Kukabili Kipindi Hiki cha Jeuri kwa Uhakika
“Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu mwenyewe amesema! Ni nani ambaye hatatabiri?—AMOSI 3:8, New World Translation
1. (a) Kwa habari ya jina la Yehova, tuna pendeleo gani zuri ajabu? (b) Yesu na Paulo walikwezaje Yehova na jina lake?
“BWANA Yehova Mwenye Enzi Kuu”—Maneno hayo yanaeleza juu ya Mtawala Mkuu Zaidi ya Wote katika ulimwengu wote kwa njia nzuri kama nini! Tofauti na vipingamizi vya madhehebu, ni pendeleo kubwa sana kuita jina la Yehova, kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kutangaza jina la Yehova na makusudi yake kwa wengine. Mwanaye, Yesu, alipokuwa duniani alitangaza hivi: ‘Roho ya Yehova i juu yangu, niwahubiri maskini habari njema.’ Akitoa sala kwa Yehova, alisema hivi juu ya wanafunzi wake: “Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo.” Naye mtume Paulo, akitaja maneno ya manabii Waebrania wa kale, alisema: “Kila atakayeliitia Jina la [Yehova] ataokoka.”—Luka 4:18; Yohana 17:26; Warumi 10:13; Yoeli 2:32.
2. (a) Amosi alimsifuje sana Yehova? (b) Kupatana na maana ya jina la Amosi, yeye alipokea mgawo gani?
2 Amosi alikuwa mmojawapo wa manabii hao wa kale. Yeye alisifu sana jina la Yehova, usemi “Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu” ukionekana mara 21 katika kitabu chake cha Biblia. Jina Amosi maana yake ni “Kubeba Mzigo.” Kweli kweli, yeye alibeba mzigo mzito wa daraka, hali moja na mashahidi washikamanifu wa Yehova leo. Amosi alikuwa mchunga-kondoo na mkuza miti ya matunda, na inaelekea hakupewa mafunzo ya kazi yake ya kiunabii. Hata hivyo, kwa wazi alifahamiana sana na Neno la Mungu, na roho ya Yehova ilikuwa juu yake ili atimize mgawo wake mgumu. Ulikuwa nini? Ulikuwa kuondoka katika nchi ya kwao ya Yuda aende akiwa misionari wa ugenini kwenye Israeli wa makabila kumi ulioasi imani upande wa kaskazini. Huko, katika Israeli, mji wake mkuu ukiwa Samaria, alipaswa kutangaza ujumbe wa maangamizi usiopendwa na wengi.
3. Ni ‘jambo la siri’ gani lililofunuliwa kwa wakati wake kupitia Amosi?
3 Je! Amosi aliukataa mgawo wake? Hata! Hizo zilikuwa nyakati za jeuri, lakini watu walipaswa kujua kukaribia kwa “siku yenye msiba” hata zaidi. Jambo kubwa maishani mwao lilikuwa ni kula na kunywa. Wakiwa wamejilaza juu ya viti na vitanda vyao vya starehe, hawakumfikiria Yehova wala ibada yake ya kweli. (Amosi 6:3-6, NW) Yehova aliazimia kuwaadhibu, lakini kwanza ilikuwa lazima wapewe onyo la kiunabii. Kupatana na hilo, Yehova mwenyewe alitangaza hivi: “Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu hatafanya jambo hata moja isipokuwa amefunulia watumishi wake manabii jambo lake la siri.”—Amosi 3:7, NW.
Utimizo wa Kisasa wa Unabii Huo
4. (a) Kwa sababu gani unabii wa kale umehifadhiwa? (b) Maana ya unabii huo inajulishwa sasa kupitia kipitio gani?
4 Je! unabii huo wa kale una maana kwetu leo? Ndiyo, una ujumbe wenye mkazo sana kwetu sisi! Neno la Mungu aliloliongoza lilikusanywa chini ya uongozi wa kimungu, na limehifadhiwa mpaka “wakati wa mwisho” kwa ajili ya faida ya watu wa Mungu ambao ‘wamefikiliwa na miisho ya zamani.’ Tunajulishwa maana yake ya kiunabii kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” kile kikundi cha Wakristo waliopakwa mafuta ambacho, Bwana, Yesu Kristo, anatumia sasa kutoa ‘chakula cha kiroho kwa wakati wake’ kwa ajili ya watu wote wa Mungu.—Danieli 12:4; 1 Wakorintho 10:11; Mathayo 24:45-47.
5. Tunapaswa kuitikiaje usemi wa Yehova katika Amosi 3:8?
5 Je! tunaliona hilo ‘jambo la siri’ la unabii wa Amosi kuwa jambo la pili kwa umaana ambalo laweza kushughulikiwa katika wakati wetu wa ziada? Kama tungalikuwa peke yetu katika pori lisilo na kitu, halafu ghafula kimya kikatizwe na mngurumo wa simba, tungetendaje? Katika hali hiyo ya kufa au kupona, je, hatungechukua hatua mara moja? Hatungekawia! Basi je, hatupaswi kutenda vivyo hivyo kwa ajili ya semi za kiunabii za Yehova? Yehova mwenyewe anatangaza hivi: “Kuna simba ambaye amenguruma! Ni nani ambaye hataogopa? Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu mwenyewe amesema! Ni nani ambaye hatatabiri?” (Amosi 3:8, NW) Basi, ni jambo la lazima kwamba tujulishe wengine unabii huo na maana yake. Lakini jinsi gani?
“Nenda, Tabiri”
6. Jumuiya ya Wakristo inafanana na Samaria wa kale katika njia zipi?
6 Amri ya Yehova kwa Amosi ilikuwa hii: “Nenda, tabiri kwa watu wangu Israeli.” (Amosi 7:15, NW) Ufalme huo wa Israeli wenye kuasi imani unafanana leo na Jumuiya ya Wakristo, ambayo maoni yayo ni ya kimwili, inategemea jeuri au kutisha kufanya jeuri ili iendelee kuwapo, na ni yenye uadui kwa Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu, na inachukia jina lake. Kwa habari ya jina “Ukristo,” Jumuiya ya Wakristo inalivaa tu kama kibandiko, kwa maana inapinga Ufalme wa Kristo wa uadilifu unaokuja. Yesu mwenyewe anataja wale wa dini za Jumuiya ya Wakristo kuwa ‘watenda maovu.’—Mathayo 7:21-23.
7, 8. (a) Kuhukumiwa maangamizi kwa Jumuiya ya Wakristo ‘kumetangazwaje’ hatua kwa hatua miakani? (b) Ni “uhuru” gani ambao umetangazwa kwa ajili ya “mateka,” na matokeo yakawa nini?
7 Tangu kusimamishwa kwa Ufalme katika mbingu mwaka wa 1914, jamii ya kisasa ya Amosi, Mashahidi wa Yehova, wametangaza siku ya kisasi cha Mungu kote kote katika Jumuiya ya Wakristo. Onyo kamili lilisikizishwa nchi za Jumuiya ya Wakristo hasa tangu 1919 mpaka 1939, na jambo hilo linaendelea kufanywa mpaka wakati wetu huu. Miaka ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, 1939-45, ilikuwa wakati wa mateso kwa Mashahidi wa Yehova, lakini pia wakati wa kufanywa tengenezo tena. Mwaka wa 1943 Shule ya Gileadi ilianza kuzoeza wamisionari kwa ajili ya mashamba ya ugenini, na kufikia mwisho wa Vita Ulimwengu ya Pili walikuwa wakitumwa katika nchi baada ya nchi ili wapanue ushuhuda wa Ufalme. Kazi katika makao ya Jumuiya ya Wakristo ikapanuliwa kwa njia hiyo, hasa katika Italia, Ureno, Spania na eneo kubwa sana la Amerika ya Latini.
8 “Nenda, tabiri,” ulikuwa ndio mwito! Jamaa zenye kujitoa zilihama Kanada, Marekani, Visiwa vya Uingereza, Ulaya na Australia na visiwa vyake zijiunge na wamisionari katika maeneo mapya ambako uhitaji ulikuwa mkubwa. ‘Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu mwenyewe alikuwa amesema.’ Roho ya Yehova imekuwa juu ya mashahidi wake ili watangaze, duniani pote, “siku ya kisasi” cha Mungu juu ya Jumuiya ya Wakristo, na pia “mateka uhuru wao” kutoka kwa utumwa wa dini ya uongo. (Isaya 61:1, 2; Zekaria 4:6) Kwa hiyo, katika kipindi cha miaka 40, kulitokea ongezeko kubwa sana katika wastani wa kila mwezi wa Mashahidi wenye kuhubiri Ufalme: kutoka 109,794 mwaka wa 1943 mpaka 2,501,722 mwaka wa 1983.
Kielelezo cha Duniani Pote
9, 10. (a) Kadiri ya tangazo hilo katika siku za Amosi ilikuwa nini, na ni jambo gani linalolingana na hilo leo? (b) Kama ilivyofananishwa na unabii wa Amosi, wanaoitwa ati ni wapagani wamekuwa na maoni gani kuhusu Jumuiya ya Wakristo?
9 Huko ni kufuata kielelezo cha siku za Amosi, wakati ambao tangazo la maangamizi lilipaswa kusikizishwa pia katika Ashdodi—makao makuu ya ibada ya kipagani karibu na Filistia—na mbali mpaka Misri. Kwa maana Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu alikuwa amesema hivi: “Tangazeni habari katika majumba ya Ashdodi, na katika majumba ya nchi ya Misri, mkaseme, Kusanyikeni juu ya milima ya Samaria, katazameni, ni mishindo mikubwa kama nini iliyomo humo, na udhalimu mwingi kama nini uliomo ndani yake. Kwa maana hawajui kutenda haki, asema [Yehova], hao wawekao akiba ya jeuri na unyang’anyi katika majumba yao.”—Amosi 3:9, 10.
10 Hali moja na hiyo, tangazo la kisasa la kisasi cha Yehova kitakachofikilizwa juu ya Jumuiya ya Wakristo limeenea mbali na kupita makao yake—kote kote Afrika, visiwa vya bahari na sehemu nyingi za nchi za Mashariki. Kwa kuwa Misri inatumiwa katika Biblia kuwa mfano wa ulimwengu wote mbovu uliotenganishwa na Mungu, basi ujumbe wa maangamizi ya Jumuiya ya Wakristo umetangazwa duniani pote. (Linganisha Isaya 19:19, 20.) Mengi ya yanayoitwa mataifa ya kipagani yanajua sana ‘mivurugo, udhalimu, udanganyifu, jeuri na unyang’anyi’ katika Jumuiya ya Wakristo. Katika karne nyingi wameona wamisionari wa Jumuiya ya Wakristo wakishiriki katika vita vinavyoletwa na maongozi ya kisiasa na mapinduzi na kuwa viongozi wa biashara ya kimataifa ya bunduki na madawa ya kurusha akili. Misionari wa Sosaiti yetu anapoanza kuzungumza na mfuasi wa dini ya Buddha, mara nyingi anakutana na kipingamizi: ‘Lakini ebu angalia hali ya kiadili ya Wakristo; sisi wafuasi wa dini ya Buddha tuna adili zilizo bora zaidi, basi kwa nini sisi tubadilike?’ Ni lazima misionari aonyeshe wazi kwamba dini ya Jumuiya ya Wakristo ni tofauti sana na Ukristo wa Biblia. Ni hapo tu anapoanza kusikilizwa.
11. Upotovu katika Samaria unafanana na nini leo?
11 Kama vile katika Samaria wa kale, ndivyo ilivyo katika Jumuiya ya Wakristo, kwa wanasiasa na maafisa, wakubwa kwa wadogo, “hawajui kutenda haki.” Zaidi ya hayo, katika nyingi ya zinazoitwa nchi za Kikristo, jeuri na uvunjaji wa sheria umejaa barabarani. (Mathayo 24:3, 12) Jambo hilo ni tofauti sana na hali zenye amani zaidi katika nchi nyingi “zisizo za Kikristo.”
12. Jumuiya ya Wakristo imekuwa ‘ikiwekaje akiba ya jeuri na unyang’anyi’?
12 “Jeuri na unyang’anyi” pia vinapangwa katika kadiri yenye kushtua katika mataifa yote. Yajapokuwa wachochezi wa vita vya ulimwengu viwili, ambavyo kwa sababu yavyo wana hatia ya damu ya mauaji ya wanadamu kama 69,000,000, mataifa ya Jumuiya ya Wakristo hayajaacha kufanya hivyo. Sasa Jumuiya ya Wakristo ni sehemu ya mng’ang’ano kati ya mataifa mawili yenye nguvu nyingi zaidi, “mfalme wa kusini” na “mfalme wa kaskazini,” na kwa sababu hiyo mataifa yake yanaunga mkono kujaribiwa kwa silaha za nyukilia zenye kuua katika maeneo yake yote.
13. Wateteaji wa kisiasa wa jeuri wameshirikije kutimiza Danieli 11:40 na Luka 21:25?
13 Alipotembelea Japani, mnenaji mkuu wa “mfalme wa kusini” alitangaza hivi: “Faida pekee ya kuwa na silaha za nyukilia ni kuhakikisha haziwezi kutumiwa—kamwe.” Basi kwa sababu gani wanazo? Ni kwa sababu Shetani, mungu wa ulimwengu huu, amenasa mataifa katika hali mbaya ambayo katika hiyo hawawezi kuponyoka. Katika kujibu ‘kusukuma’ (NW) kwa “mfalme wa kusini,” mnenaji mkuu wa “mfalme wa kaskazini” alitangaza kuelekezwa kwa makombora ya nyukilia yenye kwenda umbali wa kadiri kwenye bara la Marekani kwa “kuyaweka kwenye vituo vya bahari.” Yote hayo yanatimiza unabii wa Yesu kuhusu “huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea kwa sababu ya uvumi wa bahari na msukosuko wake.”—Danieli 11:40; Luka 21:25, NW; Ufunuo 12:9, 12.
14. Hali hiyo na matokeo yake inatukumbusha juu ya matukio katika siku za Noa katika njia zipi?
14 Tangu siku za Noa wanadamu hawajaelekewa kama leo na uharibifu, pamoja na hatari ya jeuri kubwa zaidi. Maandishi ya kihistoria ya wakati wa Noa yanasema: “[Yehova] akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote. . . . Dunia ikaharibika mbele za Mungu, dunia ikajaa dhuluma [jeuri, NW].” Kwa sababu ya uovu na jeuri hiyo, Yehova aliwaharibu waovu kwa njia ya Gharika. Kwa mara nyingine, leo, yeye anakusudia “kuwaharibu hao waiharibuo [dunia].”—Mwanzo 6:5-13; Ufunuo 11-18; Luka 17:26, 27.
Jumuiya ya Wakristo Kuliwa Nyara
15. Yehova alisababishaje “adui” afikilize hukumu juu ya Samaria?
15 Mwisho wa mpambano kati ya mataifa ya ulimwengu yenye nguvu nyingi zaidi utakuwa nini? Yehova anasema jambo fulani juu ya hilo, kama tusomavyo katika Amosi 3:11: “Basi, haya ndiyo asemayo [Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu]; Atakuwako adui, kuizunguka nchi pande zote; naye atazishusha chini nguvu zako zikutoke; na majumba yako yatatekwa nyara.” Huyo “adui” ni nani? Huko nyuma katika siku za Amosi “adui” huyo alikuwa Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru. Jeshi lenye nguvu nyingi la Ashuru liliongozwa na Yehova na kutumiwa naye kama “fimbo” ya mfano ili kutekeleza hukumu juu ya Samaria wenye kuasi imani, kama inavyosimuliwa katika Isaya 10:5, 6: “Ole wake Ashuru! fimbo ya hasira yangu, ambaye gongo lililo mkononi mwake ni ghadhabu yangu! Nitamtuma juu ya taifa lenye kukufuru, nitampa maagizo juu ya watu wa ghadhabu yangu, ateke nyara, na kuchukua mateka, na kuwakanyaga kama matope ya njiani.”
16. (a) Ufunuo sura ya 17 inasimuliaje mpambano wenye kufanana na huo leo? (b) Ni matukio gani yanayodokeza kwamba kuhukumiwa maangamizi kwa Jumuiya ya Wakristo kumekaribia?
16 Kwa jinsi iyo hiyo, Yehova ataleta Mwashuri wa kisasa mwenye silaha nyingi awe “fimbo” na “shoka” lake ili kuua Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi imani. Kweli kweli, milki yote ya ulimwengu ya dini ya uongo, Babeli Mkuu, kwa wakati huo mmoja itafanywa ukiwa na “pembe” kali—mamlaka za kisiasa zenye jeshi ambazo hata sasa ni mataifa yaliyo washiriki wa Umoja wa Mataifa. (Isaya 10:15; Ufunuo 17:5, 16, 17) Vishindo vya mpambano huo unaokaribia vinasikiwa mara nyingi katika taarifa za habari za wakati huu. Kwa mfano, hivi karibuni gazeti U.S.News & World Report lilisema hivi: “Si katika Polandi tu ambako Ukatoliki na Ukomunisti zinaelekea kupambana. Ulaya yote ya Mashariki, uhusiano kati ya kanisa na tawala za Kikomunisti umekuwa wa ugomvi tangu John Paul wa Pili ambaye ni mzaliwa wa Polandi alipokuwa Papa mwaka wa 1978. Hali mpya ya kivita inaonekana wazi kati ya maaskofu wa Katoliki ya Roma katika mataifa [yaliyo chini ya Urusi]. . . . Kung’ang’ania kwa Papa kwa uthabiti kusudi la Katoliki kumezidisha hali hiyo ya mpambano. . . . Serikali za Kikomunisti zinaonyesha wazi zina mashaka na Papa.”
17. Kitabu cha Amosi, na pia unabii mbalimbali mwingine, kinasema nini juu ya kuliwa nyara kwa dini ya uongo?
17 Kwa hiyo itatokea kama vile tu Yehova anasema katika Amosi 3:15: “Nyumba za pembe zitaangamia, nazo nyumba kubwa zitakuwa na mwisho, asema [Yehova].” Utajiri na mali za Jumuiya ya Wakristo zitafanywa ukiwa, pamoja na zile za makao yote ya dini ya uongo.—Ezekieli 7:19; Ufunuo 18:15-17.
18. (a) Ni tendo gani la kiburi ambalo “” atachukua halafu? (b) Jambo hilo litatokeza nini haraka-haraka na matokeo yawe nini kwa watu wa Yehova?
18 Hata hivyo, je, hiyo itamaanisha kufunguliwa mara moja kwa watumishi washikamanifu wa Yehova—kutokana na masuto, mateso, maonezi ambayo ulimwengu wa Shetani unamimina juu yao? Bado! Kwa maana “Mwashuri” mwenye akili ya kisiasa—ile “fimbo” na “shoka” ambalo Yehova anatumia kufikiliza hukumu juu ya Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi imani—atajiinua kwa kiburi kumpinga Yehova kwa kugeukia mashahidi wake waaminifu hapa duniani. Lakini wapi! (Isaya 10:15-19) Kama Yohana mtume alivyoona katika njozi, ‘wafalme wa dunia,’ mamlaka za kisiasa za “mnyama” wa UM, watakusanyika wafanye vita na ‘Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,’ ambaye ni Mfalme aliyetawazwa wa Mungu. Hiyo ndiyo itakayokuwa ishara ya Har–Magedoni, “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” Itaangamiza majeshi yote ya Shetani duniani na kuleta wokovu kwa ‘kila anayeliitia jina la Yehova.’—Ufunuo 16:14, 16; 19:11, 16, 19-21; Warumi 10:13.
19. Mfano wa Amosi na utimizo wa unabii wake juu ya Samaria wapasa kutia uhakika gani ndani yetu?
19 Basi, je, wewe unakabili namna gani kipindi hiki cha jeuri? Bila shaka kwa uhakika thabiti kwamba Yehova atatetea Neno lake la kiunabii! Na tukiwa tumeazimia kama Amosi, ambaye alihubiri ujumbe usiopendwa na wengi kwa watu wenye kuasi imani! Lakini wewe mwenyewe unawezaje kuokoka uingie na kufurahia Utaratibu Mpya ulio mzuri sana ambao Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu anatayarishia wale wanaompenda? Makala ifuatayo itajibu ulizo hilo.
Maulizo ya Kurudia:
◻ Amosi alikuwaje mfano mzuri kwetu katika kukabili nyakati zenye jeuri?
◻ Ni ‘jambo gani la siri’ ambalo sisi tumependelewa ‘kutangaza’ sasa?
◻ Ni kwa njia zipi Samaria wa kale unafananisha Jumuiya ya Wakristo?
◻ Kipindi hiki cha jeuri kitamalizikaje, na ni nini kinachoonyesha kwamba jambo hilo liko karibu?
[Picha katika ukurasa wa 8]
Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu alimtuma mchunga-kondoo Amosi atangaze ujumbe usiopendwa na wengi
[Picha katika ukurasa wa 11]
Kwa Babeli Mkuu, ‘Mwandiko uko Ukutani’