Kujenga Nyutu Za Kikristo Katika Watoto Wetu
MAMA ya Wanda, ambaye mume wake alikuwa amemwacha, alifanya bidii ili kujenga sifa za Kikristo katika binti yake. Kuzoeza huko kulijaribiwa wakati Wanda alipokuwa mwenye umri wa miaka 12. Wakati huo, Wanda, pamoja na ndugu na dada zake wachanga, walishurutishwa kuacha mama yake kwenda kuishi na baba yake kwa muda fulani. Baba yake hakuwa mwamini, kwa hiyo Wanda angetendaje wakati mama yake hakuwako kumtazama?
Jambo linalotukia kwa wazazi Wakristo wote ni wakati watoto wao wanapolazimika kufanya maamuzi peke yao, yanayojaribu imani yao wenyewe. Huenda watoto watenganishwe na wazazi wao, kama vile ilivyokuwa na Wanda. Huenda wakabiliane na mbano wa marika shuleni kufanya mabaya. Au huenda wakabiliane na vishawishi vyenye uvutano mwingi. Wazazi Wakristo hutumaini na kusali kwamba wakati huo ufikapo, watoto wao watakuwa na nyutu za Kikristo zilizo imara vya kutosha ili kulishinda jaribu.
Wazazi wanaweza kujengaje sifa za Kikristo zilizo imara katika watoto wao? Kabla ya kuona kilichompata Wanda, acheni tuone jinsi Biblia inatusaidia kulijibu swali hilo. Msingi wa jibu hilo unapatikana katika maneno haya ya mtume Paulo kwa Wakristo Korintho: “Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Yesu Kristo. Lakini kama mtu akijenga juu ya msingi huo, dhahabu au fedha au mawe ya thamani, au miti au majani au manyasi, kazi ya kila mtu itakuwa dhahiri. Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani.”—1 Wakorintho 3:11-13.
Msingi
Kwa nini Paulo aliandika maneno hayo? Alikuwa ameanzisha programu ya kujenga nyutu za Kikristo katika Korintho, lakini programu hiyo ilikuwa imepatwa na matatizo. Bila shaka, programu ya ujenzi ya Paulo haikuhusisha watoto wake wenyewe wa kimnofu. Ilihusisha wale ambao walikuja kuwa Wakristo kupitia kuhubiri kwake. Lakini aliwaona hao kuwa wazao wa kiroho, na yale aliyosema ni yenye thamani kwa wazazi pia.—1 Wakorintho 4:15.
Paulo alikuwa amekuja Korintho wakati fulani mapema na alikuwa ameanzisha kundi la Kikristo huko. Wale waliokuwa wameitikia kuhubiri kwake walikuwa wamefanya mabadiliko makubwa katika nyutu zao. Wengine walikuwa wamekuwa watu waliokosa maadili, wezi, wenye kuabudu sanamu, na walevi. (1 Wakorintho 6:9-11) Lakini waliweza kufanya badiliko ili kuwaza Kikristo kwa sababu Paulo alikuwa ameweka msingi mzuri. Msingi huo ulikuwa nini? “Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Yesu Kristo.”—1 Wakorintho 3:11.
Paulo aliwekaje msingi huo alipokuwa akifundisha waamini wapya hao katika Korintho? Atuambia hivi: “Mimi nilipokuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima. Maana naliazimu nisijue neno lo lote kwenu ila Yesu Kristo, naye amesulibiwa [ametundikwa kwenye mti, NW].” (1 Wakorintho 2:1, 2; Matendo 18:5) Hakuelekeza fikira kwake mwenyewe au kuipaka kweli umaridadi wa kuipa uvutio wa kiakili wa kijuujuu. Badala ya hiyo, alielekeza fikira kwa Yesu Kristo na njia ambayo huyo alikuwa ametumiwa na Mungu.
Kwa hakika, Yesu ni msingi imara wenye utukufu wa ujenzi wa Kikristo. Aliandaa dhabihu ya ukombozi. Sasa yeye ni Mfalme wa kimbingu na akiwa hivyo karibuni ataharibu adui za Mungu kwenye Har–Magedoni. Halafu atatawala kwa uadilifu wa Mungu kwa muda wa utawala wa miaka elfu moja, na akiwa Kuhani wa Juu wa Mungu, pole kwa pole atawainua jamii ya kibinadamu kwenye ukamilifu. Mtu angeweza kutaka msingi gani mwingine?
Hivyo, katika kujenga nyutu za Kikristo katika watoto wetu, tunafanya vizuri kumwiga Paulo na tuwe na hakika ya kwamba wao wathamini mambo hayo muhimu ya hakika. Kutoka uchanga wao, tunapaswa kuwafunza watoto wetu kumpenda Yesu kwa yale ambayo amefanya na anayoyafanya bado kwa ajili yetu.—1 Petro 1:8.
Ujenzi
Hata hivyo, ingawa Paulo alikuwa ameweka msingi huo mzuri, kazi ya ujenzi ilipatwa na vizuizi fulani baada ya yeye kuondoka. (1 Wakorintho 3:10) Tatizo halikuwa tofauti na lile linaloonwa na wazazi wengi leo. Wao huwalea watoto wao katika imani ya Kikristo na huhisi uhakika wa kwamba watoto wao wanafahamu kweli. Lakini wanapokuwa wa umri mkubwa zaidi, watoto hupeperuka au kukataa imani. Kwa nini? Mara nyingi ni kwa sababu ya vifaa vya ujenzi vilivyotumiwa.
Paulo alisema kwamba nyutu zaweza kujengwa kwa vifaa vya thamani: dhahabu, fedha, na mawe ya thamani. Au zaweza kujengwa kwa vifaa hafifu: miti, majani, na manyasi. (1 Wakorintho 3:12) Sasa, mjenzi akitumia dhahabu, fedha, na mawe ya thamani, ni lazima awe anajenga muundo ulio wa aina ya juu zaidi, wenye thamani ya kutokeza. Lakini mjenzi ambaye anatumia miti, majani, na manyasi anajenga ovyo tu, jengo la muda, na lililo hafifu.
Inaonekana kwamba vifaa hafifu vya kiroho vilikuwa vikitumiwa katika Korintho. Watu fulani ambao walikuwa wamefuatia kujenga juu ya msingi uliowekwa na Paulo walikuwa wakijenga kihafifu, bila kujenga miundo imara yenye kudumu. Wakorintho walikuwa wameanza kutegemea wanadamu, na kulikuwako kutengana, wivu, na ugomvi miongoni mwao. (1 Wakorintho 1:10-12; 3:1-4) Hayo yangeweza kuepukwaje? Kwa kutumia kwao vifaa vilivyo bora zaidi vyenye kudumu.
Hivyo vinafananisha sifa zenye thamani ambazo ni sehemu muhimu ya utu wa Mkristo. Sifa zipi? Mtume Petro alitaja moja: “Kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu.” (1 Petro 1:6, 7) Mfalme Sulemani alitaja mbili zaidi: hekima na utambuzi, ambazo kuwa nazo “ni bora kuliko biashara ya fedha.” (Mithali 3:13-15) Na Mfalme Daudi alitukumbusha kwamba hofu ya Yehova na uthamini wa amri zake “ni wa kutamanika kuliko dhahabu.”—Zaburi 19:9, 10.
Hivyo na vifaa vingine vyenye thamani vyaweza kujengwa katika nyutu za Kikristo ili kuwasaidia watoto wetu kuokoka majaribu. Lakini, tunaweza kuwaje na uhakika kwamba tunajenga kwa vifaa kama hivyo? Kwa kukazia mioyo fikira, ya watoto wetu na yetu wenyewe.
Kazi ya Ujenzi Iliyofanikiwa
Daraka ambalo moyo wa mzazi huwa nalo katika kazi hii ya ujenzi linaonwa katika amri iliyopewa na Yehova kwa wazazi katika taifa la kale la Israeli: “Maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako.” Halafu akaendelea kusema hivi: “Nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii.” (Kumbukumbu 6:6, 7) Hivyo, kabla ya sisi kuweza kujenga wengine, ni lazima tujijenge wenyewe. Watoto wetu wapaswa kuona katika yale tunayoyasema na kuyafanya kuwa utu wetu umefanyizwa kwa vifaa vinavyofaa.—Wakolosai 3:9, 10.
Kisha, kufundisha kwetu kunapasa kufikie mioyo yao. Yesu, mjenzi wa nyutu za Kikristo aliyefanikiwa zaidi, alifikia mioyo kwa kutumia vielezi na maswali. (Mathayo 17:24-27; Marko 13:34) Wazazi hupata kwamba njia zizo hizo za kufundisha zina matokeo mazuri sana. Wanatumia vielezi kufanya kweli za Kikristo zivutie mioyo ya watoto wao wachanga, nao hutumia maswali yenye kufikiriwa vizuri kutambua yale ambayo watoto wao wenye umri mkubwa zaidi wanafikiria kweli kweli, jinsi wanavyosababu mioyoni mwao.—Mithali 20:5.
Musa alipokuwa akijaribu kujenga katika Waisraeli tamaa ya kubaki waaminifu, alisema hivi: ‘Zishike amri za Yehova na sheria zake, mpate uheri.’ (Kumbukumbu 10:13) Vivyo hivyo, wazazi hufanya vyema si kueleza wazi tu viwango vya Mungu bali pia kuonyesha kwa kusadikisha ni kwa nini mambo kama ufuatiaji haki, usafi wa kiadili, na ushirika mzuri ni ya faida kwao.
Mwishowe, Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Watoto wapatapo ku-mjua Yehova binafsi kwenye umri wa mapema, kujifunza kusema naye juu ya matatizo yao, na kuwa na ono la yeye kuzijibu sala zao, wanakuza sehemu muhimu zaidi ya utu wa Kikristo: uhusiano wa kibinafsi pamoja na Muumba wao.
Moto
Paulo alipata kwamba wakati kazi ya ujenzi katika Korintho haikufanywa ilivyofaa, tabia za kilimwengu, kama vile mafarakano na fitina zilifanyiza shina. Hiyo ilikuwa hatari kwa sababu, kama alivyoeleza, “moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu.”—1 Wakorintho 3:13.
Moto huo ni nini? Waweza kuwa ni jaribu lolote ambalo Shetani huleta juu ya Mkristo. Huenda ikawa mbano wa marika, kishawishi cha kimwili, ufuatiaji wa mali, mnyanyaso, hata uvutano mkali wa shaka. Hakika majaribu kama hayo yatakuja. “Kazi ya kila mtu itakuwa dhahiri. Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto.” Wazazi wenye hekima hujenga nyutu za watoto wao wakitazamia kwamba watoto wao watajaribiwa na huwa na uhakika kwamba, kwa msaada wa Yehova, wao waweza kuokoka majaribu hayo. Wazazi wakiwa na mtazamo huo, watabarikiwa sana.
Ile Thawabu
Paulo alisema hivi: “Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu.” (1 Wakorintho 3:14) Mtume Paulo alipokea thawabu. Kwa Wakristo katika mji wa Thesalonike, ambapo alikuwa amefanya kazi ya ujenzi pia, aliandika hivi: “Tumaini letu, au furaha yetu, au taji ya kujionea fahari, ni nini? Je! si ninyi, mbele za Bwana wetu Yesu, wakati wa kuja kwake? Maana ninyi ndinyi utukufu wetu, na furaha yetu.”—1 Wathesalonike 2:19, 20.
Mama ya Wanda alikuwa na thawabu hiyo. Wanda mwenye umri wa miaka 12 alipojipata ametenganishwa na mama yake, mwanzoni alilia mpaka akalala. Halafu akakumbuka shauri la mama yake kuzungumza matatizo yake pamoja na Yehova katika sala. Alisali na upesi akawa na wazo la kuchunguza kitabu cha simu kuona kama kulikuwako Mashahidi wa Yehova wowote karibu. Aliwapasha habari na kujulishwa kwamba familia moja iliishi kwenye barabara hiyo chini kidogo tu kutoka kwenye nyumba ya baba yake. “Niliterema kama nini!” asema Wanda.
Akiwa na kitia moyo kutoka kwa familia hiyo, Wanda aliwaongoza ndugu na dada zake wachanga zaidi kurudia utendaji wa Kikristo. “Nilikuwa na daraka la kututayarisha kwa ajili ya mikutano,” aeleza. “Nilipaswa kufua nguo zetu, kuchana nywele zetu, na kuhakikisha tulikuwa safi na wenye kupendeza.” Ilikuwa kazi ngumu kwa msichana mchanga, lakini aliifanya. Wakati mmoja baba yake alijaribu kukomesha kuhudhuria kwao mikutano, lakini watoto walimsihi, naye akawaacha waende.
Baadaye, watoto hao waliungana tena na mama yao. Wanda alipokuwa mwenye umri wa miaka 15, akawa Mkristo aliyebatizwa, na hatimaye akaeleza juu ya tamaa yake yenye nguvu kuwa mmisionari. Naam, kazi ya mama ya Wanda ilipita jaribu. Alionea shangwe thawabu ya kuona binti yake akisimama imara peke yake kwa ajili ya kweli. Wazazi Wakristo wote na wafanikiwe vivyo hivyo wakiwa wanafanya kazi ya kujenga nyutu za Kikristo katika watoto wao.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
Ingawa, kama makala hii ionyeshavyo, wazazi hufanya bidii kujenga nyutu za Kikristo katika watoto wao, watoto wenyewe wana daraka pia. Wao, kama Wakristo wote, ni lazima wafanye kazi ya ujenzi ndani yao wenyewe. (Waefeso 4:22-24) Ingawa wazazi wana nafasi ya ajabu kusaidia katika jambo hilo, hatimaye kila mtu mmoja mmoja anapaswa kufanya uamuzi wake mwenyewe kumtumikia Yehova.