Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 4/1 kur. 23-28
  • ‘Kimbieni kwa Njia Ambayo Mtapata Thawabu’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Kimbieni kwa Njia Ambayo Mtapata Thawabu’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Kuwaogopa Wanadamu”
  • Vifungo vya Jamaa
  • Rafiki Zako Ni “Wenye Hekima” au Ni “Wapumbavu”?
  • Pata Thawabu!
  • “Msiruhusu Mtu Ye Yote Awanyang’anye Thawabu” (Makala ya Funzo la Kitabu)
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Usiruhusu Chochote Kikunyang’anye Tuzo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • “Hakuna Kitu cha Kuwakwaza” Wale Wanaompenda Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • “Kimbia Mbio Mpaka Mwisho”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 4/1 kur. 23-28

‘Kimbieni kwa Njia Ambayo Mtapata Thawabu’

Je! hamjui kwamba wakimbiaji katika mbio wanakimbia wote, lakini ni mmoja tu anayepokea thawabu? Kimbieni kwa njia ambayo mtaipata.”​—1 Wakorintho 9:24, Biblia ya New World Translation.

1, 2. (a) Balaa kubwa ingekuwa nini kwa Mkristo leo? (b) Ni shauri gani alilotoa Paulo katika 1 Wakorintho 9:24, na liliwahusuje Wakristo katika Korintho?

HUO ungekuwa upeo mkuu wa miaka 12 ya matayarisho ya jasho. Lakini mwendo unaozidi nusu kidogo wa mbio hizo, mwanariadha kijana huyo wa kike akaanguka chini, kwa ghafula ndoto yake ya kupata medali ya dhahabu ya Olimpiki ikaisha. Vyombo vya habari viliita kuanguka kwake “balaa.”

2 Hata hivyo, ingekuwa balaa kubwa zaidi kushindwa kwa shahidi wa Yehova kumaliza mbio za uzima, hasa wakati huu ambao Utaratibu. Mpya ulioahidiwa uko karibu sana! (2 Petro 3:13) Kwa kufaa, basi, mtume Paulo alisema: “Je! hamjui kwamba wakimbiaji katika mbio wanakimbia wote, lakini ni mmoja tu anayepokea thawabu? Kimbieni kwa njia ambayo mtaipata.” (1 Wakorintho 9:24, NW) Wengine katika Korintho wa kale walikuwa katika hatari ya kushindwa kwa sababu walitenda kwa uchoyo kama walivyotaka, hata kuleta hasara ya ‘kutia jeraha dhamiri’ za wengine. (1 Wakorintho 8:1-4, 10-12) Hata hivyo, kushinda mbio kulitia ndani dhabihu, kwa maana Paulo alisema: “Kila mtu anayeshiriki katika shindano anazoea kujiweza . . . mimi naupiga-piga ngumi mwili wangu na kuufanya kama mtumwa, ili, nikiisha kuhubiria wengine, mimi mwenyewe nisije nikakataliwa kwa njia fulani.”​—1 Wakorintho 9:25-27, NW.

3. (a) Ni hali gani iliyokuwako katika Kolosai ambayo ingeweza kuwazuia Wakristo huko wasimalize mbio? (b) Je! ilifaa Wakristo katika Kolosai wajifunze falsafa na mafumbo?

3 Baadaye, alipokuwa akiwaandikia Wakolosai, Paulo alionya juu ya uwezekano wa hatari nyingine​—watu ambao ‘wangewanyang’anya thawabu’ ya uzima. (Wakolosai 2:18, NW) Kwa hiyo Wakristo wangeweza ‘kukimbiaje kwa njia ya kuweza kuipata’? Je! mtume huyo alikuwa akidokeza wajifunze falsafa na mambo ya mafumbo ili wabishane kwa kufanikiwa na walimu wa uwongo? Hapana, kwa maana Wakristo walikuwa ‘wamekufa kuelekea mambo ya awali ya ulimwengu’ nao walipaswa wasijishughulishe na falsafa na mapokeo yake.​—Wakolosai 2:20.

4. Kupata ‘maarifa sahihi’ kungeweza kuwasaidiaje Wakristo katika Kolosai?

4 Kwa hiyo, Paulo aliwatia moyo waamini wenzake wakaze jitihada zao juu ya ‘kujazwa maarifa sahihi ya mapenzi ya Mungu katika hekima yote na ufahamu wa rohoni.’ Ndiyo, ‘maarifa sahihi​—wala si madhanio matupu​—yangewasaidia ‘waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Yehova, wampendeze kabisa.’ (Wakolosai 1:9, 10; ona pia Wakolosai 3:10.) Ni kweli kwamba Wakristo walio wengi katika Kolosai bila shaka waliweza kutaja mafundisho ya msingi ya Maandiko. Lakini kupitia funzo na kutafakari, walihitaji kwenda zaidi ya mambo ya msingi na ‘kuwekwa juu ya msingi wa Kristo wakiwa imara.’ (Wakolosai 1:23; 1 Wakorintho 3:11) Baada ya kuwa na kina hicho, ‘hakuna mtu ye yote angewadanganya kwa maneno ya kushawishi.’ (Wakolosai 2:4) Kupitia matumizi ya ufundi ya Neno la Mungu, wangeweza kukanusha kwa matokeo mazuri madai ya watu wo wote wenye kuabudu malaika au wafuasi wa dini ya Kiyahudi.​—Kumbukumbu la Torati 6:13; Yeremia 31:31-34.

5. (a) Toa mifano mingine ya “mambo yenye kina” ambayo Mkristo aliyekomaa anapaswa kujua na kufahamu. (b) Jambo lililompata dada mmoja linaonyeshaje hatari ya kutotwaa ‘maarifa sahihi’?

5 Lakini, wewe je, umesonga mbele ya yale “mafundisho ya kwanza” na kuangalia ndani ya “mambo yenye kina ya Mungu”? (Waebrania 6:1, UV; 1 Wakorintho 2:10, NW) Kwa mfano, je, unaweza kutambua wanyama wa Ufunuo au kueleza hekalu la kiroho ni nini? (Ufunuo, sura 13; Waebrania 9:11) Je! unaweza kueleza msingi wa Kimaandiko wa tengenezo la kisasa la Mashahidi wa Yehova? Je! umeimarishwa vizuri katika mafundisho ya Biblia? Dada mmoja Mkristo aliliona kuwa jambo gumu kutetea imani zake alipokuwa akizungumza juu ya Utatu na mwanamke mwingine. Baadaye, mwanamke huyo alimpa dada yetu vitabu vilivyochongea tengenezo la Yehova. “Nilishuka moyo sana kiroho,” anakumbuka Shahidi huyo. Jambo la kufurahisha ni kwamba, mzee mmoja aliweza kufunua madai hayo ya uwongo ya wapinzani na kurejeza imani ya dada yetu (Yuda 22, 23) “Sasa nafahamu,” asema dada huyo, “ni kwa sababu gani Sosaiti daima inasema tusali, tujifunze, na kutafakari.”

“Kuwaogopa Wanadamu”

6. (a) Ni nini kimekuwa kikwazo kwa watumishi wengine wa Mungu? Toa mifano mingine ya Kibiblia. (b) Ni nini ambacho mara nyingi kinatokeza kuogopa wanadamu?

6 “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego,” alionya mtu mwenye hekima. (Mithali 29:25) Na nyakati nyingine ‘hofu isiyofaa ya mauti’ au tamaa mbaya ya kutaka kukubaliwa na wengine inamsukuma mtu kwenye mtego huo. (Waebrania 2:14, 15) Kwa mfano, Eliya bila woga alipinga wazoeaji wa ibada ya Baali. Lakini Malkia Yezebeli alipoagiza auawe, “yeye akaogopa . . . na kuanza kwenda kwa ajili ya nafsi yake na kuja Beersheba.” (1 Fal. 19:1-3, NW) Usiku aliokamatwa Yesu, mtume Petro hali moja na hiyo alishindwa na hali ya kuogopa wanadamu. Ingawa Petro alikuwa amejivuna, “Bwana, niwapo pamoja nawe, mimi ni tayari kwenda gerezani au hata kifoni,” aliposhtakiwa kuwa ni mmoja wa wanafunzi wa Kristo, “ndipo akaanza kulaani na kuapa akisema, Simjui mtu huyu.”​—Luka 22:33; Mathayo 26:74.

7. (a) Inaelekea sababu yenyewe iliyowafanya wengine katika Kolosai watake kuchanganya Ukristo na dini ya Kiyahudi ni nini? (b) Ni nani leo ambao inaelekea wanasukumwa kwenye tendo hilo?

7 Tamaa yenye woga ya kutaka kukubaliwa huenda ikawa ndiyo iliyokuwa sababu yenyewe hasa ya wengine kutaka kuchanganya Ukristo na dini ya Kiyahudi. Wakati wafuasi wa dini ya Kiyahudi walipotokea Galatia, Paulo alifunua unafiki wao, akisema: “Wote wanaotaka kuonekana kuwa wazuri kwa mwili, wanawalazimisha ninyi kutahiriwa; wasiteswe tu.” (Wagalatia 6:12, ZSB) Je! yaweza kuwa tamaa iyo hiyo ya kutaka kukubaliwa na wengi imekuwa pia ndiyo kani yenye kutendesha wengine ambao hivi majuzi wameliacha tengenezo la Yehova?

8, 9. (a) Ni jinsi gani Mkristo leo anaweza kuonyesha anaogopa wanadamu? (b) Woga huo unaweza kushindwaje?

8 Wakristo wanapaswa kujitahidi kushinda woga wa namna hiyo. Ikiwa unasita kuhubiri katika maeneo yaliyo karibu na nyumbani mwako, au unasita kutolea ushuhuda watu wa ukoo, wafanyi kazi wenzi, au wanashule wenzako, kumbuka ulizo ambalo Yehova anauliza katika Isaya 51:12: “Wewe u nani hata ukamwogopa mtu atakayekufa, na mwanadamu atakayefanywa kuwa kama majani?” (Linganisha Mathayo 10:28.) Jikumbushe kwamba ye yote ‘amtumainiye [Yehova] atakuwa salama.” (Mithali 29:25) Petro alishinda hali yake ya kuogopa wanadamu, mwishowe akafia imani. (Yohana 21:18, 19) Na ndugu wengi leo wanaonyesha uhodari uo huo.

9 Mmisionari mmoja anayetumikia katika nchi ambayo kazi ya kuhubiri imepigwa marufuku alisema: “Inataka imani kwenda kwenye mkutano au katika utumishi, ukijua kwamba inawezekana ukashikwa na polisi.” Lakini akina ndugu huko walisema kama mtunga zaburi: “[Yehova] yuko upande wangu, sitaogopa; mwanadamu atanitenda nini?” (Zaburi 118:6) Nayo kazi katika nchi hiyo ilisitawi, hivi majuzi ikatambuliwa kisheria. Ushiriki wa kawaida katika huduma ya shambani utakusaidia wewe kwa hakika usitawishe tumaini lilo hilo kwa Yehova.

Vifungo vya Jamaa

10. (a) Ni uhitaji gani wa kindani ulio na kila mtu, na kwa kawaida unatimizwaje? (b) Toa mifano ya Biblia ya watu ambao uhusiano wao na wake zao ulikuwa wenye nguvu zaidi ya uhusiano wao na Yehova.

10 Kitabu chenye kichwa The Individual, Marriage, and the Family kinasema: “Uhitaji wa kila mtu binafsi katika jumuiya zote na katika sehemu zote za jumuiya ni uhitaji wa ‘kuwa wa fulani’ na ‘kuwa na fulani’ mwingine aliye wa maana kwake.” Uhitaji huo kwa kawaida unatimizwa kupitia mpango wa jamaa, ambao ni utokezaji wa Yehova. (Waefeso 3:14, 15) Hata hivyo, Shetani mara nyingi anatumia vibaya uhusiano tunaohisi kuelekea washiriki wa jamaa. Hisia zenye nguvu za Adamu kumwelekea mkeye kwa wazi zilimsukuma apuuze matokeo yake naye akajiunga na mkeye katika uasi. (1 Timotheo 2:14) Na vipi Sulemani? Ijapokuwa hekima yake iliyojulikana sana, “ikawa, Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakamgeuza moyo wake, afuate miungu mingine, wala moyo wake haukuwa mkamilifu kwa [Yehova], Mungu wake . . . Sulemani akafanya yaliyo mabaya machoni pa [Yehova].”​—1 Wafalme 11:4-6.

11. Eli ‘aliheshimuje wanaye kuliko Yehova’?

11 Je! unamkumbuka Eli mzee, kuhani mkuu wa Israeli? Wanaye Hofni na Finehasi walikuwa “watu wasiofaa kitu” ambao ‘hawakumjali Yehova.’ Walionyesha utovu mkubwa wa heshima kwa dhabihu za Yehova na kufanya ngono zisizo za adili “na wanawake waliokuwa wakitumika mlangoni pa hema ya kukutania.” Hata hivyo Eli alipopinga hayo, alifanya hivyo kwa upole sana (“Mbona mnatenda mambo kama hayo?”), bila kufanya jitihada yo yote ya kuwaondoa kwenye cheo chao chenye pendeleo. Ndiyo kusema, alikuwa ‘akiheshimu wanaye kuliko Yehova’ nalo hilo likatokeza kifo chake na chao!—1 Samweli 2:12-17, 22, 23, 29-34; 4:18.

12. (a) Ni onyo gani alilotoa Yesu kuhusu vifungo vya jamaa? (b) Ni wazo gani la kilimwengu ambalo wengine wanafuata watu wa ukoo wanapohusika lakini je, hilo linafaa Kimaandiko?

12 Ushikamanifu unaoelekezwa kusikofaa unaweza, basi, kukuzuia wewe katika mbio ya uzima. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Apendaye baba au mama kuliko mimi hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili.” (Mathayo 10:37; Luka 14:26) Lakini namna gani kama mpendwa angeuacha ukweli au atengwe na ushirika? Je! wewe ungefuata wazo la kilimwengu kwamba “damu ni nzito kuliko maji” na kumfuata mtu huyo wa ukoo mpaka kwenye uharibifu? Au je, ungeamini maneno ya Zaburi 27:10: ‘Hata baba yangu na mama yangu wakiniacha, Yehova atanikaribisha kwake’?

13. Wana wa Kora walithibitishaje ushikamanifu wao kwa Yehova, nao walibarikiwaje kwa ajili ya hilo?

13 Wana wa Kora walikuwa na imani kama hiyo. Baba yao aliongoza uasi wa kupinga mamlaka ya Musa na Haruni. Hata hivyo, Yehova alithibitisha kwa njia yenye mkazo kwamba aliunga mkono Musa na Haruni kwa kuua Kora na wafanya hila wenzake. Hata hivyo “wana wa Kora hawakufa.” (Hesabu 16:1-3, 28-32; 26:9-11) Kwa wazi walikataa kujiunga na baba yao katika uasi, na Yehova alibariki ushikamanifu wao kwa kuwahifadhi hai. Wazao wao baadaye walikuwa na pendeleo la kuandika visehemu vya Biblia!—Ona matangulizi ya juu ya Zaburi 42, 44-49, 84, 85,87, 88, New World Translation.

14, Ni jambo gani lililoonwa linaloonyesha baraka inayoletwa na kuweka ushikamanifu kwa Yehova juu ya ushikamanifu kwa watu wa ukoo?

14 Vivyo hivyo ushikamanifu leo unatokeza baraka. Shahidi mmoja kijana anakumbuka msimamo aliochukua yeye pamoja na nduguze wakati mama yao, ambaye alikuwa amekuwa Mkristo asiyetenda kwa muda mrefu, alipoingia katika ndoa ya uzinzi. “Tuliripoti kwa wazee,” anakumbuka, “na kwa kuwa mama hakuwa akiishi nyumbani, tuliamua kupunguza ushirika wetu naye mpaka wazee washughulikie mambo hayo. Lilikuwa ndilo jambo gumu zaidi tulilokuwa tumepata kufanya.” Mama huyo alipinga hivi, “Je! uzima wa milele wenu unamaanisha zaidi kwenu kuliko mimi? Wakajibu, “Uhusiano wetu na Yehova unamaanisha zaidi ya cho chote.” Mwanamke huyo aligutushwa aonyeshe toba ya moyo mweupe, akarejezwa kiroho, na anatumikia tena akiwa mhubiri mwenye kutenda wa habari njema.

15. (a) Wazazi wengine wameruhusuje watoto wao wenyewe wawe vikwazo? (b) Mzazi anaweza kujisaidiaje mwenyewe na watoto wake wapate uzima?

15 Wengine wameruhusu watoto wao wenyewe wawe vikwazo. Kwa kukosa kutambua kwamba “ujinga umefungwa ndani ya moyo” wa vijana, wazazi wengine wameruhusu watoto wao washirikiane kwa ukaribu na walimwengu, wahudhurie shughuli za kirafiki zenye kuchukiza, na hata kufanya matembezi na watu wa jinsia tofauti na wao wakiwa wachanga mno kutoweza kufunga ndoa. (Mithali 22:15) Mara nyingi matokeo yenye msiba ya uendekevu ni nini? Kuvunjikiwa hali ya kiroho. (1 Timotheo 1:19) Wengine hata wanazidisha kosa hilo kwa kuficha kwa hila kosa lililofanywa na watoto wao! (Mithali 3:32; 28:13) Lakini, kwa kushikilia kwa ushikamanifu kanuni za Biblia, mzazi anajisaidia mwenyewe na watoto wake kupata thawabu ya uzima wa milele.​—1 Timotheo 4:16.

Rafiki Zako Ni “Wenye Hekima” au Ni “Wapumbavu”?

16. (a) Rafiki zetu wanaweza kuwaje uvutano wenye nguvu? (b) Ni nani hasa walio rahisi kuongozwa na uvutano wa marafiki, na kwa sababu gani?

16 Kitabu Sociology: Human Society kinasema: “Tamaa ya mtu kutaka heshima ya rafikize wa karibu inatia mkazo mkubwa wa kujipatanisha na viwango vyao.” Kitabu Adolescence kinaonyesha kwamba vijana hasa wanaelekea kushindwa na mkazo huo. Kinasema: “[Hiyo ni kwa sababu] ya mabadiliko wanayopata mwilini mwao, mawazo ya kibinafsi, na uhusiano pamoja na jamaa. Kwa hiyo, wabalehe wanaanza kutumia wakati zaidi na rafiki zao na [wakati] mchache zaidi na jamaa zao.”

17. (a) Onyesha kwa mfano ukweli wa maneno ya Mithali 13:20. (b) Ni marafiki wa aina gani wanaoweza kuonwa kuwa “wenye hekima”? (c) Vijana leo wanaweza kufuataje mfano wa kijana Samweli?

17 Yasiyopasa kusahauliwa ni maneno ya Mithali 13:20: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” Msichana mmoja Mkristo anakiri hivi: “Ule ushirika mwingi mbaya ulio katika shule yetu hakika unaanza kunigeuza. Leo nilijishtukia nikienda kusema neno la matusi shuleni . . . karibu niliseme, lakini sikulisema.” Inasikitisha kusema kwamba vijana wengine Wakristo wameongozwa kwenye kufanya vitendo vizito sana vya mwenendo mbaya na wanaoitwa ati marafiki. Lakini ikiwa wewe ni kijana anayetamani kupata thawabu, tafuta rafiki wenye hekima​—wale wenye akili ya kiroho, walio wanyofu katika mwenendo wao, wenye usemi wenye kujenga. Kumbuka, kijana Samweli hakushirikiana na wana wabaya wa Eli. Alijishughulisha sana ‘akimtumikia Yehova,’ kwa njia hiyo akabaki bila kuwa na doa la upotovu wao.​—1 Samweli 3:1.

Pata Thawabu!

18. (a) Ndugu wengine, labda bila kujua, wanaweza kutuzuiaje katika mbio ya uzima? (b) Ni nini cha kutulinda na mavutano hayo yasiyofaa?

18 Basi, jihadhari na ye yote ambaye angependa kukunyang’anya thawabu ya uzima. Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba unapaswa kuwatilia shaka ndugu zako. Hata hivyo, nyakati nyingine, labda bila kujua, ndugu wengine huenda wakasema mambo yanayokuvunja moyo. (‘Mbona unajikaza mno? Kwani unafikiri ni wewe peke yako utapata uzima?’) Huenda hata wakahukumu kwa njia isiyo ya fadhili jitihada zako za moyo mweupe. (‘Mimi sioni jinsi unavyoweza kupainia ukiwa na jamaa. Hiyo ni kuumiza watoto.’) Hata hivyo, kumbuka Yesu alikataa shauri la Petro kwamba ‘asijikaze.’ (Mathayo 16:22, 23) Tumia masikio yako yaliyozoezwa kwa Biblia ‘kujaribu maneno,’ na kutovutwa na yale yasiyosikika kuwa ya kweli. (Ayubu 12:11) Kumbuka kwamba Paulo alisema: “Ye yote akishindana hata katika michezo, hapewi taji isipokuwa ameshindana kulingana na sheria.” (2 Timotheo 2:5, NW) Ndiyo, “sheria” za Mungu​—wala si maoni yasiyo ya kimaandiko​—ndizo zinazopasa kuongoza kufikiri kwako.​—Linganisha 1 Wakorintho 4:3, 4.

19, 20. (a) Ndugu za Yusufu walijaribuje kumuumiza, naye Yusufu aliitikiaje ukosefu wao wa fadhili? (b) Tunaweza kuepukaje kukwazwa na wanadamu wasiokamilika? (c) Azimio letu lapasa kuwa nini kwa habari ya thawabu, na kwa sababu gani?

19 Ni kweli kwamba nyakati nyingine huenda Mkristo mwenzako ‘akakuchoma’ kwa neno fulani lenye kusemwa bila kufikiri. (Mithali 12:18) Usiruhusu hilo likufanye uache mbio ya uzima Mkumbuke Yusufu. Ndugu zake mwenyewe walifikiria kumuua, na ingawa walizuiwa wasifanye hivyo, mwishowe walimuuza katika utumwa wa ukatili. Hata hivyo, Yusufu hakuruhusu hilo limtie uchungu au ‘amkasirikie Yehova.’ (Mithali 19:3, ZSB) Badala ya kulipa kisasi, baadaye aliwapa nafasi ya kuonyesha nia iliyobadilika. Na alipoona toba yao, “akawabusu ndugu zake wote, akalia nao.” Kama Yakobo alivyosema baadaye, “wapiga mishale [ndugu za Yusufu wenye wivu] walimtenda machungu, wakamtupia, wakamwudhi.” Hata hivyo Yusufu alilipa chuki yao kwa fadhili. Badala ya kudhoofishwa na jambo hilo, “mikono yake ikapata nguvu.”​—Mwanzo 37:18-28; 44:15–45:15; 49:23, 24.

20 Kwa hiyo badala ya kukwazwa na wanadamu wasio wakamilifu, endelea ‘kukimbia kwa njia ambayo utapata’ thawabu! Kama Yusufu, ruhusu mashambulio ya jaribu yakutie nguvu badala ya kukudhoofisha. (Linganisha Yakobo 1:2, 3.) Ruhusu upendo wako kwa Mungu uwe wenye nguvu nyingi hata mwanadamu ye yote asiwe kikwazo kwako. (Zaburi 119:165) Sikuzote kumbuka kwamba Yehova anatoa thawabu ya uzima wa milele​—thawabu isiyoelezeka, isiyowazika. Usiruhusu mtu ye yote akunyang’anye!

Je! Wewe Unakumbuka?

◻ Ni kwa sababu gani maarifa sahihi ni yenye thamani sana kwa Wakristo?

◻ Mtu anaweza kushindaje hali ya kuogopa wanadamu ambayo imezuia wengine wasipate uzima?

◻ Jamaa ya mtu mwenyewe inaweza kuwaje kikwazo?

◻ Mkristo atendeje anapoambiwa na Wakristo wenzake maneno ya kuvunja moyo au hata yenye kuumiza?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kwa kujaza akili na mioyo yetu maarifa sahihi, tunajitayarisha kukanusha mawazo yenye makosa

[Picha katika ukurasa wa 26]

Petro alimkana Yesu kwa sababu ya kuogopa wanadamu. Baadaye, mtume huyo alishinda woga huo. Ndivyo wanavyopaswa kufanya Wakristo wote wa kweli

(Makala ya Funzo la Kitabu)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki