Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote—Zambia
NYANDA pana zenye vilima na mabonde, kwenye uwanda wa juu wa meta 1,200—hapa ni Zambia, nchi iliyo katikati ya Afrika ya kati na kusini. Katika kaskazini-mashariki, Milima Muchinga imeinuka hadi meta 2,100. Ule Mto Zambezi wenye nguvu, ungurumao kwa mshindo juu ya Maporomoko ya Victoria yenye sifa ulimwenguni, hufanyiza sehemu kubwa ya mpaka wa kusini wa nchi hii inayozingirwa na mabara. Kuna unamna namna wa watu, kukiwa na vikundi tofauti vya kikabila zaidi ya 70. Lugha kubwa nane zinasemwa hapa, lakini kuna nyingine nyingi.
Katika 1911 lugha tofauti ilianzishwa na kuenezwa katika Zambia. Wageni walileta nakala za Studies in the Scriptures, na Mashahidi wa Yehova tangu hapo na kuendelea walijitahidi kueneza “lugha iliyo safi” ya kweli ya Biblia katika Zambia. (Sefania 3:9) Itikadi zisizo za kimaandiko kuhusu hali ya wafu ni jambo la ushindani. Watu wanapojifunza kweli na kuona jinsi ushirikina umewatumikisha utumwani, tokeo ni kujiweka huru!—Yohana 8:32.
Kwa kielelezo, dada mmoja mwaminifu aripoti hivi: “Mjomba wangu alipokufa kwa ghafula, mama yangu, aliye mshiriki imara wa United Church of Zambia, alifadhaika. Baada ya desturi ya mazishi ya juma zima, nilirudi kijijini kuona jinsi alivyokuwa akiendelea. Nilipofika, nilimkuta mwanamume fulani mzee-mzee nyumbani, na alipoondoka, nilimwuliza nyanya yangu huyo alikuwa nani. Alisema kwamba alikuwa mganga. Mama yangu alikusudia kumlipa ili alipize kisasi cha kifo cha ndugu yake ili kwamba nafsi yake ingeliweza kupumzika. Yeye aliamini kwamba kwa wakati huo ilikuwa ‘ikitangatanga,’ ndivyo alivyosema.
“Nyanya alinieleza zaidi kwamba ziara yangu ilikuwa baraka kwa sababu familia ilikuwa ikitafuta pesa za kumlipa mganga huyo. Akaniomba nichange, lakini kwa busara nilieleza kwamba nikiwa Mkristo, singeweza kushiriki. Nilisababu naye kutoka Zaburi 146:4, linaloonyesha kwamba wafu hawana fahamu—hivyo hakuna nafsi ‘inayotangatanga.’ Pia tulisoma Warumi 12:19, linaloonyesha wazi kwamba kisasi ni cha Yehova bali si chetu. Baada ya hayo, nilimweleza mama yangu kuhusu tumaini la ufufuo alilozungumzia Yesu, kama lilivyorekodiwa katika Yohana 5:28, 29. Alivutiwa na imani yangu yenye nguvu katika ahadi za Mungu. Upesi akaanza kujifunza na Shahidi fulani na kufanya maendeleo haraka. Alikata mahusiano yake yote na dini yake ya awali naye akaonyesha wakfu wake kwa Mungu kwa ubatizo. Sasa yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.”
Dada mwingine aripoti hivi: “Nilienda mazishi ya mke wa mjomba wangu. Nilipofika, nilikuta mjomba wangu na binamu yangu wanaumia kwa njaa. Hawakuwa wamekula chochote tangu siku ile shangazi yangu alipokufa. Nilipouliza sababu, wao walijibu kwamba kulingana na mapokeo, hawaruhusiwi kuwasha moto ili kupika. Nilijitolea kupika, lakini washiriki fulani wa familia waliogopa kwamba ikiwa nitavunja mila hii ya kipagani, kila mmoja angepatwa na kichaa!
“Nilieleza kwamba nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, naheshimu yale Biblia husema katika Mambo ya Walawi 18:30 na huwa sifuati mapokeo yasiyo ya kimaandiko. Halafu nikawaonyesha broshua Roho za Wafu. Baada ya hayo mkazo ulipungua, nami nikaanza kutayarisha chakula kwa ajili ya mjomba na watu wale wengine. Watu wa ukoo wa aliyekufa waliguswa moyo na ujasiri wangu nao wakakubali kujifunza Biblia zaidi. Tayari wamekuwa wahubiri wasiobatizwa, na familia nzima inatumaini kubatizwa karibuni.”
Ni upendezi ulioje wakati lugha iliyo safi ya kweli inapopindua mchafuko wa uwongo wa dini, hasa kusababu kulikotia mizizi yenye nguvu ambako kumetumikisha watu! Kwa baraka ya Yehova, lugha iliyo safi inaenea katika Zambia, kama ilivyo duniani pote.—2 Wakorintho 10:4.
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
HABARI ZA NCHI
Mwaka wa Utumishi wa 1994
KILELE CHA WANAOTOA USHAHIDI: 82,926
UWIANO: Shahidi 1 kwa Watu 107
HUDHURIO LA UKUMBUSHO: 363,372
WASTANI WA WAHUBIRI WALIO MAPAINIA: 10,713
WASTANI WA MAFUNZO YA BIBLIA: 108,948
IDADI YA WALIOBATIZWA: 3,552
IDADI YA MAKUTANIKO: 2,027
OFISI YA TAWI: LUSAKA
[Picha katika ukurasa wa 9]
Majengo ya tawi ya Watch Tower kwenye vitongoji vya Lusaka
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kuhubiri katika Shimabala, kusini mwa Lusaka