Usisahau Kamwe Wewe Ni Shahidi!
“‘Ninyi ni mashahidi wangu,’ ndio usemi wa Yehova, ‘na mimi ni Mungu.’”—ISAYA 43:12, New World Translation.
1. (a) Ni pendeleo gani kubwa zaidi ambalo mtu anaweza kuwa nalo duniani? (b) Neno “shahidi” linafafanuliwaje?
HAKUNA pendeleo kubwa zaidi duniani zaidi ya lile la kuwa shahidi wa Mungu wa kweli, Yehova. Shahidi ni “mtu anayetoa ushahidi katika kusudi fulani au mbele ya baraza la hukumu.” (Webster’s New Collegiate Dictionary) Yesu Kristo ndiye aliyetoa ushahidi kwa ajili ya kusudi kubwa zaidi katika ulimwengu wote—kusudi la Yehova Mungu. “Akiwa shahidi,” Biblia inasema, Yesu “alifanya tangazo zuri la peupe mbele za Pontio Pilato.” (1 Timotheo 6:13, NW) Na alipokuwa hukumuni, yeye alimwambia nini gavana huyo wa Kiroma?
2. Yesu Kristo alitoa ushuhuda juu ya nini?
2 Katika kujibu ulizo moja aliloulizwa wakati huo, Yesu alitangaza: “Wewe mwenyewe unasema kwamba mimi ni mfalme. Kwa ajili ya hili mimi nimekuja kuingia ndani ya ulimwengu, kwamba nipaswe kutoa ushuhuda kwa ule ukweli.” (Yohana 18:37, NW) Ndiyo, Yesu alionyesha wazi kwamba alikuwa amekuja ulimwenguni ili ashuhudie ukweli wa Mungu. Kwa sehemu, hiyo ilimaanisha kushuhudia cheo chake akiwa Mfalme wa Kimasihi. Pia Yesu alitoa ushuhuda kwa jina la Mungu, Yehova. Kwa hiyo, katika sala aliyotoa kwa Babaye wa kimbingu, Yesu angeweza kusema: “Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu.” (Yohana 17:6) Mpaka siku ya kufa kwake akiwa binadamu, Yesu alitambua daraka lake la kuwa shahidi wa Yehova. Kweli kweli, Yesu hakusahau kamwe alikuwa shahidi.
Mfano wa “Shahidi Aliye Mwaminifu na wa Kweli”
3. (a) Ni nani “Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli”? (b) Ilitukiaje kwa kundi katika Laodikia, naye Yesu alilipa shauri gani?
3 Yesu alitekeleza mgawo wake akiwa shahidi wa Yehova kwa uaminifu na kwa bidii. Na katika jambo hilo anawekea Wakristo walio wakfu mfano mzuri sana. La kuangaliwa pia, ni shauri la Yesu alilolipa kundi katika Laodikia. Kwa wazi kwa sababu ya kuvutwa fikira na tamaa za kimwili, kundi hili lilikuwa limekuwa “uvuguvugu” katika kutoa ushuhuda kwa ajili ya Yehova na Ufalme wa Kimasihi. Kwa hiyo Yesu aliwasihi ‘wawe na bidii na kutubu.’ Alitanguliza shauri lake kwa kundi hilo kwa maneno haya: “Haya ndiyo anenayo yeye aliye Amina, Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli.”—Ufunuo 3:14-19.
4. (a) Kwa sababu gani Yesu alijiita “Amina”? (b) Yesu alitaka Wakristo wa Laodikia wasisahau nini kamwe?
4 Kwanza, Yesu anajiita “Amina.” Kwa sababu gani? Kwa sababu Yehova alimtuma akiwa ndiye “Amina” (maana yake, “na iwe hivyo”) kwa ahadi zote za kimungu. Yesu ndiye anayetekeleza ahadi za Mungu. (2 Wakorintho 1:20) Kisha, Yesu anajitambulisha kuwa “Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli.” Kwa sababu gani? Ili kundi limtazame yeye kuwa Mfano wa kufuatwa na hivyo lipate kichocheo cha kutubu makosa yalo na kuwa lenye “bidii” tena katika kutoa ushuhuda juu ya Yehova. Mwana wa Mungu alitaka Wakristo hao katika Laodikia wasisahau kamwe kwamba wanapaswa kuwa mashahidi wa Mungu na wa Ufalme wa Kimasihi.
5. Yesu alikuwaje mfano kwa Mashahidi wa Yehova leo?
5 Yesu anataka wanafunzi wake wote wawe waaminifu na mashahidi wenye bidii mpaka mwisho wenyewe wa huu mfumo mbovu wa mambo. “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote,” Yesu alisema, “na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW; Matendo 1:6-8) Katika mambo yote mawili, aliyofanya na kusema, “Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli” alikuwa mfano wenye kutia moyo mashahidi Wakristo wa Yehova leo. Wao wanatambua pendeleo lao kubwa sana kuwa wategemezaji wa jina la kimungu na watumishi washikamanifu wa Yehova ambao wanaweka moyoni maneno haya yake: “Ninyi ni mashahidi wangu . . . na mimi ni Mungu.”—Isaya 43:10-12, NW.
Kwa Nini Kuna Uhitaji wa Kutosahau
6. (a) Kuhusu nuru ya kiroho, mashahidi wa Yehova wana pendeleo gani? (b) Huenda tukajiuliza maulizo gani?
6 Ikiwa wewe ni shahidi wa Yehova aliye wakfu na kubatizwa, daima utambue pendeleo lako kubwa la kumtumikia Mtu aliye juu zaidi katika ulimwengu wote. Kumbuka kwamba “Shahidi aliye mwaminifu” alikuwa “nuru ya ulimwengu.” (Ufunuo 1:5; Yohana 8:12) Kwa hiyo, lazima Mashahidi wa Yehova wote waangaze nuru inayohusu makusudi ya Mungu. Kama ambavyo haingefaa kuweka taa chini ya kikapu badala ya kuiweka kwenye kinara cha taa, ndivyo lisivyo jambo la akili kwa Mkristo wa kweli kuficha nuru yake. Ni lazima aangaze ili wote wanaomkaribia wapate faida ya nuru ya kiroho ambayo yeye mwenyewe anafurahia. Kwa sababu hiyo, Yesu aliwasihi wanafunzi wake hivi: “Nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:14-16) Wakiwa tengenezo, Mashahidi wa Yehova leo ni mashuhuri duniani pote—wao ni kama mji ulio juu ya mlima unaoangaza nuru mbali na karibu. Lakini je, wewe binafsi unaangaza nuru yako nyakati zote? Je! sikuzote wewe unatambua pendeleo lako ukiwa shahidi wa Yehova?
7. Ni sababu gani kubwa ya kutosahau sisi ni mashahidi wa Yehova?
7 Kwa sababu gani hatupaswi kusahau kamwe kwamba sisi ni mashahidi wa Yehova? Sababu moja kubwa ni kwamba tunaishi katika ulimwengu ambao mikazo ya maisha ya kila siku, mahangaiko ya maisha na vingi vya vivuta-fikira vyaweza kutuondosha tusiseme juu ya Mungu wa kweli na makusudi yake. Kwa ajili ya faida na onyo kwetu, Yesu alisihi: “Kesheni . . . jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.” (Mathayo 24:42-44) Kwa sababu gani akatoa onyo hilo linalofaa? Kwa sababu kuondoshwa fikira kando kunaweza kuongoza kwenye uharibifu—ndiyo, uharibifu kwa wale wenye kuondoshwa fikira kando wakati Yesu anapokuja kufikiliza hukumu juu ya huu mfumo wa mambo.—Ufunuo 19:11-21.
8, 9. Tunawezaje kufaidika kwa kufikiria watu wa siku za Nuhu walioondoshwa fikira kando?
8 Fikiria yaliyotokea katika siku za Nuhu. Lo! kulikuwako vivuta-fikira vingi sana wakati huo hata watu hawakuona umaana wo wote wa kuhubiri na kujenga safina kwa Nuhu! ‘Hawakutambua,’ wakafumaniwa kwa sababu ya vivuta-fikira nao wakaharibiwa.—Mathayo 24:36-39.
9 Basi, je, tutaondoshwa fikira kando na ulimwengu wa leo pamoja na vivuta-fikira vyake vingi? Kwa kuwa tukiondoshwa fikira kando kabisa tusitimize daraka letu tukiwa wafuasi wa Yesu kunaweza kutokeza uharibifu, na tuwe wenye kukesha daima. Tukijiweka tayari wakati wote, tusilalie kamwe madaraka yetu, hatutaharibiwa pamoja na walioondoshwa fikira kando wa ulimwengu huu.—Luka 17:26-30; 21:34-36.
10. Wakristo wote wa kweli wana mgawo gani wa lazima?
10 Kwa hiyo tusisahau kamwe tuna mgawo wa lazima wa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. (Marko 13:10) Hata sisi tuwe ni nani au hata tuwe tunafanya kazi gani katika tengenezo la Yehova, tuna daraka la kutangazia wengine tumaini letu. (Warumi 10:10; 1 Wakorintho 9:16) Katika nchi nyingi tunaweza kwenda nyumba kwa nyumba tukiwa na ujumbe wa Ufalme kwa uhuru. Lakini katika nchi ambazo kuna uhuru huo wa kuhubiri, huenda watu wakawa wenye ubaridi kuelekea dini, na huenda ukawa na mazungumzo machache kwenye milango. Ikiwa ndivyo, unahitaji kuwa macho sana kujipatia nafasi nyingine za kuangaza nuru yako.
11. Uhakika wa kwamba wafuasi wa Yesu walikuwa wa “Njia hii” unaonyesha nini juu ya utumishi anaotolewa Yehova?
11 Hata ingawa huenda ukawa na nyakati fulani zilizowekwa kando za kushiriki katika sehemu fulani fulani za kazi ya kutoa ushuhuda, mtumishi wa Yehova aliye wakfu apaswa kuwa akimsifu kwa neno na kwa tendo nyakati zote. Je! wewe unafanya hivyo? Wafuasi wa kwanza wa Yesu walisemwa kuwa ni wa “Njia hii.” (Matendo 9:1, 2) Kwa hiyo hawakuwa wakimtumikia Mungu saa chache tu katika mwezi. Utumishi wao ulikuwa njia ya maisha! Je! sisi ni kama Wakristo wa karne ya kwanza ikiwa sisi ni wahubiri wa Ufalme wasio wa kawaida ambao wanashiriki mara chache sana katika utendaji wa kutoa ushuhuda? Je! tunaweza kujiita Mashahidi wa Yehova kwa kufaa ikiwa tunasema machache au hatusemi cho chote na wengine juu ya tumaini letu?
Kutumia Wakati Wetu Tusaidie Wengine
12, 13. (a) Tunawezaje kujiimarisha kiroho? (b) Kwa sababu gani tunapaswa kutunza maandishi yanayohusu watu wenye tunaokuta kwenye huduma ya shambani?
12 Tunahitaji kutumia wakati wetu kwa njia ya hekima endapo tutasaidia wengine kwenye njia inayoongoza kwenye uzima wa milele katika Utaratibu Mpya wenye uadilifu wa Mungu. Lakini ili tusaidie wengine ni lazima sisi wenyewe tujiimarishe. Ni lazima tule chakula cha kiroho kwa ukawaida na kujijenga katika imani. Tukiwa haturidhiki na kuwa “watoto wachanga,” ni lazima “tusonge mbele kwenye ukomavu.” (Waefeso 4:14; Waebrania 6:1, NW) Katika utoaji wetu wa ushuhuda wa kawaida nyumba kwa nyumba, je, tumechukua daraka la ziada la kufuatia watu wenye mfano wa kondoo? Watu wanaposikiliza ujumbe wetu wa Biblia au kuonyeshwa kupendezwa na Neno la Mungu na Ufalme wake, sisi tunafanya nini? Je! tunapendezwa kiasi cha kuandika jina na anwani na habari tuliyozungumza, halafu kumfuatia mtu huyo mwenye kupendezwa?
13 Endapo tunakesha kiroho, tunaweza kufanyiza nafasi za kuhubiri Neno la Mungu wakati wo wote, na mahali po pote. Na tufanye hivyo tukiwa na furaha, mioyo yetu ikiwa imejaa na kufurishwa na yale ambayo tumefunzwa na Mwalimu Mkuu Zaidi wetu, Yehova.—Isaya 30:20, 21.
Uwe Macho Kutoa Ushuhuda wa Vivi Hivi
14. (a) Wengine wamejifunza ukweli wa Mungu kupitia utoaji wa ushuhuda wa namna gani? (b) Je! utoaji wa ushuhuda wa vivi hivi unapasa kuchukua mahali pa huduma ya shambani ya kawaida?
14 Wengine wanafahamiana na ukweli wa Mungu kwa sababu ya shirika na watu wa ukoo, marafiki, wafanyi-kazi-wenzi, jirani, na kadhalika. Kwa mfano, katika kikundi kimoja cha Mashahidi waliobatizwa 238, asilimia 40 walikuwa wamejifunza ukweli wa Biblia kupitia utoaji wa ushuhuda wa vivi hivi. Bila shaka, huo hauwezi kuchukua mahali pa huduma ya shambani, utendaji wako wa kawaida wa kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba au wa ziara za kurudia, na kadhalika.—Matendo 5:42; 20:20.
15. Yesu aliweka mfano wa namna gani kwa habari ya utoaji wa ushuhuda wa vivi hivi?
15 Hata hivyo, Yesu “Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli,” alituwekea mfano mzuri katika kutoa ushuhuda wa vivi hivi. Kwa mfano “alipokuwa akipita,” Yesu aliona “mtu ameketi forodhani, aitwaye Mathayo” akasema naye na kupata matokeo mazuri. (Mathayo 9:9) Zaidi ya hilo, katika pindi nyingine, ingawa Yesu alikuwa amechoka alichukua nafasi ya kusema juu ya ukweli na mwanamke mmoja aliyekuja kuteka maji katika kisima kimoja katika Sikari. Mazungumzo hayo yalifanya Wasamaria wengi wamwamini Yesu kuwa ndiye Masihi.—Yohana 4:5-30, 39-42.
16. Mtume Paulo aliweka mfano gani mzuri katika kutoa ushuhuda?
16 Mtume Paulo pia alitumia kwa faida kila nafasi azungumze juu ya Neno la Yehova. Alipokuwa Athene, Paulo alifanya hivyo kwa “wale waliokutana naye sokoni kila siku.” (Matendo 17:17) Na alipokuwa amefungiwa ndani ya nyumba katika Roma, mtume huyo “akawakaribisha watu wote waliokuwa wakimwendea, akihubiri habari za ufalme wa Mungu, na kuyafundisha mambo ya Bwana Yesu Kristo, kwa ujasiri mwingi, asikatazwe na mtu.” (Matendo 28:30, 31) Yote hayo yanapasa kutuchochea kama nini tusiache nafasi zo zote za kutoa ushuhuda!
17. Licha ya huduma ya shambani ya kawaida, kuna nafasi gani za kutolea wengine ushuhuda?
17 Licha ya huduma yetu ya shambani ya kawaida, kuna nafasi nyingine nyingi za kutoa ushuhuda. Wafanyi-kazi-wenzetu, wanashule wenzetu, watu wa ukoo na watu tunaofahamiana nao wote wanahitaji kusikia juu ya Yehova na makusudi yake. Tunaposafiri kwa bas, ndege au gari-moshi, huenda tukaweza kuanzisha mazungumzo yanayoongoza kwenye utoaji wa ushuhuda wa Ufalme. Huenda pia tukaweza kuanzisha mazungumzo yenye kuongoza kwenye kutoa ushuhuda wa Ufalme. Huenda pia tukaweza kushiriki “habari njema” pamoja na mameneja (wasimamizi) wa hoteli, wafanyi kazi wa vituo vya petroli, wafanyi kazi wa mikahawa au madereva wa teksi. Tunapokuwa nyumbani huenda tukatolea ushuhuda wauzaji-bidhaa au wenye kutuletea vitu nyumbani! Lo! hata tunapolazwa hospitali, huenda tukaweza kutolea ushuhuda wauguzi, madaktari na wagonjwa! Wanapokuwa wakipata nafuu katika hospitali, mashahidi wengi wa Yehova wamesaidia wagonjwa wengine wajifunze juu ya Utaratibu Mpya wa Mungu ambao katika huo watu watafurahia afya kamili.
18. (a) Ni jambo gani linalopendekezwa ikiwa unasita kutumia kwa faida nafasi za kutoa ushuhuda? (b) Katika kutolea ushuhuda watu wa ukoo na watu tunaofahamiana nao, tunapaswa kuonyesha sifa gani?
18 Basi, ni jambo la lazima kama nini, kwamba ukiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova utangaze ujumbe wa Ufalme katika kila nafasi! Ndiyo kusema, usisahau kamwe wewe ni shahidi! Lakini namna gani ikiwa unasita unapoona nafasi ya kutoa ushuhuda? Basi omba upewe ujasiri wa kusema ukweli. Utavuna baraka nyingi sana ambazo kama si kwa kufanya hivyo ungezikosa. (Linganisha Matendo 4:29-31.) Bila shaka, kutolea ushuhuda watu wa ukoo na watu unaofahamiana nao huenda kukawa rahisi kidogo. Lakini tumia busara, uwe mwenye fadhili na subira kwao, usifanye mambo utakavyo tu kwa sababu unawajua vizuri. Fikiria mambo ya usoni na polepole usitawishe ndani yao kuthamini ukweli wa Biblia.
Mwenendo Mwema—Sehemu ya Namna Tunavyotoa Ushuhuda
19. Kuna uhusiano gani kati ya utoaji wetu wa ushuhuda na mwenendo wetu?
19 Utoaji wetu wa ushuhuda wote si wa maneno. Mtume Paulo alikamatanisha mwenendo mwema na kuangaza nuru. Alisihi Wakristo Wafilipi ‘watende mambo yote pasipo manung’uniko wala mashindano, ili wawe wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao walikuwa wakiangaza kama mianga katika ulimwengu.’ (Wafilipi 2:14, 15) Katika ulimwengu ulioharibika kiadili na wenye giza, ni lazima shahidi wa Yehova aonekane akiangaza sana kama nuru. Kweli kweli, Mkristo mwaminifu anaonyesha lilivyo neno la ukweli kwa kutoa ushuhuda kwa maneno na anaangaza kwa sababu ya mwenendo wake mwema wa adili. Mashahidi wa Yehova wote na wajionyeshe kuwa waangazaji-washikamanifu kwa namna wanavyoishi na kwa maneno wanayosema ya ukweli wa Kimaandiko!
20. Mwenendo wetu mwema huenda ukawa na matokeo gani juu ya wengine?
20 Akikazia jambo ilo hilo, mtume Petro aliandika: “Dumisheni mwenendo wenu mwema miongoni mwa mataifa, ili. . . wapate kumtukuza Mungu katika siku ya kukaguliwa kwao kama matokeo ya kazi zenu njema ambazo wao ni mashahidi wenye kujionea.” (1 Petro 2:12, NW) Bila shaka si wote watakaomtukuza Mungu na kuwa Mashahidi wa Yehova katika siku yake ya ukaguzi. Walio wengi hawatakuja upande wa Ufalme wa Mungu wa Kimasihi na kudumisha viwango vyake vya juu vya mwenendo. Lakini kuna wengine wenye kujionea wenye mfano wa kondoo watakaoona kwamba tunawakilisha Ukristo wa kweli. Mwenendo wetu mwema utawavutia, nao watajiunga nasi katika kuhubiri “habari njema hizi za ufalme.” (Mathayo 24:14, NW) Tunakuwa wenye furaha kama nini wakati watu hao wanapomtukuza Yehova pamoja na sisi wakiwa mashahidi wake!
21. Mashahidi wa Yehova wanapaswa kufanya mapenzi ya Mungu wakiwa na nia gani?
21 Basi, fanya kazi na mapenzi ya Yehova kwa moyo wote. (Mathayo 22:37) Tambua kwamba kila Shahidi wa Yehova apaswa kuwa akimsifu Mungu wakati wote. “Sifuni Yah, enyi watu! Sifu Yehova, O nafsi yangu. Nitamsifu Yehova wakati wote wa maisha yangu.” (Zaburi 146:1, 2, NW) Ndiyo, ‘msifu Yehova wakati wote wa maisha yako.’ Na huo wakati wote wa maisha unaweza kuwa ni milele, endapo hutasahau kamwe kuwa wewe ni shahidi.—Kutoka w 6/1/84.
Wewe Umgejibuje?
◻ Ni pendeleo gani kubwa zaidi ambalo mtu anaweza kufurahia duniani?
◻ Yesu Kristo alikuwaje mfano kwa mashahidi wa Yehova leo?
◻ Mashahidi wa Yehova wote wana mgawo gani wa lazima?
◻ Je! mahali pa huduma ya shambani yako ya kawaida pachukuliwe na utoaji wa ushuhuda wa vivi hivi?
◻ Kuna uhusiano gani kati ya mwenendo wetu na utoaji wetu wa ushuhuda?
[Picha katika ukurasa wa 19]
Yesu hakusahau kamwe alikuwa shahidi wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 20]
Kwa bidii toa ushuhuda katika huduma ya shambani ya kawaida na katika utoaji wa ushuhuda wa vivi hivi