Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 2/15 kur. 23-28
  • Wema wa Yehova Katika “Siku za Mwisho” (Makala ya Funzo la Kitabu)

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wema wa Yehova Katika “Siku za Mwisho” (Makala ya Funzo la Kitabu)
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wema wa Yehova
  • Mashauri ya Mzee wa Ukoo
  • Kuiendea Nyumba ya Mungu Makundi Makundi
  • Katika Ulimwengu Huu wa Jeuri
  • Wema Mwingi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Yehova Ni Mfano Bora Sana wa Wema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Mweneo Mkubwa Ajabu wa Wema wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • “Wema Wake, Jinsi Ulivyo Mwingi!”
    Mkaribie Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 2/15 kur. 23-28

Wema wa Yehova Katika “Siku za Mwisho”

(Makala ya Funzo la Kitabu)

“Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova].”​—ISAYA 2:3.

1, 2. (a) Ni hatari gani kubwa inayowaelekea wanadamu sasa? (b) Viongozi wa ulimwengu wanasema nini juu ya Har–Magedoni?

“SIKU ZA MWISHO.” Ni kwa sababu gani unabii wa Biblia unatumia msemo huo tena na tena? Je! inamaanisha kwamba siku za wanadamu zimehesabiwa na kwamba mwishowe dunia yetu na viumbe vyote vilivyo hai juu yake vitaangamizwa katika msiba fulani wa dunia yote? Viongozi wa ulimwengu mara nyingi wanasema juu ya uwezekano huo wakiwa na hofu. Kwa mfano, katika mahoji ya televisheni Januari 13, 1985, waziri wa mambo ya nchi za kigeni wa Mosko Andrei Gromyko alionya watu wa Urusi kwamba “hatari kubwa sana, tisho kubwa sana limewakaribia wanadamu wote.” Aliongeza hivi: “Kila jambo liwezekanalo lapasa kufanywa ili kuondoa tisho hilo, ili Har–Magedoni ambayo watu wameogopeshwa kwayo kwa karne nyingi isitokee.”

2 Katika pindi kadha, Rais Ronald Reagan wa United States amezungumza pia juu ya Har–Magedoni. Gazeti Daily News la New York la Oktoba 30, 1983, lilimtaja akisema: “Ninarudia kuangalia manabii wenu wa kale katika Agano la Kale na ishara zinazotabiri Har–Magedoni, kisha najikuta nikijiuliza kama​—kama sisi ndicho kizazi kitakachoiona ikitokea.” Hivi karibuni zaidi, katika Februari 8, 1985, gazeti The Wall Street Journal liliripoti hivi: “Rais Reagan anasema anafikiria na kusema juu ya Har–Magedoni, . . . lakini bado hafanyi mipango kwa ajili ya hilo.”

3. (a) Kwa kweli Har–Magedoni ni nini? (b) Ni nini kinachomaanishwa na “siku za mwisho”?

3 Ndiyo, viongozi wa ulimwengu wanazungumza juu ya Har–Magedoni. Lakini je, wanatambua maana ya neno hilo la Biblia? Inaelekea hawajui, kwa maana Har–Magedoni si maangamizi makubwa yenye kutokezwa na wanadamu. Ni vita ya ulimwengu wote ya Mungu ambayo kupitia kwayo yeye na Mfalme-mshirika wake, Yesu Kristo, atatekeleza hukumu juu ya mataifa maovu na watu waovu. Inakuwa upeo wa “siku za mwisho.” (Danieli 10:14; Ufunuo 16:14, 16) Nasi tuelewe nini na usemi “siku za mwisho”? Tafsiri nyingine zinatafsiri usemi huo kuwa “sehemu ya mwisho ya siku hizo,” “sehemu ya baadaye ya siku hizo,” “mwisho wa baadaye wa siku hizo.” (New World Translation, Rotherham, Young) Maneno ya Kiebrania yanayotafsiriwa hivyo ni ‘a·charithʹ hay·ya·mimʹ. Kulingana na kitabu Theological Dictionary of the Old Testament, mara nyingi yanamaanisha “Wakati wa Mwisho,” ikionyesha si wakati ujao tu bali pia “jinsi historia itakavyomalizikia, yaani matokeo yake.”

4. “Wakati wa Mwisho” utasongaje ufikie upeo wake, na matokeo yawe nini?

4 Kwa miaka 70 hivi, wanadamu wamekuwa wakiishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo,” uliotabiriwa na Yesu katika Mathayo 24:3–25:46 (NW). Kipindi hicho, kinachoanzia mwaka 1914, ndio “Wakati wa Mwisho” ambao matukio yalisonga mbele hatua kwa hatua kwenye upeo wayo. Upeo huo utakuwa katika “dhiki kubwa” wakati tengenezo lote la Shetani litakapoharibiwa. (Mathayo 24:21, 22) Matokeo yake makubwa yatakuwa ni kuondolewa lawama kwa jina takatifu la Yehova.​—Ezekieli 38:16, 23.

Wema wa Yehova

5. Ni maneno gani yenye kutia moyo yanayopatikana katika Hosea 3:5?

5 Yehova ni Mungu wa kitia-moyo. Ametapanya semi zenye kusisimua kama nini katika Neno lake, Biblia Takatifu! Usemi mmoja unapatikana katika Hosea 3:5, panaposema: “Baada ya hayo wana wa Israeli watarejea, na kumtafuta [Yehova], Mungu wao, na Daudi, mfalme wao; nao watamwendea [Yehova] na wema wake kwa kicho siku za mwisho.”

6. Israeli ya kiroho imetofautianaje na madhehebu za Jumuiya ya Wakristo?

6 Mabaki ya Israeli yalirudi kutoka utumwani.Babuloni mwaka 537 K.W.K. waanze tena kumwabudu Yehova katika Yerusalemu. Hali moja na hiyo katika nyakati za kisasa, mwaka 1919 mabaki wapakwa mafuta wa Israeli wa kiroho ‘walirejea’ kutoka utumwa wa tengenezo la Shetani, ‘wakimtafuta Yehova Mungu wao’ kwa bidii. Ilikuwa tofauti kama nini na madhehebu za Jumuiya ya Wakristo! Hakuna yo yote ya hizo inayotaka kumtambua Yehova kuwa “Mungu wao.” Badala ya “kumtafuta” Yehova, wanaepuka kulitumia jina lake.

7. Watu wa Yehova wameliheshimuje jina lake?

7 Mapema katika “siku za mwisho,” toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1926, lilichapisha makala yenye mwito wa ushindani iliyokuwa na kichwa “Ni Nani Atakayemheshimu Yehova?” Mabaki waliokusanywa tena wa Israeli wa kiroho kwa ushikamanifu walijibu mwito huo, na mwaka 1931 walifurahi kulikubali jina Mashahidi wa Yehova. (Isaya 43:10, 12) Mpaka siku hii wanaendelea kushikilia jina la Yehova likiwa maarufu mbele ya wakaaji wa dunia. Mwaka 1984 walichapisha, mamilioni ya nakala katika lugha nyingi, broshua yenye kuvutia ya rangi yenye kichwa Jina la Mungu Litakaloendelea Milele (katika Kiswahili ilichapishwa mwaka 1985).

8, 9. (a) Ni nini maana ya ‘kumtafuta Daudi mfalme wao’? (b) Mfalme huyo alitawazwa wakati gani na wapi? (c) Watu wa Yehova walikujaje kuelewa jambo hilo?

8 Hata hivyo, Hosea alitabiri pia kwamba wana hao wa kiroho ‘watarejea na kumtafuta Daudi mfalme wao.’ Israeli wa kimwili wamekuwa bila mfalme tangu kupinduliwa kwa nasaba ya Daudi mwaka 607 K.W.K. Tendo hilo lilianzisha miaka 2,520 ya utawala usio wa kimungu​—“majira ya mataifa,” au Nyakati za Mataifa. (Luka 21:24; Danieli 4:16) Lakini mwaka 1914, “siku za mwisho” zilipoanza, Mungu alimweka Yule ambaye Daudi alifananisha​—Yesu Kristo​—awe Mfalme katika Sayuni, “Yerusalemu wa mbinguni.”​—Waebrania 12:22; Zaburi 2:6.

9 Watu wa Yehova duniani hawakuelewa hayo yote mara moja. Hata hivyo, kutafuta kwao ‘Daudi mfalme wao’ kulifikia upeo wakati gazeti Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1925, lilichapisha makala yenye kichwa “Kuzaliwa kwa Taifa.” Makala hiyo ilithibitisha kikamili, kwa kutegemea Ufunuo sura ya 12, kwamba Ufalme wa Kimasihi wa Yehova ulikuwa umezaliwa mbinguni mwaka 1914 na kwamba Kristo sasa ‘anatawala katikati ya maadui wake.’​—Zaburi 110:1, 2, King James Version; Zb 2:1-6.

10. (a) Ni nani ‘wanaomwendea Yehova kwa kicho,’ na jinsi gani? (b) Ni kwa sababu gani ‘kicho cha Yehova’ ni cha maana sana leo?

10 Mabaki wapakwa mafuta, na kwa kweli wote wanaojiweka wakfu kwa Yehova, wanatambua sana dhambi zao za nyakati za kwanza. Kwa unyenyekevu, ‘wamemwendea Yehova kwa kicho,’ wakiomba msamaha kwa ajili ya dhambi za wakati uliopita. Na sasa “siku za mwisho” zinaposonga mbele kuelekea upeo wazo, wenye kumpenda Yehova wanaangalia kwa uangalifu zaidi wasimkosee Mungu na sheria zake za uadilifu. Ni lazima tuendelee ‘kumwendea Yehova kwa kicho,’ tukipiga-piga miili yetu, ili tupate wokovu na kuingia katika Utaratibu Mpya wa Mungu. (1 Wakorintho 9:27) Ni lazima daima tukumbuke kwamba “kumcha [Yehova] ndio mwanzo wa hekima.”​—Zaburi 111:10.

11. (a) Ni katika njia gani Yehova ni mwema? (b) Ni kwa sababu gani twapaswa ‘kwendea wema wa Yehova kwa kicho’?

11 Lakini, ni jinsi gani tunaweza ‘kwendea wema wake kwa kicho’? Yehova ni mwema katika kila jambo. Yeye anawakilisha wema wa adili. Yeye ni kamili katika kutuandalia kila uhitaji wetu. Kwa hiyo, tunaweza kusema kwa uhakika kama Daudi: “[Yehova] ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa kitu. . . . Hakika wema na fadhili zitanifuata siku zote za maisha yangu.” (Zaburi 23:1-6) Sasa, na mpaka mwisho wa “siku za mwisho,” ni lazima ‘twendee wema wa Yehova kwa kicho,’ tukiwa na uhakika kwamba dhambi zetu zitafunikwa kwa dhabihu yenye thamani ya Mwanaye, Yesu. (1 Yohana 2:1, 2) Kwa shukrani, tunatangaza: “Ee, [Yehova], . . . Ee, mukubwa sana ni wema wako uliowekea wenye kukuogopa!”​—Zaburi 31:17, 19, Zaire Swahili Bible.

12. (a) Ni kwa jinsi gani tunaweza kufuata mfano wa Yehova wa wema? (b) Ni kwa sababu gani ni jambo la maana sana tufanye hivyo?

12 Ulimwengu wa Shetani unapozama zaidi na zaidi ndani ya tope la ubaya, na tufuate mfano wa Yehova wa wema kwa kujulisha jirani zetu habari njema za Ufalme na kwa kuonyesha sifa za kimungu maishani mwetu wenyewe. Na tusitawishe kweli kweli matunda ya roho, kutia wema, katika uhusiano wetu wote​—katika jamaa zetu, katika makundi, na tunapokutana na watu wa ulimwengu. (Wagalatia 5:22, 23; Zaburi 119:65-68) Kufanya hivyo ni kwa lazima ikiwa tutaokoka “siku za mwisho.”

Mashauri ya Mzee wa Ukoo

13. (a) Ni nani leo wanaoweza kufaidika kwa kuchunguza unabii aliotoa Yakobo akiwa mahututi kitandani? (b) Unabii huo una mashauri gani?

13 Miaka 3,700 hivi iliyopita, mzee wa ukoo Yakobo (aliyeitwa pia Israeli) alitoa unabii akiwa mahututi kitandani. Akizungumza na wanaye 12, vichwa vya makabila ya Israeli, yeye alisema: “Kusanyikeni, ili niwaambie yatakayowapata siku za mwisho.” Maneno yake yanahusu leo mabaki ya Israeli wa kiroho na kwa njia kubwa wenzi wao, “kondoo wengine.” Hakuna ye yote wa hao anayeweza kupuuza viwango vya adili vya Yehova asiadhibiwe, kama alivyofanya Reubeni, wala hawawezi kuruhusu kuwepo maelekeo ya jeuri kama yale ya Simeoni na Lawi. Badala yake, ni lazima wasitawishe sifa kama vile uhodari, kumtegemea Yehova, na kuwa wenye kuzaa matunda, kama inavyoonyeshwa na wale wana wengine wa Israeli.​—Mwanzo 49:1, 3-7, 9, 18, 22; Yohana 10:16; linganisha 2 Petro 1:8-11.a

14. Ni unabii gani mara mbili unaohusiana wa “Wakati wa Mwisho” ambao unatoa mashauri hasa kwa “kondoo wengine”?

14 Hata hivyo, shauri linalotajwa wazi-wazi linatolewa kwa “kondoo wengine” walio na mataraja ya kuokolewa wapite “Wakati wa Mwisho.” Tunaliona limesemwa, kama kwamba likaziwe, katika unabii mara mbili wa Biblia unaohusiana, kwenye Isaya 2:2-5 na Mika 4:1-5.

Kuiendea Nyumba ya Mungu Makundi Makundi

15. (a) Andiko la Isaya 2:2 limetimizwaje? (b) Wapole wanaona tofauti gani sasa, nao wanatendaje?

15 Andiko la Isaya 2:2 linasema: “Na itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya [Yehova] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi.” Kwa miaka zaidi ya 50, tangu mwaka 1935, ‘vitu vinavyotamaniwa vya mataifa yote’ vimekuwa vikikusanyika kwenye nyumba ya ibada ya Yehova, ‘vikiijaza nyumba hiyo kwa utukufu.’ ‘Kwenda makundi makundi’ huko yaelekea kunaongezeka wakati “siku za mwisho” zinapokaribia upeo. Mlima wa mfano wa ibada safi ya Yehova unakuwa maarufu zaidi, hata kwamba wapole wanaweza kuona jinsi ulivyo tofauti na “vilima” na “milima” iliyogawanyika ya ulimwengu wa Shetani unaoendekeza watu. ‘Wanatoka’ katika dini ya uwongo na kukimbilia kwa hesabu zenye kuongezeka kwenye mlima wa ibada ya Yehova.​—Hagai 2:7; Ufunuo 18:2, 4, 5; Zaburi 37:10, 11.

16. (a) Wapole wanajibu mwito gani sasa? (b) Yehova anatimizaje ahadi yake ya ‘kuyahimiza hayo’?

16 Wapole hao wanajibu mwito wa Isaya 2:3: “Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake; maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la [Yehova] katika Yerusalemu.” Tayari, Yehova anatimiza ahadi yake ya ‘kuyahimiza hayo wakati wake.’ (Isaya 60:22) ‘Mkutano mkubwa wa watu wa kila taifa’ wenye kuongezeka unamiminika kwenye ibada ya Yehova. Kati yao, 161,896 walibatizwa mwaka 1983; 179,421 mwaka 1984; na 189,800 mwaka 1985. Wanataka waokolewe wapite “siku za mwisho.”​—Ufunuo 7:9, 14.

17. (a) Mashahidi wapya wanaweza kuonyeshaje kuthamini wema wa Yehova? (b) Sisi sote tunahitaji kutii amri gani zisizo za makatazo, bali zenye maagizo mazuri?

17 Mashahidi hao wapya wanathamini wema wa Yehova kwa kuwaleta kwenye nuru ya ukweli, nao wanatamani kwa bidii kuonyesha wengine wema. Wanakaribisha maagizo anayotoa Yehova kupitia Neno lake na tengenezo lake. Torati ya Musa ilikuwa na makatazo mengi, nayo Israeli kwa kufaa ilipaswa kuyafuata. (Kutoka 20:3-17) Lakini amri mbili kubwa kwa Wakristo, kama zilivyosemwa na Yesu, ni amri zisizo za makatazo, bali zenye maagizo mazuri ya kwamba ‘tumpende Yehova Mungu wetu kwa moyo wote, nafsi yote, akili yote, na nguvu zote, na jirani yetu kama sisi wenyewe.’ (Marko 12:29-31) Kwa umoja, Mashahidi wa Yehova sasa wanatii “sheria” anayotuma Mungu kutoka “Yerusalemu wa mbinguni,” na kufuata kanuni zayo za uadilifu.

18. (a) Ni aina gani za sheria tunazohitaji kushika? (b) Kuna faida gani kutii amri zinazofaa?

18 Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba watu wa Yehova hawahitaji kufuata amri zo zote. Mtume Paulo anatukumbusha: “Mambo yote na yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu.” (1 Wakorintho 14:40) Huenda amri chache zikahitajiwa kwenye Majumba ya Ufalme yetu, kwa mfano, ili kutumia umeme (stimu) kwa njia nzuri au kuzuia watoto wasitumie nyumba ya ibada ya Mungu kuwa mahali pa kuchezea baada ya mikutano. Vichwa vya jamaa huenda wakahitaji kufanya mipango fulani ya utaratibu, kama vile kuwa na mazungumzo ya ukawaida ya andiko la Biblia kila siku nyumbani. Katika jamaa za Betheli kuna amri, kama zile zinazotaka washiriki wa jamaa wapambe habari njema kwa kuvaa na kujipamba kwa kiasi. (1 Timotheo 2:9) “Vitabu” vitakavyofunguliwa wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu bila shaka vitakuwa na amri zitakazofaidi wanadamu. Sasa ni vizuri kujizoeza kutii amri zinazofaa ambazo zinafanywa ili kuwe utaratibu na zinazofanywa kwa kusudi la kuwafikiria wengine.​—Ufunuo 20:12; 1 Wakorintho 10:24; Wafilipi 2:3, 4.

Katika Ulimwengu Huu wa Jeuri

19, 20. (a) Watu wa Yehova wameitikiaje kanuni katika Mika 4:3? (b) Kufanya hivyo kunawafaidije wakati wa “siku za mwisho”?

19 Tunakaribia haraka sana wakati ambapo mkono wa kila mtu “utainuliwa ili kushindana na mkono wa jirani yake.” (Zekaria 14:13) Ulimwengu unapokuwa wenye uvunjaji wa sheria na jeuri zaidi na zaidi, watu wa Yehova wanatendaje? Wanatenda kwa kupatana na andiko la Mika 4:3, linalosema: “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu.” Mashahidi wa Yehova wanakataa kila aina ya jeuri. “Wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Bila shaka, kufanya hivyo kutaendelea kuwa kwa faida yao wakati wote wa “siku za mwisho.” Tayari imekuwa hivyo.

20 Kwa mfano, gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1983 lilipotaja kwamba bunduki hazipasi kutumiwa na Wakristo Mashahidi wa Yehova katika New Caledonia waliondolea mbali bunduki zao. Muda mfupi baada ya hapo, kikundi cha kisiasa kimoja cha mahali hapo kikafanya msako katika mji mmoja, kikachoma kila nyumba mlimopatikana bunduki. Lakini hakuna nyumba za Mashahidi zilizoharibiwa. Kujulikana kuwa wenye hali ya kutokuwamo mara nyingi ndiko ulinzi bora zaidi, kama ambavyo imethibitika kuwa katika Ailandi ya Kaskazini, Lebanon, Zimbabwe na nchi nyinginezo.

21. (a) Tunapaswa kuitikia mwito gani, nasi tunapaswa kufanya azimio gani tukitaka kuwa furaha kweli kweli? (b) Tunaweza kuhakikishiwaje kuushiriki wema wa Yehova?

21 Sisi ni wenye furaha tukiitikia mwito wa Isaya 2:5: “Njoni, twende katika nuru ya [Yehova]”! Sote, pia, ni wenye furaha tunaojiunga katika azimio thabiti linalosemwa na nabii Mika ambaye, baada ya kusimulia usalama na amani ya kiparadiso iliyoko kati ya watu wa Mungu mwenyewe, anaendelea kusema: “Mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake, na sisi tutakwenda kwa jina la [Yehova], Mungu wetu, milele na milele.’ Hakika Yehova atawaonyesha wema wake wote wanaoendelea kujiunga kwa amani katika ibada ya kweli, waokolewe wapite “siku za mwisho.”

[Maelezo ya Chini]

a Ona matoleo ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) ya Juni 15 na Julai 1, 1962, kwa mazungumzo ya kirefu ya unabii wa Yakobo.

Maswali ya Muhtasari

◻ Unaelewa nini kuhusu “siku za mwisho”?

◻ Ni jinsi gani tunaweza ‘kumwendea Yehova na wema wake kwa kicho’?

◻ Unabii wa Yakobo akiwa mahututi kitandani unatupa mwongozo gani?

◻ Ni hatua gani za kutenda tunazoweza kuchukua kwa kupatana na Isaya 2:2-5 na Mika 4:1-5?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Hosea anatutia moyo tufuate mfano wa wema wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yakobo anasimulia sifa zinazofaa na zisizofaa

[Picha katika ukurasa wa 27]

Isaya anatukaribisha ‘tutembee katika nuru ya Yehova’

[Picha katika ukurasa wa 28]

Mika anatutia moyo ‘twende kwa jina la Yehova milele’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki