Har–Magedoni, Mashariki ya Kati, na Biblia
“MAHALI panapokaziwa fikira na matabiri yote ya kiunabii,” anadai mtungaji Hal Lindsey, “ni Taifa la Israeli.” (Kichapo The 1980’s: Countdown to Armageddon) Basi kosa la ‘mpangilio wa Har–Magedoni’ la wenye kusema unabii unapasa kufahamika kwa njia ya uhalisi ni imani yao ya kwamba Mungu anashughulika na Israeli kwa njia ya pekee. Wao wanaamini kwamba Mungu atajiingiza wakati adui za taifa hilo watakapotaka kuliharibu.
Lakini, Biblia inaonyesha kwamba taifa la Kiyahudi lilipoteza upendeleo na ulinzi wa Mungu wakati walipomkataa Mwanaye, Yesu Kristo. (Matendo 3:13, 14, 19) Yesu mwenyewe aliwaeleza waziwazi hivi: “Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu, nao watapewa taifa lingine lenye kuzaa matunda yake.”—Mathayo 21:43.
Lilikataliwa Kabisa?
Hata hivyo, walimu wa kidini John F. na John E. Walvoord (waliotajwa hapo mapema) wanabisha kwa kusema: “Mtume Paulo alionyesha kwa wazi kwamba ahadi za Agano la Kale kwa Israeli bado zingetimizwa. Paulo aliandika, ‘Basi mimi nauliza, Je! Mungu alikataa watu wake? Sivyo kwa vyo vyote!’ (Rum. 11:1, NIV)” Ingawa hivyo, wao hawataji maneno mengine yote ya mstari huo, yanayosema: “Kwa maana mimi pia ni Mwisraeli, wa uzao wa Abrahamu, wa kabila la Benyamini.” Paulo alimaanisha nini kwa kusema hivyo?
Haiwezi kuwa kwamba Paulo aliamini Waisraeli wakiwa taifa zima bado walikuwa na upendeleo wa pekee machoni pa Mungu, kwa maana mtume alionyesha “kihoro kingi na maumivu yasiyokoma katika moyo [wake]” kwa sababu wao hawakuitikia wema wa Mungu. (Warumi 9:2-5, NW) Kwenye Warumi 9:6 (NW) Paulo anaongeza hivi: “Lakini, si kama kwamba neno la Mungu [kwa Abrahamu] lilikuwa limeshindwa. Kwa maana si wote wanaotokana na Israeli [wa asili] walio ‘Israeli’ kweli kweli.” Angalia analosema Paulo: kwamba kwa sababu Wayahudi walimkataa Kristo, Mungu hakuwafikiria tena kuwa Israeli! Kundi lililopakwa mafuta la wafuasi wa Yesu Kristo ndilo sasa lililokuwa “Israeli” wa kweli kweli, chombo ambacho kupitia hicho Mungu angebariki wanadamu wote.—1 Petro 2:9; Wagalatia 3:29; 6:16; Mwanzo 22:18.
Ingawa hivyo, Mungu hakukataa Wayahudi wakiwa mmoja mmoja, kwa maana Paulo alionyesha jambo hili: “Kwa maana mimi pia ni Mwisraeli.” Ndiyo, watu mmoja mmoja ndani ya taifa la Kiyahudi, kama Paulo, wangeweza kuwa sehemu ya Israeli wa kiroho kama wangemkubali Kristo. Ni “baki” tu, kundi la wachache, waliochagua kufanya hivyo.—Warumi 11:1, 5, NW.
Watageuzwa Wakati Ujao Wafuate Ukristo?
Lakini, wengine wanatazamia badiliko kubwa la moyo upande wa Wayahudi wote wa asili. “Ile dhiki kubwa, itakayofuata tendo la kuchukuliwa hewani kwa Kanisa,” anadai mwandikaji mmoja anayechukua maana ya unabii kwa uhalisi, “ndiyo njia itakayotumiwa kugeuza Israeli [wafuate Ukristo].” Jambo la kupendeza ni kwamba, Paulo anasema hivi kwenye Warumi 11:25, 26, NW: “Hali ya kutokuwa na fahamu imetiwa katika Israeli kwa sehemu mpaka [hata, Biblia ya Union Version] hesabu kamili ya watu wa mataifa yote iwe imeingia, na kwa njia hiyo Israeli wote wataokolewa.”
Je! Paulo alikuwa akitabiri kugeuzwa wakati ujao kwa Wayahudi wengi sana wafuate Ukristo? Ingewezaje kuwa hivyo, kwa kuwa yeye mwenyewe alionyesha kwamba ni baki tu la Wayahudi ambalo lingemkubali Kristo? (Warumi 11:5) Ni kweli kwamba Paulo alisema Wayahudi wangepatwa na “hali ya kutokuwa na fahamu” kiroho hata “hesabu kamili” ya watu wa Mataifa itakapokuwa imeingia katika kundi la Kikristo.a Lakini, mwanachuo wa Kigiriki Richard Lenski anaonyesha kwamba hapo neno “hata” (“mpaka”) si lazima liwe linaonyesha wazo la kwamba watageuzwa wafuate Ukristo wakati fulani wa baadaye. (Linganisha matumizi ya “hata” kwenye Matendo 7:17, 18 na Ufunuo 2:25.) Kwa kweli Paulo anasema kwamba akili za Wayahudi wa asili zingebaki katika “hali ya kutokuwa na fahamu” moja kwa moja mpaka mwisho wenyewe. Lakini, kwa hekima Mungu anakamilisha “hesabu kamili” ya Israeli wa kiroho (144,000) kwa kuleta watu wa Mataifa wenye kuamini ndani ya kundi la Kikristo. “Na kwa njia hiyo Israeli [si kwa njia ya taifa la Kiyahudi kubadili moyo] Israeli [wa kiroho] wote wataokolewa.”
Je! Wataimiliki Nchi ya Ahadi —“Hata Milele”?
Ingawa hivyo, namna gani juu ya nchi ambako Taifa la Israeli liko? Je! Mungu anapendezwa nayo kwa njia fulani ya pekee? Watu wengi, kama vile mwalimu wa dini ya Kiprotestanti William Hurst, wanafikiri hivyo. Hurst alisema: “Hakuna eneo la ardhi katika uso wa dunia ambalo limetafutwa au kufikiriwa daima na jamii ya mataifa kuliko ardhi ya Myahudi.” Akitaja maneno ya Mwanzo 13:14, 15, anatukumbusha kwamba Mungu aliahidi angeupa uzao wa Abrahamu ardhi hiyo “hata milele.”
Hivyo je! Yehova Mungu ana wajibu wa kulinda ardhi ya Israeli isishambuliwe? Ikiwa ndivyo, ingeweza kuwa kwamba “Har–Magedoni” ya Mashariki ya Kati inakaribia sana. Hata hivyo, yale tu yaliyosemwa na Mungu akimwambia Abrahamu ni kwamba wazao wake wangeikaa nchi hiyo, si milele, bali kwa kipindi cha wakati ‘kisichojulikana.’b (Mwanzo 13:14, 15, NW) Kwa kumkataa Yesu Kristo, walipoteza haki yote ya kuwa wenyeji wa ardhi hiyo—hata ulinzi wa Mungu.
Har–Magedoni—Wapi?
Kwenye Ufunuo 16:14,16 Biblia inaonyesha kwamba porojo zenye kuongozwa na mashetani zitaelekeza viongozi wa ulimwengu kwenye “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” Andiko linaongezea hivi: “Wakawakusanya hata mahali paitwapo kwa Kiebrania, Har–Magedoni.” Je! hilo halionyeshi vita ya mwisho katika Mashariki ya Kati? Hapana, kwa maana hakuna mahali katika dunia hii panapoitwa “Har–Magedoni” (kwa uhalisi, “Mlima wa Megido”). Katika nyakati za Biblia, kulikuwa na mji wa Mashariki ya Kati ulioitwa Megido. Ulikuwa katika uwanda unaoonyeshwa katika jalada la toleo hili la gazeti. Mapigano mengi ya maana yalifanywa karibu na Megido. Lakini hakukuwa na mlima huko, wakati huo wala wakati wa sasa. Basi, lazima “Har–Magedoni” pawe ni mahali pa mfano. Mfano wa nini?
Unabii wa Ezekieli unaonyesha kwamba Har–Magedoni inafyatushwa na shambulio la jeshi la mataifa mengi juu ya “Israeli.” Washambuliaji wanaongozwa na ‘Gogu wa Magogu,’ ambaye vikosi vyake vinajibwaga kutoka “sehemu za mbali zaidi za kaskazini.” “Gogu” huyo ni nani? Hal Lindsey aliye mwalimu wa kidini mwenye kushikilia kwamba unabii unapasa kufahamika kwa njia ya uhalisi anatamka kwa uhakika (kama wengine wanavyofanya), akisema: “Kuna taifa moja tu huko ‘kaskazini ya mbali kabisa’ ya Israeli, yaani, Urusi.” Vivyo hivyo anatoa kisio la kwamba wale walio katika “jeshi” la Gogu (wanaoitwa Mesheki, Tubali, Uajemi, Ethiopia (Kushi), Puti, Gomeri, na Togarma katika Biblia) watakuwa ni rafiki za Urusi, hasa mataifa ya Kiarabu.—Ezekieli 38:1-9, 15.
Mataifa yaliyopangwa kama rafiki za Gogu, hata hivyo, hayakujulikana sana ulimwenguni siku za Ezekieli. Hivyo utimizo wa unabii ungetukia katika “miaka ya mwisho,” wakati ambao adui za muda mrefu za Israeli wa kale wangekuwa wamekwisha kumalizika duniani. (Ezekieli 38:8) Basi, “nchi ya Magogu” ya Gogu isiyojulikana sana na iliyo ya mbali haingefananisha Urusi kwa kuwa nchi hiyo inajulikana sana wala haiko mbali.
Basi je! ni nani anayekaa katika nchi ‘ya mbali’ na kufungia moyoni uadui mkali kuelekea watu wa Mungu? Kwenye Ufunuo 12:7-9, 17, Biblia inajibu: “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka . . . Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani.” Shetani alionaje kwa kutupwa kwa nguvu katika makao ya kiroho yaliyoshushwa kutoka mbinguni? Biblia inasema: “Joka akamkasirikia yule mwanamke [tengenezo la Mungu la kimbingu], akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.”
Basi, Shetani ndiye “Gogu.” Kwa makumi ya miaka, Shetani na majeshi yake ya mashetani wameendesha vita hiyo juu ya baki la Israeli wa kiroho—kundi la Kikristo lililopakwa mafuta. (Wagalatia 6:16) Wakristo hao wameenea sehemu zote za dunia; hawako mahali fulani pamoja ambapo pangeweza kushambuliwa na muungano wa askari wa Mashariki ya Kati. Lakini kama vile Ezekieli alivyotabiri kwa unabii, wao ‘wanakaa katika usalama’ chini ya ulinzi wa Mungu. (Ezekieli 38:11) Israeli ya asili ya siku hizi, ikiwa imezungukwa na jirani wenye uhasama na kupatwa na magumu ya kisiasa na kijamii nchini mwayo, ‘haikai katika usalama’ hata kidogo.
Lakini, Biblia inaonyesha kwamba tamasha ya ulimwengu itabadilika sana. ‘Babeli Mkuu,’ milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, itapatwa na uharibifu wa ghafula. (Ufunuo, sura ya 18) Dini ya uwongo itakapopatwa na zahama hiyo ya uharibifu wa ghafula, Wakristo wa kweli waliobaki wataelekea kuwa rahisi kushambulika, naye Shetani, au “Gogu,” atapandwa na mori wa kutaka kuwaharibu. Atahakikisha kwamba “wafalme wa ulimwengu wote” watakusanywa pamoja chini ya mavutano ya kishetani kwenye “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni.—Ezekieli 38:12-16; Ufunuo 16:14, 16.
Basi, “Har–Magedoni” si kisehemu kidogo sana cha mahali fulani katika Mashariki ya Kati. Bali, ni hali ya ulimwengu. Ulimwengu mzima utaungana katika kupinga Yehova Mungu na mashahidi wake. (Isaya 43:10-12) Shambulio kali sana la Shetani juu ya Wakristo wa kweli—si pigano kati ya mataifa katika eneo fulani la Mashariki ya Kati—ndilo linalochochea Mungu afanye vita kulinda watu Wake!—Ezekieli 38:18-23; Zekaria 2:8.
Basi Wakristo wa kweli leo hawajikalii tu wakiangalia Mashariki ya Kati. Jambo la kwanza wanalofikiria ni kuelekeza watu kwenye mambo ambayo hasa Neno la Mungu linasema juu ya vita hiyo inayokuja. Mashahidi wa Yehova wamesifiwa ulimwenguni pote kwa kupeleka ujumbe huo pasipo woga kwenye nyumba za watu. Hata hivyo, huenda wewe ukataka kujua ni kwa sababu gani Mungu wa upendo ataleta vita ya namna hiyo. Je! inawezekana kuiokoka? Maulizo hayo ndiyo yatakayoshughulikiwa na matoleo yetu mawili yanayofuata ya Mnara wa Mlinzi.
[Maelezo ya Chini]
a Dini za Jumuiya ya Wakristo zinashindwa kutambua kwamba hesabu fulani inayotajwa wazi, ambayo inafunuliwa katika Biblia kuwa ni 144,000, ndiyo Israeli wa kiroho. (Ufunuo 7:4) Matokeo ni kwamba wengine wanafikiri kwa kosa kwamba Paulo alitabiri ni watu wengi sana kati ya Wayahudi na hata “ulimwengu mzima wa wapagani” wangegeuzwa wafuate Ukristo. (The Jerusalem Bible) Lakini, mfano wa Paulo wa mzeituni katika Warumi, sura ya 11, unakuwa hauna maana ikiwa haihusiki hesabu fulani inayotajwa wazi.
b Ingawa neno la Kiebrania ‘oh·lam limetafsiriwa na wengine kuwa “milele,” kulingana na mjuzi Mwebrania William Gesenius, linamaanisha “wakati uliofichwa, yaani, usiojulikana wazi na mrefu, ambao mwanzo wake wala mwisho wake si hakika na haujulikani waziwazi.” Kamusi inayoitwa Nelson’s Expository Dictionary of the Old Testament inaongeza hivi: “Likiwa na kielezi ‘ad, neno hilo linaweza kumaanisha ‘mpaka kwenye wakati ujao usiojulikana.’”—Linganisha Kumbukumbu la Torati 23:3; 1 Samweli 1:22, katika tafsiri ya Biblia ya New World.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Je! matukio ya sasa katika Mashariki ya Kati ni viishara vya kukaribia kwa Har–Magedoni?
[Picha katika ukurasa wa 6]
Je! Yerusalemu ndipo mahali pakuu pa matukio yanayoongoza kwenye Har–Magedoni?