Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 8/15 kur. 5-7
  • Watu Wote ‘Ni sawa—Jinsi Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Watu Wote ‘Ni sawa—Jinsi Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wenye Usawa Katika Mwili Wenye Umoja
  • Usawa Unaotumika Leo
  • Utafutaji wa Usawa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Je, Inawezekana Kuwa na Jamii Isiyo na Ubaguzi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Baa la Sasa la Ukosefu wa Usawa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Je, Usawa wa Kijamii Ni Ndoto Tu?​—Biblia Inasema Nini?
    Habari Zaidi
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 8/15 kur. 5-7

Watu Wote ‘Ni Sawa​—Jinsi Gani?

JE! INAWEZEKANA wanaume na wanawake wa mataifa yote waone wana usalama ule ule wao kwa wao​—na kutenda kupatana na hilo? Haiwezekani katika utaratibu wa kisasa wa ulimwengu. Hata hivyo tunaweza kujipa moyo kwamba inawezekana. Kwa sababu gani? Kwa sababu kuna mamilioni ya Wakristo ambao wamethibitisha hivyo.

Inajulikana wazi kwamba Ukristo wa kweli umekamatana na usawa. Kwa mfano, mtume Paulo aliandika hivi: “Sisi si Wayahudi tena wala Wagiriki wala watumwa wala watu huru wala hata wanaume au wanawake, bali sisi sote ni sawa​—sisi ni Wakristo.” (Wagalatia 3:2, The Living Bible) Lakini je, hayo yalikuwa tu mazungumzo ya mambo mazuri yasiyoweza kuwa halisi? Kwa halisi ilikuwaje kwa Wakristo wa kwanza waliokuwa wakiishi katika ulimwengu wenye ukosefu mwingi wa usawa?

Mengi yameandikwa juu ya matokeo makubwa ambayo Wakristo wa kwanza walikuwa nayo juu ya ulimwengu wa wakati wao walipositawisha udugu ambao Yesu Kristo alifundisha. Eberhard Arnold anasema hivi katika kitabu chake The Early Christians After the Death of the Apostles:

“Maoni ya usawa ambayo Wakristo walikuwa nayo kuelekea wanadamu wenzao wote kuwa ni ndugu, wenye kushiriki hukumu ile ile na mwito ule ule kama wao wenyewe, yalitokeza usawa na ushirika katika mambo yote. Maoni hayo ya usawa yalitokeza cheo cha usawa kwa wote, daraka la usawa la kufanya kazi, na nafasi ya usawa maishani kwa wote. . . . Kuheshimiana kwa Wakristo wa wakati huo kulitokeza umoja wa jumuiya, ambao ulitegemezwa na upendo, juu ya usawa kamili wa kuzaliwa.”

Huo ulikuwa ushuhuda mzuri kama nini wa umoja kutoka kwa Mungu!

Wenye Usawa Katika Mwili Wenye Umoja

Watu mmoja mmoja katika kundi la kwanza la Kikristo walikuwa na karama na vipawa mbalimbali. Huenda ikawa wengine waliwapita wenzao katika ufundi wa muziki, hali wengine walikuwa na kumbukumbu nzuri au misuli yenye nguvu kuliko wenzao. Zaidi ya utofautiano huo, roho takatifu ilitoa karama na zawadi tofauti tofauti, ingawa tofauti hizo zilikamilishana. Kwa hiyo Paulo aliandika hivi: “Maana kama vile mwili ni mmoja, nao una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi, ni mwili mmoja; vivyo hivyo na Kristo. Kwa maana katika [roho moja] sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa tu watumwa au ikiwa tu huru.” (1 Wakorintho 12:11-13) Wote walikuwa wahubiri, hata ingawa kulikuwako utofautiano tele wa “zawadi katika wanadamu,” kama ambavyo wale waliolichunga kundi walivyosimuliwa kwa njia ya unabii.​—Waefeso 4:8; NW: Zaburi 68:18.

Waangalizi walikuwa wamekomaa kiroho na waliitwa e·pi·sko·peʹo katika Kigiriki. Akiandika juu ya kiarifa e·pi·sko·peʹo (kutoa uangalizi), neno linalohusiana na hilo, W. E. Vine anasema: “Neno hilo halidokezi kupata daraka hilo, bali kule kulitimiza. Halihusu kufikia daraja fulani, bali kutekeleza majukumu.” Wenye kufanya kazi pamoja na waangalizi hao waliowekwa rasmi walikuwa ni di·aʹko·noi, neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “wahudumu,” “watumishi wa huduma,” au “mashemasi.” W. E. Vine anasema kwamba neno hilo “kwa msingi linadokeza mtumishi, ama anayefanya kazi ya kiutumwa, au msaidizi anayetoa utumishi wa bila malipo, bila kutaja ni kazi gani.” Kwa cho chote cha vyeo hivyo, mapendeleo ya utumishi yalikuwa ndilo jambo kubwa. Cheo hakikukaziwa maana, kwani wakiwa waabudu wa Mungu walikuwa na usawa na wote walikuwa watumishi wake.

Ingawa Yesu alichagua wanaume 12 wawe mitume wake, wanawake pia walifurahia kushirikiana naye. Walikuwa wenye kutenda sana, Mariamu Magdalene, Yoana, na Susana wanatajwa kuwa wakimhudumia Yesu. Wanawake, pia, walipokea vipawa vya roho takatifu siku ya Pentekoste 33 W.K. Kwa hiyo waliweza kusema lugha za kigeni na kutoa ushuhuda peupe juu ya kweli za imani yao ya Kikristo. Hata hivyo, dada Wakristo hawakuongoza katika kufundisha kwenye makundi, bali walishiriki pamoja na ndugu kuhubiri Neno la Mungu peupe.-—Luka 8:1-3; Matendo 1:14; 2:17, 18; 18:26.

Pia, Wakristo waliweka kielelezo cha kusaidiana kwa njia ya kibinafsi. Kwa mfano, wakati wageni waliokuja Yerusalemu walipoona kazi ya kimuujiza ya mitume wakati wa Pentekoste mwaka 33 W.K., walikaa muda mrefu zaidi ya walivyokuwa wamekusudia kukaa, nao wakaishiwa chakula na pesa. Lakini Maandiko yanasema: “Wala hapakuwa na mtu mmoja miongoni mwao mwenye mahitaji; kwa sababu watu wote waliokuwa na viwanja au nyumba waliviuza, wakaileta thamani ya vitu vile vilivyouzwa” ili vigawanywe bure chini ya mwelekezo wa mitume. Hiyo ilikuwa roho bora kama nini, yenye kuonyesha upendo na usawa wa hao Wakristo wa kwanza kuwa ni halisi! Ingeweza kusemwa “walikuwa na vitu vyote shirika.”​—Matendo 4:32, 34, 35.

Usawa Unaotumika Leo

Katikati ya migawanyiko ya miundo ya kijamii ya ulimwengu leo, kujaribu kufuata mfano wa Wakristo hao wa kwanza si rahisi Lakini kufanya hivyo sikuzote kumekuwa ni mradi wa Mashahidi wa Yehova. Ni wazi kwamba wamefanikiwa sana. Kitabu Encyclopedia Canadiana kinasema:

“Kazi ya Mashahidi wa Yehova ni kufufua na kuanzisha tena Ukristo wa kwanza uliozoewa na Yesu na wanafunzi wake wakati wa karne za kwanza na pili za wakati wetu. . . . Wote ni ndugu.”

Kama ulivyofanya miaka 1,900 iliyopita udugu huo wa Kikristo leo unatoa msaada halisi nyakati za taabu. Mwezi Novemba 1980, wakati sehemu za Italia zilipotikiswa na tetemeko kubwa la ardhi, lori la kwanza lenye kubeba vifaa vya kusaidia lilifika jioni iyo hiyo katika eneo lililopatwa na msiba. Ripoti rasmi inasema:

“Akina ndugu walistaajabu jinsi msaada uliohitajiwa ulivyofika haraka. Mara moja tulitengeneza mahali petu pa kupikia ambapo chakula kilichopikwa na akina dada kiligawanywa kwa ndugu kila siku. Wale wakaaji wengine wa mji walikuwa hawajapata msaada nao walikuwa wakifanya yote waliyoweza kujifanyia wenyewe. Bila shaka, akina ndugu hawakuwa wachoyo, na chakula kilishirikiwa pamoja na wengi wasio Mashahidi.”

Baada ya kifo cha Mfalme Sobhuza wa Pili wa Swaziland mwezi Agosti 1982, Mashahidi wa Yehova, kwa sababu hawangeweza kushiriki mila za kienyeji za kuomboleza zilizo za kidini, waliteswa. Katika Uingereza Mashahidi wawili, mmoja mweupe na mwingine mweusi, walienda pamoja kwenye Makao ya Ubalozi wa Swaziland nchini mwao wakitaka hali hiyo ipozwe. Baada ya kusikiliza kwa muda, ofisa Mswazi alimgeukia Shahidi yule mweusi, mkurugenzi aliyeelimishwa sana, na kuuliza: “Lakini mbona umekuja hapa?” Akajibiwa hivi: “Kwa sababu nahangaikia hali njema ya ndugu zangu Wakristo katika nchi yenu.” Ofisa huyo aliona vigumu kuelewa jinsi mtu huyo mwenye mali alivyojifanya awe mwenye usawa na Waafrika wanaoishi katika nchi ambayo hakuwa amepata kuzuru hata.

Kwa nini usihudhurie mkutano mmoja kwenye Jumba la Ufalme la mahali penu au mkusanyiko mkubwa zaidi ujionee? Uwe kijana au mzee, maskini au tajiri, uwe una elimu ya chuoni au hujapata elimu hata kidogo, utapata jamii ambayo utajiona umekaribishwa ndani yake. Kila mmoja anaitwa ndugu au dada, na mtu mmoja mmoja hakadiriwa kwa kutegemea jamii au kabila, hali ya maisha, au cheo cha kimwili. Kila mmoja anathaminiwa kwa ajili ya utu na sifa zake za Kikristo.

Kwa kuwa na wazee na watumishi wa huduma, kielelezo cha kufundisha kinategemea muundo wa kundi la Kikristo la kwanza. Na mikutano inaonyesha hali ya usawa, au upatano, duniani pote. Kasisi mmoja wa Kanisa la Uingereza alisema hivi:

“Kila mkutano, uwe ni rasmi au la, ni mkutano muundo wa wakati huu wa kundi la Kikristo wa maagizo kamili. Washiriki wanatazamiwa wajitayarishe kwa ajili ya mikutano ya Jumapili kwa kusoma makala ya Mnara wa Mlinzi, wakifungua mitajo ya Biblia na kutafuta majibu ya maswali ambayo wameyajua kimbele. Kwenye mikutano yenyewe, kuna ushirika mzuri wa kundi. Wanategemezwa na kujua kwamba mafundisho ayo hayo yanatangazwa rasmi kila mahali ulimwenguni wakati ule ule.”

Ukienda na toleo hili la Mnara wa Mlinzi kwenye kundi la mahali penu wakati wa tarehe zilizoorodheshwa kwenye ukurasa wa 2, utaweza kufuatana na mazungumzo hayo.

Mara nyingi mazungumzo hayo yanatia ndani tumaini la wale walio katika kundi: maisha juu ya dunia-paradiso ambamo vita vitakoma na watu watatumia karama kufanya kazi zenye kujenga, wakifurahia kweli kweli “kazi ya mikono yao. Wanadamu wote watiifu wataishi chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Kufa njaa kutakuwa hakupo tena kwa maana chakula tele kitatolewa kwa wote na dunia yenye kuzaa sana. Pia mashambulio ya maradhi yatakuwa jambo la wakati uliopita, wakaaji wote wa dunia wafurahie kwa usawa uzima wa afya kamili.​—Isaya 2:4; 33:24; 65:22,23; Zekaria 8:11, 12.

Ndiyo, tumaini hilo la Kikristo ni halisi, muundo wa wakati huu wa kundi la Kikristo utaendelea mpaka Paradiso ya kidunia. Msingi imara iliokwisha kuwekwa ili kuondelewe kabisa vizuizi vyote vya kitabaka na kitaifa utapanuliwa. Tunaweza kuwaje na uhakika? Kwa sababu Biblia inatabiri kwamba Wakristo “wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha” ndipo wataendelea na ibada yao ya kweli ya Yehova Mungu. Watakuwa na msimamo wa usawa mbele zake, Wewe na jamaa yako mnaweza kuwa kati yao.​—Ufunuo 7:9-10.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova, utaona hali ya usawa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki