Je! Maono ya Miujiza ya Kidini ni Ushuhuda wa Roho ya Mungu Leo?
“SAUTI zilitokea kana kwamba nilikuwa nimejua jinsi ya kufanya katika maisha yangu yote,” ndivyo alivyoeleza mwanamke aliyeanza kusema katika “lugha.” Aliongeza kusema: “Lilikuwa jambo la asili sana na zuri sana. Nilijiona mwenye amani sana, amani ya ndani na kuwa karibu sana na Mungu. Nikalia. Hakuna jambo ambalo ungeweza kufanya isipokuwa kulia tu, ilikuwa vizuri sana.”
Mwanamke huyu ni mmoja wa mamia ya maelfu ya wale wanaodai kwamba roho ya Mungu imewapa “karama” (Kigiriki ni cha·risʹma·ta) kama zile za kuponya magonjwa, kutoa unabii na kusema lugha wasizojua. (Linganisha 1 Wakorintho 12:4, 9, 10.) Mara nyingi matukio hayo yanafuatana na maono ya miujiza ya kidini, ambayo kitabu Encyclopcedia Britannica (chapa ya 1974) kinaeleza kuwa “maono ya ndani-ndani ya kuwa na njozi ya Mungu au maono ya uhusiano wa mtu au umoja na mungu.”
Matokeo hayo ya ndani yenye nguvu yakifuatana na “maono” hayo yameongoza wengi katika kusadiki kwamba wamepokea roho takatifu ya Mungu. Je! kweli maono ya miujiza ya kidini ni ushuhuda wa roho ya Mungu leo?
Katika historia yote ya wanadamu watu mmoja mmoja wasiohesabika wa aina zote za imani ya kidini wametoa ushuhuda wa kwamba wametokewa na miujiza. Kwa mfano, maono kama hayo yalikuwa mengi katika “dini za mambo ya siri” za kale za kipagani nayo yalionwa kuwa ushuhuda wa “kuzaliwa upya” katika maana ya kisiri. Lakini ijapokuwa maono haya yalikuwa yenye kupendeza, hayakutokana na Mungu, kwa maana Biblia yasema hivi juu ya desturi hizo za kidini: “Vitu vile [mataifa] wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu.”—1 Wakorintho 10:20.
Kitabu cha Biblia cha Ayubu kinasimulia usemi wa Elifazi, Mtemani ambao katika huo anaeleza maono ya miujiza ya kidini: “Pepo [roho] ilipita mbele ya uso wangu; na nywele za mwili wangu zilisimama. . . . mfano ulikuwa mbele ya macho yangu; kulikuwa kimya, nami nilisikia sauti.” (Ayubu 4:15, 16) Walakini, maono hayo yaliyotokezwa na pepo au roho hayakutokana na Mungu, kwa sababu Mungu alimkemea Elifazi ‘kwa kuwa hakunena yaliyo sawa katika habari zangu.’—Ayubu 42:7.
Namna gani leo? Je! ingeweza kuwa kwamba maono ya miujiza ya kidini ambayo watu fulani husema yanatokana na ‘kuzaliwa kwa roho takatifu’ hayatokani na Mungu hata kidogo? Ni wazi hivyo, kwa maana maono hayo mazuri huenda bado yakafuatana na desturi ambazo Mungu anakataa. Kwa mfano, katika kitabu chake kiitwacho Patterns of Prophecy, mtungaji wacho, Alan Vaughan anasema juu ya kuwa katika hali ya kuona maajabu: “Namna ya maono yenye upendo inatokana mara nyingi na hali hii, nayo hali ya ndani ya kujisikia vizuri inazuka na kutokeza maono yenye karama ya miujiza. “Lakini badala ya kuona uwezo wa maajabu kama ushuhuda wa roho ya Mungu, Biblia inaonyesha desturi za mambo ya siri kama vile kuwa na uwezo wa kuona vituko vya miujiza na kujua mambo yasiyojulikana na wengine kuwa ni desturi zinazohusiana na mashetani au “pepo wabaya.”—Matendo 16:16; Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Waefeso 6:12.
Kwa wazi, basi, maono ya miujiza ya kidini au uwezo mwingine wa ajabu si ushuhuda wa roho ya Mungu. Kwa kweli, huenda yanatokana na mashetani. Kwa hiyo, mtu anawezaje kujua kama kweli ana roho takatifu ya Mungu?
Ushuhuda wa hili ungeonekana hasa kwa jinsi mtu anavyojiendesha mwenyewe kila siku. Kama mtume Paulo anavyoeleza: “Ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho.” (Warumi 8:9) Roho ya Mungu inakuwa ndiyo nguvu inayoongoza mwenendo wa Mkristo katika kupingana na nguvu mbaya ya “mwili” wenye dhambi. Kitabu Theological Dictionary of the New Testament kinalinganisha wazo hili na maneno ya Paulo, katika Warumi 7:20, “dhambi ikaayo ndani yangu.”
“Kukaa kwa dhambi ndani ya mtu kunaonyesha kumtawala . . . Si mgeni anayepita, bali inakuwa bwana wa nyumba kwa vile inavyoendelea kuwapo. . . walakini, Paulo anaweza kusema vivyo hivyo kwa habari ya ubwana wa Roho hiyo. . . . ‘Kukaa’ huku si maono ya ndani yenye furaha na shauku nyingi sana.”
Mtu anawezaje kujiweka chini ya “ubwana” wa roho ya Mungu katika maisha yake? Bila shaka si kwa kujaribu kusitawisha “Maono Yanayopita Maono Yote” kwa kupuza makusudi tu “ule ujumbe wa fahamu,” kama kitabu kinachosema juu ya “mambo ya mafumbo” kinavyotia moyo. Biblia inashauri hivi: “Msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.” (Warumi 12:2) Vivyo hivyo tunasoma katika Wakolosai 3:9-11 hivi: “Mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake; mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba.”
Kwa hiyo ili mtu awe na roho ya Mungu, yampasa kwanza ‘ageuze nia yake’ kwa njia ya kupata “ufahamu sawasawa” wa yanayokubaliwa na Mungu. Maana yake inampasa mtu ajifunze Biblia kwa uangalifu. Kisha yampasa awe ‘mtendaji wa neno,’ akifuatisha maisha yake na kanuni za kimungu ambazo amejifunza.—Yakobo 1:22-25.
Lakini je! roho ya Mungu iliyowajia Wakristo wa karne ya kwanza haikujionyesha wazi kwa miujiza waliyowezeshwa kufanya? Mungu aliwapa Wakristo nguvu za pekee wakati huo. Lakini nguvu hizi zilitimiza kusudi la pekee. Katika njia hii Mungu alitoa ushuhuda kwa njia ya “ishara na ajabu na nguvu za namna nyingi” kuonyesha kwamba ‘watu wa jina lake’ duniani hawakuwa tena kundi la Kiyahudi bali walikuwa kundi la Kikristo. (Waebrania 2:4; Matendo 15:14) Mara uhakika huo ulipothibitishwa kusingekuwa tena na uhitaji wa nguvu hizo za miujiza. Miujiza hiyo ilitumiwa na kundi la Kikristo wakati wa mwanzo wake tu nayo ilipaswa ‘ibatilike.’ (1 Wakorintho 13:8) Hivyo, Yesu hakusema kwamba wafuasi wake wa kweli wangejulikana kwa kuwa na maono yenye shauku nyingi sana au kwa kufanya miujiza, bali kwa kupendana.—1 Wakorintho 12:29, 30; 13:2; Yohana 13:35.
Bila shaka roho ya Mungu pamoja na tunda lake la “upendo” ingesitawisha umoja kati ya wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo. (Wagalatia 5:22; Waefeso 4:3-6; 1 Yohana 3:23, 24; 4:12, 13) Lakini watu wanaotazamia maono ya miujiza ya kidini au vituko na “maono” mengine kuwa ushuhuda wa roho ya Mungu wamefanyiza mara nyingi mtengano zaidi katika Jumuiya ya Wakristo ambayo tayari imetengana sana. Akieleza juu ya haya, kasisi mhubiri wa injili Donald G. Miller anaandika katika kitabu chake The Authority of the Bible hivi:
“Imani ya Kipentekoste inadai kutegemea maono. Madhehebu za kisasa zinazodai kusema katika lugha na madhehebu zinazodai kuponya magonjwa kwa miujiza zinajitetea kwa njia ya maono. Imani ya Christian Science inategemeza maono. Mwisho utakuwaje? Ikiwa maono ya kipekee ndiyo yanayoamua . . . kila mtu atakuwa akifanya yanayoonekana kuwa sawa machoni pake. . . . Hata yakikubaliwa na kikundi, mwishowe huelekea kufanya kikundi kimoja kigawanyike na kuwa vikundi vingi vilivyotengana, na kila kimoja kikiwa na maono ya pekee yaliyopotoka ya kudai kujitegemea.”
Maono ya kidini yenye shauku nyingi wala “karama” za kufanya miujiza sio ushuhuda wa roho ya Mungu leo. Huenda maono hayo hata yakahusiana na desturi ambazo Biblia inalaumu. Wale wote wanaotaka kuongozwa na roho ya Mungu yawapasa ‘wageuze upya nia zao’ kupitia kwa ufahamu ulio sawasawa wa Neno la Mungu na kuacha matendo yao yaonyeshe “utu mpya” wa Kikristo.—Warumi 12:2; Wakolosai 3:9, 10.