Namna Unavyoweza Kuvumilia Misiba
“KWA UVUMILIVU upande wenu mtajipatia nafsi zenu.” Yesu Kristo alisema maneno hayo alipokuwa akitoa unabii kuhusu “wakati wa mwisho.” (Luka 21:19, NW; Danieli 12:4) Katika maneno hayo, mambo mawili haya yanaonekana wazi: (1) Uvumilivu unahitajiwa kabisa ili kuokoa uhai wetu, na (2) inawezekana kuvumilia.
Lakini unaweza kuvumilia namna gani? Ili kujibu ulizo hilo, kwanza tunahitaji kujua sababu gani Yehova anaruhusu taabu na mateso yapate watumishi wake.
Taabu na Mateso—Kwa Sababu Gani?
Sababu kubwa ni kwamba Shetani alitokeza shtaka ushindani juu ya ufaaji na uadilifu wa enzi kuu ya Yehova. (Mwanzo 3:1-19) Yehova amefanya mpango wa kukanusha shtaka hilo kwa ajili ya jina lake mwenyewe na kwa ajili ya wengine.
Pia Mungu ameruhusu watu wake wataabike kwa makusudi yanayoweza kutufaidi sana tukiwa na maoni yanayofaa juu ya masumbuko hayo. Kwa mfano, tukivumilia chini ya jaribu bila kuweka uchungu moyoni kwa sababu ya misiba yetu, tunathibitisha kwamba imani yetu ni ya kweli, namna ya imani inayompendeza Mungu. (1 Petro 1:6, 7; Waebrania 11:6) Lakini masumbuko yanaweza pia kuonyesha vikosa vya utu kama kiburi, kukosa subira, na kupenda starehe. Kwa msaada wa roho ya Mungu, tunaweza kujitahidi tushinde vitabia hivyo na ‘kujivika kwa ukamili zaidi utu mpya.’—Wakolosai 3:9-14.
Mtunga zaburi alieleza jambo hilo vizuri sana kwa ajili yetu, akisema: “Ilikuwa vema kwangu kuwa naliteswa, nipate kujifunza amri zako.” (Zaburi 119:71) Ni maoni mazuri kama nini juu ya masumbuko! Hakuna kulalamika au kunung’unika. Hakuna hangaiko la kichoyo juu ya hasara ya kibinafsi ambayo labda ililetwa na masumbuko hayo. Bali, hapo panaonyesha utambuzi wenye hekima kwamba yale ambayo Yehova aliruhusu yapate mtunga zaburi yangeweza kumsaidia athamini miongozo ya Yehova kwa ukamili zaidi. Je! sisi tunaruhusu hali ya kutaabika iwe na matokeo kama hayo juu yetu?
Mtume Paulo alifaidika na dhiki aliyopata katika wilaya ya Esia. Kwanza, msiba huo ulimfanya amtegemee Yehova kwa ukamili zaidi. Pia ulikazia imani ya mtume katika ufufuo, kwa maana yeye alivumilia magumu yake kwa tumaini kamili katika “Mungu, awafufuaye wafu.” (2 Wakorintho 1:8-10) Ndiyo, Paulo alifurahia faida kadha kwa sababu ya uvumilivu wake akiwa chini ya taabu.
Ndivyo ilivyo kwa Wakristo wale walio na maoni yanayofaa juu ya masumbuko leo. Katika Zimbabwe, nchi iliyokuwa na vita ya kupambana na askari wavamizi, kundi la watu wa Yehova lilihamishwa likaingizwa katika kijiji chenye ulinzi. Kwa sababu ya hali za vita, kila mmoja wa wale wazee watatu waliowekwa rasmi katika kundi hilo alikuwa amefiwa na mtoto. Isitoshe, watu wa kwao walikuwa wakiwakaza sana wazazi hao Wakristo waache imani yao kwa kutuliza roho ambazo zilisemwa kuwa zilikuwa zimekasirishwa. Wazee walionaje? Akiwasemea wote watatu, mmoja wao alisema: “Wakati taifa linapoendelea na vita, hata sisi tunaendelea na vita pamoja na roho waovu. Sisi tuna faida inayowazidi adui zetu kwa sababu tuna tumaini, tumaini lililo hai. Kwa hiyo, hata tukifa piganoni, maadamu tumekufa tukiwa waaminifu kwa Yehova tutafufuliwa. Tutakuwa tumewashinda adui.” Wanaume watatu hao waaminifu hawakuacha kamwe kuona kwamba Yehova ana uwezo wa kuwakomboa. Kwa kuona msimamo wao imara, hata sisi tunapaswa kusadiki kwamba tunaweza kuvumilia!
Wakati Mateso Yanapokuwa ya Ukatili!
‘Lakini namna gani mateso yakiwa ya kinyama, ya kutumia njia za kutesa-tesa watu kwa ukatili?’ huenda wewe ukauliza. ‘Hapo kweli tunaweza hata kuvumilia na tusiishiwe na imani yetu?’ Wakristo wa kwanza waliweza kuvumilia kutendwa vibaya sana bila kuacha imani yao ili wakubaliane na watesi.
Vivyo hivyo, imani kamili katika Yehova ilionyeshwa na Mkristo wa kisasa anayeishi katika eneo la mashambani lililo peke yalo huko Zimbabwe. Yeye alikuwa peke yake katika pindi hii kwa sababu mke wake alikuwa ameenda kutembelea binti yao aliyeolewa. Kwa ghafula, alifikiwa na wanaume wenye silaha wakamtolea mashtaka ya uwongo kwa sababu ya msimamo wake wa Kikristo. Baada ya kumpiga vikali, wanaume hao walifunganisha matufali yenye moto kati ya miguu yake na pia wakamwagiza atembee juu ya matufali hayo. Halafu akaachwa peke yake afe. Kwa sababu badiliko la ghafula la hali za eneo hilo zilikuwa zimefanya isiwezekane kusafiri, mke wa mwanamume huyo hakuujua mkasa wa mumeye. Majirani waliagizwa wasimsaidie au sivyo wauawe. Kwa hiyo akabaki akiwa peke yake katika hali hiyo kwa muda wa miezi mitatu kamili, kila siku akitazamia kufa.
Mwanamume huyo Mkristo mwenye kutaabika aliweza kujiendeleza kwa kunywa maji na kula ugali nyumbani kwake. Lakini kwa sababu ya vile alivyokuwa ametendwa vibaya, hakuweza kutembea. Basi, wakati kuni zilizokuwa karibu zilipomalizika, akalazimika kuvunja-vunja viti na meza na kutumia vitu hivyo kuwa kuni za kuwasha moto apike. Maji aliyokuwa nayo yakashika kutu na kujawa na wadudu. Sehemu za mwili wake zilizoungua zikaanza kuoza.
Ndugu huyo alikuwa katika hali hiyo wakati mke wake alipoweza mwishowe kurudi nyumbani baada ya miezi mitatu. Ebu wazia alivyojisikia alipomwona! Bila kukawia, mke wake akafanya matayarisho kumpeleka hospitali. Ili afanye hivyo, alilazimika kumchukua akiwa katika kigari cha kusukuma kubebea vitu akamfikisha kwenye kituo cha basi cha karibu zaidi, kisha kutoka hapo amfikishe mjini kwenye hospitali. Majuma matatu baadaye, mwanamume huyo aliruhusiwa atoke hospitali akaenda nyumbani kwa binti yake, ambako alipokea msaada wa kiroho na kitia-moyo kwa washiriki wa kundi la Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo.
Ni nini kilichosaidia muunga-mkono huyo mshikamanifu wa Ufalme wa Mungu avumilie kutendwa unyama? Yeye alikaa peke yake kabisa muda wa miezi mitatu. Alitazamia kabisa kufa. Hata hivyo, alipoulizwa alijisikiaje wakati wa taabu hiyo alijibu, “Nilijisikia kwamba Yehova alikuwa pamoja nami wakati wote.” Hakulalamika dhidi ya watesi wake wala kunung’unika juu ya yaliyokuwa yamempata—aliloonyesha ni usadiki imara tu kwamba Yehova hawaachi kamwe watumishi wake washikamanifu.—Zaburi 37:28.
Ndiyo, Wakristo wanaweza kuvumilia. Wanajua kwamba Yehova akiruhusu dhiki, anafanya hivyo kwa kusudi zuri na inawezekana kuvumilia. Neno la Mungu na pia yaliyowapata wengine yanatuhakikishia jambo hilo. (Mathayo 24:13) Lakini, mara nyingi tunapovumilia majaribu tunahitaji kufarijiwa, sivyo? Lakini tugeukie wapi tupate faraja kama hiyo?