Sababu Gani Iwe Hivyo?
SABABU gani dhuluma imeenea sana? Maandiko mawili katika Biblia yanasaidia kutujibu ulizo hilo. La kwanza limo katika Yeremia sura ya 10, mstari wa 23, na linasema hivi:
“Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”
Hilo linaonyesha kwamba mwanadamu hakupewa uwezo wa kujisimamia mwenyewe. Kwa sababu gani? Kwanza, kwa sababu kwa kuzaliwa yeye ni mwenye dhambi. Mungu mwenyewe alisema: “Mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.” (Mwanzo 8:21) Ndiyo sababu sheria na desturi za mwanadamu zinaendeleza aina zote za uonezi. Kwa mfano, wengi wanapendelea kula sumu kupitia sigara au kutengeneza silaha zenye kuruka angani za kuangamiza watu wengi badala ya kuwapa maji masafi yaliyo matamu au chakula cha kutosha wale wenye uhitaji.
Pia mwanadamu hana hekima ya kutosha. Kwa hiyo, kama ilivyokuwa kwa kisa cha Roi, sheria zilizokusudiwa ziwe za haki zaweza kuelekeza kwenye dhuluma mbaya sana. Ingawa watu wengi mmoja mmoja na matengenezo mengi yanafanya kazi kwa bidii ili kuleta haki katika afya, ugawanyaji wa chakula na hali za kiuchumi, hawawezi kufanya hivyo. Katika visa vingi, hawajui jinsi ya kufanya hivyo.
Ukweli ni kwamba mwanadamu hakukusudiwa ‘ajielekeze,’ au ajisimamie akiwa na mamlaka au uhuru kamili. Alikusudiwa asimamiwe na mamlaka ya juu zaidi, Mungu, Na kwa kuwa, katika historia, watu wengi wamekataa utawala wa Mungu, nguvu nyingine kubwa ya kiroho imejiingiza iwaongoze. Roho hiyo inatajwa katika andiko la pili linalosaidia kueleza sababu ya wingi mkubwa wa dhuluma leo. Linasema:
“Ulimwengu wote unatawaliwa na yule Mwovu.”
Hayo ni maneno ya mtume Yohana. (1 Yohana 5:19, HNWW) “Yule mwovu” ni nani? Kwa wazi ni Shetani Ibilisi, ambaye pia anaitwa “mungu wa huu mfumo wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4, NW) Shetani na mashetani wake ni wenye nguvu sana zaidi yetu. Hawapendezwi kuona kukiwapo wingi wa haki. Kwa kweli, maadamu kuna dhuluma, watu wanaondoshwa kwenye njia ya kumtafuta Mungu, na wengine hata wanamlaumu kwa ajili ya dhuluma. Kwa hiyo, dhuluma inatimiza vizuri kusudi la Shetani.
Biblia inatuambia hivi: “Kwa kuwa [Yehova] hupenda haki, wala hawaachi watauwa wake.“(Zaburi 37:28) Basi, ni kwa sababu gani akaruhusu wanadamu wajitawale wenyewe na kuwa chini ya uongozi wa Shetani, na kwa hiyo wapatwe na dhuluma na uovu mwingine? Makala inayofuata itazungumza jambo hilo.