Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 7/15 kur. 5-7
  • Har–Magedoni—Vita Inayoongoza Kwenye Amani ya Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Har–Magedoni—Vita Inayoongoza Kwenye Amani ya Kweli
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Amani—Kwa Kufutilia Mbali Njia za Kupiga Vita
  • Amani—Ni kwa Wale Tu Wanaoitaka
  • Amani—Miaka Elfu na Baada ya Hapo
  • Har-magedoni—Mwanzo Wenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Har–Magedoni—Si Mambo Haya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Amani ya Kweli—Kutoka Chanzo Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Har-magedoni Lini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 7/15 kur. 5-7

Har–Magedoni​—Vita Inayoongoza Kwenye Amani ya Kweli

KWA kutumia lugha ya wale wanaoshughulika na mawasiliano ya kimataifa, neno linalotumiwa kueleza hali ya ulimwengu leo ni MAD—Mutual Assured Destruction (Uangamizano Ulio Hakika). Neno hilo linafaa sana. Katika miaka 40 iliyopita tangu kombora la kwanza la atomi lilipolipuliwa katika vita juu ya Hiroshima, Japani, silaha za nyukilia za ulimwengu zimeongezeka kwa kadiri isiyoaminika. Ripoti nyingine zinadai kwamba zinafikia kiasi kinacholingana na tani milioni 12 za baruti, au karibu tani tatu kwa kila mtu duniani!

Akiwa “hakuiumba [dunia] ukiwa, [bali] aliiumba ili ikaliwe na watu,” Yehova Mungu, hataruhusu wala kwa kweli hawezi kuruhusu mataifa yaendelee katika mwendo wayo wa kujiua. (Isaya 45:18; ona pia Zaburi 104:5.) Kabla hayajapata nafasi ya kutumia silaha zao zote za kuuana, na kwa kufanya hivyo wajiangamize na mazingira, Mfanyizaji na Mwenyeji wa dunia na kila kitu kilicho juu yake atainuka atende. Ameahidi kwamba hiyo itakuwa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,” Har–Magedoni ya Kibiblia!—Ufunuo 16:14, 16.

Kwa hiyo, Har–Magedoni, haitakuwa vita nyingine tu ya kumaliza ugomvi uliopo wa kisiasa ambao umeshinda kumalizwa. Itatimiza mambo ambayo mwanadamu katika vizazi vyote angeweza kutumaini tu bila kuyatimiza yeye. Itaondoa visababishi vyote vya vita vya kibinadamu. Italeta amani ya kweli duniani. Zaidi ya yote, itarudisha utawala wa haki wa Mwenyeji wa dunia, Yehova Mungu, juu ya uumbaji wake wote. Yehova Mungu, juu ya uumbaji wake wote. Yote hayo yatatimizwaje? Ebu tuone.

Amani—Kwa Kufutilia Mbali Njia za Kupiga Vita

Sababu mojapo ya mataifa kushindwa kuondolea mbali vita ni kwamba hawajaweza kufutilia mbali njia za kupiga vita. Hata ingawa wanajua kwamba urundikaji wenye kuongezeka sana wa silaha ni wa kuelekea kujiua, hawana nia ya kuacha au kupunguza. Litakuwa jambo la “kustaajabisha” kweli kweli Yehova atakapochukua hatua na kutimiza yale ambayo mataifa hawawezi kufanya: “Upinde auvunja-vunja naye au kata-kata mkuki; magari ya vita ayateketeza katika moto.”​—Zaburi 46:8, 9, NW.

Katika wakati uliopita Yehova ameonyesha uwezo wake wa kufanya zisifanye kitu silaha za ufundi zaidi au zilizo kali zaidi ambazo mataifa wangeweza kutumia. Kwa mfano, aliokoa watu wake, Waisraeli, walioelekea kuwa wasio na kinga kutoka kwa nguvu za kijeshi za mamlaka ya ulimwengu ya kwanza, Misri, kwa kutumia nguvu za asili za maji ya Bahari Nyekundu. (Kutoka 15:3-5) Vivyo hivyo, silaha za ufundi mwingi wa kushambulia za Mfalme Yabini Mkanaani, “magari ya vita mia tisa yenye panga za chuma,” (NW) chini ya amri ya mkuu wa jeshi Sisera, yalizuiwa yasitende wakati Yehova alipofungua nguvu za mafuriko ya ghafula. Majeshi ya adui yalitupwa katika mvurugo kamili, na kufanya wamalizwe mpaka mtu wa mwisho kabisa. Matokeo yakawa ‘nchi kustarehe miaka arobaini.’​—Ona Waamuzi, sura ya 4 na 5:21, 31.

Jambo la maana ni kwamba pigano hilo lenye ushindi kamili dhidi ya majeshi ya Mfalme Yabini lilitukia katika bonde la mto Kishoni, “karibu na maji ya Megido.” (Waamuzi 5:19-21) Kwa hiyo linatangulia kutuonyesha kwa mkazo mkubwa ushindi kamili wa Yehova katika vita inayokuja ya Har–Magedoni.

Sisi hatujui nguvu za “ajabu-ajabu,” ziwazo zote, atakazotumia Yehova dhidi ya maadui wake. Tunalojua ni kwamba anaweza kutumia nguvu zinazoweza kuangamiza kabisa mipango ya kijeshi ya mataifa. Kwa mfano, wanasayansi wanajua kwamba mdundo wa simakumeme yenye nguvu nyingi​—unaweza kuharibu kabisa mifumo ya upashanaji habari na ya uongozaji wa mambo ya kijeshi ya taifa, na hivyo kufanya kila jambo liwe katika hali ya mvurugo. Ni jambo la akili kwamba Yehova atafanya silaha zote za mataifa ziwe bure ili kuweka msingi wa amani kamili.

Amani—Ni kwa Wale Tu Wanaoitaka

Mara nyingi imesemwa kwamba vita vinapiganwa na watu, wala si silaha zinazopigana. Kwa hiyo, ingawa ni jambo la lazima kwamba njia za kupiga vita zifagiliwe mbali, hilo peke yake halitahakikisha kuwapo kwa amani ya kudumu. Ni jambo la akili kwamba tukitaka kuona amani ya kweli, ni lazima chuki za kisiasa, za rangi na za kitaifa, ambazo zinagawanya ulimwengu katika vikundi na madhehebu nyingi viondolewe pia. Yehova Mungu atafanya hilo kwa kutimiza jambo ambalo mamilioni ulimwenguni pote wamekuwa wakisali: “Ufalme wako uje.”​—Mathayo 6:9, 10.

Hata ingawa unabii mbalimbali wa Biblia unaonyesha wazi kwamba Ufalme wa Kimasihi mikononi mwa Yesu Kristo ulisimamishwa mbinguni katika mwaka wa 1914 wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, haukukaribishwa na mataifa. Hakuna lo lote la mataifa lililokubali kuweka chini silaha zalo na kuacha enzi yao. Badala yake, katika kung’ang’ania kama vichaa utawala wa ulimwengu, yalihusika katika ugomvi wa vita kubwa zaidi iliyokuwa imepata kutokea kufikia wakati huo.

Zaburi ya pili inaeleza hali ilivyo kwa njia ya kiunabii: “Mbona mataifa wanafanya ghasia, na makabila wanatafakari ubatili? Wafalme wa dunia wanajipanga, na wakuu wanafanya shauri pamoja, juu ya [Yehova], na juu ya masihi wake.” Ndiyo sababu amri ya Yehova.kwa Mfalme wake aliyewekwa, Yesu Kristo, ni hii: “Utawaponda kwa fimbo ya chuma, na kuwavunja kama chombo cha mfinyanzi.”​—Zaburi 2:1, 2, 9; 110:2.

Ushindi huo wa Mfalme mpakwa-mafuta wa Mungu unasimuliwa kirefu kwa njia ya mfano katika Ufunuo 19:11–20:3. Yesu Kristo, Neno la Mungu, kwa kuungwa mkono na majeshi ya kimalaika, anaonekana ameketi juu ya farasi mweupe, “kwa haki ahukumu na kufanya vita. . . . Na upanga mkali hutoka kinywani mwake ili awapige mataifa kwa huo.” Machinjo ya waovu yanayofuata ni makubwa sana. Katika ushindi wake juu ya wote, Mfalme huyo mshindi ndipo atakaposhughulika na mkosaji anayesababisha ole na mateso yote ya dunia. Njozi katika Ufunuo inasimulia jambo hilo kama kwamba limekwisha kutimizwa, ikisema: “Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu.”

Amani—Miaka Elfu na Baada ya Hapo

Je! unaweza kuwazia miaka elfu ya amani itamaanisha nini kwa wanadamu? Wenye maarifa wanatambua kwamba njaa, maradhi, na umaskini kati ya mataifa yangeweza kuondolewa ikiwa kisehemu kidogo tu cha mamia ya mabilioni ya dola zinazotumiwa juu ya silaha kila mwaka kingetumiwa kupambana na mambo hayo. Fikiria yatakayotimizwa wakati mali za dunia zitakapotumiwa kwa njia yenye kujenga. Haikuwa ndoto ya kutamani tu ya mwotaji-ndoto Isaya alipoongozwa na roho ya Mungu atabiri juu ya utawala wa “Mfalme wa amani,” Yesu Kristo: “Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe.”​—Isaya 9:6, 7.

Swali lenye uharaka ni hili: Je! wewe utaokoka uharibifu kwenye Har–Magedoni upate kufurahia amani isiyo na mwisho? Huenda ukauliza, ‘Nifanye nini ili niokoke?’ Shauri la Biblia ni hili: “Mtafuteni [Yehova], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].” (Sefania 2:2, 3) Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia ufanye hivyo. Ndipo Har–Magedoni itakuwa kwako, si vita inayoleta uharibifu kamili, bali vita inayoongoza kwenye amani ya kweli.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Katika Bahari Nyekundu Yehova alionyesha uwezo wake wa kufanya silaha kali-kali za vita zisifanye kitu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki