Utafutaji wa Usawa
HAKUNA mtu anayependa ajione kuwa si mtu. “Mimi ni bora kama mtu mwingineye yote” ni usemi wa kawaida. Je, hatuchukizwi na mtu kujionyesha kuwa bora kuliko wengine? Kwa msingi, inatuliza kuhisi tuna usawa na wengine. Lakini, ni rahisi kufikiri na kusema juu ya usawa kuliko ilivyokuwa nao, kama ambavyo wengi wameona.Fikiria mfano huu.
Mwaka 1776 makoloni ya Uingereza katika Amerika ya Kaskazini yalitangaza dai lao la serikali ya kujitawala. Tangazo la Uhuru lao lenye kujulikana sana lilitangaza kati ya kweli ambazo zingejitokeza wazi’ kwamba watu wote waliumbwa wakiwa na usawa.” Yaliendelea kutangaza kwamba ilikuwa haki ya raia wote kufurahia “uzima, uhuru, na utafutaji wa furaha.”
Wakati makoloni hayo 13 yalipojitenga na Uingereza, idadi yayo ya watu ilikuwa karibu milioni tatu. Kati yao, zaidi ya nusu milioni walikuwa watumwa. Ilichukua karibu miaka mia moja kuondoa utumwa katika United States ya Amerika. Thomas Jefferson, mbuni mkuu wa Tangazo hilo, aliendelea kuwa na watumwa maisha yake yote. Malengo ya Tangazo hilo yalikuwa mazuri, lakini wakati ulihitajiwa ili hata sehemu ya usawa huo wa msingi upatikane.
Duniani pote wengi wangali hawana uhuru mwingi, au wanabaguliwa. Kwa kutambua hivyo, watu mbalimbali wanatoa maisha zao ili wajaribu kuondoa aina zote za uonezi na ukosefu wa usawa. Kichapo kimoja cha karibuni cha Umoja wa Mataifa juu ya habari ya uhuru kinataja zaidi ya mara kumi na mbili juu ya kuwa na usawa na juu ya uhitaji wa kuwa na usawa. Kwa wazi ungali ni mradi ulio mgumu kufikiwa. Kwa sababu gani?
Tatizo ni kwamba usawa una sehemu nyingi nao si jambo rahisi kuelezeka. Watu wanautafuta usawa kwa njia tofauti, ikitegemea hali zao. Basi, ni kwa kadiri gani, inaweza kusemwa kwamba watu wana usawa? Sisi tunaweza kutazamia nini kwa kufaa, sasa na katika wakati ujao, kuhusu usawa pamoja na wanadamu wenzetu?
Usawa—Ni Halisi Jinsi Gani Leo?
Mwana-mfalme na maskini huenda wakazaliwa katika mji ule ule siku ile ile, lakini utajiri na pendeleo laelekea kuwa la mmoja kama vile umaskini utakavyompata yule mwingine. Hilo ni jambo moja tu linaloonyesha ni kwa sababu gani haiwezi kusemwa kwamba watu wote leo wanazaliwa wakiwa sawa.
Mengi yanategemea jumuiya tunamoishi na viwango vya usawa ambavyo imesitawisha miakani. Kitabu Encyclopcedia Britannica kinalijumlisha vizuri jambo hilo hivi:
“Kwa lazima jumuiya zote zinafanya mipango ya kushiriki utajiri, uweza, na faida nyingine. Kati ya watu mmoja mmoja na vikundi mipango hiyo inaonyesha viwango vyote vya usawa na ukosefu wa usawa.”
Katika jumuiya yo yote, kila mtu ana jambo la pekee la kutoa ambalo ni yeye tu anaweza kulitoa. Kwa hiyo wengine wamejaribu kutokeza karama na uwezo wa wote na kugawanya kwa usawa utajiri na matokeo yake. Ndiyo sababu ya usemi huu wa kikomunisti: “Kutoka kwa kila mtu kulingana na uwezo wake, mpaka kwa kila mtu kulingana na mahitaji yake.” Pia: “Kutoka kwa kila mtu kulingana na uweza wake, mpaka kwa kila mtu kulingana na kazi yake.” Ijapokuwa falsafa hizo zinaonekana zinavutia, ukosefu wa usawa unaendelea chini ya mifumo yote ya serikali za kibinadamu.
Ukweli ni kwamba, badala ya kuendeleza kusudi la usawa, mifumo fulani ya kisiasa imetafuta kujifaidi na unaosemwa kuwa ukosefu wa usawa. Kumbuka mkazo wa Nazi juu ya “jamii iliyo bora.” Lakini kuwapo kwa jamii iliyo bora kumekwisha kuonyeshwa kitambo kuwa si kweli. Isipokuwa tofauti zilizo wazi za umbo la mwili, “elekeo la kuwapo kwa tofauti halisi za jamii katika tabia na akili linakuwa gumu kuthibitisha,” tukinakili tena maneno ya kitabu Encyclopcedia Britannica. Usawa huo wa jamii ni wa msingi.
Elimu na Uwezo
Elimu yaweza kuwa kitu cha kusawazisha sana wakati vifaa vyayo vinapopatikana kwa urahisi, lakini sikuzote haiwi hivyo. Katika nchi nyingi, fedha zinazopatikana kwa jasho zingali lazima zilipwe hata kwa ajili ya masomo yaliyo ya msingi sana.
Kwa mfano, katika nchi moja ya upande wa kizio cha kusini, ni asilimia 20 tu ya watu walio na elimu. Ni jambo la kawaida kukuta huko jamaa ambayo watoto wawili wenye umri kupita wengine wana elimu nzuri kiasi lakini wanaobaki hawapati elimu yo yote, kwa sababu tu fedha za jamaa hazifanyi hilo liwezekane. Nchi nyingine zinazositawi zina matatizo ayo hayo.
Hali hiyo inaelekea kuendeleza ukosefu wa usawa kwa sababu, katika jumuiya yetu ya kisasa, maendeleo yawezekanayo kiuchumi hasa ni ya wale walio na elimu tu. Hata hivyo, madigrii (shahada) ya vyuo vikuu fulani yanatafutwa zaidi ya yale ya vyuo vikuu vingine kwa sababu yana sifa zaidi. Kwa hiyo elimu siyo jibu lenyewe hata kidogo la tatizo la ukosefu wa usawa leo.
Haki za Msingi
Tabia zinazorithiwa zaweza kuamua kwamba wanadamu hawawezi kamwe kufanana katika kila jambo, hata hivyo je, wewe hukubali kwamba katika mambo fulani ya msingi kwapasa kuwe usawa? Je! wanadamu hawangekuwa katika hali bora zaidi kama maendeleo yangefanywa katika sehemu hizi:
USAWA WA KIJAMII AU KIKABILA: Tunaweza kuondoaje aibu inayokamatanishwa na jamii au kabila moja au tabaka moja juu ya nyingine? Chuki zinatia mizizi sana na kusababisha matatizo mengi. Ni mambo gani yanayoweza kufanywa ili kuhakikisha watu wanatendewa kwa usawa, na kuwapa heshima wanayostahili?
CHAKULA: Unapoona watoto wanaokufa njaa na mamilioni wanaokufa kila mwaka kwa ajili ya kukosa chakula cha kujenga mwili au maradhi yanayoambatana na ukosefu huo, unatendaje? Imethibitishwa sana kwamba kunaweza kuwa chakula cha kutosha idadi ya watu ulimwenguni. Basi, kwa nini kusiwe ugawanyaji ulio na usawa zaidi wa chakula ili kupunguza taabu hizo?
KAZI: Ukosefu wa kazi unaweza kuleta maumivu ya moyo na kukata tamaa—hata kujiua. Je! haiwezekani wote waajiriwe kazi ya kujipatia malipo? Je! hakuwezi kuwa nafasi ya usawa wa kazi kwa wote?
ELIMU: Je! watu wote hawapaswi kupata angalau elimu ya msingi, ili ukosefu wa elimu uondolewe? Badala ya kuelekea kuongeza tofauti kati ya tabaka (‘matajiri kuzidi kuwa matajiri na maskini kuzidi kuwa maskini’), je, elimu haiwezi kusaidia kufanya hali iwe bora zaidi kwa wote? Hasa hilo lingekuwa hivyo kama elimu ingeshughulikia mengi zaidi ya mambo ya kiufundi, kama ingetia ndani uadilifu na kanuni za uhusiano bora kati ya wanadamu.
Hakika, utakubali kwamba taraja la usawa lingali mbali sana!