishara ya mwanzo wa utawala wa uadilifu kuelekea dunia kupitia Ufalme wa Mungu. Ulionyesha ishara ya maangamizi kwa waovu. Ulitoa ishara ya “siku za mwisho” za huu mfumo wa mambo usiomcha Mungu. (2 Timotheo 3:1) Ulionyesha ishara ya dakika za mwisho za mwanzo wa dunia-Paradiso.
Kuna sababu nyingine kwa nini mwaka wa 1914 ni mwaka uliotiwa alama ambao unakuhusu wewe. Sababu hizo zitachunguzwa katika makala zitakazokuja za Mnara wa Mlinzi.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Gazeti Mnara wa Mlinzi, la kule-e-e nyuma Desemba 1879, lilitaja mwaka 1914 kuwa ni tarehe iliyotiwa alama
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Utawala wa Mungu ulikuwa umezuiwa mpaka Nyakati za Mataifa zilipofikia mwisho
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Nyakati za Mataifa zilipokwisha, Yehova alimpa Yesu Kristo uwezo wa kutawala
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Mwaka 1914 ulikuwa ishara ya wakati ambao Kristo alianza kutawala akiwa Mfalme katika serikali ya kimbingu ya Mungu
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
Unabii mwingine, unaopatikana katika sura ya tisa ya Danieli unakaza fikira juu ya kufika kwa kibinadamu kwa Masihi—Mfalme wa wakati ujao wa Ufalme wa Mungu—hata unataja mwaka wenyewe wa kuonekana kwake! Kipindi cha “majuma sabini” kinahusika. (Danieli 9:24-27) Kwa ujumla inatambuliwa na wenye kujifunza Biblia kwamba kila siku ya majuma hayo ya kiunabii inalingana na mwaka mmoja. Kwa kuwa mmoja wa unabii wa Danieli ulitabiri kwa usahihi kufika kusikoonekana kwa Masihi, au Kristo, katika Ufalme wa kimbingu wa Mungu.
[Chati/Picture katika ukurasa wa 8]
MAANA YA NDOTO YA MFALME HUYO KWAKO WEWE
Mti Utawala wa Kimungu
Mti Uliokatwa na Mwaka wa 607 K.W.K Kufungwa Kwa Pingu utawala wa Mungu kupitia wafalme wa Kibinadamu wamalizika
Nyakati Saba za Mataifa Miaka 2,520 ya Utawala wa serikali
za kinyama
Pingu Zaondolewa Mwaka 1914 W.K., Utawala wa
Mungu Kupitia Mfalme wa Kimbingu, Kristo Yesu, Waanza
[Picha katika ukurasa wa 5]
Katika toleo lake la Agosti 30, 1914, gazeti la New York The World lilivuta fikira kwenye uhakika wenye kutokeza kwamba Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote (Mashahidi wa Yehova) walikuwa wametaja mwaka 1914 kuwa tarehe iliyotiwa alama katika unabii wa Biblia