Neno la Mungu Li Hai
Ruthu Alithamini Watu wa Mungu
MWANAMKE kijana mwenye sura ya kuvutia hapa ni Ruthu, ambaye aliishi katika Moabu, mashariki mwa Bahari ya Chumvi. Hata ingawa alilelewa kati ya Wamoabi walioabudu miungu ya uongo, yeye anataka sana kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova, pamoja na watu wake wa Israeli. (Hesabu 25:1-5) Anapopata nafasi ya kufanya hivyo, anaichukua kwa bidii nyingi ambayo inamfanya apendeke sana kwa waabudu wengine wa Yehova ambao wanamjua yeye kuwa “mwanamke mwema.”—Ruthu 3:11.
Njaa kali katika Israeli ilimpa Ruthu nafasi hiyo ya kumtumikia Yehova. Kwa sababu ya njaa hiyo kali, jamaa moja ya watu wanne kutoka mji wa Bethlehemu ilihamia nchi ya Moabu. Ni jamaa inayoonekana hapa—Elimeleki, mkeye Naomi na wana wao Maloni na Kilioni. Lakini muda mfupi baada ya hapo Elimeleki anakufa. Baadaye Maloni anamwoa Ruthu, na Kilioni anaoa msichana mwingine Mmoabi anayeitwa Orpa. Kwa hiyo akiwa na mume na mama-mkwe wenye kumwabudu Yehova, Ruthu apata kumjua Mungu wa kweli.
Hata hivyo, muda usio mrefu baadaye, Maloni na Kilioni wote wawili wanakufa, na kuwaacha wanawake hao watatu bila waume na bila watoto. Unaweza kuwazia huzuni yao. Watafanyaje? Naomi apata habari kwamba ile njaa kali katika Israeli imekwisha. Kwa hiyo anaamua kurudi kwa watu wake Bethlehemu. Ruthu na Orpa wanampenda mama-mkwe wao sana na wanaenda pamoja naye. Lakini baada ya kusafiri kwa muda mfupi barabarani, Naomi, kama unavyoweza kuona, anawaambia wasichana hao hivi: ‘Rudini nyumbani mkakae na mama zenu.’
Naomi anawabusu wasichana hao kwaheri ya kuonana, nao wanaanza kulia. “La, sivyo; lakini tutarudi pamoja nawe kwa watu wako,” wasema wakilia. Naomi anasihi hivi: ‘Enyi binti zangu, ni lazima mrudi.’ Kwa hiyo Orpa anafunga safari ya kurudi nyumbani. Lakini, Ruthu haendi.
Naomi anamgeukia Ruthu na kusema: ‘Rudi pamoja na dada-mkwe wako aliyefiwa na mumeye.’ Lakini Ruthu anajibu kwa bidii yenye usadikisho: “Usinisihi nikuache, nirejee nisifuatane nawe; maana wewe uendako nitakwenda, na wewe ukaapo nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Ruthu 1:1-17) Kwa hiyo Ruthu arudi pamoja na Naomi na kuwa sehemu ya watu wa Mungu wa Israeli.
Je! wewe, kama Ruthu, umepata kumjua Mungu wa kweli, Yehova, na watu wanaomwabudu yeye? Ikiwa ndivyo, na uazimie vivyo hivyo kuunga mkono kwa ushikamanifu watumishi wa Yehova leo sawa na alivyofanya Ruthu zamani za kale!
[Map on page 18]
(For fully formatted text, see publication)
BAHARI YA CHUMVI
MOABU