Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 10/1 kur. 7-11
  • Tuombeane

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tuombeane
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mambo Ambayo Sala Inaweza Kutufanyia Sisi
  • Sababu Gani Tuombeane?
  • Kuombea Umoja, Mwongozo na Hekima
  • Kuomba Kuhubiri Kufanikiwe Yajapokuwa Mateso
  • Kwa Ajili ya Afya Njema ya Kiroho
  • Faida za Kuombeana
  • “Salini kwa Ajili ya Mtu na Mwenzake”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Zawadi ya Sala
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Kumkaribia Mungu Katika Sala
    Mungu Anataka Tufanye Nini?
  • Mkaribie Mungu Kupitia Sala
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 10/1 kur. 7-11

Tuombeane

“Tuombeeni.”​—2 WATHESALONIKE 3:1.

1-3. (a) Kwa sababu gani watu wa Yehova wanaweza kumfikia yeye kwa sala wakiwa na uhakika? (b) Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuwa watu wa sala?

YEHOVA ndiye ‘Msikiaji mkuu wa sala.’(Zaburi 65:2, NW) Kwa hiyo, watumishi wake washikamanifu wanaweza kumfikia wakiwa na uhakika kwa maombi yao ya unyenyekevu na maneno ya kushukuru. Hakika, Mashahidi wa Yehova wana sababu nyingi za kuwa watu wa sala.

2 Sababu moja ni kwamba Yesu Kristo aliwafundisha wafuasi wake kusali. Yeye aliwaambia: “Msalipo, semeni, Baba, Jina lako litakaswe, Ufalme wako uje, Utupe siku kwa siku riziki yetu. Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila tumwiaye. Na usitutie majaribuni.” (Luka 11:2-4) Kwa kufaa sala hiyo ilimweka Mungu kwanza na ikatia maombi ya kibinafsi. Sala hiyo Iliyo Mfano wa Kufuatwa pia ilionyesha kwamba sala zetu hazipasi kukosa kukumbuka watu wengine.

3 Pia mitume wa Yesu waliwasihi waamini wenzao wawe watu wa sala. Kwa mfano, mtume Paulo alisema, “Katika kusali, mkidumu” na, “Ombeni bila kukoma.” (Warumi 12:12; 1 Wathesalonike 5:17) Na mtume Petro alisema: “Lakini mwisho wa mambo yote umesonga karibu sana. Kwa hiyo, mwe timamu katika akili, na kuwa wenye kukesha kwa habari ya sala.” (1 Petro 4:7, NW) Ni mashauri mazuri sana kama nini!

Mambo Ambayo Sala Inaweza Kutufanyia Sisi

4. Ni jambo gani linalotakiwa ikiwa sala za watumishi wa Mungu walio wakf zitasikiwa?

4 Mshairi mwenye kujulikana Alfred Tennyson aliandika hivi: “Sala inatokeza mambo mengi zaidi ya yale ambayo ulimwengu huu unawazia,” Ni kweli kama nini! Lakini ikiwa watumishi wa Mungu walio wakf watasikiwa, ni lazima sala zao zielekezwe kwa Yehova kupitia Yesu Kristo katika imani, lazima zipatane na mapenzi ya kimungu na lazima zisemwe kwa njia inayofaa. (Yohana 14:6; 1 Yohana 5:13-15) Kwa kupendeza, imekwisha kusemwa hivi: “Mungu haangalii uzuri wa maneno ya sala zako, jinsi yalivyo ya kiungwana; wala namna namna za sala zako, jinsi zilivyo ndefu; wala wingi wa sala zako, jinsi zilivyo nyingi; wala sala zako zilivyo za akili, jinsi zilivyo za utaratibu; bali unyofu wazo ndio anaoangalia.”​—Mhudumu Mpyuriti Mwingereza wa karne ya 17 Thomas Brooks.

5. (a) Sala inaweza kutufanyia nini sisi? (b) Kuhusu sala, tutafikiria ulizo gani?

5 Kusali kwa ukawaida, kwa unyofu wa moyo, kunatuvuta karibu zaidi na Yehova. Sala ya unyofu, ya bidii inatusaidia tutimize mgawo wetu wa kuhubiri. (Mathayo 24:14; 28:19, 20; 2 Wakorintho 2:17) Inatusaidia tufanye maamuzi ambayo yanampendeza Baba yetu wa kimbingu. Pia sala inatusaidia tuvumilie mateso na kudumisha ukamilifu kwa Mungu. (Zaburi 109:3, 4; 119:86) Inatupa nafasi ya kutoa shukrani za moyoni kwa Yehova. Na pia kuna sala ya kuombeana. Lakini kuhusu hiyo, sala hizo zinawezaje kufaidi sisi na waamini wenzetu?

Sababu Gani Tuombeane?

6. Yesu aliombea nani, na kwa hiyo sisi tunaweza kuombea nani?

6 Yesu, Mfano wetu, alisali kwa ajili ya wanafunzi wake. Kwa bidii yeye alimwomba Yehova hivi: “Mimi nawaombea hao; siuombei ulimwengu; bali hao ulionipa, kwa kuwa hao ni wako.” Ingawa Yesu alikufa kwa ajili ya ulimwengu wa wanadamu, yeye hakuuombea “ulimwengu” wa jamii ya kibinadamu iliyotenganishwa na Mungu. Hata hivyo, Yesu aliombea wale waliotoka katika ulimwengu huo na kuweka imani, katika yeye. (Yohana 3:16, 17; 17:8, 9; linganisha 2 Petro 2:5; 3:6.) Kwa sababu ya mfano wa Yesu, basi, kwa kufaa tunaombea watu hao mmoja mmoja wenye utawa.

7. Ni mfano gani wa mitume unaochochea watu wa Yehova waombeane?

7 Mtume Paulo aliomba kuhusu waamini wenzake. Kwa mfano, yeye aliwaambia Wakristo katika Efeso: “Kwa sababu hiyo mimi nami, tangu nilipopata habari za imani yenu katika Bwana Yesu, na pendo lenu kwa watakatifu wote, siachi kutoa shukrani kwa ajili yenu; nikiwakumbuka katika sala zangu.” (Waefeso 1:15, 16) Zaidi ya hayo, Paulo hakusita kutia sala ya kumwombea yeye na wengine. Baada ya kuwasihi Waefeso ‘wavae suti kamili ya silaha za kiroho’ na kukubali ‘upanga wa roho, neno la Mungu,’ yeye aliongeza kusema hivi: “Huku kwa kila namna ya sala na kusihi mkiendelea kuomba katika kila pindi katika roho. Na kwa kusudi hilo endeleeni kuwa wenye kuamka kwa uendelevu wote na kusihi kwa ajili ya watakatifu, pia kwa ajili yangu, kwamba uweza wa kusema nipewe mimi kwa kufumbuliwa kinywa changu, pamoja na uhuru wa kusema ili kujulisha siri takatifu ya habari njema.” (Waefeso 6:11-19, NW) Mfano huo wa kimtume pia unawasukuma watu wa Yehova waombeane.

8. Kwa sababu gani inafaa Wakristo wapakwa-mafuta na wale wa “mkutano mkubwa” waombeane?

8 Mashahidi wa Yehova ni sehemu ya udugu wa ulimwenguni pote. Wafuasi waliozaliwa kwa roho wa Kristo waliomo kati yao wana ‘ushirika,’ pamoja na Mungu, Mwanaye na Wakristo wapakwa mafuta wenzao. (1 Yohana 1:3, 7) Lakini, Yesu alidokeza kwamba wanafunzi wake wote wangekuwa na upendo kati yao, na mtume Petro alisema: “Muupende ushirika mzima wa ndugu.” (1 Petro 2:17, NW; Yohana 13:34, 35) Basi, inafaa kama nini kwamba Wakristo wapakwa mafuta na wenzi wao, “mkutano mkubwa,” waombeane! (Ufunuo 7:9) Lakini mambo gani yatiwe katika sala hizo?

Kuombea Umoja, Mwongozo na Hekima

9. Kwa sababu gani tunapaswa kuombea umoja wa udugu wetu wa Kikristo?

9 Tunapaswa kuombea umoja wa upendo katika udugu wetu wa Kikristo. Yesu aliomba kwamba wafuasi wake wawe na umoja na yeye na Babaye, na Paulo aliwasihi waabudu wenzake wa Yehova wawe na ‘umoja unaofaa katika akili ile ile na namna ile ile ya kuwaza.’ (1 Wakotintho 1:10; Yohana 17:20, 21) Roho halisi ya udugu sikuzote imekuwa alama ya kuthibitisha wale waliojitoa kwa Yehova. “Jinsi ilivyo vema, na kupendeza, Ndugu wakae pamoja, kwa umoja!” (Zaburi 133:1-3) Na njia moja ya kushiriki kuleta umoja huo ni kwa kuuombea.

10. Kwa sababu gani tuombe uongozi na kuungwa mkono na roho takatifu?

10 Tunapaswa kuomba kwamba kupitia roho yake Yehova atatoa uongozi na kuunga mkono utendaji mbalimbali wa watu wake. Huenda wengine wakawa na migawo migumu sana katika utumishi wa Mungu​—mambo hayangeweza kutimizwa kwa nguvu za kibinadamu peke yake. Kwa hiyo Wakristo hao washikamanifu, na sisi wenyewe, tunahitaji msaada wa Yehova kupitia roho takatifu yake.​—Zekaria 4:6; linganisha Luka 11:13; Matendo 8:14, 15.

11. Kwa habari ya hekima, tunaweza kuomba kwa kufaa jinsi gani?

11 Tunaweza kuomba kwamba ndugu zetu wapewe hekima kutoka kwa Mungu. Paulo aliomba kwamba Wakristo katika Kolosai ‘wajazwe maarifa sahihi ya mapenzi ya Mungu katika hekima yote na ufahamu wa kiroho; ili waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Yehova, wampendeze kabisa.’ (Wakolosai 1:9, 10) Pia inafaa kusali kwamba wale wanaoongoza kazi ya kuhubiri na kutayarisha vichapo vyetu wawe na “roho ya hekima.” (Waefeso 1:15-17) Je! wewe unaomba kwa ajili ya wale wanaosimamia kazi ya kuhubiri Ufalme na kutayarisha vichapo vinavyotoa ‘chakula cha kiroho kwa wakati wake’?​—Mathayo 24:45-47.

Kuomba Kuhubiri Kufanikiwe Yajapokuwa Mateso

12. Andiko la 2 Wathesalonike 3:1 linahusianaje na kuombea wengine?

12 Pia tunapaswa kuomba kwamba waamini wenzetu wafanikiwe kueneza ujumbe wa Ufalme. Paulo alisihi: “Ndugu, tuombeeni, neno la [Yehova] liendelee [kusonga kwa haraka], na kutukuzwa vile vile kama ilivyo kwenu.” (2 Wathesalonike 3:1; linganisha Waefeso 6:18, 19.) Ndiyo, Paulo aliwauliza waamini wenzake wasali kwamba yeye na wenzi wake wafanikiwe kutangaza ‘neno la Yehova.’ Sisi, pia, twapaswa kuomba Neno la Mungu lienezwe kwa kasi na kusogezwa mbele kwa faida za Ufalme. Bila shaka, sala hizo zinatia ndani wengine​—wale wote wanaofanya mapenzi ya Yehova kwa bidii katika hizi “siku za mwisho.”​—2 Timotheo 3:1-5.

13. (a) Andiko la 1 Timotheo 2:1, 2 linadokeza nini kuhusu sala kwa ajili ya maafisa walimwengu? (b) Tunaweza kuombea nini tukiteswa tukiwa watangazaji wa Ufalme?

13 Kwa kufaa watu wa Yehova wanaweza kuomba kuhusu maafisa wa kilimwengu. Paulo alisema: “Basi, kabla ya mambo yote, nataka dua, na sala, na maombezi, na shukrani, zifanyike kwa ajili ya watu wote; kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka.” Maneno yanayofuata ya Paulo yanadokeza kwamba sala hizo hasa ni kwa ajili ya watu wa Mungu, yaani, “tuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu.” (1 Timotheo 2:1, 2) Kwa kupendeza, wahamishwa Wayahudi katika Babuloni waliambiwa waombe kwa ajili ya amani ya mji huo, ‘kwa maana katika amani yake wangepata amani.’ (Yeremia 29:7) Kwa hiyo, tukiwa Mashahidi wa Yehova, kwa kufaa tunaomba kuhusu maafisa walimwengu ili sisi na ndugu zetu wa kiroho tuwe na maisha ya utulivu, yasiyo na mvurugo ili kutuwezesha tutimize mgawo wetu tukiwa watangazaji wa Ufalme. Lakini tukiteswa, tunaweza kuomba tukiwa na uhakika kwamba sisi na Mashahidi wenzetu tupewe msaada wa kimungu unaohitajiwa ili kusema neno la Mungu kwa ujasiri chini ya hali hizo. Na tunaweza kuwa na uhakika kwamba sala hizo zitajibiwa.​—Matendo 4:29-31; 5:29.

14. Tuna msingi gani wa Kimaandiko wa kuomba kwamba ndugu zetu wanaoteswa wapate msaada na faraja ya Mungu?

14 Hakika inafaa kuomba kwamba ndugu zetu wanaoteswa wapokee faraja na msaada wa Yehova. Katika mkoa wa Esia, ambapo mji wa Efeso ulikuwa, mtume Paulo ‘alikazwa sana, hata akawa hana uhakika ataishi.’ We! huenda akawa alipigana na wanyama-mwitu katika uwanja mmoja katika Efeso! Kwa vyo vyote, Paulo aliwaambia Wakristo katika Korintho: “Ninyi pia mnaweza kusaidia kwa kusihi kwenu kwa ajili yetu, ili shukrani zitolewe na wengi kwa ajili yetu kwa yaliyo ya fadhili tuliyopewa kwa ajili ya nyuso nyingi za namna ya sala.” (2 Wakorintho 1:8-11, NW; Matendo 19:23-41; 1 Wakorintho 15:32.) Basi, bila shaka, twapaswa kuomba kwamba ndugu na dada zetu wanaoteseka wapate msaada na faraja ya Yehova leo.​—2 Wakorintho 1:3-7.

15. Tunaweza kufanya nini kwa ajili ya waamini wenzetu wanaoteswa hata ikiwa sisi wenyewe tumefungwa gerezani?

15 Watumishi wenzi wa Yehova kwa hakika wanahitaji sala zetu wanapokabili mateso, dhiki au hatari. Nyakati hizo, huenda tukawa tumetenganishwa nao na huenda tusiweze kuwasaidia katika njia nyingineyo. Sisi wenyewe huenda tukawa tumefungwa gerezani! Hata hivyo, tunaweza kutokeza faida kubwa kwa kuombea waamini wenzetu. Maadamu tuko hai, adui zetu hawawezi kuzuia sala hizo. Huenda hata ikawa sala ya kimya, lakini hila shaka ina matokeo.​—Linganisha Nehemia 2:4-6.

Kwa Ajili ya Afya Njema ya Kiroho

16. Kwa kupatana na 2 Wakorintho 13:7, tunawezaje kuombea Wakristo wenzetu?

16 Kwa kufaa pia tunaweza kuomba kwamba Wakristo wenzetu ‘wasifanye lo lote lililo baya, lakini wafanye lile lililo jema.’ (2 Wakorintho 13:7) Sala ya namna hiyo ya upendo, isiyo ya choyo inaonyesha kwamba kweli kweli sisi tunataka waendelee kuishi katika kibali ya kimungu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Tunawaombea ninyi sikuzote, ili Mungu awahesabu kuwa mmekustahili kuitwa kwenu, akatimiza kila haja ya wema na kila kazi ya imani kwa nguvu.” (2 Wathesalonike 1:11) Epafra aliomba kwamba Wakristo Wakolosai ‘wasimame wakiwa wakamilifu na kuthibitika sana katika mapenzi ya Mungu.’ (Wakolosai 4:12) Ingawa maneno hayo yalielekezwa kwa Wakristo wapakwa-mafuta, sala zetu leo kwa kufaa zaweza kutia ndani maoni kama hayo kwa ajili ya wale wote waliojitoa kwa Yehova.

17. Ni sala zipi zinazofaa kuhusu afya ya kiroho ya ndugu zetu?

17 Tunaweza kuomba kuhusu afya ya kiroho ya waabudu wenzetu. Ikiwa wengine wanakuwa wagonjwa kiroho, wazee waliowekwa kwa kufaa wanawaombea na kuomba pamoja nao, wakitafuta nafuu yao. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na [Yehova] atamwinua.” (Yakobo 5:13-16; 1 Samweli 12:18-25) Katika sala zetu za kibinafsi tunaweza kutaja waamini wenzetu kwa jina na kuwatakia wabaki wakiwa ‘wenye afya katika imani.’ (Tito 1:13, NW; 2:1, 2) Bila shaka, ni kosa kuombea wale wanaokataa uandalizi wa Mungu wa kufunika dhambi.​—Waebrania 10:26-29.

Faida za Kuombeana

18, 19. Nyingine za faida za kibinafsi za ni zipi?

18 Tunaweza kuwa na hakika kwamba faida nyingi zitapatikana tukiombeana. Kwa mfano, sala zetu zitakuwa zenye mambo mengi ya maana. Kuombea waamini wenzetu bila shaka kutafanya nia yetu kuwaelekea iwe bora zaidi. Hakika, sala hizo zitaelekea kutufanya tuwe wenye subira zaidi, kuongeza hali yetu ya kutokuwa na choyo, kuwa wenye kupenda zaidi, wenye kuhangaikia zaidi wengine. Zaidi ya hayo, sala kwa ajili ya ndugu na dada za kiroho zitamwonyesha Yehova kwamba tunapendezwa na tengenezo lake, utendaji mbalimbali walo na hali njema yalo.

19 Kuna faraja kubwa kujua kwamba ndugu na dada zetu za kiroho wanatuombea, hali moja na sisi tunavyowaombea. Ni vizuri kama nini kujua kwamba sala zetu kwa ajili ya mashahidi wenzetu wa Yehova zinasikiwa na “Msikiaji wa sala”! Kwa hiyo, ili kusogeza faida za Ufalme huku tukiendeleza upendo na umoja kati yetu, na tuombeane.

Jibu Lako Ni Nini?

◻ Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuwa watu wa sala?

◻ Sala inaweza kutufanyia nini?

◻ Kwa sababu gani tuombeane?

◻ Kuhusiana na waamini wenzetu, tunaweza kuomba juu ya mambo gani?

◻ Nyingine za faida za kuombeana ni zipi?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Je! ninyi mnaombea mashahidi wenzenu wa Yehova wafanikiwe kueneza ujumbe wa Ufalme?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Ni mara ngapi ninyi mnaomba kwa ajili ya Wakristo wanaoteswa?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki