Njoni Kwenye “Ongezeko la Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya ya 1984!
HAKUNA mtu anayefahamu vizuri zaidi ya Yehova Mungu mwenyewe, juu ya uhitaji wa watumishi wake duniani kukutana katika makusanyiko makubwa. Hiyo ndiyo sababu yeye alipanga watu wake wa kale Israeli wawe wakikutana mara tatu kila mwaka katika mahali alipokuwa amepachagua, Yerusalemu. Wakiwa huko walisikia sheria ya Yehova Mungu ikisomwa, wakapokea kitia-moyo na bila shaka wakafurahia kusimuliana namna Yehova Mungu alivyokuwa amewabariki.—Kutoka 23:14-17; 34:23; Kumbukumbu la Torati 16:16, 17; 2 Mambo ya Nyakati 8:13.
Lakini, zaidi ya Waisraeli kukusanyika kwa ajili ya sikukuu hizo walikusanyika pia katika pindi za pekee, kama kwenye wakf wa hekalu la Mfalme Sulemani, na sherehe za wakf huo ziliendelea kwa muda wa siku 14, kisha wakakusanyika kwa ajili ya mzinduo wa kuta za Yerusalemu zilizojengwa upya katika wakati wa Nehemia.—1 Wafalme 8:65, 66; Nehemia 12:27-43.
Kwa hiyo mashahidi wa kisasa wa Yehova wamekuwa wakifanya makusanyiko muda wa miaka zaidi ya 100, tangu mwaka wa 1879, wakiwa na mwongozo mzuri wa Kimaandiko. Kufikia sasa, kwa muda usiopungua miaka 37, sisi tumekuwa tukikutana mara tatu kwa mwaka kama Waisraeli wa kale, mara mbili kwa ajili ya makusanyiko ya mizunguko yetu na mara moja kwa ajili ya kusanyiko la wilaya, la kitaifa au la mataifa yote.
Ripoti za “Umoja wa Ufalme” Kusanyiko la Wilaya la mwaka jana zilikuwa za kusisimua sana!a Akina ndugu walihisi zaidi ya nyakati zote zilizotangulia umoja wa duniani pote. Katika nchi nyingi mahudhurio yalipanda sana yakafikia vilele vipya. Kwa mfano, nchi ya Kiafrika ya Zambia, ikiwa na wahubiri 57,034, iliripoti hudhurio la jumla ya watu 417,122 kwenye makusanyiko 24. Hudhurio hilo lilikuwa kiasi cha mtu mmoja kati ya kila watu 15 wa nchi hiyo! Je! ripoti kama hizo hazichochei ndani yetu tamaa ya kuwa kwenye makusanyiko ya mwaka huu ya “Ongezeko la Ufalme”?
Sababu Kuna Uhitaji wa Kukusanyika
Kwa sababu gani tunahitaji kukusanyika pamoja kwa muda wa siku tatu na nusu ili kujitia nguvu kiroho? Petro anatukumbusha hivi: “Kwa kuwa vitu vyote hivyo vitafumuliwa hivyo, ninyi yawapasa kuwa watu wa namna gani katika vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa, mkingojea na kukaribisha akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.”—2 Petro 3:11, 12, NW.
Mwaka baada ya mwaka vishawishi na mikazo inaongezeka ili kutuepusha kutenda hivyo “vitendo vitakatifu vya mwenendo.” Hata inaweza kusemwa kwamba kila siku ulimwengu unazidi kuwa wenye jeuri, unazidi kuwa mbovu, unazidi kuwa na mapotovu, unazidi kuwa wenye ufisadi, unazidi kushuka tabia na kuwa na ukosefu wa maadili. Na kila upande vyombo vya utangazaji wa habari vinathibitisha hivyo, magazeti, radio, sinema na televisheni. Hasa wale kati yetu tunaolazimika kushirikiana na walimwengu ili kuchuma riziki au kupata elimu tunaona hali yetu ya kiroho ikishambuliwa nyakati zote.
Zaidi ya hilo, kuna mikazo mingi kama nini ya kutuepusha kutenda “matendo ya utawa,” kufanya ile kazi yenye sehemu mbili ya kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu na kufanya wanafunzi wa Kikristo! Ulimwengu wa kibiashara unatukaza na kutushawishi tuwe watu wa kufuatia mambo ya kimwili—tutumie wakati mwingi sana, nishati nyingi sana na fedha nyingi sana kujipatia vile vinavyoitwa vitu vizuri vya maisha mpaka ije kuwa kwamba ni wakati na nishati chache zinazobaki ili kufanya utumishi mtakatifu. Katika habari hii viwanda vinavyotengeneza vitu vya kujifurahisha vinaelekea kutokeza hatari kubwa hata zaidi kwa watu wa Mungu. Yesu alituonya vizuri juu ya mambo hayo, akisema: “Lakini jiangalieni ili mioyo yenu isije ikalemewa na kula kupita kiasi na kunywa kupita kiasi na masumbufu ya maisha, na kwa ghafula siku ile iwafyatukie kama mtego. . . . Endeleeni kukesha, basi, wakati wote mkifanya dua ili ninyi mpate kufaulu katika . . . kusimama mbele ya Mwana wa mtu.”—Luka 21:34-36, NW.
Programu yetu ya “Ongezeko la Ufalme” Kusanyiko la Wilaya imetayarishwa kwa njia ya kuwapa wahudumu wote wa Mungu msaada wanaohitaji ili waweze kweli kweli kuishi kulingana na kanuni za uadilifu za Yehova na ili wawe na vifaa vizuri kuliko vya nyakati zote zilizotangulia vya kutangaza Ufalme na kufanya wanafunzi.
Fanya Mipango Sasa Uhudhurie
Hasa tunataka kukumbuka kwamba makusanyiko haya yana urefu wa siku tatu na nusu, kuanzia alasiri ya Alhamisi. Mwaka huu utumishi wa shambani utakuwako alasiri ya Ijumaa. Kwa kulinganisha hesabu za hudhurio la siku ya Ijumaa na lile la Jumatatu, ulizo linatokea juu ya kama wengine wetu wangeweza kufanya jitihada kubwa zaidi ili wawepo wakati kusanyiko litakapoanza alasiri ya Alhamisi. Moja la mambo makuu zaidi ya kusanyiko ka mwaka jana lilikuwa ile hotuba ya Ijumaa yenye kusema “Muziki Unaomsifu Yehova,” na wakati huo tangazo lenye kusisimua lilitolewa juu ya kitabu cha nyimbo kilicho kipya ambacho kinakuja, hata visehemu tisa vya midundo mitamu vikafunguliwa visikiwe, huo ukiwa ni mwonjo mdogo wa vile kitabu cha nyimbo kilicho kipya kingekuwa. Itakuwa furaha kwa wengi kati yetu (wenye kusema Kiingereza) katika majira haya ya kusanyiko kuchanganya sauti zetu na za ndugu zetu tutakapokuwa tukikitumia hicho kitabu cha nyimbo cha Kiingereza kilicho kipya, wakati wa siku nne za kusanyiko!
Walio wengi kati yetu tunapata likizo fulani kila mwaka. Je! wengi zaidi kati yetu hatuwezi kupanga kulitia ndani kusanyiko zima katika likizo hilo? Au kama sivyo, hatungeweza kujinyima mshahara wa siku mbili kwa ajili ya karamu kubwa ya kiroho? Katika Honduras ndugu wengine wamepoteza kazi zao kwa sababu tu ya kuomba wakati wa kutokuwa kazini ili wahudhurie kusanyiko. Dada mmoja wa huko aliomba siku mbili za kutokufanya kazi ili ahudhurie “Umoja wa Ufalme” kusanyiko kisha akatishwa kwamba angefutwa kazi. Mwanasheria mmoja, ambaye mke wake ni Shahidi, alipata habari hizo naye akampangia dada huyo kazi yenye mshahara mkubwa zaidi baada ya kusanyiko.
Kitabu 1984 Yearbook kinaeleza kwamba ndugu wa Kispania na Kireno zaidi ya 30,000 walisafiri mwendo wote wa kwenda Ubelgiji ili wakahudhurie kusanyiko, katika wakati ambao makusanyiko hayangeweza kufanywa katika nchi zao wenyewe. Kinaeleza pia magumu ambayo ndugu wa Alaska wanapata ili kuhudhuria makusanyiko. Juu ya jitihada zilizofanywa na ndugu Msamoa ili kuhudhuria kusanyiko katika Fiji, tunasoma hivi: “Yeye hakuwa kijana, bali alikuwa mzee; hakuwa mwenye nguvu, bali mgonjwa-mgonjwa; hakuwa mwenye miguu mizuri, bali mwenye mguu uliojikunja; hakuwa na kipawa cha macho mazuri, bali alikuwa kipofu katika jicho moja. Ili afike kusanyikoni alihitaji pesa, na ili azipate ilikuwa lazima akusanye nazi. Alibeba nazi karibu 15 safari moja-moja mwendo wa maili mbili na kuzipeleka mahali alipokuwa akizifulia, kisha akatoa nyama yazo na kuitandaza ikauke, halafu akaiuza hiyo nyama ya nazi, au mbata.” Ilimchukua zaidi ya majuma manne kujipatia pesa za kutosha kulipia safari yake. Sisi na tujipige moyo konde (tujikaze) ili tuhudhurie!
Pia, inatupasa tukumbuke kwamba makusanyiko yetu hayawi ya kutujenga kiroho tu, bali mara nyingi yanafanya vilevile ushuhuda mkubwa upewe kwa watu wa nje. Kwa mfano, angalia maneno ambayo mwandishi wa habari alilazimika kusema katika toleo la Novemba 1983 la gazeti la Kigiriki Galaxias juu ya kusanyiko letu la “Umoja wa Ufalme” katika Athene. Baada ya kutoa maelezo yenye mambo mengi sana ya programu ya kila siku, yeye alisema hivi:
“Mtu awe au asiwe anakubali maoni ya Mashahidi Wakristo wa Yehova, kutembea kwake kwenye Uwanja wa ‘Apollo’ wakati wa vipindi vya Mashahidi Wakristo wa Yehova kulikuwa tukio lililomshangaza sana mtu huyo. . . . Hakuna mtu anayeweza kukana kwamba imani yao imegeuza sana maisha yao ya kibinafsi au, kwa kutumia maneno mengine, kwamba wao wanaishi kulingna na imani yao. Ingawa wao wana juhudi, si watu wa kushikilia sana mambo yao kiujinga. Wao wanampenda Mungu, lakini wanapenda wanadamu pia.”
Kila shahidi Mkristo wa Yehova, na pia watu wale wengine wote wanaopenda kweli na uadilifu, afanye kila jitihada ahudhurie kusanyiko la “Ongezeko la Ufalme”—tangu mwanzo hata mwisho!
[Maelezo ya Chini]
a Hesabu isiyo kamili inaonyesha kwamba, kwenye makusanyiko 401 ya ulimwenguni pote, hudhurio la jumla lilikuwa watu 3,276,942, na Mashahidi wapya 38,832 walibatizwa.