Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 3/1 kur. 26-30
  • Kupata Shangwe ya Ushindi Katika “Siku za Mwisho”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupata Shangwe ya Ushindi Katika “Siku za Mwisho”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Manabii wa Amani
  • Shambulio la Gogu
  • ‘Siri Zafunuliwa’
  • “Msukumano” wa Kisasa
  • “Niko Dhidi Yako, Ewe Gogu”
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Gogu wa Magogu Ataharibiwa Hivi Karibuni
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2017
  • Simameni, Mkauone Wokovu wa Yehova!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 3/1 kur. 26-30

Kupata Shangwe ya Ushindi Katika “Siku za Mwisho”

“Yuko Mungu mbinguni afunuaye siri, naye [amejulisha] . . . mambo yatakayokuwa siku za mwisho.”​—DANIELI 2:28.

1. (a) Unabii wa Yeremia, Ezekieli, na Danieli unatupendeza sana sisi leo jinsi gani? (b) Ni kwa sababu gani maandishi hayo yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yalihifadhiwa?

YEREMIA, EZEKIELI, DANIELI—majina hayo yanatukumbusha unabii mbalimbali wenye kusisimua kama nini! Karibu miaka 2,600 iliyopita, watumishi hao watatu walio hodari wa Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova waliishi wakapita siku za mwisho za Yerusalemu ulioasi imani, ingawa walikuwa wakitumikia katika sehemu tofauti tofauti na chini ya hali zilizotofautiana sana. Lakini kila mmoja wao akiwa katika kikao chenye kufaa alitabiri kuhusu matukio ambayo yangefikia upeo katika “siku za mwisho” za baadaye. Maandishi hayo yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yamehifadhiwa ili yatie moyo wote wanaopenda Mungu na uadilifu. na wanaotaka kuokoka “dhiki kubwa” inayokaribia katika wakati wetu.​—Mathayo 24:3-22; Warumi 15:4.

2. Ni kwa sababu gani Yeremia alihitaji nguvu kutoka kwa Yehova?

2 Yeremia alitabiri akiwa Yerusalemu. Msiba ulipokaribia, watawala pamoja na watu walikuwa ni wavunjaji wa sheria na waliopotoka. Kwa hiyo, Yehova alimtia nguvu nabii wake kama “ukuta wa boma la shaba” ili asimame imara katikati ya ubaya wao.​—Yeremia 15:11, 20; 23:13, 14.

Manabii wa Amani

3. Ni maneno gani ya uwongo waliyokuwa wakisema manabii?

3 Kuhusu viongozi wa kidini wenye kuvunja sheria wa Yerusalemu, Yehova alitangaza hivi kupitia Yeremia: “Msisikilize maneno ya manabii wakiwatabiria; huwafundisha ubatili; hunena maono ya mioyo yao wenyewe: hayakutoka katika kinywa cha [Yehova]. Daima huwaambia wao wanaonidharau, [Yehova] amesema, Mtakuwa na amani.” Manabii hao wa uwongo walikuwa wakisema, “Amani, Amani,” kumbe hakukuwa amani.​—Yeremia 23:16, 17; 6:14.

4. Wengi katika Jumuiya ya Wakristo wanashikilia tumaini gani?

4 Hali moja na hiyo, katika Jumuiya ya Wakristo iliyoasi imani leo, kuna manabii wa amani. Wengi wao wanashikilia kile ambacho Papa Paulo wa Sita alieleza kuwa ndicho “tumaini la mwisho la upatano na amani,” Umoja wa Mataifa. Karibuni, baraza hilo litatangaza mwaka 1986 kuwa Mwaka wa Kimataifa wa Amani. Katika kutangaza kusudio lake la kushiriki katika Mwaka huo, Makao ya Papa yalitangaza kwamba yanalo “tumaini kwamba Mwaka huu utatokeza matokeo yanayotakiwa na utatia alama hatua ya maana katika kuleta uhusiano wa amani kati ya makundi ya watu na mataifa.” Lakini je, ni jambo linalopatana na mambo ya uhakika kutazamia mataifa yalete amani ya kweli?

5. Yehova anatabiri nini, na jambo hilo litatimizwaje katika “siku za mwisho”?

5 Mungu mwenyewe anaeleza yatakayotokea hivi: “Tazama, tufani ya [Yehova], yaani, ghadhabu yake, imetokea; ni dhoruba ya kisulisuli; itapasuka, na kuwaangukia waovu vichwani. Hasira ya [Yehova] haitarudi, hata atakapokwisha kuyatimiza makusudi ya moyo wake; katika siku za mwisho mtalifahamu neno hili kabisa.” (Yeremia 23:19, 20; ona pia 30:23, 24.) Ndiyo, viongozi wa dini ya uwongo watakuja kuelewa maana ya “siku za mwisho” kwao. Lakini kuzifikiria kwao kwa vyo vyote kutakuwa ni kuchelewa mno!—Linganisha Ufunuo 18:10, 16; 19:11-16; Mathayo 24:30.

6. Kutakuwa na matokeo gani ya furaha kwa wengi?

6 Hata hivyo, kwa furaha, watu wengi waliokuwa wakati mmoja watumwa wa dini ya uwongo ‘wanazifahamu.’ Wanajibu mwito huu: “Tokeni kwake [dini ya uwongo], enyi watu wangu.” kwa kuwa hawataki kushiriki katika dhambi zake wala kupokea sehemu ya hukumu ya Mungu itakayoletwa juu yake. Ikiwa wewe ni mmoja wao, endelea kutii yanayosemwa na Neno la Mungu juu ya “siku za mwisho” na kipindi kitukufu cha amani kitakachofuata.​—Ufunuo 18:2, 4, 5; 21:3, 4.

Shambulio la Gogu

7. Ezekieli alitabiri akiwa chini ya hali gani?

7 Inakuwaje kwa watu wa Mungu wenyewe wakati wa “siku za mwisho”? Acheni nabii Ezekieli atuambie. Akiwa kijana, bila shaka alimjua Yeremia, lakini ndipo Ezekieli alipopelekwa mpaka Babulonia. Huko, kando ya mto Chebari, aliagizwa mwaka 613 K.W.K. atende akiwa nabii wa Yehova na mlinzi kwa ajili ya Wayahudi waliokuwa utumwani, utumishi aliotekeleza kwa uaminifu kwa miaka angalau 22. Hata hivyo, unabii wake mbalimbali ni wa kufikia mbali zaidi ya wakati wake mwenyewe. Katika sura za 38 na 39, anaeleza juu ya ‘Gogu wa Magogu.’

8, 9. (a) Ni suala gani kubwa linalopasa kusuluhishwa, na wakati gani? (b) Gogu ni nani, ni nani wanaomfuata, naye anafuata mwongozo gani? (c) Yehova atamfanya nini Gogu?

8 Huyu ‘Gogu wa Magogu’ ni nani? Ni nani adui mkubwa zaidi wa Yehova ambaye Yehova anapaswa kumaliza kati yake na yeye suala kuu la “siku za mwisho,” lile suala la enzi kuu ya ulimwengu wote? Adui huyo ni Shetani Ibilisi, ambaye Mfalme-Mchungaji, Yesu Kristo, alimtupa chini kutoka mbinguni baada ya kutawazwa Kwake mwenyewe mwaka 1914. Gogu aliyeshushwa na mwenye hasira amefungiwa sasa kwenye makao ya kiroho yenye mipaka, “nchi ya Magogu,” kwenye ujirani wa dunia hii. Hiyo maana yake ni “ole kwa nchi” kwa sababu Gogu anajua kwamba wakati unakwisha wa kutekeleza mwongozo wake mbovu wa ‘ukiweza tawala, ukishindwa haribu.’​—Ezekieli 37:24-28; 38:1, 2; Ufunuo 11:18; 12:9-17.

9 Ezekieli anakariri Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova akisema: “Tazama, mimi ni juu yako, Ewe Gogu, mkuu [mtawala wa ulimwengu] . . . nami nitakugeuza na kutia kulabu katika mataya yako, nami nitakutoa, pamoja na jeshi lako lote, . . . watu wengi pamoja nawe.” (Ezekieli 38:3-6; Yohana 12:31) Ndiyo, Gogu ana watu wengi pamoja naye, kwa maana “ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, NW) Hata hivyo, Yehova anaweza kuweka kulabu za mfano katika mataya ya Gogu ili amwongoze. Lakini kwa sababu gani, na jinsi gani?

10. (a) Tofauti na mataifa, Mashahidi wa Yehova wanaweka tumaini lao wapi? (b) Ni kwa sababu gani Gogu na kundi lake wanaghadhibika? (c) Ni lazima tufanye nini ili tuokolewe?

10 Kwa kusukumwa na Gogu, mataifa yenye nguvu sana leo yanabishana kwamba amani ya ulimwengu inategemea kurundika kwayo silaha za nyukilia zinazozidi kuwa zenye kuogopesha daima. Na mataifa mengine yanaunga mkono. Hata hivyo, watu wa Mungu “waliokusanyika toka mataifa” wamekataa silaha za jeuri. Mashahidi wa Yehova ndio “taifa” pekee duniani linaloweza kusema kikweli, “Sisi twamtumaini Mungu.” (Isaya 2:4; 31:1; Mithali 3:5) Mashahidi hao wa Yehova wanaopenda amani ‘wanakaa kwa usalama, wote wakikaa pasipo kuta, wala hawana makomeo wala malango.’ Wanakaa “katikati ya dunia,” kwa maana katika mataifa yote, wako katikati ya jukwaa wakiwa ndio watu pekee ambao Gogu hajafaulu kuumiza kwa mashambulio yake. (Ezekieli 38:11, 12) Kwa hiyo, Gogu wa Magogu mwenye ghadhabu analeta tengenezo lake lote la kishetani kwenye eneo la vita. Kama simba angurumaye, Shetani asiye na adili kabisa anajitayarisha kufanya shambulio la kufa na kupona. Ili tuokoke, ni lazima ‘tumpinge, tukiwa thabiti katika imani.’​—1 Petro 5:8, 9.

11. Yehova ‘anamletaje Gogu ashambulie nchi Yake,’ na kwa kusudi gani?

11 Yehova anamwagiza Ezekieli hivi: “Basi, mwanadamu, tabiri, umwambie Gogu, Bwana [Yehova] asema hivi; Katika siku ile watu wangu, Israeli [wa kiroho], watakapokaa salama, hutapata habari?” Gogu na kundi lake wanaonea kijicho usalama na fanaka wanayoona kati ya Mashahidi wa Yehova leo. Wanaghadhibika kwamba hawajifanyi “sehemu ya ulimwengu” wa Shetani. Kwa hiyo Yehova anamchokoa Gogu, kumwamsha ashambulie Mashahidi wake wasio na kinga. Yehova anamwambia Gogu hivi: “Nawe utapanda juu uwajilie watu wangu, Israeli, kama wingu kuifunika nchi; itakuwa katika siku za mwisho, nitakuleta upigane na nchi yangu, ili mataifa wanijue nitakapotakaswa kwako. Ewe Gogu, mbele ya macho yao.”​—Ezekieli 38:14, 16; Yohana 17:14, 16, NW.

12. Kulingana na Ezekieli 38:18-23, matokeo ya shambulio la Gogu ni nini?

12 Gogu mwenye ghadhabu anasonga ashambulie “nchi” yenye kufanikiwa ya watu wa Yehova. Lakini, je, Gogu ndiye pekee aliyeghadhibika? Namna gani ghadhabu ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova kuelekea Gogu na vibaraka wake? Katika Ezekieli 38:18-23 Yehova anaeleza jinsi ‘atakavyojitakasa mbele ya macho ya mataifa’ kwa kumwangamiza Gogu na kundi lake, Bwana Mwenye Enzi Kuu mwenyewe anatangaza hivi: “Watajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova].” Jina lake tukufu litaondolewa lawama!

‘Siri Zafunuliwa’

13. Danieli aliwekeaje mfano mzuri Mashahidi vijana?

13 Ezekieli alipokuwa akitabiri kati ya Wayahudi waliohamishwa karibu na Babuloni, Danieli kijana, aliyekuwa wa nasaba ya Kiyahudi ya wana wa kifalme, alikuwa akielimishwa katika baraza la kifalme la Nebukadreza. Huko, akiwa mshika ukamilifu, aliwawekea mfano mwema watumishi wote wa Yehova walio vijana leo.​—Danieli 1:8, 9.

14. Ni katika jambo gani Danieli kijana alimpa Mungu sifa yote?

14 Katika mwaka wa pili baada ya kuanguka kwa Yerusalemu, Nebukadreza alitiwa wasiwasi mwingi na ndoto moja. Alipoamka, alishindwa hata kuikumbuka ndoto hiyo. Lakini Danieli mwenye kumwogopa Mungu alimjulisha mfalme ndoto yenyewe na ufasiri wayo. Kwa kufanya hivyo, alimpa Mungu sifa yote, akamwambia mfalme hivi: “Yuko Mungu mbinguni afunuaye siri, naye amemjulisha mfalme Nebukadreza mambo yatakayokuwa siku za mwisho.” (Danieli 2:28) Tunajifunza nini kwa ndoto hiyo na inavyohusu “siku za mwisho”?

15, 16. Tafsiri ya ndoto ya Nebukadreza ni nini?

15 Hapa twaona sanamu kubwa sana, ambayo kwa sehemu kubwa imetengenezwa kwa madini tofauti tofauti zenye kufuatana. Danieli anaeleza kwamba madini hizo zinafananisha mfululizo wa falme na kumwambia Nebukadreza hivi, “Wewe u kichwa kile cha dhahabu,” kwa wazi akiwa anazungumza juu ya nasaba ya wafalme wa Babulonia. Mamlaka nyingine za ulimwengu zinafuata, kifua na mikono ya fedha kufananisha Umedi na Uajemi, tumbo na viuno vya shaba kufananisha Ugiriki, miguu ya chuma kufananisha Roma na, baadaye, mamlaka ya ulimwengu ya Uingereza na Amerika. (Danieli 2:31-40) Wakati wote wa “majira ya mataifa,” tangu mwaka 607 K.W K. mpaka 1914 W.K., mamlaka hizo zimetawala katika ufalme wa ‘mungu wa ulimwengu huu.’​—Luka 21:24; 4:5, 6; 2 Wakorintho 4:4.

16 Hata hivyo, ni “wakati wa siku za mwisho” kwamba “mbegu za wanadamu,” yaani, watu wa kawaida tu, wanajitokeza. Katika nchi nyingi watawala ambao ni wafalme, makaiseri na matzari wanaondolewa kisha badala yao kunakuwa na watawala wanaoleta mabadiliko makubwa na pia watawala wa kidemokrasi. Utawala mbaya wa kibinadamu duniani unakuwa mchanganyiko wa tawala za ukatili za kidikteta na namna namna za serikali za kidemokrasi zinazofuata mapendezi ya watu. Kama vile chuma na udongo, vitu hivyo havichangamani. Hata katika Umoja wa Mataifa hawasikizani bali wanashiriki katika mabishano na matishano. Kweli kweli, ‘umekuwa ufalme uliogawanyika.’​—Danieli 2:41-43.

17. Unabii unatimizwaje katika “siku za mwisho”?

17 Kwa hiyo, katika “siku za mwisho,” suala la utawala wa ulimwengu linafikia upeo wake. Suluhisho ni nini? Tazama! Tayari Ufalme wa Mungu wa Kimasihi unatenda tangu mwaka 1914. Huo ndilo “jiwe” lililokatwa toka kwenye “mlima” wa enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote. Hakuna mwanasiasa ye yote wa kibinadamu anayeshiriki kufanya hivyo! Lione likija, likiwa kwenye njia yake barabara, kwa usahihi kabisa. Kwa wakati wake Mungu, linaigonga miguu ya sanamu hiyo na kuisaga-saga tikitiki iwe unga. Kama vile makapi mbele ya upepo, utawala wa kibinadamu unaondolewa, pasibaki masalio hata kidogo. Lakini “jiwe” hilo​—Ufalme wa Mungu mkuu na Kristo wake​—linakuwa mlima mkubwa na kuijaza dunia yote. Ufalme huo ‘hautaangamizwa kamwe wala watu wake hawataachiwa enzi yake.’ Utasimama milele. Jinsi tunavyomshukuru Yehova kwa kutangulia ‘kufunua’ siri hizo!​—Danieli 2:29, 44, 45.

“Msukumano” wa Kisasa

18. (a) Ni njozi gani ya baadaye aliyopewa Danieli? (b) Ni jambo gani lenye kutokeza kuhusu njozi hiyo?

18 Hata hivyo, Danieli alikuwa na jambo zaidi la kusema juu ya serikali za kibinadamu na “siku za mwisho.” Miaka 70 hivi baada ya kujulisha ndoto ya Nebukadreza, Danieli mwenye umri mkubwa alikuwa angali katika Babuloni lakini akitumikia chini ya Koreshi (Sairasi), mfalme wa Uajemi. Alipokuwa kando ya mto Hidekeli, malaika alimtokea, akasema: “Nimekuja kukufahamisha mambo yatakayowapata watu wako katika siku za mwisho maana maono hayo ni ya siku nyingi bado.” (Danieli 10:14) Malaika huyo aliendelea kusimulia kwa kindani sana watawala na matukio ambayo yangetokea katika historia ya Waajemi. Wagiriki, Wamisri, Waroma, ya Kijeremani, ya Uingereza na Amerika, na namna namna za utawala wa kisoshalisti. Inatokeza kama nini kwamba historia yote hii, yenye kuchukua miaka zaidi ya 2,500, ingeweza kuandikwa kimbele! Jambo hilo linatupa uhakika mkubwa katika Neno la kiunabii lililoongozwa kwa roho ya Yehova Mungu!a

19. Unabii huo unatabiri juu ya matukio gani ya kisasa?

19 Unabii huo unaeleza kwamba, baada ya muda, mataifa mawili makubwa yangetokea, “mfalme wa kusini” na “mfalme wa kaskazini.” Hatimaye, malaika huyo anasema, mfalme wa kaskazini “atajitukuza na kujiadhimisha juu ya kila mungu, naye atanena maneno ya ajabu”​—si maneno yanayofaa, kwa maana ‘anamtukuza mungu wa ngome.’ Kinyume cha “mfalme” huyo mwenye majivuno kuna “mfalme wa kusini.” ambaye pia ana uwezo mwingi wa kijeshi. Kama ilivyotabiriwa, wafalme hao wawili ‘watashindana’ (‘watasukumana,’ NW) Vita ya maneno ya kisasa kati ya mataifa hayo makubwa inaonyesha kwa njia nzuri jambo hilo. Nyakati nyingine ‘wanasukumana’ kwa ufidhuli wanapobishania usawa wa silaha za nyukilia, huku wakizidisha sana matayarisho yao ya vita kufikia upeo.​—Danieli 11:36-45.

20. Ni jambo gani linaloamua matokeo, na “Mikaeli” anahusikaje katika hilo?

20 Ingawa unabii huo unatabiri kwamba “mfalme wa kaskazini” ataingia kwa nguvu kama upepo wa kisulisuli katika nchi nyingi, jambo hilo halitakuwa lenye kuamua matokeo. Jambo lenye kuamua linasemwa katika Danieli 12:1: “Wakati huo Mikaeli atasimama jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana. wa watu wako.” Mikaeli huyo ni Yesu Kristo, ‘aliyesimama’ katika Ufalme wake mwaka 1914, mara moja akamtupa Shetani kutoka mbinguni. Na ni huyo ‘Mfalme wa wafalme’ anayechukua hatua katika Har–Magedoni awaangamize “wafalme wa nchi” wote kutia wale wa “kaskazini” na “kusini.”​—Ufunuo 12:7-10; 19:11-19.

21. Basi, matokeo ni nini katika “siku za mwisho”?

21 Huko, kwenye upeo wa “siku za mwisho,” matokeo yatakuwa wazi. Ufalme wa Mungu utashinda. Malaika huyo anaendelea kueleza kwa maneno haya: “Kutakuwa na wakati wa taabu mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo.”​—Danieli 12:1; linganisha Yeremia 25:31-33; Marko 13:19.

22. Tukiwa watu wa Mungu, unabii huo unapasa kuwa na matokeo gani kwetu na tukiwa na taraja gani?

22 Je! tunapaswa kuogopa wakati huo wa dhiki na taabu? Hatupaswi kuogopa ikiwa tuko upande wa Yehova, kwa maana malaika huyo anaendelea kusema: “Wakati huo watu wako wataokolewa; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile. “(Danieli 12:1) Basi, acheni sote, tujikaze katika funzo la Biblia la bidii na kujitahidi kumtumikia Yehova. Hivyo, katika “siku za mwisho,” na tukute majina yetu yameandikwa katika “kitabu cha ukumbusho” cha Mungu ‘kinachoandikwa mbele zake kwa ajili ya hao waliomcha Yehova, na kulitafakari jina lake.’ (Malaki 3:16) Kwa kufanya hivyo, tutapendelewa kushiriki katika ushindi wake “katika siku za mwisho.”

[Maelezo ya Chini]

a Kwa maelezo marefu, ona kitabu “Your Will Be Done on Earth,” kilichochapishwa mwaka 1958 na Sosaiti yetu, kurasa 220-323.

Kwa habari ya “siku za mwisho”​—

◻ Yeremia alitabiri matokeo gani kuhusu amani ya ulimwengu?

◻ Shambulio la Gogu linatokeza kusuluhishwa kwa suala gani, na jinsi gani?

◻ Ndoto ya Nebukadreza inaelekeza kwenye upeo gani mkubwa?

◻ Mashindano ya nguvu kati ya “wafalme” hao wawili yatafikiaje mwisho?

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

ALAMA iliyokubaliwa na Umoja wa Mataifa iwe ya Mwaka wayo wa Amani ya Kimataifa (1986) inaonyesha matawi ya mzeituni, njiwa, na mikono ya kibinadamu. Maana ya vitu hivyo inaelezwa hivi: “Njiwa ni mfano wa amani kwa kushirikiana na tawi la mzeituni lililo ishara ya Umoja wa Mataifa. Mikono ya kibinadamu inayotegemeza njiwa aliye tayari kuruka inakazia sehemu ya wanadamu katika kudumisha amani.”

Katika kizazi hiki cha nyukilia, hakika kuna uhitaji mkubwa wa kuleta amani na kuidumisha. Lakini je, mikono ya kibinadamu inaweza kutimiza hilo? Yeremia anatukumbusha hivi: “Ee [Yehova], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Na nabii huyo anaongeza ombi hili: “Ee [Yehova], . .. hasira yako uwamwagie mataifa wasiokujua.”​—Yeremia 10:23-25.

Njiwa na jani la mzeituni ni kutoka maandishi ya Biblia juu ya siku za Noa. (Mwanzo 8:11) Amani ilirejezwaje wakati huo? Ilikuwa kupitia tendo la Mungu, gharika ya duniani pote iliyofagia kizazi kilichopotoka cha wanadamu. Yesu alisema kwamba “siku za Noa,” pamoja na jeuri na ubaya wazo, zilikuwa unabii wa wakati wa “kuwapo” kwake, ambako ni sasa.​—Mathayo 24:37-39, NW; Mwanzo 6:5-12.

Kwa mara nyingine, “Mungu wa amani” lazima afagilie mbali mfumo wa mambo wa kishetani, ndipo “Mfalme wa amani,” Yesu Kristo, ataleta amani ya milele.​—Warumi 16:20; Isaya 9:6, 7; 33:7.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Yeremia anaelekeza kwenye tumaini la kweli la amani

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ezekieli anatuonya tujitayarishe sasa kwa ajili ya shambulio la Gogu

[Picha katika ukurasa wa 29]

Danieli anafunua matokeo ya “siku za mwisho”

(Makala ya Funzo la Kitabu)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki