Maisha na Huduma ya Yesu
Apendelewa Kabla ya Kuzaliwa
MALAIKA Gabrieli ametoka tu kumwambia mwanamke kijana Mariamu kwamba atazaa mtoto mvulana ambaye atakuwa mfalme wa milele. Lakini Mariamu anamuuliza, ‘Itawezekanaje, kwa kuwa sijalala na mwanamume?’
‘Roho takatifu ya Mungu itakuja juu yako,’ anaeleza Gabrieli, ‘na kwa sababu hiyo mvulana huyo ataitwa Mwana wa Mungu.’ Ili kumsaidia Mariamu, Gabrieli aendelea kusema hivi: ‘Mtu wa jamaa yenu, Elisabeti mzee, ambaye watu walisema hawezi kuwa na watoto, sasa ana mimba ya miezi sita.’ Mariamu aamini Gabrieli na kusema: ‘Na iwe kwangu kama ulivyosema.’
Upesi baada ya hapo Gabrieli aondoka, Mariamu ajitayarisha na kwenda akamwone Elisabeti anayeishi pamoja na mumeye Zekaria katika nchi ya milima-milima ya Yudea. Kutoka nyumba ya Mariamu katika Nazareti kwenda huko, ni safari ndefu ya labda siku tatu au nne.
Mwishowe Mariamu anapofika katika nyumba ya Zekaria, anaingia na kutoa salamu. Anapofanya hivyo Elisabeti anajawa na roho takatifu, naye amwambia Mariamu hivi: ‘Wewe umebarikiwa kati ya wanawake, na amebarikiwa mtoto utakayezaa. Ni pendeleo kubwa kujiwa na mama ya Bwana yangu! Kwa maana, tazama! mara tu niliposikia salamu yako, mtoto katika tumbo langu aliruka kwa furaha nyingi.’
Akiwa na furaha nyingi, Mariamu anasema: ‘Tangu sasa na kuendelea watu wote wataniita mimi mwenye furaha, kwa sababu ya mambo makubwa ambayo Mungu amenifanyia.’ Mariamu anakaa na Elisabeti kwa miezi mitatu hivi, na bila shaka anasaidia sana wakati wa majuma hayo ya mwisho ya Elisabeti kuwa na mimba. Hakika ni jambo zuri kwamba wanawake hawa wawili waaminifu, wote wakiwa na mtoto tumboni kwa msaada wa Mungu, wanaweza kuwa pamoja katika wakati huu wa baraka wa maisha yao!
Umeona pendeleo alilopewa Yesu hata kabla ya kuzaliwa? Elisabeti alimwita “Bwana yangu,” na mtoto wake ambaye alikuwa bado hajazaliwa aliruka kwa furaha Mariamu alipotokea mara ya kwanza. Kwa upande mwingine, wengine walimtendea Mariamu na mtoto wake ambaye alikuwa bado kuzaliwa kwa heshima ndogo, kama tutakavyoona baadaye. Hata hivyo, katika makala yetu ifuatayo, tutajifunza zaidi juu ya mtoto wa Elisabeti, Yohana. Luka 1:26-56.
◆ Gabrieli alisema nini ili amsaidie Mariamu afahamu angekuwa na mimba?
◆ Yesu alipewaje heshima kabla hajazaliwa?
◆ Mariamu alikaa na Elisabeti kwa muda gani, na kwa sababu gani ilifaa kwamba Mariamu akae na Elisabeti wakati huo?