1914—Kizazi Ambacho Hakitapita
“KIZAZI hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia,” Yesu alisema. (Mathayo 24:34) Lakini maana ya neno “kizazi” ni nini?
Katika kitabu chake The Generation of 1914, profesa wa historia Robert Wohl anatoa ufafanuzi usio wa kawaida anaposema: “Kizazi cha kihistoria hakifafanuliwi kwa mipaka ya tarehe zake wala vipimo vyake. Si kisehemu cha tarehe . . . Kinafanana zaidi na mahali penye uvutano wa sumaku ambapo katikati pana jambo lililoonwa au mfululizo wa mambo yaliyoonwa. . . . Jambo la lazima ili kutambua kizazi ni hali fulani yenye kutajwa ambayo inatoa wazo la ukomo wa wakati uliopita . . . Hali hiyo yenye kutajwa sikuzote inaletwa na matukio makubwa ya kihistoria kama vita, mapinduzi, magonjwa ya kuambukia, njaa kubwa, na maharibiko ya uchumi.”
Kwa maoni hayo, ile Vita Kuu ya 1914-18 na misiba iliyofuatana nayo kwa hakika ilifanyiza “hali yenye kutajwa” ya kutia alama kizazi. Kama ambavyo Profesa Wohl anavyoeleza: Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilitokeza “ukomo mkubwa kwa wakati uliopita. Wale walioishi wakaipita vita hiyo hawangeweza kamwe kuondoa usadikisho wa kwamba ulimwengu mmoja ulikuwa umekoma na mwingine ukaanza katika Agosti 1914.”
Yesu alitumia neno “kizazi” nyakati nyingi katika hali tofautitofauti na likiwa na maana mbalimbali. Lakini yeye alimaanisha nini alipozungumza juu ya ‘kizazi ambacho hakingepita’? Wengine wamefasiri kuwa “kizazi” kina maana ya kipindi cha miaka 30, 40, 70 au hata 120. Lakini, kwa kweli kizazi kinahusiana na watu na matukio, wala si hesabu fulani ya miaka iliyowekwa.
Neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “kizazi” katika Biblia limefafanuliwa kuwa, “Wale waliozaliwa wakati ule ule . . . Yenye kushirikishwa na hilo ni maana hii: kundi la watu wa rika moja, kipindi kimoja cha wakati.” (Kitabu The New International Dictionary of New Testament Theology) “Jumla ya hesabu ya wale waliozaliwa wakati ule ule, ikipanuliwa itie ndani wote wanaoishi katika kizazi fulani cha wakati, watu wa rika moja.” (Kitabu A Greek-English Lexicon of the New Testament kutoka Chapa ya Tano ya Walter Bauer ya 1958) Mafafanuzi hayo yanatia ndani wale waliozaliwa kuzunguka wakati wa tukio la kihistoria na wale wote walio hai wakati huo.
Ikiwa Yesu alitumia “kizazi” katika maana hiyo na tukiitumia kuhusu 1914, basi sasa vitoto vya kizazi hicho vina miaka 70 au zaidi. Na wengine waliokuwa hai mwaka 1914 wana miaka 80 na kitu au 90 na kitu, wachache hata wamefika miaka 100. Kungali mamilioni mengi ya kizazi hicho ambao wangali hai. Baadhi yao ‘hawatapita hata hayo yote yatimie.’—Luka 21:32.
Tangu mwaka wa 1914 tumeishi kupitia vita vya ulimwengu viwili na mapigano mengine mengi makubwa, pamoja na njaa kubwa-kubwa, matetemeko ya ardhi, magonjwa yenye kuambukia na mambo kama hayo. (Luka 21:10, 11) Hata hivyo Yesu alisema: “Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.” (Mathayo 24:34) Kwa hiyo, huenda wewe ukauliza: Ni matukio gani mengine makubwa ambayo yanabaki yaonwe na kizazi cha 1914? Na je, kweli kweli yanaweza kutimia katika kipindi cha wakati ambacho kimebaki kabla ya kizazi hicho kumalizika?
Halafu ni Mambo Gani Yanatokea?
Hasa ni tangu mwaka 1919 Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakitimiza kwa kadiri kubwa unabii wa Yesu ujapokuwa upinzani wa duniani pote: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) Naam, hiyo ndiyo kazi ambayo lazima ikamilishwe kwa kadiri ya kumridhisha Yehova kabla ya mwisho kuja.
Ni matukio gani mengine ambayo lazima yatokee katika kipindi kilichobaki kabla ya kizazi cha 1914 kumalizika? Biblia inataja waziwazi matukio fulani makubwa-makubwa ambayo yataongoza mpaka kwenye “dhiki kubwa” na kuwa sehemu yake. Dhiki hiyo itafikia upeo katika Har–Magedoni, “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” (Mathayo 24:21; Ufunuo 16:14, 16) Ni jambo lenye uharaka kwamba wewe ujue matukio hayo ni nini na kwamba uchukue hatua ya kujilinda iliyo ya lazima kabla haijawa kuchelewa mno.—Sefania 2:3.
Tukio mojalapo hayo lilitabiriwa na mtume Paulo aliposema: “Ninyi wenyewe mwajua sana kwamba siku ya Yehova inakuja sawasawa kama mwivi usiku. Wakati wo wote wanaposema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao papo kwa hapo.” Unabii huo unaonyesha wazi kwamba, kabla tu ya mwisho wa mfumo huu wa mambo, “amani na usalama” utatangazwa kwa njia fulani isiyo ya kawaida, iwe itafanywa hivyo na Umoja wa Mataifa au na viongozi wa kisiasa na kidini peke yao. Ni jambo gani litakalofuata tangazo hilo? Paulo alisema: “Ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao papo kwa hapo.”—1 Wathesalonike 5:2, 3, NW.
Je! Dini Yako Inapasa Kufikiriwa Kweli Kweli?
Je! uharibifu huo unaweza kukupata? Je! wewe ni mshiriki wa mojawapo dini nyingi za ulimwengu? Je! wewe unajua jinsi Mungu anavyoziona dini hizo? Wakati ujao wazo ni nini?
Kwa kutumia mfano wa “kahaba mkuu” mwenye jina “Babeli Mkuu,” mtume Yohana aliyeongozwa na roho ya Mungu alisimulia juu ya mfumo ambao umejifaidi kwa karne nyingi kwa ushirika wa karibu pamoja na “wafalme wa nchi” wenye mamlaka ya kisiasa. “Kahaba” huyo amefaidika pia kwa shughuli za pamoja na “wafanya biashara,” yaani, sehemu ya kibiashara ya ulimwengu. Ni mfumo gani huo ambao pia umepiga ubwana juu ya “jamaa na makutano na mataifa na lugha”? Ni dini ya uongo! Ndiyo, dini zote ambazo ni za uongo kwa maoni ya Yehova Mungu ndizo zinazofanyiza huyo “kahaba mkuu,” ambaye kwa kweli ni milki ya ulimwengu. Lakini wakati ujao ulio karibu una mambo gani kwake?—Ufunuo 17:1-8, 15; 18:15-17.
Ufunuo 17:16 unadokeza kwamba sehemu za kisiasa zenye kutaka mapinduzi zilizomo katika Umoja wa Mataifa (“mnyama mwekundu sana”) zitamchukia kahaba huyo wa kidini na kumfanya ukiwa. Tayari, sehemu zenye nguvu sana zenye kupinga kuwapo kwa Mungu na zenye kupinga dini zilizomo katika UM zimechukua hatua za kukomesha dini katika milki zao. Lakini tendo lenye moto zaidi latazamiwa katika wakati ujao ulio karibu wakati sehemu hizo za kisiasa zitakapofanya ukiwa si Jumuiya ya Wakristo tu bali pia zile milki nyingine kubwa za kidini. Ni jambo la akili kukata maneno kwamba majeshi hayo yenye kumpinga Mungu yatashambulia Mashahidi wa Yehova pia ambao wanatangaza Ufalme wa Mungu kwa uaminifu. Hiyo itakuwa kama kwamba ni kumshambulia Mungu mwenyewe na kumfanya Mungu naye ashambulie, yaani, Vita ya Mungu ya Har–Magedoni!—Ufunuo 17:3, 12-16; 16:14-16; Ezekieli 38:10-12, 18-23; Zekaria 2:8.
Je! Kuna Wakati wa Kutosha?
Kwa maoni ya kibinadamu kabisa, ingeweza kuonekana kwamba matukio hayo hayangeweza kutokea hata kabla ya kizazi cha 1914 kumalizika. Lakini utimizo wa matukio yote yaliyotabiriwa yanayohusu kizazi cha 1914 hautegemei tendo la pole la kibinadamu. Neno la kiunabii la Yehova kupitia Kristo Yesu ni hili: “Kizazi hiki [cha 1914] hakitapita hata hayo yote yatimie.” (Luka 21:32) Na Yehova, ambaye ndiye chanzo cha unabii ulioongozwa kwa roho yake na usioshindwa, atatimiza maneno ya Mwanaye katika muda mfupi.—lsaya 46:9, 10; 55:10, 11.
Je! kuna mifano yo yote ya unabii wa Biblia ya wakati uliopita uliotimizwa, wanadamu wajapotia mashaka na kukosa kusadiki? Ndiyo, na tunaweza kuchunguza kifupi mmojawapo. Mwaka wa 33 W.K., Yesu alitabiri kuhusu Yerusalemu na hekalu lake: “Haya mnayoyatazama, siku zitakuja ambapo halitasalia jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa. Lakini, hapo mtakapoona mji wa Yerusalemu umezungukwa na majeshi, ndipo jueni ya kwamba uharibifu wake umekaribia.”—Luka 21:6, 20.
Miaka 33 baadaye, jeshi la Kiroma, likiongozwa na Seshio Galo, lilishambulia Yerusalemu na lilikuwa limekaribia kushinda. Bila sababu yenye kuelezeka, hata hivyo, Jenerali Galo akaamuru majeshi yake yaondoke. Basi, baadhi ya Wayahudi huenda wakawa waliwaza kwamba mji wao mtakatifu haungeharibiwa. Lakini wazo hilo halikuendelea muda mrefu. Miaka minne baadaye, majeshi ya Kiroma yakiongozwa na Tito yalirudi na kuuharibu Yerusalemu na hekalu lake.
Kwa hiyo unabii wa Yesu ukatimia mpaka mambo madogo-madogo aliyosema. Ni kama G. A. Williamson alivyosema katika utangulizi wake wa kitabu The Jewish War cha Yosefo: ‘Kama hatungekuwa na vyanzo vingine vya habari zaidi ya injili tungeshawishwa tutie shaka kwamba maonyo ya Yesu yalitiwa chumvi. Je! ingewezekana kwamba halingebaki jiwe hata moja juu ya jingine, lisitupwe chini, kwenye Hekalu kubwa hilo? Kweli kweli iliwezekana; hilo ni jambo hakika la kihistoria. Uharibifu huo ulikuwa kamili kabisa. Masimulizi hayo yote yenye msiba yalikuwa yametabiriwa kwa usahihi wenye kushangaza sana.’
Kama vile unabii mbalimbali wa Yesu kuhusu Yerusalemu ulivyotimizwa wakati wa kipindi kile kile cha maisha cha kizazi cha mwaka wa 33 W.K., ndivyo unabii wake mbalimbali kuhusu “wakati wa mwisho” utakavyotimizwa wakati wa kipindi cha maisha cha kizazi cha 1914. (Danieli 12:4) Maana yake ni kwamba mataraja mazuri ajabu yako si mbele tu ya kizazi hicho bali pia mbele ya wote wanaoishi leo. Kwa sababu gani? Kwa sababu Yesu alisema pia kuhusu umaana wa matukio yanayohusu kizazi hicho: “Mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.”—Luka 21:28, 31.
Ukaribu wa Ufalme wa Mungu leo unamaanisha mwisho wa mifumo ya wakati huu yenye kugawanya ya kisiasa na ya kibiashara. Unamaanisha kuletwa kwa serikali mpya ya uadilifu kwa ajili ya wanadamu wote watiifu. Wewe unaweza kuchagua uzima wa milele chini ya mpango huo wa “mbingu mpya na dunia mpya.” (2 Petro 3:13, NW; Yohana 17:3) Ndiyo, huenda ukaishi uone Utaratibu Mpya huo ulioahidiwa, pamoja na waokokaji wa kizazi cha 1914—kizazi ambacho hakitapita.
[Picha katika ukurasa wa 5]
“Ulimwengu mmoja ulikuwa umekoma na mwingine ukaanza katika Agosti 1914”
[Picha katika ukurasa wa 6]
‘Wanaposema “Amani na Usalama!” uharibifu wa ghafula utakuwa juu yao’
[Picha katika ukurasa wa 7]
Wewe, pamoja na waokokaji wa kizazi cha 1914, huenda ukaishi uone Utaratibu Mpya