Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 11/1 kur. 4-7
  • Ndoto Inafunua Kwamba Wakati Umesonga Sana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ndoto Inafunua Kwamba Wakati Umesonga Sana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jambo Hilo Lina Maana Gani Kwetu Sisi?
  • Zile “Nyakati Saba”​—Toka Wakati Gani Mpaka Wakati Gani?
  • Wakati Umesonga Sana Kadiri Gani?
  • Mfalme Atawala!
    “Ufalme Wako Uje”
  • Kufumbua Fumbo la Ule Mti Mkubwa
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
  • Mfuatano wa Matukio Katika Biblia Unaonyesha Nini Kuhusu Mwaka wa 1914?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • 1914 ni Mwaka Uliotiwa Alama—Kwa Sababu Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 11/1 kur. 4-7

Ndoto Inafunua Kwamba Wakati Umesonga Sana

“[YEHOVA] ndiye . . . Mungu aliye hai, Mfalme wa milele.” (Yeremia 10:10) Hakuna wakati ambao yeye ameacha uongozi wa ulimwengu wake wote. Hilo ni jambo ambalo Mfalme Nebukadreza wa Babuloni wa kale alishindwa kutambua. Ili kumkazia mfalme huyo mpagani kwamba “Aliye juu anatawala katika ufalme wa wanadamu,” Mungu alimfanya aote ndoto na kuwezesha Danieli mtumishi Wake afasiri maana yayo.​—Danieli 4:17, 18.

Ndoto hiyo ilihusu mti mkubwa sana. “Urefu wake ulifika [mwishowe] mpaka mbinguni, na kuonekana kwake mpaka mwisho wa dunia.” Kwa amri ya Mungu, mti huo ulikatwa, lakini kisiki kikafungwa kwa pingu za chuma na shaba. Zilipasa kukaa hivyo mpaka “nyakati saba” zipite juu ya kisiki hicho, halafu mti huo ungeweza kukua tena.​—Danieli 4:10-17.

“Ule mti uliouona,” Danieli akaeleza, “ni wewe, Ee mfalme . . . na mamlaka yako.” Nebukadreza angekatwa aangushwe. Angepoteza ufalme wake, ndiyo, hata utimamu wa akili yake, akiwa amehukumiwa adhabu ya kutanga-tanga makondeni kama mnyama-witu kwa muda wa “nyakati saba.” Ni baada tu ya kile kipindi kilichowekwa kumalizika ndipo zile pingu za mfano zingeondolewa, na hapo mfalme aruhusiwe kurudiwa na utimamu wake wa akili na kiti chake cha kifalme.​—Danieli 4:20-27.

Sawasawa na ilivyotabiriwa, “hayo yote yakampata mfalme Nebukadreza. (Danieli 4:28) Tafsiri ya Lexicon Linguae Aramaicae Veteris Testamenti inasema kwamba zile “nyakati saba” za ndoto ya Nebukadreza zilikuwa miaka saba halisi. Kwa kuwa Nebukadreza alitawala kwa miaka 43 (624-581 K.W.K.), huo ni mkataa unaofaa.

Jambo Hilo Lina Maana Gani Kwetu Sisi?

Sikuzote Yehova ameiendesha enzi kuu yake ya ulimwengu mzima kama vile anavyoona inafaa. Kwa muda fulani alifanya hivyo duniani kupitia lile taifa la Israeli, ambalo watawala walo wa kidunia walisema kwa kufaa kuwa ‘waliketi katika kiti cha enzi ya Yehova.’ (1 Mambo ya Nyakati 29:23) Lakini, wakati Israeli walipogeuka wakawa waasi-imani Yehova aliruhusu ukoo wa wafalme wa taifa hilo katika wazao wa Mfalme Daudi upinduliwe.

Basi, ilifaa kama nini kwamba muda mfupi baada ya hapo Mungu angempa Mfalme Nebukadreza dalili fulani​—mtu yule yule aliyeruhusiwa kuharibu Ufalme Wake wenye kufananisha​—kwamba kwa vyo vyote jambo hilo halikumaanisha kwamba enzi kuu halali ya Mungu ilikuwa imefikia mwisho. Lilikuwa jambo la maana kama nini amkazie huyo na Mataifa yote yasiyo ya Kiyahudi ambayo baadaye yangekanyaga-kanyaga Ufalme wenye kuwakilisha Mungu kwamba hali hiyo ingekuwapo kwa muda tu!

Hivyo kituo cha wakati ambapo ndoto hiyo ilitolewa, mtu yule aliyepewa hicho, na kichwa cha habari ya enzi kuu ya kimungu ambacho ndoto hiyo ilikazia, ni mambo yanayoonyesha kwamba ndoto hiyo ilimaanisha jambo kubwa zaidi ya vile ilivyomaanisha kwa Nebukadreza. Yanadokeza kwamba kama mti uliokatwa ukaanguka na kufungwa pingu, utawala wa kimungu uliokuwa umeonyeshwa katika Yerusalemu, na sasa ukawa umeharibiwa, haungerudishwa mpaka pingu hizo za kizuizi ziondolewe baada ya “nyakati saba.” Wakati huo, Mtawala mwenye kuwakilisha Mungu, “aliye mnyenyekevu zaidi sana kati ya wanadamu,” hiyo ikirejezea Masihi aliyeahidiwa, angesimamishwa katika Ufalme wake. Kwa habari ya wakati ambao Mungu angefanya hivyo, wanafunzi wa Yesu waliomba ishara.​—Danieli 4:17; Mathayo 24:3, NW.

Kuna dalili nyingine pia za kuonyesha kwamba matumizi hayo yenye kuhusu wakati wa baadaye sana ya ndoto ya Nebukadreza ni sahihi. Unabii ulioandikwa kwenye Danieli 9:24-27 ulielekeza kwenye mwaka barabara wa kufika kwa Masihi zaidi ya miaka 500 baadaye.a Sasa ikiwa wakati wa kuja kwa Masihi akiwa mwanadamu kulitabiriwa kwa usahihi kamili hivyo, je! si jambo la akili la kukata shauri kwamba wakati wa kurudi kwake kusikoonekana katika mamlaka ya Ufalme ambako ndiko kwa maana zaidi kungetabiriwa kwa usahihi kamili jinsi hiyo hiyo? Ni nani mwingine angefaa zaidi kufanya hivyo isipokuwa Danieli? Kumbuka, pia, kwamba Danieli alipokwisha kuandika njozi zake na unabii mwingi wa ndoto, kutia na ile ya mti wa Nebukadreza, yeye aliambiwa hivi: “Yafunge maneno haya, ukakitie muhuri kitabu, hata wakati wa mwisho.” Kwa sababu gani mpaka wakati huo? Kwa sababu katika wakati huo “maarifa [ya kweli, NW] yataongezeka.” Ikiwa yale ambayo Danieli aliandika yangebaki yametiwa muhuri, yasiweze kufahamika, mpaka “wakati wa mwisho,” je! jambo hilo halingeonyesha kwamba maandishi yake yangekuwa na umaana wa kiunabii wakati wa kipindi hicho?​—Danieli 12:4.

Zile “Nyakati Saba”​—Toka Wakati Gani Mpaka Wakati Gani?

Alipokuwa akitoa ishara yake, Yesu alisema juu ya “nyakati saba,” akaziita “nyakati zilizowekwa za mataifa.” Yeye alisema: “Yerusalemu [utaendelea kukanyagwa] na mataifa, mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa zitakapotimizwa.” (Luka 21:24, NW) Maelezo ya chini katika Oxford NIV Scofield Study Bible (1984) yanatuambia kwamba “zile ‘nyakati za Mataifa yasiyo ya Kiyahudi’ [fasiri ya Biblia ya King James Version juu ya “nyakati zilizowekwa za mataifa”] zilianza wakati Yuda ilipotekwa chini ya uongozi wa Nebukadreza. . . . Tangu wakati huo Yerusalemu umekuwa ‘ukikanyagwa na Mataifa’ kama vile Kristo alivyosema.”

Zile “nyakati saba” au “nyakati zilizowekwa za mataifa” zingeendelea kwa muda gani? Ni wazi kwamba zingeendelea kwa muda mrefu kuliko miaka saba halisi yenye siku 360 kila mmoja (kama vile miaka ya Kibiblia ilivyohesabiwa), na hizo zingejumlika ziwe siku 2,520. Kanuni ya Kimaandiko inaonyesha kwamba inatupasa tubadilishe kila siku iwe mwaka mmoja. (Ona Hesabu 14:4; Ezekieli 4:6; linganisha Ufunuo 12:6, 14.) Kuhesabu hivyo kungemaanisha kwamba zile “nyakati saba” ziliendelea kwa miaka 2,520. Ikiwa zilianza na uharibifu wa Yerusalemu 607 K.W.K., zingemalizika mwaka wa 1914 W.K.

Kwa zaidi ya miongo mitatu kabla ya 1914, Mashahidi wa Yehova walivuta fikira za watu kwenye umaana wa tarehe hiyo. Lakini, jambo la kupendeza ni kwamba kichapo International Crisis kilichotungwa na Eugenia Nomikos na Robert C. North (1976), kinasema kwamba kulikuwa na “ushuhuda kidogo au hakukuwa na wo wote wa kuonyesha kuinuka taratibu au kuongezeka haraka sana kwa mapigano na mikazo kuongoze moja kwa moja kwenye kutokea kwa vita. “Kinyume cha hayo, “hata kufikia mwisho-mwisho wa 1913 na mwanzo-mwanzo wa 1914 . . . mahusiano kati ya mataifa makubwa-makubwa yalionekana kuwa matulivu kuliko vile yalivyokuwa yamekuwa kwa miaka mingi.” Hata hivyo leo, miongo saba baadaye, wanahistoria kwa kweli wanasema kwamba 1914 ulikuwa kituo cha kugeukia mambo katika historia ya kibinadamu. Kwa mfano, kitabu cha marejezo cha Kijeremani kinachoitwa Meyers Enzyklopadisches Lexikon kinasema kwamba “matokeo ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza yalikuwa ya kimapinduzi kweli kweli na yaliingia kwa ndani sana katika maisha za karibu vikundi vyote vya mataifa, kiuchumi na pia kijamii na kisiasa.”

Matokeo ya kisiasa ya matukio ya 1914 yanajulikana vizuri. Mabadiliko ya kijamii yaliyotokezwa na mwaka huo yametajwa katika kitabu cha Virginia Cowles kinachoitwa 1913: An End and a Beginning “mwaka 1913 uliweka alama ya kikomo cha kipindi,” anaandika mwanamke huyo. Kuhusu matokeo ya kiuchumi, Ashby Bladen, makamu-msimamizi wa cheo kikuu katika Shirika la Bima ya Maisha ya Ulinzi ya Amerika, anaandika hivi: “Kabla ya 1914 mifumo ya kifedha na utoaji wa fedha ilikuwa ikipatana. . . . Mtu akichukua Agosti 1914 kuwa ukiweka alama ya mstari wa kugawanya kati yayo, tofauti zilizopo kati ya karne ya 19 na 20 ni kubwa sana. Katika pande nyingi za shughuli za kibinadamu kumekuwa na mgeuzo wa elekeo. . . . Sababu moja kubwa ilikuwa kukatwa kwa uhusiano uliokuwa kati ya mfumo wa utoaji wa fedha na thamani iliyo katika fedha kulikoanza 1914. . . . Kuvunjika kwa uhusiano huo kulikuwa tukio lenye maana kubwa.. . . 1914 uliweka alama ya geuzo kubwa la mfumo huo, na mwishowe likawa lenye msiba.”

Wakati Umesonga Sana Kadiri Gani?

Ushuhuda wa kwamba ishara ya Yesu sasa inaendelea kutimizwa unapatikana kwa urahisi kama vile ilivyo rahisi kupata habari za kila siku katika magazeti na televisheni. Nao unatoa uthibitisho wenye kukata maneno kwamba ushuhuda wa tarehe zenye kuunga mkono 1914 kama ulivyofunuliwa katika ndoto ya Nebukadreza ni sahihi. Kwa hiyo leo, 1986, inamaanisha kwamba tayari tuna miaka 72 ya kuwa katika “wakati wa mwisho.” Yesu aliahidi kwamba washiriki fulani wa kizazi cha watu waliokuwa na umri wa kutosha kushuhudia mwanzo wa wakati huo bado wangekuwa hai wakati ile dhiki kubwa ingeumalizia wakati huo.​—Ona Mathayo 24:34.

Jambo hilo linapasa kutuchochea kama nini tuendelee kuwa chonjo, macho yetu yakiwa yamekazwa juu ya ufunuo wa kimungu unaoonyesha jinsi wakati umesonga sana! Ni jambo la maana kama nini kwamba tuepuke kukosa subira, kujaribu kuharakisha kipima-saa cha kimungu, tuje tu kukata tamaa! Kwa upande mwingine, ni jambo la maana kama nini kwamba tujihadhari tusiwe na kinaya, kujaribu kupunguza mwendo wa saa hiyo, tuje tu kuchelewa! Kumbuka, jambo linalohusika ni kubwa kuliko hatari ya kuachwa tu na basi, gari-moshi, au ndege. Hatari iliyopo ni ile ya kukosa kupata uzima wa milele katika mfumo mpya wa mambo wa Mungu. Na hilo litakuwa ni jambo lililo zuri mno tusiweze kutaka kulikosa!

[Maelezo ya Chini]

a Ili kupata maelezo juu ya jambo hilo, ona kitabu “Ufalme Wako Uje,” kurasa 56-63, kilichochapishwa 1981 (katika Kiswahili ni mwaka 1983) na Sosaiti yetu.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Ni Wakati Gani Hasa “Nyakati Saba” Zilipomalizika?

Watu fulani wanabisha kwamba hata kama “nyakati saba” ni za kiunabii na hata kama zina urefu wa miaka 2,520, bado Mashahidi wa Yehova wanakosea juu ya umaana wa 1914 kwa sababu wao wanaanzia kuhesabu mahali pasipofaa. Watu hao wanadai kwamba Yerusalemu uliharibiwa 587/6 K.W.K., wala si katika 607 K.W.K. Kama hiyo ingekuwa kweli, ingebadili mwanzo wa “wakati wa mwisho” kwa miaka karibu 20. Lakini, katika 1981, Mashahidi wa Yehova walichapisha ushahidi wenye kusadikisha (“Ufalme Wako Uje,” kurasa 127-140, 186-189) ili kuunga mkono tarehe ya 607 K.W K. Zaidi ya hilo, je! wale wanaojaribu kuunyang’anya mwaka 1914 umaana wa Kibiblia wanaweza kuthibitisha kwamba 1934—au hata mwaka mwingineo wote kwa habari hiyo​—umekuwa na mambo mengi zaidi, ya kutazamisha zaidi, na kustaajabisha zaidi katika historia ya ulimwengu kuliko ulivyokuwa mwaka wa 1914.

[Chati katika ukurasa wa 6]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

“Nyakati [saba] zilizowekwa” Wakati wa mwisho za mataifa” (Miaka 2,520)

607 K.W.K. 33 W.K. 1914 W.K. 1986 W.K.

Yerusalemu “Yerusalemu” “Wakati wa miaka 72 ndani

wa kidunia bado waendelea mwisho” ya “wakati wa

waharibiwa “kukanyagwa” waanza mwisho”

(Luka 21:24) (Danieli 12:4) Mt. 24:3, 12, 22

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ndoto ya Nebukadreza ina matumizi makubwa sana yanayokuhusu wewe!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki