Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 4/1 kur. 18-22
  • Simama Imara Ushindane na Hila za Shetani!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Simama Imara Ushindane na Hila za Shetani!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Silaha Zetu za Kiroho
  • Sifa za Kikristo Zikiwa Misaada
  • Piga Moyo Konde Usimame Imara
  • Tunaweza Kuwapinga Roho Waovu Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Simama Imara Dhidi ya Hila za Shetani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • “Vaeni Suti Kamili ya Silaha Kutoka kwa Mungu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • “Vaeni Mavazi Kamili ya Silaha Kutoka kwa Mungu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 4/1 kur. 18-22

Simama Imara Ushindane na Hila za Shetani!

“Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani.”—WAEFESO 6:11.

MASHAHIDI walio wakfu wa Yehova ambao wanaishi kulingana na mapendeleo yao wanafurahia paradiso ya kiroho. Akisimulia hali yao ya kisasa kwa unabii, Isaya nabii wa Mungu aliandika hivi: “Ndipo hukumu itakaa katika jangwa, na haki itakaa katika shamba lizaalo sana. Na kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na matumaini daima.” —Isaya 32:16, 17.

Ili tuendeleze hali hiyo ya furaha, ni lazima tujihadhari daima, kwa maana Shetani Ibilisi anaona kijicho juu ya makao yetu ya kiroho yenye furaha na ufanisi. Karibuni akiwa Gogu wa Magogu atatokeza shambulio la kufa au kupona juu ya watu wa Yehova. (Ezekieli 38:8-12) Lakini yeye hajikalii kitako tu sasa hivi. Kwa kweli, akijua kwamba amebaki na kipindi kifupi tu cha wakati, amewakasirikia zaidi watumishi wa Yehova sasa kuliko hapo kwanza.—Ufunuo 12:12, 17.

Shetani ndiye anayeongoza ulimwengu huu wa wanadamu wasio waadilifu. (Waefeso 2:1, 2; 1 Yohana 5:19) Wote hao wako upande wake wa lile suala kuu la enzi kuu ya ulimwengu mzima. Wanatoa jibu hakika juu ya shaka lililotokezwa na Shetani kama wanadamu wo wote wanaweza kuendeleza ukamilifu wao kwa Yehova Mungu. (Mithali 27:11) Hata inapokuwa kwamba ni Wakristo wachache tu wanaothibitisha Ibilisi kuwa mjisifu mwenye kujigamba bure na mwongo mpujufu, jambo hilo linamkasirisha sana. Kwa hiyo anatumia kila hila, kila njia ya kiufundi aliyo nayo, awashinde watumishi hao waaminifu wa Yehova. Kwa hiyo, “tunako kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” —Waefeso 6:12, NW.

Basi, ingefaa ujiulize, ‘Mimi naweza kusimamaje imara nishindane na Adui huyo mwenye uwezo mwingi? ’ Kama vile tumeona, yeye anatumia udhaifu wa mwili wenye dhambi kunasa Wakristo. Huenda sisi binafsi tusiwe na udhaifu wa uvivu, lakini huenda tukawa wenye kiburi. Huenda tusiwe watu wa kujitia katika anasa kwa habari ya raha za kimwili, lakini huenda tukawa wenye pupa ya faida ya vitu vya kimwili. Hivyo tunahitaji kufanya bidii tushinde udhaifu wetu mbalimbali, tumpinge Ibilisi ili atukimbie.—Yakobo 4:7.

Silaha Zetu za Kiroho

Adui yetu anaendelea kutumia-tumia mara nyingi hila zile zile. Kwa hiyo kwa kujifunza Neno la Mungu tunaweza kuamshwa tuzione hila ambazo Shetani amekuwa akitumia tangu nyakati za Biblia, na tunaweza kujifunza namna ya kusimama imara tushindane naye. Mtume Paulo aliandika: “Vaeni suti ya silaha kamili kutoka kwa Mungu mpate kuweza kusimama imara kushindana na hila za Ibilisi.” Pia alisihi hivi: “Chukueni suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu, ili mpate kuweza kupinga sana katika ile siku mbovu na, mkiisha kuwa mmefanya mambo yote sana sana, msimame imara.” Angalia kwamba Paulo anakazia kuvaa “suti kamili kutoka kwa Mungu.” Ingekuwa hatari kukosa hata kipande kimoja cha silaha hizo zilizotolewa na Mungu, kwa maana Shetani angeona hivyo kisha aweze kushambulia mahali hapo penye ukosefu. Jambo hilo lingeweza kutuangamiza kiroho. —Waefeso 6:11, 13, NW.

Mtume anaanza kwa kutusihi hivi: “Simameni imara, basi, vikiwa viuno vyenu vimefungwa mshipi wa ukweli.” (Waefeso 6:14, NW ) Mshipi wa kijeshi wa nyakati za kale ulikuwa ukanda wa ngozi uliovaliwa kiunoni. Mara nyingi ulipambwa kwa vinundu vidogo vya madini, ukaleta ulinzi mwingi zaidi. Pia ulisaidia kushikilia upanga au kisu cha shujaa wa vita. Maana yake nini Mkristo kufungwa mshipi wa ukweli viunoni pake? Kufungwa mshipi wa ukweli wa Neno la Mungu maana yake ni kushikwa sana nalo, hivi kwamba tunaweza kutumia maandiko kujibu maulizo. Kama vile mshipi wa kijeshi ulivyokuwa ulinzi, ndivyo ukweli utakavyotupa sisi uhakika wa kuchukua mizigo yetu na kutulinda. Basi, pasipo shaka kushughulisha akili zetu na kweli za Mungu kutatusaidia tusimame imara kushindana na Shetani.

Halafu mtume anatuambia ‘tuvae bamba la chuma la kifuani la uadilifu.’ (Waefeso 6:14, NW ) Katika nyakati za Biblia bamba la chuma la kifuani lilikuwa na vitu kama magamba yaliyoungana ya madini ngumu na lilitumika kulinda moyo hasa. Ili kuvaa hilo bamba la kifuani la uadilifu ni lazima, juu ya yote, ‘tulinde mioyo yetu.’ (Mithali 4:23) Ni hapo tu tunapoweza kusimama imara tushindane na Shetani kwa kusukumwa tutumikie Yehova na kuishi maisha safi yatakayotuzuia tusiwe na mavutano machafu kati ya watu wa Yehova.—1 Petro 1:14-16.

Halafu Paulo anataja kwamba ‘nyayo zetu zivishwe vifaa vya habari njema za amani.’ (Waefeso 6:15, NW ) Linalomaanishwa hapo ni nini? Ni kwamba tuendelee kuwa watendaji sana katika kuuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa njia yenye amani, sawasawa na vile Yesu alivyowaagiza wale waeneza-evanjeli 70: “Nyumba yo yote mtakayoingia, semeni kwanza, Amani iwemo nyumbani humu.” (Luka 10:5) Sisi hatuendi kubishana na watu. Bali, tunaenda kuwapelekea faraja, furaha, amani ya akilini na tumaini. Shetani atajaribu kuchochea upinzani na ushindani katika wasikilizaji fulani ili kutufanya sisi tutende namna moja na wao. Basi, ili kusimama imara tushindane na njia za werevu za Shetani, tunahitaji kuwa wenye busara na subira, tuwe “hali zote kwa watu wote.”—1 Wakorintho 9:19-23.

Akiendelea kusema, mtume anashauri hivi: “Chukueni ngao kubwa ya imani, ambayo kwayo mtaweza ninyi kuyazima makombora yote yanayowaka moto ya mwovu.” (Waefeso 6:16, NW ) Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “ngao kubwa” hapo linamaanisha moja iliyo kubwa vya kutosha kuweza kulinda sehemu kubwa sana ya mwili. Kwa habari ya ‘makombora yanayowaka moto,’ nyakati nyingine Warumi walifanya vishale vya matete yenye shimo ndani vilivyokuwa na mahali pa kuwekea mafuta yenye kuwaka. Labda Paulo alikuwa akitaja vishale hivyo vyenye moto.

Shetani anarusha namna mbalimbali za ‘makombora yanayowaka moto’ kuwaelekea Wakristo. Kati ya “makombora” hayo kuna dhihaka, suto na uchongezi ambao adui za watu wa Mungu wanawaelekezea. “Makombora” hayo yanaweza pia kuwa jitihada za wengine kujaribu kuwavunja moyo mashujaa Wakristo kwa sababu ya kudhaniwa kwamba matokeo ya utendaji wao ni haba katika huduma au kudhaniwa hawana maendeleo katika kushinda udhaifu mbalimbali wa kimwili. Pia kuna maneno makali, mengine ya uchokozi na ya usingiziaji. Nyakati nyingine, Shetani amejeruhi Wakristo kwa kuamsha hamu yao ya kutaka kujua hekima ya kilimwengu kuhusiana na mafumbo ya mambo yasiyoonekana au kufuata falsafa zinazoeleza mwanadamu alitoka wapi na anaelekea mahali gani. Inakupasa ufanye bidii kuepuka hizo “fumbo za Shetani.” Je! wewe unafanya hivyo?—Ufunuo 2:24.

Ili tulinde mioyo yetu isipatwe na “makombora yanayowaka moto” ya Shetani, tunahitaji ngao ya imani, iliyo kubwa na yenye nguvu. Ukubwa wake na kinga itakayotolewa nayo itatutegemea sana sisi. Tutapata ulinzi unaohitajiwa kwa kadiri ambayo sisi tutakomboa wakati kujifunza Biblia kibinafsi, kutafakari Neno la Mungu na kushirikiana na mashahidi wenzetu wa Yehova. Bila shaka, tunahitaji kutumia mambo tunayojifunza, kwa maana “imani pasipo matendo imekufa.” (Yakobo 2:26) Hivyo, moja ya njia nzuri zaidi za kupanua na kutia imani yetu nguvu, na hivyo kuweza kusimama imara, ni kufanya jitihada nyingi za kukaza imani kikiki ndani ya wengine.

Paulo anaendelea kusema hivi: “Pia, mwipokee kofia ya chuma ya kukinga kichwa ya wokovu.” (Waefeso 6:17, NW ) Nyakati za kale, kofia nyingine za kukinga kichwa zilikuwa za matete, nyingine zikawa ni za kitani iliyojazwa vitu vyororo na kushonwa pamoja. Au nyingine zikawa ni za ngozi na nyingine za chuma. (1 Samweli 17:38) Lakini kofia yetu ya kiroho inayokinga kichwa imefanywa kutokana na nini? Paulo aliwaambia Wakristo Wathesalonike hivi: “Tunapaswa kuwa na kiasi. Tunapaswa kuvaa . . . tumaini letu la wokovu kama kofia ya chuma.” (1 Wathesalonike 5:8, Habari Njema kwa Watu Wote) Ndiyo, tumaini linaweza kweli kutulinda tusipigwe-pigwe wala tusikatwe-katwe na Shetani na mawakili wake. “Tumaini halielekezi kwenye kukata tamaa” likiwa lina nguvu na msingi wake ni Biblia. (Warumi 5:5, NW ) Tumaini la namna hiyo litatulinda na porojo za utafutaji wa vitu vya kimwili, kwa maana litatusukuma tutafute kwanza Ufalme wa Mungu.—Mathayo 6:33; Luka 12:31.

Mwisho, tunakifikia kile kipande chetu kimoja kilicho cha kushambulia, “upanga wa roho, yaani, neno la Mungu.” (Waefeso 6:17, NW ) Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “upanga” hapo linamaanisha upanga mfupi unaofanana na kisu cha kupigania, na hiyo inatokeza wazo la watu kupambana wakiwa karibu-karibu. Tukiwa na maarifa sahihi ya Neno la Mungu, tunaweza kutoboa mafundisho ya uongo na kuyakata yaanguke, hiyo ikifunua wazi kwamba si ya akili na hasa yanapingana na Maandiko Matakatifu. (2 Wakorintho 10:4) Hatufanyi hivyo kwa sababu ya kiburi bali kwa kuongozwa na unyenyekevu na kupenda Mungu, ukweli na wanadamu wenzetu. Linalofurahisha ni kwamba, kwa msaada wa vichapo vya Ukristo wa kweli, tunaweza ‘kulishika kwa imara neno la uzima.’—Wafilipi 2:16, NW.

Sifa za Kikristo Zikiwa Misaada

Zaidi ya kuwa na silaha zetu za kiroho, sifa za Kikristo zitatusaidia pia tusimame imara kushindana na Ibilisi. Kwa kuwa Shetani anatumia kiburi kuvuta watu, tukiwa na unyenyekevu na roho ya akili timamu tutasaidika kupigana naye. Kwa kweli, hakuna Mkristo anayepaswa ‘kufikiri mengi zaidi juu yake mwenyewe kuliko inavyohitajiwa kufikiri.’ Tukiisha kufanya yote tuliyogawiwa, inatupasa tuweze kusema: “Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya.” Zaidi ya hilo, tunahitaji fadhili zisizostahilika za Mungu ili kusimama imara tushindane na Shetani, na ili kuzipata ni lazima tuwe wanyenyekevu kwa maana “Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.”—Warumi 12:3, NW; Luka 17:10; Yakobo 4:6, UV.

Kujiweza ni sifa nyingine ya Kikristo itakayotusaidia tusimame imara kushindana na Shetani. Tukishindwa kuzuia misisimuko yetu ya ndani, kama hasira, au kupita kiasi katika chakula, kinywaji au ngono tutaachiwa pengo la kupatwa na mashambulio na mavutano ya Ibilisi. Wakati ‘tulipojiendesha wenyewe kupatana na tamaa za mwili wetu,’ kusema kweli tulikuwa tukitembea “kulingana na mfumo wa mambo ya ulimwengu huu, kulingana na mtawala [Shetani Ibilisi] wa mamlaka ya hewa, roho inayotenda kazi sasa katika wana wa kuasi.” (Waefeso 2:1-3, NW ) Tukiruhusu mawazo na maoni machafu ya kichoyo yatusimamie, tutakuwa katika hatari ya kunaswa na Ibilisi tufanye mapenzi yake. (2 Timotheo 2:26) Ili tusimame imara kushindana naye, ni lazima tuzoee kuzuia sana mawazo na maoni yetu ya moyoni, na pia maneno na matendo yetu. Lazima tuzitie nidhamu akili zetu zifikirie mambo mema, ya uadilifu, safi na ya kupendeka.—Wafilipi 4:8.

Hasa upendo usio wa kichoyo utatusaidia tusimame imara kushindana na Shetani Ibilisi. Yeye ni mwepesi kutuvuta kwa kutumia kitabia cho chote cha kichoyo anachoweza kuona ndani yetu. Kadiri ambayo mashambulio ya Shetani yatashindwa kutupata itategemea kadiri ambayo upendo usio wa kichoyo unatushughulisha katika utumishi na ibada ya Yehova. Atawezaje kutupata ikiwa tunampenda Yehova kwa moyo wetu wote, nafsi yote, akili na nguvu zote? Upendo pia unatufanya tuhangaikie wokovu wa wengine, na jambo hilo linatusaidia tuhakikishe wokovu wetu wenyewe. (Marko 12:30, 31; 1 Timotheo 4:16) Maadamu tunaonyesha upendo kwa namna zake mbalimbali, wala Shetani wala ye yote wa mawakili wake, wanaoonekana na wasioonekana, hataweza kudhoofisha msimamo wetu wa kushindana nao.—1 Wakorintho 13:4-8.

Ili tuweze kusimama imara tushindane na hila za Shetani, ni lazima pia tutumie sala kwa ukamili. Kwa sababu gani? Kwa sababu hatuwezi kushinda kwa nguvu zetu wenyewe. Tunahitaji msaada kutoka juu. Baada ya kueleza namna silaha za kiroho zilivyo, Paulo alisihi waamini wenzake watumie ‘kila namna ya sala na kusihi, wakiendelea kuomba kila pindi katika roho.’ Kwa kusudi hilo walipaswa ‘kuendelea kuamka kwa uendelevu wote na kusihi kwa ajili ya watakatifu,’ kutia ndani mtume.—Waefeso 6:18, 19, NW.

“Kila namna ya sala” ni kutia ndani nini? Namna moja ya sala ni sifa. Kwa sababu ya vile Yehova alivyo, kwa sababu ya mambo mbalimbali yanayoonyesha ubora wake na pia kwa sababu ya cheo chake katika ulimwengu mzima, yeye anastahili kusifiwa nasi. (Zaburi 33:1) Namna nyingine ya sala ni kutoa shukrani. Nasi tuna sababu nyingi kama nini za kumpigia asante Mpaji wa “kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili”! (Yakobo 1:17) Kwa kufaa sana, tunashauriwa ‘tumshukuru Yehova kwa fadhili zake, na maajabu yake kwa wanadamu.’ (Zaburi 107:31) Tukiwa na mioyo na akili zenye kuthamini mambo tutasaidika tusimame imara kushindana na Shetani.

Maombi ni namna nyingine ya sala. Tunaweza kwa kufaa kuomba mambo kama hekima (Yakobo 1:5), roho takatifu (Luka 11:13), msamaha wa dhambi (1 Yohana 1:9; 2:1, 2) na baraka ya Mungu juu ya jitihada zetu (Zaburi 90:17). Pia kuna kusihi. Maana yake ni kumlalamia Yehova Mungu kwa bidii, kama nyakati za mkazo mwingi au hatari. Hivyo Paulo alipofungwa gerezani aliomba kwamba sala ya kusihi itolewe kwa ajili yake. (Waefeso 6:18-20, NW ) Hakika namna hizo za sala zitatusaidia tusimame imara kushindana na Shetani.

Piga Moyo Konde Usimame Imara

Leo watu wa Yehova wakiwa pamoja kwa ujumla wanafurahia kweli kweli baraka za paradiso ya kiroho. Lakini ili sisi mmoja mmoja tuendelee kushiriki ubarikiwa huo hatuwezi kujikalia kitako tukiwa na matumaini ya kwamba tutaupata kwa vyo vyote tu. Lazima tujihadhari nyakati zote, tusimame imara kushindana na Adui yetu, Shetani Ibilisi.—1 Petro 5:8, 9.

Ibilisi ana hila nyingi, kama vile tumeona, na njia yake ya werevu ni kuvunja ukamilifu wetu na kutufanya tuache kumtumikia Yehova Mungu. Lakini Shetani hatatushinda tukiendelea kuvaa silaha zetu za kiroho zinazotoka kwa Mungu, tukiendelea kusitawisha matunda ya roho yake kama vile upendo na kujiweza, na kudumu katika sala. Hivyo, tukiwa na msaada wenye upendo kutoka kwa Mungu wetu, Yehova, tutakuwa na vifaa kamili tusimame imara kushindana na hila za Shetani.—Kutoka w10/15/84.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Sala ya ukawaida itasaidia jamaa ipinge mashambulio ya Shetani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki