Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 2/1 kur. 8-13
  • Roho Takatifu, Zawadi Kutoka kwa Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Roho Takatifu, Zawadi Kutoka kwa Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nguvu ya Roho Takatifu
  • Kazi za Muujiza
  • Maandiko Yenye Pumzi
  • Kutegemea Roho Takatifu
  • Roho ya Mungu Katika Karne ya Kwanza
  • Faidika Kutokana na Roho Takatifu ya Mungu
  • ‘Kwa Jina la Roho Takatifu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Kuongozwa na Roho ya Mungu Katika Karne ya Kwanza na Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Kuitambua Roho Takatifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Tembea kwa Roho na Uishi Kulingana na Wakfu Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 2/1 kur. 8-13

Roho Takatifu, Zawadi Kutoka kwa Yehova

“Je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW] hao wamwombao?”—LUKA 11:13.

1, 2. (a) Yesu alifanya ahadi gani juu ya roho takatifu, na kwa nini hilo linafariji kweli kweli? (b) Roho takatifu ni nini?

KATIKA vuli ya mwaka 32 W.K., Yesu alipokuwa akihuburi habari njema katika Yudea, alisema na wanafunzi wake juu ya ukarimu wa Yehova. Alitumia mifano yenye nguvu na kisha akafanya ahadi nzuri ajabu, akisema hivi: “Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW] hao wamwombao?”—Luka 11:13.

2 Maneno hayo ni yenye kufariji kama nini! Tunapovumilia msukosuko wa siku za mwisho wa ulimwengu huu, kukabili uadui wa Shetani na roho waovu wake, na kupigana na mbetuko yetu wenyewe yenye dhambi, inachangamsha moyo kweli kweli kujua kwamba Mungu atatuimarisha kwa roho yake. Kwa kweli, kuvumilia kwa uaminifu hakuwezekani bila utegemezo huo. Je! wewe umepata kuiona nguvu ya roho hiyo, ambayo ni nguvu ya utendaji ya Mungu mwenyewe? Je! unaelewa ni kwa kadiri gani yaweza kukusaidia? Je! wewe huitumia kikamili?

Nguvu ya Roho Takatifu

3, 4. Toa kielezi cha uwezo wa roho takatifu.

3 Ebu fikiria kwanza nguvu ya roho takatifu. Kumbuka kile kilichotukia mwaka 1954. Huo ndio wakati bomu la gesi haidrojeni lilipolipuliwa Bikini Atoll katika Pasifiki Kusini. Mara tu baada ya bomu hilo kulipuka, kisiwa hicho kizuri kilimezwa kwa moto mkubwa na kugongwagongwa kwa mlipuko wenye nguvu iliyo sawa na ile ya uzani wa tani milioni 15 za TNT (trinitrotolueni). Nguvu hiyo yote ya uharibifu ilitoka wapi? Lilikuwa tokeo la kubadili sehemu ndogo tu ya yureniamu na haidrojeni zilizofanyiza kiini cha bomu, kuwa nishati. Vipi, ikiwa wanasayansi wangeweza kufanya kinyume cha lile walilotimiza katika Bikini? Tuseme wangeweza kuikamata nishati hiyo yenye moto na kuibadili kuwa kilo chache za yureniamu na haidrojeni. Huo ungalikuwa ufanisi ulioje! Hata hivyo, Yehova alifanya jambo sawa na hilo lakini kwa kadiri iliyo kubwa zaidi wakati ambao “aliziumba mbingu na nchi.”—Mwanzo 1:1.

4 Yehova ana akiba kubwa ya nishati-msukumo. (Isaya 40:26) Katika uumbaji, ni lazima iwe alitumia sehemu fulani ya nishati hiyo wakati alipoumba vitu vyote vifanyizavyo ulimwengu wote mzima. Alitumia nini katika utendaji huo wa uumbaji? Roho takatifu. Twasoma hivi: “Kwa neno la BWANA [Yehova, NW] mbingu zilifanyika, na jeshi lake lote kwa pumzi ya kinywa chake.” (Zaburi 33:6) Na usimulizi wa kitabu cha Mwanzo kuhusu uumbaji husomwa hivi: “Roho [kani ya utendaji, NW] ya Mungu ikatulia juu ya uso wa maji.” (Mwanzo 1:2) Roho takatifu ni kani yenye uwezo kama nini!

Kazi za Muujiza

5. Roho takatifu hutenda kazi katika njia zipi za fahari?

5 Roho takatifu bado hutenda kazi katika njia za fahari sana. Inaongoza na kuelekeza tengenezo la Yehova la kimbingu. (Ezekieli 1:20, 21) Kama ile nishati iliyotolewa na bomu ya haidrojeni, yaweza kutumiwa kwa kuharibu ili kutekeleza hukumu juu ya adui za Yehova, lakini pia hiyo imetenda kazi katika njia nyinginezo zinazotufanya tushangae.—Isaya 11:15; 30:27, 28; 40:7, 8; 2 Wathesalonike 2:8.

6. Roho takatifu iliwategemezaje Musa na wana wa Israeli katika shughuli zao pamoja na Misri?

6 Kwa mfano, yapata 1513 K.W.K., Yehova alimtuma Musa ajitokeze mbele ya Farao wa Misri ili kuomba uhuru kwa ajili ya wana wa Israeli. Kwa miaka 40 iliyotangulia, Musa alikuwa amekuwa mchungaji katika Midiani, kwa hiyo ni kwa nini Farao amsikilize mchungaji? Kwa sababu Musa alikuja katika jina la Mungu wa pekee wa kweli, Yehova. Ili kuthibitisha hilo, Yehova alimpa nguvu afanye miujiza. Hiyo ilivutia sana hivi kwamba hata makuhani Wamisri wakalazimika kukiri hivi: “Ni chanda cha Mungu”!a (Kutoka 8:19) Yehova alileta mapigo kumi juu ya Misri, la mwisho likimlazimu Farao aache watu wa Mungu waondoke Misri. Farao alipowafuata kwa ukaidi pamoja na jeshi lake, Waisraeli walitoroka wakati njia ilipofunguliwa kimuujiza kwenye Bahari Nyekundu. Jeshi la Misri liliwafuata na kuzama baharini.—Isaya 63:11-14; Hagai 2:4, 5.

7. (a) Ni baadhi gani ya sababu kwa nini roho takatifu ilifanya miujiza? (b) Ingawa miujiza iliyotendeshwa na roho takatifu haitukii tena, ni kwa nini kurekodiwa kwayo katika Biblia kunafariji?

7 Naam, Yehova alifanya miujiza yenye nguvu kwa ajili ya Waisraeli katika wakati wa Musa, na katika nyakati nyinginezo pia, kupitia roho yake. Ni nini lililokuwa kusudi la miujiza hiyo? Iliendeleza makusudi ya Yehova, ilijulisha jina lake, na kuonyesha nguvu zake. Na nyakati nyingine, kama kwa Musa, ilithibitisha kwa uthabiti kwamba mtu alikuwa na utegemezo wa Yehova. (Kutoka 4:1-9; 9:14-16) Hata hivyo, miujiza yenye kutendeshwa na roho takatifu imekuwa michache katika muda wote wa historia.b Yaelekea, watu walio wengi katika nyakati za Biblia hawakushuhudia kamwe mmojawapo, na leo haitukii tena. Hata hivyo, sisi tunaposhindana leo na matatizo ambayo huenda yakaonekana kuwa hayawezi kusuluhishwa, je, haifariji kujua kwamba tukimwomba Yehova katika imani, atatupa roho ile ile iliyomtegemeza Musa mbele ya Farao na kuwafungulia Waisraeli njia kupitia Bahari Nyekundu?—Mathayo 17:20.

Maandiko Yenye Pumzi

8. Daraka la roho takatifu katika kutoa zile Amri Kumi lilikuwa nini?

8 Baada ya ukombozi wao kutoka Misri, Musa aliwaongoza Waisraeli kuelekea Mlima Sinai, ambapo Yehova alifanya agano nao na kuwapa Sheria yake. Sehemu kuu ya Sheria hiyo iliyotolewa kupitia Musa ilikuwa zile Amri Kumi, na nakala zazo za awali zilichongwa kwenye ubamba wa jiwe. Jinsi gani? Kwa roho takatifu. Biblia husema hivi: “Hapo BWANA [Yehova, NW] alipokuwa amekwisha zungumza na Musa katika mlima wa Sinai, akampa hizo mbao mbili za ushuhuda, mbao mbili za mawe, zilizoandikwa kwa chanda cha Mungu.”—Kutoka 31:18; 34:1.

9, 10. Roho takatifu ilikuwaje yenye utendaji katika uandikaji wa Maandiko ya Kiebrania, na hilo laonekanaje wazi kutokana na maneno yaliyotumiwa na wanafunzi wa Yesu?

9 Kuongezea zile Amri Kumi, Yehova kupitia roho yake alilitolea Israeli mamia ya sheria na kanuni za kuongoza maisha ya wanaume na wanawake waaminifu. Na maandiko mengine yenye pumzi yangefuata. Karne kadhaa baada ya siku ya Musa, Nehemia alishuhudia hivi katika sala ya peupe kwa Yehova: “Kwa miaka mingi ukachukuliana nao [Waisraeli], nawe ukawashuhudia kwa roho yako kwa vinywa vya manabii wako.” (Nehemia 9:30) Unabii mwingi mbalimbali uliotamkwa na manabii hao ulirekodiwa. Zaidi ya hayo, roho takatifu iliwasukuma wanaume waaminifu waandike historia takatifu na nyimbo za sifa za kuhisiwa moyoni.

10 Paulo alikuwa akisema juu ya maandiko hayo yote aliposema hivi: “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16; 2 Samweli 23:2; 2 Petro 1:20, 21) Kwa kweli, walipokuwa wakinukuu maandiko hayo, wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza mara nyingi walitumia maneno kama vile ‘roho takatifu . . . ilisema kwa kinywa cha Daudi,’ ‘roho takatifu ilisema vema kupitia Isaya,’ au ‘kama isemavyo roho takatifu.’ (Matendo 1:16; 4:25; 28:25, 26; Waebrania 3:7, NW) Ni baraka iliyoje kwamba roho takatifu hiyo hiyo iliyoongoza uandikaji wa Maandiko Matakatifu imeyahifadhi hivi kwamba yanaweza kutuongoza na kutufariji leo!—1 Petro 1:25.

Kutegemea Roho Takatifu

11. Ni utendaji gani wa roho ulioonekana kuhusu ujenzi wa tabenakulo?

11 Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi chini ya Mlima Sinai, Yehova aliwaamuru wajenge tabenakulo (hema) kuwa kitovu cha ibada ya kweli. Wangeweza kutimizaje hilo? “Musa akawaambia wana wa Israeli, Angalieni, BWANA [Yehova, NW] amemwita kwa jina lake Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, wa kabila ya Yuda; naye amemjaza roho ya Mungu, katika hekima, na akili, na ujuzi, na kazi ya ustadi kila aina.” (Kutoka 35:30, 31) Roho takatifu iliimarisha ustadi wowote wa kiasili ambao Bezaleli alikuwa nao, naye angeweza kusimamia kwa mafanikio ujenzi wa muundo huo wa ajabu.

12. Roho iliwaimarishaje watu mmoja mmoja katika njia zisizo za kawaida baada ya wakati wa Musa?

12 Katika wakati wa baadaye, roho ya Yehova ilitenda kazi juu ya Samsoni, ikimpa nguvu ipitayo ile ya kibinadamu kumwezesha akomboe Israeli kutoka kwa Wafilisti. (Waamuzi 14:5-7, 9; 15:14-16; 16:28-30) Baadaye zaidi, Sulemani alipewa hekima ya pekee akiwa mfalme wa watu wa Mungu walioteuliwa. (2 Mambo ya Nyakati 1:12, 13) Chini yake, Israeli lilifanikiwa kuliko wakati mwingine wowote ule, na hali yalo yenye furaha ikawa kielelezo cha mibaraka ambayo watu wa Mungu wataonea shangwe chini ya Utawala wa Mileani wa Yesu Kristo, Sulemani Mkubwa Zaidi.—1 Wafalme 4:20, 25, 29-34; Isaya 2:3, 4; 11:1, 2; Mathayo 12:42.

13. Rekodi ya roho ikiwaimarisha Bezaleli, Samsoni, na Sulemani inatutiaje moyo leo?

13 Ni baraka iliyoje kwamba Yehova hufanya roho hiyo hiyo ipatikane kwetu! Tunapohisi kwamba hatufai kutimiza mgawo fulani au kushiriki katika kazi ya kuhubiri, twaweza kumwomba Yehova atupe sisi roho ile ile aliyompa Bezaleli. Tunapopata ugonjwa au kuvumilia mnyanyaso, roho ile ile iliyompa Samsoni nguvu ipitayo ile ya kawaida itatuimarisha—ingawa, bila shaka, si kimuujiza. Na tunapokabili matatizo magumu au kulazimika kufanya maamuzi ya maana, twaweza kumwomba Yehova, aliyempa Sulemani hekima ipitayo ile ya kawaida, atusaidie tutende kwa hekima. Halafu, kama Paulo, tutasema hivi: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Wafilipi 4:13) Na ahadi ya Yakobo itatumika kwetu: “Mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.”—Yakobo 1:5.

14. Ni nani, katika nyakati za kale na za leo, ambao wametegemezwa na roho takatifu?

14 Roho ya Yehova ilikuwa juu ya Musa pia katika kazi yake ya kuhukumu taifa. Wengine walipowekwa rasmi kumsaidia Musa, Yehova alisema hivi: “Nami nitatwaa sehemu ya roho iliyo juu yako na kuiweka juu yao; nao watachukua mzigo wa watu hawa pamoja nawe, ili usiuchukue wewe peke yako.” (Hesabu 11:17) Hivyo, wanaume hao hawakulazimika kutenda kwa nguvu zao wenyewe. Roho takatifu iliwategemeza. Katika pindi za baadaye twasoma kwamba roho ya Yehova ilikuwa juu ya watu wengine mmoja mmoja. (Waamuzi 3:10, 11; 11:29) Samweli alipompaka Daudi mafuta kuwa mfalme wa Israeli wa wakati ujao, rekodi husema hivi: “Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya BWANA [Yehova, NW] ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile.” (1 Samweli 16:13) Wale wenye madaraka mazito leo—ya familia, ya kundi, au ya kitengenezo—waweza kufarijika kujua kwamba roho ya Mungu bado hutegemeza watumishi wake wanapoangalia wajibu wao mbalimbali.

15. Roho takatifu imeimarisha tengenezo la Yehova katika njia gani (a) katika siku za Hagai na Zekaria? na (b) leo?

15 Miaka elfu hivi baada ya siku ya Musa, wale waaminifu kutoka miongoni mwa wana wa Israeli walirudi Yerusalemu kutoka Babuloni wakiwa na utume wa kujenga upya hekalu. (Ezra 1:1-4; Yeremia 25:12; 29:14) Hata hivyo, vizuizi vigumu vilitokea na walivunjika moyo kwa miaka mingi. Hatimaye, Yehova aliwainua manabii Hagai na Zekaria wawatie moyo Wayahudi wasitegemee nguvu yao wenyewe. Lakini kazi hiyo ngumu ingetimizwaje? “Si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema BWANA [Yehova, NW] wa majeshi.” (Zekaria 4:6) Na hekalu likajengwa, kwa utegemezo wa roho ya Mungu. Watu wa Mungu leo wametimiza mengi vivyo hivyo. Kuhubiriwa kwa habari njema kumepanuka kotekote duniani. Mamilioni ya watu mmoja mmoja wanaelimishwa katika ukweli na uadilifu. Mikusanyiko inapangwa. Majumba ya Ufalme na ofisi za tawi zinajengwa. Mengi ya hayo yamefanywa wakati wa upinzani mkali. Lakini Mashahidi wa Yehova hawajashuka moyo, wakijua kwamba ki-ila kitu ambacho wametimiza kimekuwa, si kwa nguvu ya kijeshi, wala kwa uwezo wa kibinadamu, bali kwa roho ya Mungu.

Roho ya Mungu Katika Karne ya Kwanza

16. Watumishi wa Yehova wa kabla ya Ukristo waliona nini kuhusu utendaji wa roho ya Mungu?

16 Kama vile tumeona, watumishi wa Mungu wa kabla ya Ukristo walitambua vizuri uwezo wa roho ya Mungu. Waliitegemea iwasaidie wakamilishe wajibu mbalimbali mzito na kutimiza mapenzi ya Mungu. Walijua pia kwamba Sheria na maandiko matakatifu mengineyo yalipuliziwa roho, yakiandikwa chini ya uvutano wa roho ya Yehova na hivyo yalikuwa ‘Neno la Mungu.’ (Zaburi 119:105) Lakini, vipi juu ya enzi ya Kikristo?

17, 18. Ni baadhi gani ya maonyesho ya kimuujiza ya roho katika enzi ya Kikristo, nayo yalitumikia kusudi gani?

17 Karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu iliona pia utendaji mbalimbali wa ajabu wa roho ya Mungu. Kulikuwako utoaji unabii uliopuliziwa roho. (1 Wakorintho 14:1, 3) Katika kutimiza ahadi ya Yesu kwamba roho takatifu ingewakumbusha wanafunzi wake juu ya mambo yote aliyokuwa amesema na ingewafundisha sehemu nyingine zaidi za kweli, vitabu kadhaa viliandikwa chini ya uvutano wa roho takatifu. (Yohana 14:26; 15:26, 27; 16:12, 13) Na kulikuwako miujiza, kama itakavyozungumziwa katika makala yetu ifuatayo. Kwa kweli, karne ya kwanza ilitangulizwa na muujiza wa ajabu. Yapata mwaka 2 K.W.K., kitoto cha kipekee kingezaliwa, na ikiwa ishara, mama yake mchanga angekuwa bikira. Hilo lingewezekanaje? Kwa njia ya roho takatifu. Rekodi yasema hivi: “Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].”—Mathayo 1:18; Luka 1:35, 36.

18 Yesu alipokua akawa mtu mzima, aliondolea mbali roho waovu, aliwaponya wagonjwa, hata kuwafufua wafu katika nguvu ya roho takatifu. Wengine wa wafuasi wake pia walifanya miujiza na kazi za uwezo. Uwezo huo mbalimbali wa pekee ulikuwa zawadi kutoka kwa roho. Kusudi lao lilikuwa nini? Sawa na vile miujiza ya mapema ilivyofanya, uwezo huo mbalimbali uliendeleza makusudi ya Mungu na kufunua uwezo wake. Isitoshe, ulionyesha ukweli wa dai la Yesu kwamba alikuwa ametumwa kutoka kwa Mungu; na baadaye, ulithibitisha kwamba kundi la Kikristo la karne ya kwanza lilikuwa taifa la Mungu lililoteuliwa.—Mathayo 11:2-6; Yohana 16:8; Matendo 2:22; 1 Wakorintho 12:4-11; Waebrania 2:4; 1 Petro 2:9.

19. Imani yetu inaimarishwaje na usimulizi wa Biblia wa miujiza ya Yesu na mitume wake?

19 Hata hivyo, mtume Paulo alisema kwamba maonyesho ya kimuujiza ya roho kama hayo yalikuwa kwa ajili ya hali changa ya kundi na yangekoma, kwa hiyo sisi leo hatuioni miujiza kama hiyo yenye kuletwa na roho takatifu. (1 Wakorintho 13:8-11) Hata hivyo, miujiza iliyofanywa na Yesu na mitume wake ina upendezi mwingi zaidi ya kuwa tu historia. Inaimarisha imani yetu katika ahadi ya Mungu kwamba ugonjwa na kifo hazitakuwapo chini ya utawala wa Yesu katika ulimwengu mpya.—Isaya 25:6-8; 33:24; 65:20-24.

Faidika Kutokana na Roho Takatifu ya Mungu

20, 21. Twaweza kujifaidije na uandalizi wa roho takatifu?

20 Roho hiyo ni nguvu yenye uwezo kama nini! Lakini Wakristo waweza kujifaidije nayo leo? Kwanza, Yesu alisema twapaswa kuomba tuipate, basi kwa nini usifanye hivyo hasa? Sali kwa Yehova akupe zawadi hiyo nzuri ajabu si katika nyakati za mkazo wa mawazo tu bali pia kwenye kila pindi. Kwa kuongezea, soma Biblia ili kwamba roho takatifu iweze kusema nawe kupitia Neno la Mungu (Linganisha Waebrania 3:7). Tafakari juu ya yale unayosoma na kuyatumia ili kwamba roho takatifu iweze kuwa na uvutano maishani mwako. (Zaburi 1:1-3) Zaidi ya hayo, shirikiana—na mtu mmoja mmoja, katika makundi, na kwenye makusanyiko—na wengine wanaoitegemea roho ya Mungu. Roho takatifu huwaimarisha sana kama nini wale wanaombariki Mungu wao “katika makusanyiko”!—Zaburi 68:26.

21 Je! Yehova si Mungu mwenye ukarimu? Yeye asema tunahitaji tu kumwomba roho takatifu naye atatupatia. Ni jambo la upumbavu kama nini kutegemea hekima na nguvu zetu wenyewe wakati tunaweza kupata msaada wenye nguvu kama huo! Hata hivyo, kuna mambo mengine yanayohusika na roho ya Mungu yanayotuathiri tukiwa Wakristo, na hayo yatazungumziwa katika makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

a Maneno “chanda cha Mungu” kwa kawaida hurejezea roho takatifu.—Linganisha Luka 11:20 na Mathayo 12:28.

b Mingi ya miujiza iliyorekodiwa katika Biblia ilitukia katika wakati wa Musa na Yoshua, Eliya na Elisha, na Yesu na mitume wake.

Je! Waweza Kujibu Maswali Yafuatayo?

◻ Yehova aliumbaje vitu vyote katika ulimwengu wote mzima?

◻ Ni baadhi gani za njia ambazo katika hizo roho takatifu ilitenda kazi katika nyakati za kabla ya Ukristo?

◻ Tunafarijiwaje leo kujua kile ambacho roho takatifu ilitimiza katika nyakati za kale?

◻ Tunaweza kujifaidije na uandalizi wa roho takatifu?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Roho iliyompa Samsoni nguvu ipitayo ile ya kibinadamu yaweza kutupa uwezo kwa ajili ya kila jambo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki