“Msiruhusu Mtu Ye Yote Awanyang’anye Thawabu”
(Makala ya Funzo la Kitabu)
“Msiruhusu mtu ye yote awanyang’anye thawabu ambaye anapendezwa na unyenyekevu wa kujisingizia . . . akiwa amefurishwa bila sababu inayofaa na hali yake ya akili yenye maoni ya kimwili.”—WAKOLOSAI 2:18, New World Translation.
1, 2. Wengi wametendaje kinyume cha faida za milele za wanadamu wenzao, na je, unaweza kutaja mifano zaidi ya hilo katika Biblia?
MTENDA dhambi wa kwanza binadamu, Hawa, aliongozwa kwenye kifo chake na kiumbe mjanja wa kiroho mwenye nguvu zinazopita zile za kibinadamu. Mtenda dhambi wa pili, Adamu, alishawishwa na mkeye—binadamu dhaifu.—1 Timotheo 2:14; Mwanzo 3:17.
2 Hawa alikuwa wa kwanza wa mwandamano wa watu ambao maombi yao, kama yangalifuatwa yangaliharibu faida za milele za wanadamu wenzao. Sikiliza maneno yao kama yanavyosikika katika Biblia yote! Mkeye Potifa amwambia Yusufu hivi: “Lala nami.” (Mwanzo 39:7) Mkeye Ayubu: “Umkufuru Mungu, ukafe.” (Ayubu 2:9) Waisraeli wakimwambia Haruni hivi: “Haya! katufanyizie miungu.” (Kutoka 32:1) Petro akimwambia Yesu Kristo: “Jihurumie, Bwana; hutapatwa kamwe na hayo yaliyokusudiwa.”—Mathayo 16:22, NW.
3. Paulo alitoa onyo gani katika Wakolosai 2:18, na kwa sababu hiyo ni maswali gani yanayotokea?
3 Mara nyingi sana maombi hayo yameleta uharibifu kwa watumishi wa Yehova. Kwa hiyo ingawa ni kweli kwamba Wakristo wana “kushindana... juu ya majeshi ya pepo,” mara nyingi wanadamu wenzao ndio hatari ya karibu. (Waefeso 6:12) Kwa hiyo mtume Paulo alionya hivi: “Msiruhusu mtu ye yote awanyang’anye thawabu.” (Wakolosai 2:18, NW) Thawabu hiyo ni nini? Na ni kwa sababu gani wengine wa watumishi wa Yehova wameipoteza kwa kukubali kushindwa na uvutano wa wanadamu wasiokamilika? Katika kujibu, ebu tuchunguze hali katika Kolosai zilizomfanya Paulo atoe onyo hilo.
4, 5. (a) Ni mavutano gani ya kidini yaliyokuwako katika Kolosai? (b) Dini ya Mafumbo ilikuwa nini, nayo matokeo yake yenye hatari huenda yakawa yalitokeza uvutano gani?
4 Kolosai palikuwa mahali pa mchanganyiko wa dini. Wafirgia wakazi wa hapo walikuwa watu wenye kuongozwa na maono ya ndani walioshiriki sana mambo ya uchawi na ushirikina wa ibada ya sanamu. Halafu kulikuwa na wakaaji wa mji huo Wayahudi, waliokuwa wangali watumwa wa dini ya Kiyahudi, Kukaribiana kwa Kolosai pia na njia kuu ya kibiashara kulitokeza mmiminiko wa wageni daima. Inaelekea, wageni hao walipenda kutumia wakati wao wa starehe wakieleza au kusikiliza jambo jipya. (Linganisha Matendo 17:21.) Jambo hilo lilitokeza mwenezo wa falsafa mpya, kati yazo pole kwa pole ukatokea ugnosti (dini ya mafumbo). Asema hivi mwanachuo E. 0. White: “Dini ya mafumbo ilikuwa mawazo yaliyoenea kama nadharia ya mageuzi ilivyo leo. Inaelekea ilikuwa maarufu katika karne ya kwanza au mapema na ikafikia upeo wake katika [karne] ya pili. Iliunganisha dhana za kifalsafa, ushirikina, sherehe za nusu-uchawi, na nyakati nyingine sherehe za kidini zenye kushikiliwa kwa wivu mwingi bila sababu na hata za matusi.”
5 Katika mazingira hayo, dini katika Kolosai yaelekea ilikuwa jaribio lililokuwa likiendelea—mchanganyiko wa dini ya Kiyahudi, falsafa ya Kigiriki, na dini ya mafumbo ya upagani. Je! Ukristo, pia, wangeingia katika mchanganyiko huo?
‘Wanyang’anywa Thawabu’—Jinsi Gani?
6. (a) Maneno ya Paulo yangaliweza kuzuiaje uvutano wa falsafa za kipagani na dini ya Kiyahudi? (b) Ni kwa sababu gani Wakristo walihitaji ‘kuangalia’?
6 Barua ya Paulo yenye nguvu kwa Wakolosai ingalizuia uvutano wa ye yote ambaye angalitaka kuunganisha dini ya Kiyahudi na falsafa ya kipagani pamoja na Ukristo. Kwa kurudia-rudia, alielekeza fikira kwenye Kristo. Paulo aliandika hivi: “Ndani yake yeye [Kristo, wala si kwa mfuasi ye yote wa dini ya Kiyahudi au mwanafalsafa mpagani] hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika.” Wakolosai walisihiwa ‘waenende vivyo hivyo katika yeye [Kristo]; wakiwa na shina na wenye kujengwa katika yeye; na kufanywa imara kwa imani.’ Kama sivyo, wangepotezwa. Kwa hiyo Paulo alionya hivi: “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, ,kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo.”—Wakolosai 2:3, 6-8.
7. (a) Ni kwa sababu gani huenda ikawa mafundisho ya wanafalsafa wapagani na wafuasi wa dini ya Kiyahudi yalivutia Wakristo wengine? (b) Ni kwa sababu gani mafundisho yao kwa kweli yalikuwa “madanganyo matupu”?
7 Labda wengine wa wafuasi wapya wa Yesu Kristo walijisikia wakitamani maajabu ya mambo ya mafumbo au msisimuo wa falsafa. Huenda ikawa Wakristo fulani wa Kiyahudi walikuwa wangali na tamaa-tamaa ya mapokeo yaliyobatilishwa ya dini ya Kiyahudi. Mafundisho ya wanafalsafa wapagani na wafuasi wa dini ya Kiyahudi kwa sababu hiyo yangewavutia watu hao. Hata hivyo, ijapokuwa walimu hao wa uwongo walionekana kuwa wenye usadikishi au ufasaha sana, hawakutoa cho chote isipokuwa “madanganyo matupu.” Badala ya kueleza wazi neno safi la Mungu, walikuwa wakirudia kama kasuku tu “mafundisho ya awali ya ulimwengu”—falsafa, maagizo, na masadikisho yasiyofaa kitu. Kufuata mawazo hayo yenye kosa kungemaanisha msiba kwa Mkristo. Kwa hiyo, Paulo alisema: “Msiruhusu mtu ye yote awanyang’anye thawabu.”—Wakolosai 2:18, NW.
8. (a) “Thawabu” ilikuwa nini, na ni maandiko gani yanayounga mkono jibu lako? (b) Wakristo wapakwa mafuta wangaliweza kunyang’anywaje “thawabu”?
8 “Thawabu” hiyo ilikuwa ni uzima usioweza kufa katika mbingu. Ulifananishwa na thawabu aliyopewa mkimbiaji mshindi baada ya mbio za miguu zenye kuchosha sana. (1 Wakorintho 9:24-27; Wafilipi 3:14; 2 Timotheo 4:7, 8; Ufunuo 2:7) Hatimaye, ni Yehova Mungu peke yake kupitia Yesu Kristo angeweza kumnyang’anya mtu ustahili katika mbio za uzima. (Yohana 5:22, 23) Hata hivyo, kama mwalimu wa uwongo angemleta Mkristo kwenye mafundisho yake, jambo hilo lingaliweza kuwa na matokeo ya kumnyang’anya thawabu hiyo. Mwenye kudanganywa angeenda mbali sana na ukweli hata ashindwe kumaliza mbio hizo!
Utu wa Walimu wa Uwongo
9. Ni mambo gani manne yaliyotambulisha walimu wa uwongo kati ya Wakolosai?
9 Basi, je, kulikuwako njia yo yote ya kumtambua mtu aliyekuwa na nia ya ‘kumnyang’anya Mkristo thawabu’? Ndiyo, kwa maana Paulo alieleza namna utu wa walimu wa uwongo ulivyokuwa katika Kolosai. Mtu wa namna hiyo (1) “anapendezwa na unyenyekevu wa kujisingizia na namna ya kuabudu malaika”; (2) ‘“akichukua msimamo wake kwa’ mambo aliyokuwa ameona; (3) “akiwa amefurishwa bila sababu inayofaa na hali yake ya akili yenye maoni ya kimwili”; ,na huku (4) “yeye hashikilii kwa uthabiti kichwa,” Yesu Kristo.—Wakolosai 2:18, 19, NW.
10. Walimu wa uwongo ‘walipendezwaje na unyenyekevu wa kujisingizia’?
10 Ni udanganyifu wa ujanja kama nini! Kwa kupuuza lawama ya Yesu juu ya kufunga kula ili kujionyesha, mwalimu wa uwongo aliweka kibandiko chenye kuvutia cha unyenyekevu. (Mathayo 6:16) Kweli kweli, mwalimu huyo wa uwongo ‘alipendezwa’ kujionyesha amefunga kula na namna nyingine za kujinyima kwa kidini. (Wakolosai 2:20-23) Sura yake ya uso wenye huzuni ilifanywa kwa uangalifu ili kuonyesha utawa wa uwongo. Kweli kweli, mwalimu huyo wa uwongo alikuwa ‘akizoea uadilifu wake mbele ya watu ili aonwe nao.’ (Mathayo 6:1, NW) Lakini yote hayo yalikuwa ni kujifanya, “unyenyekevu wa kujisingizia.” Kama kitabu The Expositor’s Bible kinavyosema: “Mtu anayejua yeye ni mnyenyekevu, naye anaridhika kwa kujisikia ndivyo alivyo akitumia kando za macho yake yenye huzuni kuangalia-angalia kwenye kioo cho chote anachoweza kujiona, si mnyenyekevu hata kidogo.”—Italiki ni zetu.
11. (a) Kuabudu malaika kulikuwa nini? (b) Kuna ushuhuda gani kwamba kuabudu malaika kuliendelea katika Kolosai?
11 Hata hivyo, unyenyekevu huo wa uwongo ulifanya zoea la ujinga—“kuabudu malaika,” lielekee kuwa lenye kusadikika. Paulo haelezi ni jinsi gani hasa ibada hiyo ilifanywa. Hata hivyo, ushuhuda ni kwamba ilikuwa namna ya ibada ya uwongo iliyokuwapo katika eneo la Kolosai kwa karne nyingi. Baraza la karne ya nne kwenye mji wa Laodikia uliokuwa karibu liliona ni jambo la lazima kutangaza hivi: “Wakristo hawapaswi kuliacha Kanisa la Mungu, na . .. kuitia majina ya malaika. . . . Kwa hiyo, ye yote, akipatikana anazoea ibada hiyo ya sanamu inayofanywa faraghani, na alaaniwe.” Hata hivyo, mwanatheolojia na mwanachuo wa karne ya tano, Theodoreti, anadokeza kwamba “uovu huu” wa ibada ya malaika ungali ulikuwako siku zake. Mpaka leo hii, Kanisa Katoliki “linatia moyo waaminifu wapende, waheshimu, na kuomba malaika,” likiendelea kuwa na “Misa na Vyeo vya Kimungu kwa heshima ya malaika walinzi.”—New Catholic Encyclopedia, kitabu cha Kwanza, ukurasa 515.
12. Ni kwa njia gani huenda ikawa walimu wa uwongo walidhani kwamba kuabudu malaika kulikubalika?
12 Akitumia namna ya msingi ya kuwaza inayofanana na ile ya wanatheolojia wa Katoliki, huenda mwalimu wa uwongo akawa alisema: ‘Malaika wana pendeleo zuri ajabu! Je! kwani Torati ya Musa haikutolewa kupitia kwao? Je! kwani hawako karibu na Mungu mbinguni? Hakika tunapaswa kuwapa hawa wenye nguvu heshima wanayostahili! Je! kufanya hivyo hakungeonyesha unyenyekevu wa kweli upande wetu? Ingawaje, Mungu yuko juu sana, nasi wanadamu tuko chini sana! Kwa hiyo, malaika wanaweza kutumikia kuwa wapatanishi wetu katika kumkaribia Mungu.’
13. (a) Je! kuabudu malaika kunakubalika? (b) Mwalimu wa uwongo alichukuaje “msimamo wake kwa” mambo aliyokuwa ameona’?
13 Hata hivyo, kuabudu malaika kwa namna yo yote, ni kosa. (1 Timotheo 2:5; Ufunuo 19:10; 22:8, 9) Lakini mwalimu wa uwongo alijaribu kusukuma kando katazo hilo ‘“akichukua msimamo wake kwa” mambo aliyokuwa ameona.’ Kulingana na kitabu The Vocabulary of the Greek Testament, usemi huo ulitumiwa “katika dini za mafumbo kuonyesha upeo wa unyago, wakati mwenda unyagoni ‘anapokanyaga’ mwingilio wa maisha mapya ambayo sasa atayashiriki na mungu.” Kwa kutumia maneno ya kipagani, Paulo alifanyia mzaha njia ambayo mwalimu wa uwongo alijivunia kuwa na ufahamu wa pekee—labda hata akidai kuwa aliona maono yanayopita hali za kibinadamu.
14. Walimu wa uwongo walikuwa ‘wamefurishwaje na hali ya kimwili ya akili’?
14 Hata ingawa alidai kuwa wa kiroho, mwalimu wa uwongo alikuwa amefurishwa kweli kweli bila sababu inayofaa na hali yake ya akili yenye maoni ya kimwili. Mwili wenye dhambi uliongoza maoni na makusudio yake. “Akiwa amefurishwa” na kiburi na ukaidi, akili yake ilikuwa kwenye ‘matendo mabaya.’ (Wakolosai 1:21) Jambo baya zaidi ya yote, hakuwa akishikilia kwa imara kichwa, Kristo, kwa maana alikuwa akikazia zaidi madhanio ya walimwengu zaidi ya mafundisho ya Yesu.
Je! Kungali na Hatari?
15. (a) Ni maoni gani yanayoonwa kati ya Wakristo fulani leo? (b) Maoni hayo yanatoka wapi, nayo yakoje yakilinganishwa na mashauri ya Biblia?
15 Thawabu ya uzima wa milele—uwe ni wa kimbingu au juu ya dunia-paradiso—ingali inatolewa kwa watumishi wa Yehova. Ni kweli kwamba wafuasi wa dini ya Mafumbo na wanadini wa Kiyahudi walikwisha zamani. Hata hivyo kuna watu mmoja mmoja ambao huenda sasa wakamzuia Mkristo asipate thawabu hiyo. Huenda wasifanye hivyo kwa makusudi. Hata hivyo, kwa sababu wamejiruhusu waongozwe isivyofaa na ‘elimu ya bure na madanganyo matupu’ ya mfumo huu, huenda wakasema:
‘Mimi najaribu kuwa mnyofu, lakini ni vigumu unapoendesha biashara. Huu ni ulimwengu mkatili, na nyakati nyingine ni lazima kutenda kinyume cha yanayofaa.’ (Linganisha maoni hayo na Mithali 11:1; Waebrania 13:18.)
“Ati ungali mke wa nyumbani? Nyakati zimebadilika! Tafuta kazi ya kuajiriwa na utumie maisha yako!’ (Linganisha Mithali 31:10-31.)
‘Najua kazi yangu inazuia sana mikutano na huduma ya shambani. Lakini mtindo wetu wa maisha unataka pesa nyingi. Na kuna ubaya gani kuwa na vitu vichache vizuri?’ (Tofautisha kuwaza huko na Luka 21:34, 35; 1 Timotheo 6:6-8.)
‘Mimi nachoka kusikia wazee wakisema daima juu ya utumishi wa shambani! Nafanya kazi juma lote nami nastahili starehe mwishoni mwa juma.’ (Linganisha Luka 13:24; Marko 12:30.)
‘Si kila mtu anayeweza kupainia. Isitoshe, katika uchumi wa leo unahitaji elimu ya chuo kikuu ikiwa utafaulu.’ (Tofautisha na Mathayo 6:33; 1 Wakorintho 1:19, 20; 1 Timotheo 6:9-11.)
Kuwaza kwa kibinadamu na kimwili ni sehemu ya “mafundisho ya awali ya ulimwengu”—maagizo na masadikisho ya msingi ya walimwengu! Kukubali kushindwa nayo kwaweza kusababisha umizo la kiroho lisiloweza kurekebishwa.
16. Wengine leo wanaweza kuwaje waamuzi wanafiki?
16 Watu wanaojifanya kuwa waamuzi na walimu wanaweza kutokeza hatari nyingine. Kama wale katika Kolosai, wanabisha juu ya mambo ya kibinafsi tu. Mara nyingi ni wenye “unyenyekevu wa kujisingizia.” (Wakolosai 2:16-18, NW) Nia yao kwamba ni watakatifu zaidi ya wengine inaonyesha maoni mabaya—tamaa ya kujikweza juu ya wengine. Mara nyingi ni wenye “haki kupita kiasi,” wakifanya haraka kupita kiasi cha yale ambayo “mtumwa mwaminifu” amesema au kuchapisha. Kwa hiyo huenda wakachochea magomvi juu ya mambo kama vile tafrija, utunzaji wa afya, mitindo ya mavazi na kujipamba, au matumizi ya vileo. (Mhubiri 7:16; Mathayo 24:45-47) Kwa njia hiyo mkazo unaondolewa kwenye mambo ya kiroho na kuwekwa kwenye tamaa za kimwili.—Linganisha 1 Timotheo 6:3-5.
17, 18. (a) Wengine ‘wamechukuaje msimamo wao kwa’ mambo ya kibinafsi, na ni kwa sababu gani hilo ni jambo hatari? (b) Somo letu lifuatalo litazungumza juu ya nini?
17 Leo, wengine hata wanafikia kadiri ya ‘kuchukua msimamo wao kwa’ maoni ya kibinafsi ya Maandiko, au wanadai wana ufahamu wa pekee. Mwanamke mmoja, aliyekuwa amebatizwa kwa mwaka mmoja tu, alidai kuwa ni mpakwa mafuta naye alifikiri kwamba jambo hilo liliyapa maoni yake uzito. Kwa hiyo akaonyesha tamaa nyingi ya “kufundisha na kutia moyo wengine” wapate cheo fulani rasmi.(Lakini ona 1 Timotheo 2:12.) Kwa kuwa Yehova anachukia “kiburi na majivuno,” Wakristo wanapaswa kuwa na kiasi juu ya maoni yao. (Mithali 8:13) Wanaepuka mtego wa ‘kufurishwa bila sababu inayofaa na hali yao ya akili.’ (Wakolosai 2:18) Wo wote wanaosisitiza juu ya mawazo yao ya kibinafsi na kuharibia sifa mashauri ya “mtumwa mwaminifu” aliyewekwa na Kristo hawashikilii kichwa kwa uthabiti. Basi, kwa uhakika, mashahidi washikamanifu wa Yehova wanapaswa kujihadhari na uvutano usio wa kimungu ambao unaweza kuwanyang’anya thawabu ya uzima.
18 Shetani angali anatumia wanadamu kuzuia wanadamu wenzao wasipate uzima. Ni njia gani nyingine ambazo Ibilisi anatumia kutendesha mbinu hiyo? Na shahidi wa Yehova anawezaje kuishikilia thawabu kwa dhati? (Itaendelezwa)
Je! Wewe Unakumbuka
◻ Ni mavutano gani ya kidini yaliyohatirisha Wakristo katika Kolosai wa kale?
◻ Tabia za kuwatambulisha wale waliotaka kunyag’anya Wakristo “thawabu” zilikuwa gani?
◻ Wakristo wengine leo wanaonyeshaje kwamba wamevutwa na “mafundisho ya awali ya ulimwengu”
◻ Walimu wa uwongo wanaweza kuongozaje Wakristo kwenye mwendo mbaya?
[Picha katika ukurasa wa 25]
‘Ibada ya malaika’ ilihatarisha kundi la Kikristo katika Kolosai. Ibada ya sanamu kama hiyo inaendelea kati ya Wakristo wa kujidai leo
[Picha katika ukurasa wa 27]
Jihadhari na wale ambao wangependa kukuvuta kwa mawazo ya kilimwengu!