Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 2/1 kur. 4-7
  • Manabii Wawongo Leo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Manabii Wawongo Leo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ukweli Kuhusu Ufalme
  • Kwa Nini ni Jambo la Maana?
  • Ainabinadamu Chini ya Ufalme wa Mungu
  • Ufalme wa Mungu—Tumaini Peke Yake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Mafundisho ya Yesu Kuhusu Ufalme wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Ufalme Wa Mungu
    Amkeni!—2013
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 2/1 kur. 4-7

Manabii Wawongo Leo

YEREMIA alitumikia akiwa nabii wa Mungu katika Yerusalemu wakati mji ulipokuwa umejaa ibada ya sanamu, ukosefu wa adili, ufisadi, na umwagaji wa damu isiyo na hatia. (Yeremia 7:8-11) Hakuwa nabii wa pekee aliyekuwa akitenda kazi wakati huo, lakini wengi wa wale wengine walikuwa wanajitumikia wenyewe na wenye kufisidi. Katika njia gani? Yehova atangaza: “Kwa maana, tangu aliye mdogo hata aliye mkubwa miongoni mwao, kila mmoja ni mtamanifu; na, tangu nabii hata kuhani, kila mmoja hutenda mambo ya udanganyifu. Wameiponya jeraha ya watu wangu kwa juu juu tu, wakisema, Amani, Amani, wala hapana amani.”—Yeremia 6:13, 14.

Manabii wawongo walijaribu kufanya ionekane kuwa ujapokuwa ufisadi wote huo nchini, mambo yalikuwa sawa, na watu walikuwa na amani pamoja na Mungu; lakini haikuwa hivyo. Hukumu ya Mungu iliwangojea, kama Yeremia alivyotangaza bila woga. Nabii wa kweli Yeremia, si wale manabii wawongo, ndiye alitetewa wakati Yerusalemu ulipoharibiwa kabisa na askari-jeshi wa Babuloni katika 607 K.W.K., hekalu likaharibiwa, na watu ama wakauawa ama wakapelekwa utumwani Babuloni iliyokuwa mbali. Wachache wenye kuhurumiwa waliobaki nchini walikimbilia Misri.—Yeremia 39:6-9; 43:4-7.

Manabii wawongo walikuwa wamefanya nini? “Basi kwa sababu hiyo mimi ni juu ya manabii hao, asema BWANA [Yehova NW], wanaompokonya kila mtu jirani yake maneno yangu.” (Yeremia 23:30) Manabii wawongo waliiba uwezo wa matokeo ya kusikiliza maneno ya Mungu kwa kuwatia watu moyo wasikilize uwongo badala ya onyo la kweli kutoka kwa Mungu. Walikuwa wakisema, si “matendo makuu ya Mungu,” bali mawazo yao wenyewe, mambo ambayo watu walitaka kusikia. Ujumbe wa Yeremia ulikuwa kwa hakika umetoka kwa Mungu, na kama Waisraeli wangalitenda kulingana na maneno yake, wangaliokoka. Manabii wawongo ‘waliiba maneno ya Mungu’ na wakaongoza watu kwenye msiba. Ni kama tu vile Yesu alisema kuhusu viongozi wa kidini wasio waaminifu wa siku yake: “Waacheni; hao ni viongozi vipofu wa vipofu. Na kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili.”—Matendo 2:11; Mathayo 15:14.

Sawa na siku ya Yeremia, leo kuna manabii wawongo wanaojidai kumwakilisha Mungu wa Biblia; lakini wao pia huiba maneno ya Mungu kwa kuhubiri mambo yanayoondoa watu mbali na yale ambayo Mungu anasema, kupitia Biblia. Katika njia gani? Acheni tujibu swali hilo kwa kutumia, kama kiwango cha kupimia, fundisho la msingi la Biblia la Ufalme.

Ukweli Kuhusu Ufalme

Ufalme wa Mungu ulikuwa kichwa kikuu cha fundisho la Kristo, na unatajwa zaidi ya mara mia moja katika Gospeli. Mapema katika huduma yake, Yesu alisema: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” Alifundisha wafuasi wake wasali: “Ufalme wako uje.”—Luka 4:43; 11:2.

Ule Ufalme ni nini, basi? Kulingana na The New Thayer’s Greek English Lexicon, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ufalme” katika Biblia humaanisha kwanza, “uwezo wa kifalme, umaliki, mamlaka, utawala” na pili, “eneo linalotawalwa na mfalme.” Kutokana na hilo tungeweza kukata maneno kiakili kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali halisi inayotawalwa na Mfalme. Je! hivi ndivyo ilivyo?

Naam, ndivyo ilivyo, na Mfalme si mwingine ila Yesu Kristo. Kabla ya kuzaliwa kwa Yesu malaika Gabrieli alimwambia Mariamu: “Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na Bwana [Yehova, NW] Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake.” (Luka 1:32) Kupokea kwa Yesu enzi huthibitisha kwamba yeye ni Mfalme, Mtawala wa kiserikali. Pia uthibitisho wa kwamba Ufalme ni serikali halisi ni ule unabii wa Isaya: “Kwetu sisi mtoto amezaliwa, kwetu sisi mwana tumepewa: na serikali itakuwa mabegani mwake . . . Kwa mweneo wa serikali yake na amani hakutakuwa na mwisho.”—Isaya 9:6, 7, King James Version.

Yesu anatawala akiwa wapi? Katika Yerusalemu? La. Nabii Danieli aliona njozi ya Yesu akipokea Ufalme, na njozi yake inaonyesha Yesu akiwa mbinguni. (Danieli 7:13, 14) Hilo lakubaliana na vile Yesu alivyosema kuhusu Ufalme. Mara nyingi aliuita “ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 10:7; 11:11, 12) Lakubaliana pia na maneno ya Yesu kwa Pilato wakati Yesu alipokuwa jaribuni mbele yake: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa.” (Yohana 18:36) Je! mhubiri au padri wako amekufundisha kwamba Ufalme wa Yesu ni serikali halisi, inayotawala kutoka mbinguni? Au amekufundisha kwamba Ufalme ni kitu tu kilicho moyoni? Ikiwa ndivyo, amekuwa akiiba maneno ya Mungu kutoka kwako.

Kuna uhusiano gani kati ya serikali ya Ufalme na zile namna zote tofauti-tofauti za serikali za kibinadamu? Kulingana na Encyclopedia of Religion kilichohaririwa na Mircea Eliade, Mwanamapinduzi wa Kidini Martin Lutheri, alipokuwa akizungumzia Ufalme, alidokeza: “Serikali ya kilimwengu . . . pia yaweza kuitwa ufalme wa Mungu.” Wengine hufundisha kwamba wanadamu, kwa jitihada zao wenyewe, wanaweza kufanya serikali za kibinadamu zikaribie zaidi kuwa kama Ufalme wa Mungu. Katika 1983 Baraza la Makanisa Ulimwenguni lilisema kwa uthabiti: “Tunaposhuhudia tamaa yetu halisi ya amani kwa matendo hususa, Roho ya Mungu inaweza kutumia jitihada zetu hafifu za kufanya falme za ulimwengu zikaribie zaidi kuwa kama ufalme wa Mungu.”

Angalia, hata hivyo, kwamba katika sala ya Bwana (ya “Baba Yetu”), Yesu alifundisha wafuasi wake waombe Ufalme wa Mungu uje na ndipo tu akawaambia waombe: “Mapenzi yako [ya Mungu] yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:10) Yaani, wanadamu hawafanyi Ufalme uje kwa kufanya mapenzi ya Mungu. Ni kuja kwa Ufalme ambako kunafanya mapenzi ya Mungu yafanywe duniani. Jinsi gani?

Sikiliza lile ambalo unabii wa Danieli sura ya 2, mstari 44, unavyosema: “Na katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, . . . utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu.” Haishangazi kwamba Yesu alisema Ufalme wake haukuwa sehemu ya ulimwengu huu! Badala yake, Ufalme huo utaziharibu falme, serikali, za dunia hii na kuchukua mahali pazo katika kutawala wanadamu. Ikiwa serikali ya ainabinadamu yenye kutolewa na Mungu, itahakikisha kwamba mapenzi ya Mungu yanafanywa duniani.

Sababu ya tendo hilo lenye badiliko kubwa kwa upande wa Ufalme hueleweka wazi tunapoona ni nani anayeuthibiti ulimwengu huu. Mtume Yohana aliandika: “Dunia yote pia hukaa katika [uwezo wa, NW] yule mwovu. (1 Yohana 5:19) “Yule mwovu” ni Shetani Ibilisi, ambaye Paulo alimwita “mungu wa dunia hii.” (2 Wakorintho 4:4) Mashirika katika ulimwengu ambao Shetani Ibilisi ndiye mungu wao hayawezi kwa njia yoyote kutambulishwa na Ufalme wa Mungu.

Hii ni sababu kwa nini Yesu hakujiingiza katika siasa. Wakati watukuzaji taifa Wayahudi walipojaribu kumfanya awe mfalme, aliwaepuka. (Yohana 6:15) Kama tulivyoona, alimwambia Pilato waziwazi: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu.” Na kupatana na hili, alisema juu ya wafuasi wake: “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:16) Kwa hiyo, viongozi wa kidini wanaofundisha kwamba kuja kwa Ufalme wa Mungu kunaharakishwa na maendeleo katika mfumo wa mambo huu na wanaotia moyo makundi yao kufanyia kazi mradi huo ni manabii wawongo. Wanaiba uwezo na matokeo ya kusikiliza lile ambalo Biblia kwa kweli husema.

Kwa Nini ni Jambo la Maana?

Je! hayo yote ni mabishano ya kiakili? Hata kidogo. Mafundisho yasiyofaa kuhusu Ufalme wa Mungu yameongoza watu wengi vibaya na hata yameathiri mwendo wa historia. Kwa mfano, kichapo Théo, ensaiklopidia ya Katoliki ya Kiroma, husema: “Watu wa Mungu wanasonga mbele kuelekea Ufalme wa Mungu ulioanzishwa na Kristo duniani . . . Kanisa ndilo mbegu ya Ufalme huo.” Utambulisho wa Kanisa Katoliki na Ufalme wa Mungu ulipatia kanisa uwezo mkubwa sana wa kilimwengu wakati wa Enzi za Kati za ushirikina. Hata leo, mamlaka za kanisa hujaribu kuchochea mwendo wa mambo ya ulimwengu, wakipendelea mifumo mingine ya kisiasa na kuwa dhidi ya mingine.

Mfafanuzi mmoja alitoa maoni mengine yaliyoenea leo aliposema: “Njia ya mapinduzi makuu ndiyo ufalme kwa sababu mapinduzi ni kule kuja pamoja kwa watu katika ubinadamu mpya, wakichochewa na ishara ya kimungu inayotolewa kupitia mwanadamu wa kweli—Yesu . . . Gandhi . . . akina Berrigan.” Kufundisha kwamba Ufalme wa Mungu unaweza kuendelezwa kwa utendaji wa kisiasa na kudharau mambo ya hakika juu ya Ufalme kumeongoza viongozi wa kidini washindanie vyeo vya kisiasa. Kumeongoza wengine wahusike katika fujo za raia na hata kushiriki katika vita vya kuvizia. Haya yote hayapatani hata kidogo na ukweli wa kwamba Ufalme sio sehemu ya ulimwengu huu. Na viongozi wa kidini wanaojiingiza sana katika siasa wako kando sana na kutokuwa sehemu ya ulimwengu, kama Yesu alivyosema wanafunzi wake wangekuwa. Wale wanaofundisha kwamba Ufalme wa Mungu utafikiwa kupitia utendaji wa kisiasa ni manabii wawongo. Wanaiba maneno ya Mungu kutoka kwa watu.

Ikiwa viongozi katika Jumuiya ya Wakristo kwa kweli wangefundisha lile ambalo Biblia husema, makundi yao yangejua kwamba Ufalme wa Mungu utatatua matatizo kama vile umaskini, magonjwa, ubaguzi wa rangi, na uonezi. Lakini itakuwa kwa wakati aliouweka Mungu na katika njia ya Mungu. Haitakuwa kupitia matengenezo ya mifumo ya kisiasa, yatakayopitilia mbali Ufalme ufikapo. Ikiwa makasisi hao wangalikuwa manabii wa kweli, wangalifundisha makundi yao kwamba wakati wangojeapo Ufalme wa Mungu uchukue hatua, wanaweza kupata msaada halisi kutoka kwa Mungu, wa kushughulikia matatizo yanayosababishwa na ukosefu wa haki wa ulimwengu huu.

Hatimaye, wangalifundisha makundi yao kwamba hali mbaya zilizo duniani zinazosababisha dhiki nyingi zilitabiriwa katika Biblia na ni ishara kwamba kuja kwa Ufalme ku karibu. Naam, Ufalme wa Mungu utaingilia hivi karibu na kuchukua mahali pa matengenezo ya kisiasa yaliyopo. Hiyo itakuwa baraka iliyoje!—Mathayo 24:21, 22, 36-39; 2 Petro 3:7; Ufunuo 19:11-21.

Ainabinadamu Chini ya Ufalme wa Mungu

Kuja kwa Ufalme wa Mungu kutamaanisha nini kwa ainabinadamu? Je! waweza kujiwazia mwenyewe ukiamka kila asubuhi ukiwa na nguvu nyingi? Hakuna yeyote ujuaye aliye mgonjwa au anayekufa. Hata wapendwa wako waliokufa wamerudishwa kwako kupitia ufufuo. (Isaya 35:5, 6; Yohana 5:28, 29) Hakuna tena wasiwasi wa kiuchumi unaosababishwa na mambo ya kibiashara ya ubinfsi au mifumo ya kiuchumi isiyosawazika. Una makao yako yenye starehe na shamba linalotosha la kupanda vyote unavyohitaji kulisha familia yako. (Isaya 65:21-23) Unaweza kutembea kila mahali wakati wowote wa mchana au usiku bila woga wa kushambuliwa. Hakuna vita tena kamwe—hakuna lolote la kutisha usalama wako. Kila mtu anapendezwa na masilahi yako. Waovu hawako. Upendo na uadilifu vinatawala. Je! waweza kuwazia wakati kama huo? Huo ndio aina ya ulimwengu utakaoletwa na Ufalme.—Zaburi 37:10, 11; 85:10-13; Mika 4:3, 4.

Je! haya ni mawazio tu? Sivyo. Soma maandiko yaliyotajwa katika fungu lililotangulia, na utaona kwamba kila kitu kilichosemwa hapo kinaonyesha ahadi dhahiri za Mungu. Ikiwa bado hata sasa hujaona wazi lile ambalo Ufalme wa Mungu waweza kufanya na utafanyia ainabinadamu, basi mtu fulani ameiba maneno ya Mungu kutoka kwako.

Kwa furaha, mambo hayataendelea kubaki hivyo. Yesu alisema kwamba katika siku zetu “habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Gazeti unalosoma ni sehemu ya kazi hii ya kuhubiri. Twakutia moyo uepuke kudanganywa na manabii wawongo. Chunguza zaidi Neno la Mungu upate kweli juu ya Ufalme wa Mungu. Halafu, jitiishe mwenyewe kwa Ufalme huo, ambao ni uandalizi wa Mchungaji Mkuu, Yehova Mungu. Kwa kweli, ndio tumaini la pekee la mwanadamu, na halitashindwa.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Lutheri alifundisha kwamba serikali ya kibinadamu ingeweza kuonwa kama Ufalme wa Mungu

[Hisani]

Kwa hisani ya Trustees of the British Museum ya Uingereza

[Picha katika ukurasa wa 7]

Akiwa kama Mchungaji mwenye upendo, Yehova kupitia Ufalme wake ataleta hali ambazo wanadamu hawezi kuleta

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki