Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 1/1 kur. 11-16
  • Kujenga kwa Vitu Visivyoweza Kuchomwa na Moto

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujenga kwa Vitu Visivyoweza Kuchomwa na Moto
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwenye Kujenga Ni Nani?
  • Weka Msingi Unaofaa
  • Vile Vifaa Visivyoweza Kuchomwa na Moto
  • Je! Watasimama “Moto” Ukiwapata?
  • Je, Kazi Yako Itastahimili Moto?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Kujenga Nyutu Za Kikristo Katika Watoto Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Kuwasaidia Watu Wamkaribie Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Unapofundisha, Fikia Moyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 1/1 kur. 11-16

Kujenga kwa Vitu Visivyoweza Kuchomwa na Moto

“Wengine watatumia dhahabu au fedha au mawe ya thamani kujenga juu ya msingi; wengine watatumia mti au majani au nyasi kavu”​—1 WAKORINTHO 3:12, Today’s English Version.

1, 2. (a) Ni jambo gani lingeumiza moyo kuliko kuona nyumba ya mtu ikichomeka na kumalizika? Wahudumu Wakristo wanakatishwaje tamaa nyakati nyingine kwa njia inayofanana na hiyo?

KWA uhakika ni jambo la kusikitisha wakati nyumba ya kupendeza inapochomeka na kumalizika. Lingekuwa jambo la kuhuzunisha zaidi kama wewe ndiwe ungekuwa umeijenga! Kuona kitu ulichoshughulikia wakati wako wote na kujitahidia kikichomeka kungekuwa jambo la kuumiza sana moyo. Hata hivyo maumivu hayo si kitu yakilinganishwa na yale yanayopata mzazi Mkristo ambaye mwana au binti yake anaacha ukweli afuate mambo ya ulimwengu. Ni mambo machache yangeweza kuumiza mtu kuliko kuona mtoto wake akiingia katika uharibifu huo wa kiroho.

2 Maoni ya moyoni ya wazazi hao huenda yakafanana kidogo na hali ya kukata tamaa ambayo wewe uliye mhudumu Mkristo huenda ukawa ulipatwa nayo. Labda ulianza funzo la Biblia pamoja na mtu kisha ukatumia miezi au hata miaka ukimsaidia kufikia maarifa ya ile kweli. Unamwona akihudhuria mikutano na hata akianza kushiriki katika huduma ya shambani. Lakini, kwa ghafula, analegea kiroho na kuwa asiyetenda, labda hata kurudia mazoea mabaya ya zamani. Inakatisha tamaa kama nini!

3. Kwa kuelekeana na hali kama hizo, kwa kawaida ni maulizo gani yanayotokea, na majibu yanategemea nini?

3 Linalosikitisha ni kwamba jambo hilo linatukia mara kwa mara. Kwa hiyo ni kawaida kuuliza hivi: Kwa sababu gani linatukia? Tunaweza kufanya lo lote kuzuia jambo hilo? Ingawa huenda hali ya moyo wa mtu mwenyewe ikawa sababu, kwa kadiri fulani majibu ya maulizo hayo yanategemea jibu la ulizo jingine: Unapofundisha wengine, je! wewe unajenga juu ya msingi unaofaa kwa vitu visivyoweza kuchomwa na moto? Tunapoelewa wazi maana ya kufanya jambo hilo na namna ya kulifanya, hiyo inakuwa njia ya kusaidia wale tunaofundisha​—wanafunzi wetu wa Biblia na watoto wetu​—wasimame imara katika ukweli.

Mwenye Kujenga Ni Nani?

4. Kwenye 1 Wakorintho 3:10, 11, Paulo anafananisha mhudumu Mkristo na nani, na namna gani?

4 Katika kujibu, tunageukia 1 Wakorintho sura ya 3, ambapo Paulo anafananisha mhudumu Mkristo na mjenzi. Tunasoma: “Kwa kadiri ya neema ya Mungu niliyopewa, mimi, kama mkuu wa wajenzi mwenye hekima, naliuweka msingi, na mtu mwingine anajenga juu yake. Lakini kila mtu na aangalie jinsi anavyojenga juu yake. Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Yesu Kristo.”​—Mistari 10, 11.

5. (a) Kulingana na maneno yanayozunguka habari inayohusika, ni ujenzi wa namna gani unaozungumzwa na Paulo? (b) Mhudumu Mkristo ‘anajenga’ watu katika maana gani?

5 Paulo anasema juu ya ujenzi wa namna gani? Basi, angalia maneno yanayozunguka habari hiyo: “Ninyi ni. . . jengo la Mungu.” “Ninyi mmekuwa hekalu la Mungu.” (1 Wakorintho 3:9, 16) Kwa hiyo ni kazi ya ujenzi wa mfano, unaohusu watu. Ndiyo kusema, mhudumu Mkristo ‘anajenga’ watu katika maana ya kwamba anajaribu kujenga katika watu wanaopendezwa utu wa Kikristo, kuwafanya wawe wanafunzi.​—Mathayo 28:19, 20, NW.

6, 7. (a) Maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 3:9-15 yanakaza fikira juu ya daraka la nani? (b) Hata hivyo, ujenzi wa muungano unahusikaje? (c) Kufikiria zaidi maneno ya Paulo kutatusaidia kuona nini?

6 Je! hiyo ni kuonyesha kwamba mwalimu Mkristo ndiye mwenye daraka peke yake juu ya ukuzi wa mwanafunzi? Hata kidogo. Kwanza, sisi ni “wafanya kazi pamoja na Mungu.” Ingawa maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 3:9-15 yanakaza fikira juu ya daraka la mwenye kujenga, au mwenye kufundisha, kwa kweli ni ujenzi wa muungano ambamo hata mwanafunzi anahusika. Tunaweza kuulinganisha na kutayarisha askari kwa ajili ya pigano. Huenda wengine wakamzoeza na kumpa vifaa, lakini askari akiisha kwenda katika pigano lazima yeye apige vita, akitumia mambo ambayo amejifunza. Uhai wake wenyewe unategemea kufanya hivyo! Vivyo hivyo, mwenye kufundisha anajaribu kujenga Mkristo halisi, mmoja anayeweza kupinga mikazo na vishawishi vya mfumo huu. Hata hivyo, wakati uo huo mwanafunzi ana daraka; lazima atumie katika maisha yake mambo anayojifunza.​—Mathayo 7:24-27; Wafilipi 2:12, 13.

7 Ingawa hivyo, uhakika unabaki wa kwamba mwenye kufundisha ana daraka zito. Tunapozidi kufikiria maneno ya Paulo, tutaona umaana wa kufundisha Neno la Mungu kwa matokeo mazuri ili kujenga katika wengine uthamini kwa Baba yetu wa kimbingu.

Weka Msingi Unaofaa

8. Katika ujenzi huu wa mfano, msingi ni nini?

8 Kabla hujaweza kusimamisha jengo, lazima kwanza uweke msingi. Kwa hiyo katika ujenzi wa kufanya wanafunzi, msingi ni nini? Paulo anajibu: “Msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Yesu Kristo.” (1 Wakorintho 3:11) Ndiyo, msingi unaofaa ambao tunapaswa kujenga juu yake ni Yesu Kristo.​—Linganisha Waefeso 2:20-22 na 1 Petro 2:4-6.

9. (a) Katika kufundisha wengine, ni nini linalohusika katika kuweka Kristo awe msingi? (b) Kwa sababu gani ni jambo la maana wanafunzi wetu wa Biblia waelewe ukweli mzima juu ya Yesu?

9 Tunaweza kuwekaje Kristo awe kama msingi tunapofundisha wengine? Kwanza, lazima tufundishe ukweli juu ya Yesu na kusaidia wengine wajenge maisha zao kwa kutegemea ukweli huo. Hiyo ni pamoja na kuwasaidia wamwamini Yesu kuwa Msaidiaji wetu na Yeye ambaye kupitia kwake Yehova anatoa ukombozi. (Mathayo 20:28; 1 Yohana 2:1, 2) Lakini si hilo tu. Yesu Kristo ndiye kichwa kilichowekwa cha kundi la Kikristo. (Wakolosai 1:18) Yeye ndiye Mfalme pia anayestahili kutawala dunia, na akiwa katika cheo hicho ‘atamaliza ushindi’ wake karibuni kwenye Har–Magedoni. (Ufunuo 6:1, 2) Basi, kwa wazi kuweka Kristo awe msingi kunahusu kufundisha ukweli mzima juu yake, kusaidia wengine waelewe daraka la Yesu katika utimizo wa kusudi la Mungu. Kwa sababu gani hilo ni jambo la maana sana? Wanafunzi wetu wakimwamini Yesu kuwa Mfalme anayetawala wa Mungu, hawatavunjwa moyo kwa wepesi na hali za ulimwengu na matatizo ya maisha ya kila siku.​—Isaya 28:16; 1 Petro 2:6-8.

10. (a) Kulingana na Waefeso 3:17-19, ni nini zaidi linalohusika katika kuweka Kristo kuwa msingi? (b) Tunaachaje Kristo ‘akae katika mioyo yetu’?

10 Lakini, mambo mengi zaidi ya hayo yanahusika katika kumweka Kristo awe msingi. Inatupasa tuwe na lengo lile lile alilokuwa nalo mtume Paulo. Sala yake kwa ajili ya Waefeso ilikuwa kwamba “Kristo akae kupitia imani yenu katika mioyo yenu kwa upendo; ili mwe na mizizi na kusimamishwa juu ya msingi, mpate kuweza kabisa kushika kwa akili pamoja na watakatifu wote ulio upana na urefu na kimo na kina, na kuujua upendo wa Kristo unaopita maarifa, ili ninyi mpate katika kila jambo kujawa na ujazi wote ambao Mungu anatoa.” (Waefeso 3:17-19, NW) Angalia kwamba ‘kuwa na mizizi na kusimamishwa juu ya msingi’ kunahusu kuwa na Kristo ‘akikaa katika mioyo yetu.’ Hiyo maana yake nini? Kristo ‘anakaa katika mioyo yetu’ tunapoacha mfano na mafundisho yake yaongoze maoni na matendo yetu.

11, 12. (a) Tunaweza kusaidiaje wengine waache Kristo ‘akae katika mioyo yao’? (b) Zaidi ya kujifunza juu ya Yesu, ni jambo gani jingine linalohusika?

11 Tunaweza kusaidiaje wale tunaofundisha waache Kristo ‘akae katika mioyo yao’? Kuingiza maarifa ndani yao kunahitajiwa kabisa, kwa maana wanapaswa “kushika kwa akili” “upana na urefu na kimo na kina” cha ukweli wa Neno la Mungu, hasa kama unavyohusiana na maisha na mafundisho ya Yesu Kristo. Tunataka wanafunzi wetu wajipatie “nia ya Kristo,” wamjue sana sana kuwa mtu aliye hai, mwenye fahamu za kujisikia. (1 Wakorintho 2:16) Hilo litagusa mioyo yao.

12 Lakini angalia kwamba Paulo alisema hivi pia: “Na kuujua [Kigiriki, gnonaiʹ, kujua “kwa kutenda, kupitia kupatwa na jambo lenyewe hasa”] upendo wa Kristo unaopita maarifa.” Tunaweza kujua “upendo” wa Kristo kwa kujifunza inayoyasema Biblia juu ya mwendo wa maisha yake na namna alivyoshughulika na wengine. Lakini, ni kwa kuiga utu wa Yesu kwamba tunaweza kuthamini kikweli maoni yake. Kwa njia hiyo, kwa kupatwa na jambo lenyewe hasa, tunapata kujua “upendo wa Kristo unaopita maarifa.”

13, 14. (a) Tunaweza kusaidiaje wanafunzi wetu waige sifa za Yesu? (b) Kwa sababu. gani kujaribu kuwa kama Yesu kutasaidia wanafunzi wetu wakuze uhusiano mwema pamoja na Yehova? (c) Zaidi ya kukaza fikira juu ya kuweka msingi unaofaa, ni jambo gani jingine ambalo lazima tukazie fikira?

13 Kwa hiyo unapoweka msingi, elekeza fikira za mtu kwenye sifa za Yesu​—upendo wake (Yohana 15:13, 14), uchangamfu na kujisikia (Mathayo 11:28-30), unyenyekevu (Yohana 13:1-15) na huruma (Marko 6:30-34), hizo zikiwa ni chache tu kati yazo. Mtie mwanafunzi wako moyo aige sifa hizo katika njia yake ya maisha. Kufanya hivyo kutatokeza msingi mzuri wa kujengea sifa nyingine za maana. Nyakati nyingine, mnapozungumza masimulizi ya Biblia juu ya Yesu, huenda ukahitaji kutua na kuuliza: ‘Wewe unaona Yesu akionyesha sifa gani? Wewe unaweza kuonyeshaje sifa hii kwa ukamili zaidi katika maisha yako?’ Eleza kwamba kuiga utu wa Yesu kutasaidia mwanafunzi wa Biblia akuze uhusiano wenye nguvu na wa kindani pamoja na Yehova. Namna gani hivyo? Kwa sababu Yesu alifuata kwa ukamilifu sana utu wa Baba yake hivi kwamba tunapojaribu kuiga Yesu tunakuwa hasa tukimwiga Yehova mwenyewe!—Yohana 14:9.

14 Kuwa na msingi unaofaa ni jambo la maana, lakini unatosha? Paulo anajibu: “Lakini acheni kila mmoja aendelee kuchunga namna yeye anajenga juu yake.” Ndiyo, viko namna gani vifaa tunavyotumia katika kusimamisha jengo litakalokaa juu ya msingi?

Vile Vifaa Visivyoweza Kuchomwa na Moto

15, 16. (a) Kwenye 1 Wakorintho 3:12, ni wazi Paulo anaonyesha utofautiano gani? (b) Kwa kutumia mfano wa Paulo, ni ulizo gani linaloulizwa?

15 Hiyo inatuleta kwenye mstari wa 12 wa 1 Wakorintho sura ya 3, ambapo Paulo alizungumza vifaa mbalimbali vya kujengea: “Lakini kama mtu akijenga juu ya msingi huo, dhahabu au fedha au mawe ya thamani, au miti au majani au manyasi.” Hakika hivyo ni vifaa vingi vinavyotofautiana! Je! Paulo anapendekeza tujenge kiasi kidogo cha kila kifaa ndani ya wanafunzi wetu? Inaonekana sivyo. Angalia namna tafsiri nyingine zinavyosema: “Wengine watatumia dhahabu au fedha au mawe ya thamani kujenga juu ya msingi; wengine watatumia mti au majani au nyasi kavu.” (TEV) “Juu ya msingi huu mnaweza kujenga kwa dhahabu, fedha na mawe ya thamani, au kwa mti, majani na nyasi kavu.” (The Jerusalem Bible) Kwa hiyo ni wazi Paulo anatofautisha namna mbili za majengo. Kwa upande mmoja tunaweza kusema kuna jumba zuri la kifalme lililopambwa dhahabu, fedha na vito vya thamani nyingi. Tofauti na hilo kuna kijumba kilichoezekwa kwa majani ambacho kimejengwa kwa mbao au vigingi vinavyotegemeza kuta za nyasi kavu zilizochanganywa na matope.

16 Basi, kwa kutumia mfano wa Paulo, ulizo ni hili: Katika kufundisha wengine, wewe unajenga “majumba ya kifalme” au “vijumba vya nyasi”? Sababu inayofanya vijana wengine na wapya-wapya waanguke huenda ikawa kwamba si wote wanaojengwa kwa vifaa vile vile. Tofauti ni nini? Hali iliyokuwa katika kundi la kale katika Korintho inaonyesha tofauti kati ya kujenga kwa vifaa visivyoweza kuchomwa na moto na vile vinavyochomeka.

17, 18. (a) Ni tatizo gani zito lililokuwa katika kundi huko Korintho wa kale, na Paulo alinyoshaje mambo? (b) Kwa hiyo ni jambo gani kuu la kuamua kama tunajenga kwa “dhahabu” au “majani”?

17 Paulo alikuwa ametimiza sehemu yake katika kuweka msingi unaofaa, lakini inaonekana wengine katika Korintho walikuwa wakijenga juu ya msingi huo kwa ‘miti, majani na manyasi’​—vifaa hafifu vinavyofananisha sifa zisizo za kudumu. (1 Wakorintho 3:12) Hivyo, Paulo alilazimika kuandikia ndugu wa huko hivi: “Mafarakano yako kati yenu. Ninalomaanisha ni hili, kwamba kila mmoja wenu anasema: ‘Mini ni wa Paulo,’ ‘Lakini mimi ni wa Apolo,’ ‘Lakini mimi ni wa Kefa,’ ‘Lakini mimi ni wa Kristo.’ Kristo yuko akiwa amegawanyika.” (1 Wakorintho 1:11-13, AW) Kwa hiyo washiriki wa kundi waligawanyika katika vikundi-vikundi. Na kwa sababu gani? Kwa sababu walihesabia wanadamu fulani ubora wa kupita kiasi. Paulo aliwanyosha, akaeleza: “Basi Apolo ni nani? na Paulo ni nani? Ni wahudumu ambao kwao mliamini . . . Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu.”​—1 Wakorintho 3:5-7.

18 Kwa ufupi, tatizo lilikuwa hili: Kwa sababu walihesabia wanadamu ubora wa kupita kiasi kwa kuwafuata, washiriki wengine wa kundi katika Korintho hawakuwa na uhusiano wa kindani wenye nguvu pamoja na Yehova. Hilo ni jambo kuu katika kujua kama tunajenga kwa “dhahabu” au “majani,” kama tunajenga “majumba ya kifalme” au “vijumba vya nyasi” vya mfano.

19. (a) Nikwanjiaganihuendamwenyekufundisha akaelekeza fikira nyingi mno kwake mwenyewe au kwa mwanadamu mwingine bila kukusudia? (b) Ikiwa tunataka kujenga kwa ‘dhahabu, fedha na vito vyenye thamani,’ lazima tujaribu kufanya nini?

19 Kuna somo lenye thamani la kujifunza kutokana na habari hiyo. Huenda watu fulani wakasema, ‘Lakini mimi sifundishi wengine kufuata mwanadamu ye yote.’ Lakini, tunaweza kufanya hivyo kwa wepesi ingawa silo kusudi letu. Kwa mfano, ikiwa wakati mwanafunzi anapouliza maulizo tunasema-sema,‘Ndugu (au Dada) Fulani husema kwamba . . . ,” je! huenda bila kukusudia tukawa tunaelekeza fikira nyingi mno kwenye mwanamume au mwanamke asiye mkamilifu? Au ikiwa wakati maulizo yanapoulizwa tunasema, ‘Mimi sijui sana, lakini ningesema hivi,’ je! huenda bila kutaka tukawa tukivuta fikira nyingi mno kwetu wenyewe? Kumbuka, ni jambo jepesi sana kwa mwanafunzi kukuza maoni ya kumtukuza mwalimu wake. (Linganisha Matendo 10:25, 26 na Ufunuo 19:10.) Ikiwa tunataka kujenga “majumba ya kifalme,” tunahitaji kujiangalia tusijenge wafuasi wa wanadamu. Badala ya hivyo, lazima tusaidie wanafunzi wetu wakuze uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Ili kutimiza kusudi hilo lazima tujenge kwa ‘dhahabu, fedha na vito vyenye thamani.’ Hivyo vinafananisha nini?

20. ‘Dhahabu, fedha na mawe ya thamani’ vinafananisha nini? (Mithali 3:13-15)

20 Ulinganisho wa maandiko kama Zaburi 19:7-11, Mithali 2:1-6 na 1 Petro 1:6, 7 unaonyesha kwamba dhahabu, fedha na vito vyenye thamani vinatumiwa nyakati nyingine kwa njia ya mfano kufananisha sifa mbalimbali, kama imani yenye nguvu, hekima ya kimungu, utambuzi wa kiroho, ushikamanifu, uthamini wenye upendo kwa Yehova na sheria zake. Sifa hizo zinahitajiwa kabisa ili mtu awe na uhusiano wa kindani wenye nguvu pamoja na Yehova Mungu. Sifa hizo zinafanyiza ujenzi wa utu ambao lazima tujenge katika wale tunaofundisha. Je! wewe unafundisha kwa njia hiyo?

Je! Watasimama “Moto” Ukiwapata?

21. (a) Kwa sababu gani ni jambo la maana sana tujenge sifa za kudumu katika wale tunaofundisha? (b) “Moto” unafananisha nini?

21 Kwa sababu gani ni jambo la maana sana tusaidie kujenga sifa hizo za kudumu katika wale tunaofundisha? Mtume Paulo anaendelea kueleza hivi: “Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani.” (1 Wakorintho 3:13) Kwa hiyo “moto” utathibitisha ni kwa njia gani hasa sisi tunajenga. Hapa “moto” unafananisha nini? Je! ni mateso ya kimwili yenye jeuri? Ni wazi sivyo. Kwa maana angalia kwamba “kazi ya kila mtu” itapitishwa kwenye “moto.” Si Wakristo wote wanaopata mateso yenye jeuri. Kwa hiyo “moto” unafananisha mkazo wo wote au kishawishi cho chote kinachoweza kuharibu hali ya kiroho ya mtu.

22. Ni mengine gani kati ya majaribu ya mfano wa moto ambayo yanaweza kupata watu fulani?

22 Kwa wengine huenda “moto” ukaja katika namna ya suala la kutokuwamo. Kwa mfano, huenda wengine wakakazwa washiriki katika utendaji mbalimbali wa kisiasa au sivyo wafungwe gerezani. (Yohana 15:19) Nyakati nyingine huenda “moto” ukaja kwa njia ya werevu zaidi. Labda ni kishawishi cha kutazama sinema au vipindi vya televisheni vinavyoonyesha ngono na jeuri. Kwa vijana Wakristo huenda “moto” ukaja katika namna ya kuweza kusumbuliwa-sumbuliwa ili wafanye ngono, kukaribishwa-karibishwa watumie dawa za kulevya au kukazwa washiriki katika tafrija ya ulimwengu inayoshusha tabia. Ile tamaa ya asili ya kutaka kukubaliwa na wengine inaweza kukaza sana vijana Wakristo wakubaliane na wenzao.​—1 Yohana 2:16.

23. (a) Kwa habari ya kuelekeana na majaribu hayo, ni maulizo gani yanayotokezwa, na majibu yanategemea nini? (b) Ni jambo gani litakalozungumzwa katika makala inayofuata?

23 Wakristo wa kweli walio wengi wameshinda majaribu hayo ya mfano wa moto. Lakini, jambo la kusikitisha ni kwamba wengine wameshindwa. Kwa hiyo, tunahitaji kujiuliza: Wakati wapya ambao tumefundisha watakapoelekeana na “moto,” itakuwaje kwao? Je! watakuwa kama lile jumba zuri la kifalme lililopambwa kwa dhahabu, fedha na mawe ya thamani yasiyoweza kuchomwa na moto, kisha wasimame imara? Au watakuwa kama kile kijumba kilichojengwa kwa miti, majani na manyasi, kisha wachomeke? Bila shaka, mengi yanategemea mwanafunzi mwenyewe. Ingawa hivyo, wakati ule ule mengi yanatutegemea sisi walimu​—namna sisi wenyewe tumejenga. Kwa hiyo ulizo hili linabaki: Wewe unajengaje sifa hizo za kudumu katika wale unaofundisha? Hilo litazungumzwa katika makala inayokuja.

Wewe Unaweza Kueleza:

◻ Namna ujenzi wenye muungano unavyohusika katika kufundisha wengine?

◻ Namna unavyoweka Kristo kuwa “msingi”?

◻ Ni mambo gani mtu anaweza kujifunza kutokana na lililotukia katika kundi la Korintho wa kale?

◻ “Moto” ni nini, na namna hilo linavyokazia umaana wa kujenga sifa za kudumu katika wengine?

[Picha katika ukurasa wa 11]

When Unapofundisha wengine, je! unajenga kwa vitu visivyoweza au vinavyoweza kuchomwa na moto?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki