Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme
Mpanuko Kwenye “Kitovu”
KATIKA mambo ya viwandani, mji wa Kitwe, Zambia, mara nyingi unaitwa “kitovu” cha eneo la Shaba Nyekundu. Hiyo ni kwa sababu mji wa Kitwe uko katikati kabisa ya wilaya inayochimbua madini hiyo. Lakini Kitwe ni kitovu cha namna nyingine pia—sehemu ya kati ya utendaji wa kitheokrasi katika Zambia. Tangu mwaka 1962 afisi ya tawi imekuwa huko, na wakati wa makumi mawili hayo ya miaka hesabu ya wahubiri katika Zambia imekuwa karibu maradufu, kutoka 30,129 mwaka 1962 kufikia kilele cha 58,925 katika mwaka 1984. Hudhurio la Ukumbusho mwaka 1984 lilikuwa 393,431, na hiyo ni mtu mmoja kwa kila 16 kati ya watu wote wa Zambia.
Kwa kuwa na ongezeko hilo la haraka sana, jengo la tawi la zamani upesi likawa halitoshi. Kwanza, jengo la sasa lilipanuliwa tu, kikaongezwa chumba kingine cha kulia ili kitumiwe na wafanya kazi wa makao makuu, na pia nafasi ya kuwekea vitu na ya vitabu. Lakini, baada ya muda mfupi tawi la Zambia liliingia katika shughuli ya kuchapa vitabu vya habari za Biblia. Na baada ya muda mfupi sana ile nafasi ndogo ya kuchapia ikawa na msongamano sana hata ikawa haitoshi watu kupita-pita au kuwekea vitu. Pia, kwa kuwa afisi ya tawi ilikuwa katika eneo lililozungukwa na makao ya watu, ilikuwa vigumu kuendesha shughuli ya kiwandani bila kusumbua majirani.
Kwa hiyo akina ndugu katika Zambia wakajaza ombi la kutaka uwanja wa kujengea kiwanda kipya. Lakini, halikuwa jambo rahisi kupata uwanja huo. Uwanja wa kwanza walioambiwa wangepewa ulikataliwa na baraza la mji ukasemwa kwamba ‘umepangiwa matumizi ya kiserikali.’ Lakini, ndugu mmoja alijitokeza akatoa sehemu fulani ya ardhi iliyokuwa mali yake. Mara tu baada ya akina ndugu kupata hati zote zilizohitajiwa ili uwe wao, waliajiri shirika la kimataifa linalofanya ramani za ujenzi ili lizichore na kuzipeleka kwenye baraza la mji zikaidhinishwe. Habari za tukio hilo ziliwateremesha akina ndugu katika Zambia! Wengi walikuja kusaidia ujenzi huo wenye kufanywa chini ya usimamizi wa ndugu mmoja aliye fundi wa ujenzi wa kondrati. Kwa muda wa miaka miwili tu, jengo hilo lilimalizika mwaka wa 1984.
Ilikuwa pindi yenye furaha kweli kweli wakati programu ya kuyaweka wakfu majengo hayo ilipofanyika. Ingawa akina ndugu waliambiwa kwamba viti vingekuwa vichache mno kwenye programu, zaidi ya 4,000 kutoka sehemu zote za Zambia walihudhuria mkutano huo! Walisisimuka kumsikia mratibu wa tawi akihutubu juu ya historia ya kazi katika Zambia na kuonyesha namna Yehova ameitegemeza kazi huko. Baada ya hapo, maono fulani yalisikiwa yakitolewa na wazee wa kazi. Nyakati za zamani, wengine walikuwa wametumikia wakiwa mapainia wa pekee katika nchi kama Tanzania, Kenya, na Uganda muda ambao kazi huko ilikuwa ikisimamiwa na tawi la Zambia. Sasa nchi hizo zinaangaliwa na tawi lililoanzishwa Kenya.
Ndugu John McBrine, aliyekuwa akizuru kutoka Zimbabwe akiwa mwangalizi wa eneo la dunia, alimalizia programu kwa kuwatia moyo ndugu wa Zambia wayatumie vizuri majengo hayo mapya. Vitabu vyenye kutokezwa kwenye kiwanda hiki vitaendeleza kusudi la ibada safi na kusaidia watu wenye mioyo myema wayafikie maarifa ya ukweli! Na bila shaka matokeo ya jambo hilo yatakuwa nini? Ni mpanuko zaidi kwenye kitovu cha utendaji wa kitheokrasi katika Zambia!
[Picha katika ukurasa wa 21]
Majengo mapya ya tawi la Sosaiti yetu huko Kitwe, Zambia