Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Je! Mashahidi wa Yehova wanahesabu uzoelevu wa kunywa pombe kuwa ugonjwa?
Watu wengi wanasema juu ya uzoelevu wa kunywa pombe kuwa ugonjwa, kulingana na ufafanuzi wenye maelezo mengi wa neno hilo. Wachunguzi, matabibu na watu wanaosaidia wazoelevu wa kunywa pombe ni kati ya wenye kusema hivyo, kwa maana wengi wao wanatumia maneno kama “maradhi” au “ugonjwa” katika kueleza au kufafanua uzoelevu wa kunywa pombe. Kwa mfano, kichapo Science Digest cha Mei 1984 kinasema hivi:
“Uzoelevu wa kunywa pombe bado ni maradhi yanayohitaji yachunguzwe ili sababu ijulikane ni nini. Ingawa wakati mmoja ulifikiriwa kuwa ni kasoro ya akili tu, sasa unawaziwa kuwa unasababishwa pia na hali za urithi katika chembe za uzazi na pia katika kemikali za mwili . . . Uchunguzi wa hivi majuzi unaunga mkono ushuhuda wa hapo zamani kidogo uliotolewa nchi ya Uswedi kuwa matumizi mabaya ya pombe mara nyingi yanakuwa ni mazoea ‘yanayosafiri’ ndani ya jamaa.”’—Ukurasa 16.
Hata hivyo, kuna sababu ya kujihadhari na maoni ya kwamba uzoelevu wa kunywa pombe ni maradhi (ugonjwa). Watu fulani walio wazoelevu wa kunywa pombe, na wengine, wamekuwa na maelekeo ya kutetea uzoelevu wao wa kunywa au kunywa kupita kiasi, wakidai kwamba hawawezi kuzuia jambo hilo, kwa maana ni ugonjwa. Wengine wanaelekea kuwa na maoni ya kwamba ikiwa mtu alizaliwa akiwa na mwili unaotaka kuzoelea kunywa pombe, au ikiwa kemikali za mwili wake hazichukuani na pombe kwa njia inayofaa, basi yeye hawezi kulaumiwa kuwa mkosa adili.
Lakini, Wakristo wanahangaikia hasa maoni ya Mungu juu ya mambo. Maoni yake ni maadilifu, yana usawaziko na ni ya daima, tofauti na maoni ya matabibu na wachunguzi wa matendo yanayosababishwa na hali za akilini, ambayo huenda yakapendwa sana kwa muda, kisha yabadilishwe au yaachwe baadaye. Neno kamilifu la Yehova linakataza ulevi waziwazi kabisa, likiupanga kati ya mambo yanayoweza kuzuia mtu asiingie katika Ufalme wa Mungu. (Wagalatia 5:19-21) Andiko la Warumi 13:12, 13 linashauri hivi: “Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia; basi na tuyavue matendo ya giza, na kuzivaa silaha za nuru. Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ulafi na [si kwa sherehe zenye makelele mengi na vipindi vyenye ulevi, NW], si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu.” Hata kama watu fulani wamezaliwa wakiwa na miili inayotaka kuzoelea kunywa pombe, hilo likiwa ni jambo ambalo linafanya wengine walione hilo kuwa tatizo la kutibiwa au ugonjwa, Wakristo wanatambua kwamba ukosefu wa adili unahusika.
Mtume Petro aliwaandikia Wakristo hivi: “Maana wakati wa maisha yetu uliopita watosha kwa kutenda mapenzi ya Mataifa; kuenenda katika ufisadi, na tamaa, na ulevi, na karamu za ulafi, na vileo, na ibada ya sanamu isiyo halali; mambo ambayo wao huona kuwa ni ajabu ya ninyi kutokwenda mbio pamoja nao katika ufisadi ule ule usio na kiasi, wakiwatukana.” (1 Petro 4:3,4) Petro mwenyewe alikuwa mtu asiyekuwa mkamilifu na alielewa hali ya kibinadamu. Hata hivyo hakusema kwamba Wakristo wote walikuwa wamegeuka wakaacha kutumia divai kupita kiasi isipokuwa wale waliokuwa wamerithi matatizo ya kuelekea kuzoelea unywaji wa pombe. Kwa kweli, mtume Paulo alisema kwamba hapo kwanza Wakristo wengine walikuwa wamekuwa waasherati, wevi, walevi na wanyang’anyi. Lakini hata liwe ni jambo gani lililokuwa limewaelekeza kwenye matatizo hayo ya kiadili, wangeweza kubadilika na walifanya hivyo. Paulo alisema: ‘Mmetakaswa, mmehesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika roho ya Mungu wetu.’—1 Wakorintho 6:9-11.
Kwa hiyo uzoelevu wa kunywa pombe uwe au usiwe ni ugonjwa, ni lazima tushike kiwango cha juu kilicho chema ambacho kimewekwa katika Neno la Mungu. Mtu ye yote ambaye amekuza uzoelevu wa kutumia pombe—iwe ni kupitia ukosefu wa kujiweza, hali za kabila lake au jamaa yao, au hata kwa sababu ya kasoro fulani ya kimwili—anapaswa kujitahidi kuuacha, labda apate msaada wa mtu mwenye huruma. (Ona Awake! la Julai 8, 1982, kurasa 4-12.) Hivyo ‘hataendelea kuishi katika tamaa za wanadamu [za mwili, NW], bali katika mapenzi ya Mungu, wakati wake uliobaki.’—1 Petro 4:2.