“Vita Si Yenu Bali Ni ya Mungu”
“Mwaminini [Yehova]... ndivyo mtakavyofanikiwa.”—2 MAMBO YA NYAKATI 20:20.
1. Yehoshafati anamfananisha Yesu aliyetawazwa katika njia zipi?
YEHOSHAFATI wa Yuda alikuwa mfalme mwema. ‘Hakuacha kufanya yaliyo mema machoni pa Yehova.’ (2 Mambo ya Nyakati 20:32) Jina lake linamaanisha “Yehova Ni Hakimu.” Yeye alikweza jina la Yehova, akamtumaini yeye ampe uongozi katika njia ya uadilifu na ampe msaada wa kuhukumu watu Wake. Alihakikisha kwamba waliagizwa katika sheria ya Yehova.Yeye binafsi alienda kati ya Wayudea kuwatia moyo warudie ibada ya Yehova ya kweli. Alifanya ufalme huo uwe tengenezo kwa ajili ya ibada ya kitheokrasi. Katika yote hayo, kwa kufaa yeye anafananisha Mfalme, Yesu Kristo, aliyetawazwa karibuni katika kiti chake cha ufalme mwaka wa 1914 na ambaye anakusanya sasa watu wa Yehova kwa ajili ya wokovu, huku majeshi ya kishetani yakikusanya mataifa kuelekea kwenye vita ya mwisho ya Har–Magedoni.—Mathayo 25:31-34; Ufunuo 16:13, 14, 16.
2. (a) Ni hatari gani kubwa iliyowatokea Wayudea? (b) Ni hali gani kama hiyo ambayo Mashahidi wa Yehova wanakabili leo? (c) Ni sehemu gani za ulimwengu wa Shetani zinazofanana na Amoni, Moabu na Mlima Seiri?
2 Yehoshafati alipokwisha kushughulikia kurudisha tena utaratibu wa kitheokrasi katika Yuda, hatari kubwa ilitokea. Adui mwenye nguvu nyingi, “jamii kubwa,” alikuja kutoka sehemu za Amoni, Moabu na Mlima Seiri, akaleta hatari ya kuangamiza watu wa Mungu. (2 Mambo ya Nyakati 20:1, 2, 22) Hali ya leo ni kama hiyo. Mashahidi wa Yehova, wakiwa “si wa ulimwengu,” wanachukiwa na ulimwengu wa Shetani na mara nyingi wanateswa kwa ukatili na maadui wa Mungu. (Yohana 15:19; 1 Yohana 5:19) Utawala juu ya nchi ya watu wa Mungu—Yuda (maana yake ikiwa, “Sifa”)—lilikuwa ndilo suala katika wakati wa Yehoshafati. Lakini wakati huu, kwa kufuata kielelezo cha Amoni na Moabu wa kale, mamlaka za kisiasa za wakati huu na biashara kubwa-kubwa (kutia wenye kutengeneza silaha za “siku ya maangamizi”) wanang’ang’ania utawala wa ulimwengu. Kwa kufanya hivyo, wanaingilia kinguvu pia makao yaliyo kwa haki mali ya Ufalme wa Mungu wa Kimashihi, tangu mwaka wa 1914. (Ufunuo 11:15, 18) Mlima Seiri wa kale ulikuwa kiti cha utawala wa Edomu wenye kuasi imani, wazao wa ndugu-pacha wa Yakobo, Esau. Basi, kwa kufaa, wana wa Mlima Seiri walifananisha waasi-imani wenye kiburi wa Jumuiya ya Wakristo leo.—Mwanzo 32:3.
3. Tendo la Yehoshafati na Wayudea linafananaje na lile la Mashahidi washikamanifu leo?
3 Sasa akiwa anahatirishwa na majeshi hayo yenye kushambulia, Mfalme Yehoshafati angeweza kufanya nini? Haya basi, watumishi washikamanifu wa Yehova hufanya nini sikuzote wanapokabili hatari, mateso au kuhatirishwa kwa maisha zao? Yehoshafati ‘alielekeza uso wake amtafute Yehova.’ Na kutoka miji yote ya Yuda watu ‘wakaja kumtafuta Yehova’ katika nyumba yake ya ibada ya kweli.—2 Mambo ya Nyakati 20:3-5.
4. (a) Watu wa Yehova wanaweza kutazamia hali gani? (b) “Mkutano mkubwa” wenye kuendelea kuongezeka unategemea wokovu kutoka wapi?
4 Huo ni mfano mzuri kama nini kwa watu wa Mungu leo! Kipindi hiki cha jeuri kinasonga kuelekea upeo wacho kwenye Har–Magedoni. Hali katika ulimwengu wa Shetani hazitapungua jeuri. (2 Timotheo 3:1, 13) Mara nyingi, maisha yenyewe ya watu wa Yehova huenda yakawa hatarini. Tutapata wapi ulinzi? Unapatikana katika umoja wetu wa ibada. Kwenye Majumba ya Ufalme yetu na vituo vingine vya funzo la Biblia, tunakutana tule chakula cha kiroho chenye kuendeleza uhai na kupanga utumishi wetu wa peupe wa kumsifu Yehova. Kwa furaha, “mkutano mkubwa” unaendelea kujitokeza, kutoka mataifa yote, ili ujiunge na watu wa Mungu katika “utumishi mtakatifu” (NW) wao. Wapya hao wanamiminika kwenye ‘mlima wa nyumba ya ibada ya Yehova.’ Kufanya hivyo kunamaanisha wokovu wao pia.—Ufunuo 7:9, 15; Isaya 2:3, NW.
5. “Ua mpya” wa Yehoshafati unadokeza nini kuhusiana na tengenezo la Yehova leo?
5 Yehoshafati ‘alisimama nyumbani mwa Yehova, mbele ya ua mpya.’ Kwa wazi mpango wa ujenzi wa mfalme huyo katika Yuda ulikuwa ni pamoja na kupanua majengo ya ibada kwenye hekalu la Yerusalemu. Vivyo hivyo leo, chini ya uelekezo wa Mfalme, Yesu Kristo, anayetawala sasa, mpango bora sana wa ujenzi wa kiroho umeendelea, hata kwamba katika ua wa kidunia wa hekalu la Yehova kuna nafasi ya kutosha kwa ajili ya mamilioni ya “mkutano mkubwa” wasio wa kikuhani. Inapendeza kama nini kuwa humo!—Zaburi 27:1-5.
Kumgeukia Yehova
6. (a) Ni mambo gani yaliyotiwa ndani ya sala ya Yehoshafati? (b) Tunaweza kupataje nguvu nyakati za majaribu?
6 Kwenye nyumba ya Yehova, Yehoshafati aliliweka jambo lote mbele ya Mungu wake katika sala. Yeye alikiri Uufalme wa Yehova, uwezo na ukuu, na alirudia kazi za Yehova kwa ajili ya watu wake. Alitaja sala ya bidii ya Sulemani wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu na kwa unyenyekevu akamalizia kwa kusema: “Hatujui tufanyeje; lakini macho yetu yatazama kwako.” (2 Mambo ya Nyakati 20:5-12; 6:12-14, 34, 35) Je! wewe umepata kuwa katika hali kama hiyo—wakati ilipoonekana hakuna mahali pa kugeukia? Katika nyakati za mitume, mara nyingi Paulo alikuwa katika hali za shida kama hizo. Alilazimika kumtegemea sana Yehova. Lakini sikuzote angeweza kusema, “Niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu.” Kwa maana wakati alipojisikia hoi kabisa, utegemeo wake kamili kwa Yehova ukawa chanzo cha nguvu zisizoshindika. Wewe, pia, unaweza kuwa mwenye nguvu!—2 Wakorintho 12:10; Mithali 18:10.
7. Wayudea hao walikuwa wakitii agizo gani la Musa?
7 Kama unaweza, ebu wazia, tamasha huko kwenye eneo kubwa la hekalu katika Yerusalemu: “Wakasimama Yuda wote mbele za [Yehova], pamoja na wadogo wao, na wake zao, na watoto wao.” (2 Mambo ya Nyakati 20:13) Bila shaka walikumbuka agizo la moja kwa moja la Musa juu ya kusudi la makusanyiko kama hilo, kama ilivyoandikwa katika Kumbukumbu la Torati 31:12. Palikuwako nafasi ya kusimama tu kwenye kusanyiko hilo kubwa, wakati jamaa hizo zilipokuwa zikimngojea Yehova kwa heshima, zikiwa chonjo na tayari kufanya agizo lake.
Kipitio cha Yehova
8. Tambulisha kipitio cha kuleta habari (a) katika siku za Yehoshafati (b) katika siku zetu.
8 Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu angejibuje sala ya Yehoshafati? Yehova alitoa kipitio cha kuleta habari. Mleta-habari huyo alikuwa Yahazieli, wa kabila la Lawi. Ingawa Yahazieli hakuwa kuhani, Yehova alimchagua atangaze mojawapo ujumbe wenye kuchochea zaidi wa kutia moyo katika Maandiko yote. Jambo la maana lilikuwa kwamba ‘alijiliwa na roho ya Yehova, katikati ya kusanyiko.’ (2 Mambo ya Nyakati 20:14) Je! Yehova ametoa kipitio chenye kufanana na hicho katikati ya watu wake leo? Kwa hakika, amefanya hivyo! Yesu alitaja hilo katika unabii wake wa “umalizio wa mfumo wa mambo” (NW) kuhusiana na jamii iliyopakwa mafuta ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” ambaye Bwana anampa amana “vitu vyake vyote” hapa duniani.—Mathayo 24:3, 45-47.
9. (a) Jina la Yahazieli lilifaa jinsi gani? (b) Ujumbe wa Yehova ulikuwa nini, na jambo hilo linatutia moyo sisi wakati huu jinsi gani?
9 Jina la Yahazieli maana yake ni “Mungu Huona.” Kweli kweli Mungu angeweza kuona yote yaliyohusika katika hatari hiyo. Angeweza kutangulia kuona mwendo ambao watu wa Mungu walipaswa kuchukua. Yeye angeweza kuona matokeo ya mwisho. Kwa hiyo, Yehova aliwapasha ujumbe gani kupitia Yahazieli? Sikiliza! Ulikuwa huu: “Sikieni, Yuda wote, nanyi mkaao Yerusalemu, na wewe mfalme Yehoshafati; [Yehova] awaambia hivi, Msiogope, wala msifadhaike kwa ajili ya jeshi kubwa hili; kwani vita si yenu bali ni ya Mungu.” (2 Mambo ya Nyakati 20:15) Lo! lazima umati huo wenye umoja uwe ulifurahi sana! Na jinsi tunavyofurahi leo kujua kwamba, hata Shetani na vibaraka wake atushambulie jinsi gani—hata imani na ukamilifu wetu ujaribiweje—sisi, kama jamii ya watu wenye umoja, tunaweza kuweka utegemeo wetu kamili kwa Yehova, tukiwa na uhakika kwamba yeye atatupigania vita!—Kutoka 15:2, 3; Zaburi 24:8; 37:3-7; Zekaria 14:3.
Tendo la Umoja Linatakiwa!
10. (a) Wayudea hao walipaswa kukabili jaribu gani la ukamilifu? (b) Ni kazi gani inayoongoza mpaka kwenye ‘tendo la ajabu’ la Yehova?
10 Hata hivyo, Wayudea hao hawakuwa wasimame tu bila kufanya lo lote, wakingojea wokovu wo wote ambao Yehova angeleta. Walipaswa kuwa jamii ya watu wenye kutenda! Ni lazima waonyeshe utii kwa Yehova na kufanya mambo kwa njia yake endapo wangeokoka. Bila shaka wengi wao walikuwa na maoni kwamba maagizo yaliyotoka kwa Yehova kidogo yalikuwa yasiyo ya kawaida. Jambo hilo liliujaribu ukamilifu wao. Vivyo hivyo, kabla Yehova hajatenda ‘kazi yake ya ajabu, tendo lake la ajabu,’ katika kuharibu Jumuiya ya Wakristo mwanzoni mwa “dhiki kubwa,” anataka mashahidi wake washiriki kwa umoja katika kazi ambayo huenda ikaonekana kuwa ya ajabu kwa wengi. Ni utumishi mtakatifu wao wa kwenda kwenye nyumba za watu, tena na tena, ili kuwaonya juu ya uharibifu unaokaribia.—Isaya 28:21; Mathayo 24:14, 21.
11, 12. (a) Ni amri gani ya ajabu iliyotolewa na Yahazieli, lakini Wayudea waliitikiaje? (b) Sisi, pia, tunawezaje kuonyesha utegemeo kwa Yehova?
11 Jambo hilo linaonyeshwa na maagizo yaliyotolewa na Yahazieli kwa watu wa Yuda. Akizungumza juu ya majeshi ya adui, alisema: “Kesho shukeni juu yao. . . . Hamtahitaji kupigana vita, jipangeni, simameni, mkauone wokovu wa [Yehova] ulio pamoja nanyi, enyi Yuda na Yerusalemu; msiogope, wala msifadhaike; kesho tokeni juu yao; kwa kuwa [Yehova] yu pamoja nanyi.” (2 Mambo ya Nyakati 20:16, 17) Umati huo usio na silaha wa wanaume, wanawake na watoto uliamriwa utoke dhidi ya majeshi yaliyoungana ya adui!—Linganisha Zaburi 148:12, 13.
12 Yehoshafati na Wayudea walithamini sana uelekezo aliotoa Yehova kupitia Yahazieli. “Yehoshafati akainama kichwa, kifulifuli; wakaanguka mbele za [Yehova] Yuda wote na wakaao Yerusalemu, wakimsujudia [Yehova].” (2 Mambo ya Nyakati 20:18) Yehoshafati Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, alionyesha utegemeo huo wa kujitiisha kwa Yehova alipokuwa angali duniani, na tunaweza kuwa na uhakika atakuwa akimtegemea Yehova apewe maagizo ya vita wakati ‘Yehova katika mkono wake wa kuume; ataseta wafalme, siku ya ghadhabu yake.’ (Zaburi 110:5, 6) Hali moja na hiyo, Mashahidi wa Yehova leo wanafurahi ‘kumsujudia’ Mungu wanayetumaini, huku wakitumikia katika nyua zake.—Zaburi 84:10-12; 122:1-4.
13. Ni nani leo, wanaomsifu Yehova “kwa sauti kuu sana,” na matokeo yamekuwa nini?
13 Kulingana na 2 Mambo ya Nyakati 20:19, waimbaji wa hekalu “wakasimama ili wamsifu [Yehova], Mungu wa Israeli, kwa sauti kuu sana.” Na ni nani, leo, chini ya uelekezo wa mabaki wapakwa mafuta, wanaotumia “sauti kuu sana” kumsifu Yehova mbele ya maadui wake? Hakika mbele kabisa ya watu wa Yehova ni kikundi chenye kuendelea kupanuka cha wahudumu mapainia. Mapainia wasaidizi na wa kawaida, mapainia wa pekee na wamisionari—wale wanaoongoza katika kumsifu Yehova nje shambani—waliongezeka kwa asilimia 19 mwaka wa 1983. ‘Kuimba’ kwao kulitimiza sehemu kuu sana ya saa za kustaajabisha 436,720,991—ongezeko la asilimia 13.5—zilizotumiwa katika huduma ya Kikristo mwaka-jana.
14. Kwa kufuata mfano wa Wayudea, wengi sasa wanaonyeshaje imani kwa matendo?
14 Huko Yerusalemu haukuwa wakati wa mtu kusinzia-sinzia. Kwa kutii, watu hao “wakaamka asubuhi na mapema, wakaenda nje katika jangwa la Tekoa.” (2 Mambo ya Nyakati 20:20) Walitaka sana kuonyesha imani yao kwa matendo. (Linganisha Yakobo 2:14.) Vivyo hivyo, wahudumu wa Mungu leo mara nyingi wanahitaji kuanza kazi yao mapema. Mapainia ambao ni wake wa nyumbani na wengine ni lazima waamke mapema waangalie kazi za nyumbani ili wapate kutumia asubuhi nzima katika utumishi wa Yehova. Kuna watu huko nje katika ulimwengu wa Shetani ‘wanaougua na kulia,’ na ambao lazima watiwe alama ya wokovu waipite “dhiki kubwa.” Mashahidi wa Yehova wameazimia kuwapata.—Linganisha Ezekieli 9:4.
Haya Songeni Mbele Kwenye Vita!
15. (a) Wayudea walipaswa kuweka imani yao katika nani? (b) Tunawezaje ‘kufanikiwa’ leo?
15 Maandishi katika 2 Mambo ya Nyakati 20:20 yanaendelea kusema: “Walipokuwa wakitoka, Yehoshafati akasimama, akasema, Nisikieni, enyi Yuda nanyi wenyeji wa Yerusalemu; mwaminini [Yehova], Mungu wenu, ndivyo mtakavyothibitika; waaminini manabii wake, ndivyo mtakavyofanikiwa.” Hali moja na hiyo, kichwa cha kundi la Kikristo, Mfalme wetu ambaye sasa anatawala, amewapa watu wake kitia-moyo kikubwa wawe waaminifu. Tunakiona katika vifungu kama hivi vifuatavyo: Mathayo 10:27, 28; 24:9-13; Yohana 16:33. Imani katika Yehova, imani katika wale anaotumia kuwa wanenaji, ndiyo, imani katika tengenezo lake! ‘Tunapotoka’ kwenda kwenye utumishi wa Yehova leo, ni jambo la maana kama nini tuwe na imani kama hiyo! Hiyo ndiyo njia hakika ya kufanikiwa—ya kufikiwa na Mashahidi wote waliojiweka wakfu na kubatizwa ambao wana imani katika Yehova na mipango yake. Hiyo ni pamoja na uandalizi wake bora sana wa uzima wa milele, uliowezeshwa kupitia dhabihu ya Mwanaye.—Yohana 3:16; 17:3.
16. (a) Ni ‘waimbaji’ gani ambao mara nyingi wanaongoza kwenda nje katika utumishi? (b) Wote wanamsifuje Yehova katika “uzuri wa utakatifu”?
16 Na zaidi, Yehoshafati alifanya “shauri na watu, akawaweka wale watakaomwimbia [Yehova], na kumsifu katika uzuri wa utakatifu, wakitoka mbele ya jeshi, na kusema, Mshukuruni [Yehova]; kwa maana fadhili zake ni za milele.” (2 Mambo ya Nyakati 20:21) Hapo waimbaji wa hekaluni waliongoza katika kwenda vitani. Hali moja na hiyo, chini ya uelekezo wa mabaki wapakwa-mafuta kuna mapainia na wamisionari, waangalizi wasafirio na wake zao, pia wale wanaotumikia katika makao ya Betheli, na pia wazee wa kundi na watumishi wa huduma, ambao mara nyingi wanakuwa mbele kabisa katika kufanya utumishi mtakatifu, wakiwachochea kwenye utendaji wale wote wanaoshirikiana na makundi. Wote hao wanampa Yehova sifa “katika uzuri wa utakatifu,” wakipiga hatua kwenda nje katika utaratibu wa kitheokrasi. Uzuri [pambo, NW] wao wa kiroho ni pamoja pia na ‘utu mpya wa Kikristo, unaoonyesha haki na utakatifu wa kweli.’ (Waefeso 4:24; Wagalatia 5:22, 23) Ni pendeleo kama nini leo kuwa sehemu ya wasongaji-mbele hao wa duniani pote, wenye kutukuza jina la Yehova na fadhili za upendo!—Zaburi 144:1, 2; 136:1-26.
17. (a) Kwa sababu gani watu wa Mungu ‘hawakuhitaji kupigana vita’? (b) Ni “shauri” gani la Yehova linaloleta maangamizi kwa dini ya uongo?
17 Yehova alikuwa amewaambia watu wake hivi: “Hamtahitaji kupigana vita.” Na ndivyo ilivyokuwa. “Walipoanza kuimba na kusifu,” Yehova akaweka waoteaji dhidi ya majeshi yenye kuja kushambulia, hata ‘wana wa Amoni, na Moabu, na wa mlima Seiri, waliokuja juu ya Yuda; wakapigwa.’ (2 Mambo ya Nyakati 20:17, 22, 23) Jambo hilo linaonyesha waziwazi kama nini linalokaribia kuupata ulimwengu wa Shetani! Kama kitabu cha Ufunuo 17:16, 17 kinavyoonyesha, Yehova ana “shauri” juu ya Babeli Mkuu, Jumuiya ya Wakristo ikiwa sehemu yake yenye lawama zaidi. Yeye atafanya mataifa-washiriki wa wa kijeshi wa Umoja wa Mataifa wawe na “shauri” ilo hilo, kwa kugeukia dini ya uongo, ili kuifanya ukiwa na kuiharibu. Mfumo mkubwa wa kuasi imani wa Jumuiya ya Wakristo, kama wale Waedomi kutoka Mlima Seiri, utapondwa kabisa!
18. Amoni na Moabu wa kisasa zitaharibiwaje katika Har–Magedoni?
18 Lakini, huo sio mwisho wa mambo! Amoni na Moabu ya kisasa zingali zitakuwa zimebaki! (Linganisha Ufunuo 18:9, 10, 15-17.) Wangali watakuwa na nia ya kuwaharibu wasifaji wa Yehova, ambao ndio Wayudea wa leo. Lakini utakuwa umefika wakati wa Yehova kufikiliza hukumu. Kama ambavyo Ufunuo 19:11-16 unavyosimulia, Mfalme, Yesu Kristo, atatoka ili ‘akanyage shinikizo la mvinyo ya ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi,’ aharibu sehemu zilizobaki za mfumo wa ulimwenguni pote wa Shetani. Kwenye upeo wa vita kuu hiyo, mabaki yenye wazimu ya mataifa ya kisiasa na vibaraka wao wa kijeshi bila shaka watapigana wao kwa wao kwa kutumia silaha zao za kuangamiza. Ndivyo ilivyokuwa kwa Amoni na Moabu, ‘walipojitia kuharibu kila mtu mwenziwe.’ Lakini Yehova hatawaruhusu kamwe watumie vifaa vya nyukilia kufikia kadiri ya kuharibu watu wa Mungu au kazi ya mikono yake, dunia yetu.—Ufunuo 11:18; Isaya 45:12, 18; Zaburi 115:16.
19. (a) Wayudea wa kisasa wataitikiaje waangaliapo uwanja wa vita? (b) Ni nini kinachofananishwa na ‘kukusanyika katika bonde la Baraka’?
19 “Hata Yuda walipofika mnara wa kulindia wa jangwani, wakalitazama hilo jeshi; nao, angalia, walikuwa maiti walioanguka nchi, wala hapana aliyeokoka.” Wakati ‘Wayudea’ wa kisasa, pamoja na waabudu wenzi wao, watakapoangalia matokeo ya vita ya Har–Magedoni, watamsifu Yehova kwa ajili ya ushindi huo mkubwa. Hawatahitaji kula nyara halisi, lakini watafurahi kukusanyika katika “bonde la Baraka” la mfano. Kwa furaha, “mkutano mkubwa” usio wa kikuhani utaingia katika dunia iliyosafishwa, chini ya utawala wa Ufalme, wakiwa wanatazamia sana pendeleo lao linalokuja—kuifanya dunia iwe bustani iliyo paradiso. Kwa miaka elfu moja makao ya kifalme ya Yehoshafati Mkuu Zaidi, Yesu Kristo, hayatakuwa na matata yo yote, na Mungu wake, Yehova, ataendelea kutoa pumziko kote kote.—2 Mambo ya Nyakati 20:24-30.—Kutoka w7/1/84.
Kurudia 2 Mambo ya Nyakati 20
◻ Ni nani leo wanaofanana na majeshi ya Amoni, Moabu na Mlima Seiri?
◻ Ni nani wanaofananishwa na Yehoshafati, Yahazieli na Wayudea?
◻ Wayudea wa kisasa wameitikiaje vizuri?
◻ Ni jambo gani linalotupa uhakika juu ya yatakayokuwa matokeo ya “dhiki kubwa”?
[Picha katika ukurasa wa 14, 15]
Kama Yehoshafati, Yesu aliyetawazwa sasa anasaidia watu wa Mungu ‘wafanikiwe’ katika kumsifu Yehova