Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 9/15 kur. 9-14
  • Uvumilivu—Muhimu kwa Wakristo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uvumilivu—Muhimu kwa Wakristo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uvumilivu—Maana Yao
  • Uvumilivu—Kwa Nini?
  • Vumilia Hadi Mwisho—Jinsi Gani?
  • “Mfikirieni Sana Yeye Ambaye Amevumilia”
    ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • “Acheni Uvumilivu Ukamilishe Kazi Yake”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Shikamana na Tengenezo la Yehova
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Uvumilivu Unaopata Ushindi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 9/15 kur. 9-14

Uvumilivu—Muhimu kwa Wakristo

“Katika imani yenu tieni . . . saburi [uvumilivu, NW].”—2 PETRO 1:5, 6.

1, 2. Kwa nini ni lazima sisi sote tuvumilie hadi mwisho?

MWANGALIZI mmoja asafiriye pamoja na mke wake walikuwa wakimtembelea Mkristo mwenzao aliyekuwa katika miaka yake ya 90. Alikuwa ametumia miongo kadhaa katika huduma ya wakati wote. Walipokuwa wakiongea, ndugu huyo mwenye umri mkubwa zaidi aliyakumbuka baadhi ya mapendeleo aliyokuwa amefurahia katika miaka iliyopita. “Lakini,” akaomboleza huku machozi yakianza kutiririka usoni pake, “sasa siwezi kufanya mengi.” Mwangalizi huyo asafiriye alifungua Biblia yake, akasoma Mathayo 24:13, ambapo Yesu Kristo ananukuliwa akisema: “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.” Kisha mwangalizi huyo akamtazama ndugu huyo mpendwa na kusema: “Mgawo wa mwisho ambao sisi sote tunao, haidhuru tunaweza kufanya mengi kadiri gani au machache kadiri gani, ni kuvumilia hadi mwisho.”

2 Naam, tukiwa Wakristo ni lazima sisi sote tuvumilie hadi mwisho wa mfumo huu wa mambo au hadi mwisho wa maisha zetu. Hakuna njia nyingine ya kupokea kibali cha Yehova ili kupata wokovu. Tumo katika shindano la mbio la kupata uhai, na ni lazima “tupige mbio kwa saburi [uvumilivu, NW]” mpaka tufike mwisho. (Waebrania 12:1) Mtume Petro alikazia umaana wa sifa hiyo alipowahimiza Wakristo wenzake hivi: “Katika imani yenu tieni . . . saburi [uvumilivu, NW].” (2 Petro 1:5, 6) Lakini uvumilivu ni nini hasa?

Uvumilivu—Maana Yao

3, 4. Kuvumilia kunamaanisha nini?

3 Kuvumilia kunamaanisha nini? Kitenzi cha Kigiriki kwa neno “-vumilia” (hy·po·meʹno) humaanisha kihalisi “kuendelea au kufululiza kuwa chini.” Hilo hutokea mara 17 katika Biblia. Kulingana na watunga-kamusi W. Bauer, F. W. Gingrich, na F. Danker, hilo humaanisha “kuendelea kusimama badala ya kutoroka . . . , kusimama imara, kukabiliana na hali.” Nomino ya Kigiriki kwa neno “uvumilivu” (hy·po·mo·neʹ) hutokea zaidi ya mara 30. Kuhusu neno hilo, A New Testament Wordbook, cha William Barclay, chasema: “[Uvumilivu] ni nia inayoweza kustahimili mambo, si kwa sababu tu ya kukata tamaa, bali kwa [sababu ya kuwa na] tumaini jangavu . . . Ni ile sifa inayomfanya mtu aendelee kusimama akikabili magumu. Ni ile sifa iwezayo kugeuza jaribu lililo gumu zaidi liwe utukufu kwa sababu inatazama ng’ambo ya maumivu hadi kwenye mradi.”

4 Basi, uvumilivu hutuwezesha tusimame imara na tusikose kuwa na tumaini tunapokabili vizuizi au magumu. (Warumi 5:3-5) Hutazama ng’ambo ya maumivu yaliyopo hadi kwenye mradi—ile tuzo, au zawadi, ya uhai wa milele, iwe ni mbinguni au duniani.—Yakobo 1:12.

Uvumilivu—Kwa Nini?

5. (a) Kwa nini Wakristo wote ‘wanahitaji kuwa na uvumilivu’? (b) Majaribu yetu yanaweza kugawanywa katika vikundi gani viwili?

5 Tukiwa Wakristo, sisi sote ‘tunahitaji kuwa na uvumilivu.’ (Waebrania 10:36, Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa nini? Kwa msingi ni kwa sababu ‘tunaangukia katika majaribu mbalimbali.’ Maandishi ya Kigiriki hapa kwenye Yakobo 1:2 hudokeza kabiliano lisilotazamiwa au lisilopendeza, kama vile wakati mtu anapokabiliwa na mnyang’anyi. (Linganisha Luka 10:30.) Tunaangukia majaribu yanayoweza kugawanywa katika vikundi viwili: yale yaliyo ya kawaida kwa wanadamu kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa, na yale yanayotokea kwa sababu ya ujitoaji kimungu wetu. (1 Wakorintho 10:13; 2 Timotheo 3:12) Baadhi ya majaribu hayo ni gani?

6. Shahidi mmoja alivumiliaje alipokabiliwa na ugonjwa wenye maumivu?

6 Ugonjwa mahututi. Kama vile Timotheo, ni lazima Wakristo fulani wavumilie ‘magonjwa ya mara kwa mara.’ (1 Timotheo 5:23) Hasa tunapokabili ugonjwa wenye kuendelea, labda wenye maumivu mengi, ndipo tunahitaji kuvumilia, kusimama imara, kwa msaada wa Mungu na tusikose kuwa na tumaini letu la Kikristo. Fikiria kielelezo cha Shahidi mmoja katika miaka yake ya mapema ya 50 aliyeshindana vikali na kwa muda mrefu, dhidi ya tezi lenye kudhuru na lenye kukua upesi. Kupitia upasuaji wa visa viwili aliendelea kuwa thabiti katika azimio lake la kutokubali kutiwa damu mishipani. (Matendo 15:28, 29) Lakini tezi hilo lilitokea tena tumboni mwake, likaendelea kukua karibu na uti wa mgongo wake. Lilipoendelea kukua, alipatwa na maumivu makali ya kimwili yasiyowazika ambayo hayakuweza kupunguzwa na kiasi chochote cha dawa. Lakini, alitazama ng’ambo ya maumivu yaliyopo hadi kwenye zawadi ya uhai katika ulimwengu mpya. Aliendelea kushiriki tumaini lake jangavu pamoja na madaktari, wauguzi, na wageni. Alivumilia hadi mwisho kabisa—mwisho wa uhai wake. Huenda ikawa tatizo lako la afya si lenye kutisha uhai au lenye maumivu kama lile lililompata ndugu huyo mpendwa, lakini huenda bado likawa mtihani mkubwa wa uvumilivu.

7. Uvumilivu hutia ndani maumivu ya aina gani kwa baadhi ya ndugu na dada zetu wa kiroho?

7 Maumivu ya kihisiamoyo. Mara kwa mara, baadhi ya watu wa Yehova hukabili “huzuni ya moyo” inayosababisha ‘roho iliyopondeka.’ (Mithali 15:13) Mshuko mkubwa wa moyo ni jambo la kawaida katika “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1, NW) Science News la Desemba 5, 1992, liliripoti hivi: “Viwango vya mshuko mkubwa wa moyo, ambao mara nyingi ni wenye kulemaza vimeongezeka katika kila kizazi kinachofuata ambacho kimezaliwa tangu 1915.” Kuna visababishi tofauti-tofauti vya mshuko huo wa moyo, kuanzia sababu zinazohusu viungo vya mwili hadi maono yasiyopendeza yanayoumiza sana. Kwa Wakristo fulani, uvumilivu unahusisha shindano la kila siku la kusimama imara wanapokabili maumivu ya kihisiamoyo. Lakini, hawakati tamaa. Wanaendelea kuwa waaminifu kwa Yehova yajapokuwa machozi.—Linganisha Zaburi 126:5, 6.

8. Twaweza kukabili jaribu jipi la kifedha?

8 Majaribu mbalimbali tunayokabili yaweza kutia ndani matatizo makubwa ya kiuchumi. Wakati ndugu mmoja katika New Jersey, U.S.A., alipopoteza kazi yake kwa ghafula, kwa kueleweka alikuwa na wasiwasi juu ya namna ya kulisha familia yake na kutopoteza nyumba yake. Hata hivyo, hakukosa kuwa na tumaini la Ufalme. Alipokuwa akitafuta kazi nyingine, alitumia fursa hiyo kwa faida yake akitumikia akiwa painia-msaidizi. Hatimaye, alipata kazi.—Mathayo 6:25-34.

9. (a) Kumpoteza mpendwa katika kifo kunaweza kutakaje uvumilivu? (b) Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba si vibaya kulia machozi ya huzuni?

9 Ikiwa umempoteza mpendwa katika kifo, unahitaji uvumilivu unaodumu muda mrefu baada ya wale walio karibu na wewe kurudia utaratibu wao wa kawaida. Huenda hata ukaona kwamba inakuwa vigumu kwako hasa kila mwaka karibu na wakati mpendwa wako alipokufa. Kuvumilia hali hiyo ya kupoteza mpendwa hakumaanishi kwamba ni vibaya kulia machozi ya huzuni. Ni jambo la asili kuomboleza kifo cha mtu tuliyempenda, na hilo halionyeshi hata kidogo ukosefu wa imani katika tumaini la ufufuo. (Mwanzo 23:2; linganisha Waebrania 11:19.) Yesu ‘alilia machozi’ baada ya Lazaro kufa, ingawa Yeye alikuwa amemwambia Martha hivi kwa hakika: “Ndugu yako atafufuka [atainuka, NW].” Na Lazaro aliinuka!—Yohana 11:23, 32-35, 41-44.

10. Kwa nini watu wa Yehova wana uhitaji wa pekee wa uvumilivu?

10 Kuongezea kuvumilia majaribu yaliyo ya kawaida kwa wanadamu wote, watu wa Yehova wana uhitaji wa pekee wa uvumilivu. “Mtakuwa watu wa kuchukiwa na watu wa mataifa yote kwa ajili ya jina langu,” Yesu akaonya. (Mathayo 24:9) Alisema hivi pia: “Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi.” (Yohana 15:20) Kwa nini kuwe chuki na mnyanyaso huo wote? Kwa sababu haidhuru kule tunakoishi kwenye dunia hii tukiwa watumishi wa Mungu, Shetani anajaribu kuvunja uaminifu-maadili wetu kwa Yehova. (1 Petro 5:8; linganisha Ufunuo 12:17.) Hivyo mara nyingi Shetani amesababisha mnyanyaso mwingi, akitahini sana uvumilivu wetu.

11, 12. (a) Mashahidi wa Yehova na watoto wao walikabili mtihani gani wa uvumilivu katika miaka ya 1930 na miaka ya mapema ya 1940? (b) Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawasalimu mfano wa kitaifa?

11 Kwa kielelezo, katika miaka ya 1930 na miaka ya mapema ya 1940, Mashahidi wa Yehova pamoja na watoto wao katika United States na Kanada walinyanyaswa kwa sababu hawakusalimu mfano wa kitaifa kwa sababu za dhamiri. Mashahidi hustahi mfano wa kitaifa wanamoishi, lakini wanaitii ile kanuni iliyoandikwa katika Sheria ya Mungu kwenye Kutoka 20:4, 5: “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunai. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu.” Wakati watoto wengine wa shule walio Mashahidi walipofukuzwa shuleni kwa sababu walitamani kuelekeza ibada yao kwa Yehova Mungu pekee, Mashahidi walianzisha Shule za Ufalme ili kuwafunza. Wanafunzi hao walirudia shule za umma wakati Mahakama Kuu Zaidi ya United States ilipotambua msimamo wao wa kidini, kama vile mataifa yaliyonurishwa yanavyofanya leo. Hata hivyo, uvumilivu wenye moyo mkuu wa vijana hao unatumika ukiwa kielelezo chema hasa kwa vijana Wakristo ambao huenda wakakabili dhihaka sasa kwa sababu wanajitahidi kuishi kulingana na viwango vya Biblia.—1 Yohana 5:21.

12 Majaribu mbalimbali tunayokabili—yale yaliyo ya kawaida kwa wanadamu na pia yale tunayokabili kwa sababu ya imani yetu ya Kikristo—huonyesha sababu kwa nini tunahitaji uvumilivu. Lakini tunaweza kuvumiliaje?

Vumilia Hadi Mwisho—Jinsi Gani?

13. Yehova hutoaje uvumilivu?

13 Watu wa Mungu wana manufaa dhahiri kuliko wale wasiomwabudu Yehova. Ili kupata msaada, tunaweza kumwendea “yule Mungu ambaye hutoa uvumilivu.” (Warumi 15:5, NW) Lakini, Yehova hutoaje uvumilivu? Njia moja ambayo anafanya hivyo ni kupitia vielelezo vya uvumilivu ambavyo vimeandikwa katika Neno lake, Biblia. (Warumi 15:4) Tunapotafakari vielelezo hivyo, tunatiwa moyo kuvumilia na pia tunajifunza mengi juu ya jinsi ya kuvumilia. Fikiria vielelezo viwili vyenye kutokeza—ule uvumilivu wenye moyo mkuu wa Ayubu na ule uvumilivu wa Yesu Kristo usio na dosari.—Waebrania 12:1-3; Yakobo 5:11.

14, 15. (a) Ayubu alivumilia majaribu gani? (b) Ayubu aliwezaje kuvumilia majaribu aliyokabili?

14 Ni hali zipi zilizotahini uvumilivu wa Ayubu? Alipatwa na magumu ya kiuchumi wakati alipopoteza mali zake nyingi. (Ayubu 1:14-17; linganisha Ayubu 1:3.) Ayubu alihisi maumivu ya kupoteza wapendwa wakati watoto wake wote kumi walipouawa katika dhoruba. (Ayubu 1:18-21) Alipatwa na ugonjwa mahututi, wenye maumivu mengi. (Ayubu 2:7, 8; 7:4, 5) Mke wake mwenyewe alimsonga ampe Mungu kisogo. (Ayubu 2:9) Mashirika wa karibu walisema mambo yenye kuumiza, yasiyo na fadhili, na yasiyo kweli. (Linganisha Ayubu 16:1-3 na Ayubu 42:7.) Hata hivyo, katika hayo yote, Ayubu alisimama imara, akidumisha uaminifu-maadili. (Ayubu 27:5) Mambo aliyovumilia yanafanana na majaribu ambayo watu wa Yehova hukabili leo.

15 Ayubu aliweza kuvumiliaje majaribu hayo yote? Jambo moja hasa lililomtegemeza Ayubu lilikuwa tumaini. “Yako matumaini ya mti,” akajulisha. “Ukikatwa utachipuka tena, wala machipukizi yake hayatakoma.” (Ayubu 14:7) Ayubu alikuwa na tumaini gani? Kama ionyeshwavyo katika mistari michache baadaye, yeye alisema hivi: “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena? . . . Wewe ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa [au, hamu] ya kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15) Naam, Ayubu alitazama ng’ambo ya maumivu yake ya wakati huo. Alijua kwamba majaribu yake yasingedumu milele. Zaidi sana, angalipaswa avumilie hadi kifo. Tazamio lake lenye tumaini lilikuwa kwamba Yehova, anayetamani kwa upendo kuwafufua wafu, angemrudisha kwenye uhai.—Matendo 24:15.

16. (a) Tunajifunza nini juu ya uvumilivu kutokana na kielelezo cha Ayubu? (b) Tumaini la Ufalme lapaswa liwe halisi kwetu kwa kadiri gani, na kwa nini?

16 Tunajifunza nini kutokana na uvumilivu wa Ayubu? Ili kuvumilia hadi mwisho, ni lazima tusikose kamwe kuwa na tumaini letu. Kumbuka pia, uhakika wa tumaini la Ufalme humaanisha kwamba kuteseka kokote tunakokabili ni ‘kwa muda tu’ kwa kulinganishwa. (2 Wakorintho 4:16-18) Tumaini letu lenye thamani kubwa linategemea kwa uthabiti ahadi ya Yehova juu ya wakati fulani ujao ulio karibu ambapo “atafuta kila chozi katika macho [yetu], wala mauti haitakuwapo tena, wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:3, 4) Tumaini hilo, ambalo “halitahayarishi,” ni lazima lilinde fikira zetu. (Warumi 5:4, 5; 1 Wathesalonike 5:8) Ni lazima liwe halisi kwetu—halisi sana hivi kwamba kwa macho ya imani, twaweza kujiona wenyewe tukiwa katika ulimwengu mpya—wakati ambapo hatung’ang’ani tena na ugonjwa na mshuko wa moyo bali tukiamka kila siku katika afya njema na wenye akili isiyojaa matatizo; wakati ambapo hatuhangaiki tena juu ya misongo mikubwa ya kiuchumi bali tukiishi katika usalama; wakati ambapo hatuombolezi kifo cha wapendwa bali tukiwa na msisimuko wa kuwaona wakiwa wamefufuliwa. (Waebrania 11:1) Bila tumaini hilo tunaweza kulemewa sana na majaribu yetu ya wakati huu hivi kwamba tunakata tamaa. Tukiwa na tumaini letu, tuna kichocheo kilichoje cha kuendelea kupiga vita, ili kuendelea kuvumilia hadi mwisho!

17. (a) Yesu alivumilia majaribu gani? (b) Kule kuteseka kwingi ambako Yesu alivumilia kwaweza labda kuonwa kutokana na jambo gani? (Ona kielezi-chini.)

17 Biblia yatuhimiza ‘tumtazame kwa mkazo’ Yesu na ‘kumfikiria kwa ukaribu.’ Yeye alivumilia majaribu gani? Baadhi yayo yalitokana na dhambi na kutokamilika kwa wengine. Yesu alivumilia ‘maongezi-kinyume yenye kufanywa na watenda dhambi’ na pia matatizo yaliyotokea miongoni mwa wanafunzi wake, kutia ndani mabishano yao ya mara kwa mara juu ya ni nani aliyekuwa mkuu zaidi. Zaidi ya hayo, alikabili mtihani wa imani usio na kifani. ‘Alivumilia mti wa mateso.’ (Waebrania 12:1-3, NW; Luka 9:46; 22:24) Ni vigumu hata kuwazia kule kuteseka kiakili na kimwili kulikohusika katika maumivu ya kutundikwa na ile aibu ya kuuawa akiwa mkufuru.a

18. Kulingana na mtume Paulo, ni mambo gani mawili yaliyomtegemeza Yesu?

18 Ni nini kilichomwezesha Yesu avumilie hadi mwisho? Mtume Paulo ataja mambo mawili yaliyomtegemeza Yesu: “maombi na dua” na pia “furaha iliyowekwa mbele yake.” Yesu, yule Mwana mkamilifu wa Mungu, hakuona aibu kuomba msaada. Alisali “pamoja na kulia sana na machozi.” (Waebrania 5:7; 12:2) Hasa wakati jaribu lake kuu zaidi lilipokuwa likikaribia ndipo aliona ni lazima kusali mara kwa mara na kwa bidii ili kupata nguvu. (Luka 22:39-44) Kwa kuitikia maombi ya Yesu, Yehova hakuliondoa lile jaribu, bali alimwimarisha Yesu kulivumilia. Yesu alivumilia pia kwa sababu alitazama ng’ambo ya mti wa mateso hadi kwenye thawabu yake—ile furaha ambayo angekuwa nayo katika kuchangia utakaso wa jina la Yehova na kufidiwa kwa familia ya kibinadamu kutoka katika kifo.—Mathayo 6:9; 20:28.

19, 20. Kielelezo cha Yesu kinatusaidiaje kuwa na maoni halisi juu ya yale yanayohusika katika uvumilivu?

19 Kutokana na kielelezo cha Yesu, twajifunza mambo kadhaa yanayotusaidia kuwa na maoni halisi juu ya yale yanayohusika katika uvumilivu. Mwendo wa uvumilivu si rahisi. Ikiwa tunaona vigumu kuvumilia jaribu fulani, kuna faraja kujua kwamba ilikuwa vivyo hivyo hata kwa Yesu. Ili kuvumilia hadi mwisho, ni lazima tusali mara kwa mara ili kupata nguvu. Nyakati fulani, tunapokuwa chini ya jaribu huenda tukahisi hatustahili kusali. Lakini Yehova hutualika tumwagie mioyo yetu ‘kwa sababu yeye hutujali.’ (1 Petro 5:7, NW) Na kwa sababu ya yale ambayo Yehova ameahidi katika Neno lake, amejiwajibisha kutoa “nguvu inayozidi iliyo ya kawaida” kwa wale wanaomwitia kwa imani.”—2 Wakorintho 4:7-9, NW.

20 Nyakati fulani ni lazima tuvumilie kwa machozi. Kwa Yesu maumivu ya mti wa mateso hayakuwa sababu hasa ya kushangilia. Badala ya hivyo, furaha ilikuwa katika ile thawabu iliyowekwa mbele yake. Katika hali yetu si jambo halisi kutazamia kwamba sikuzote tutahisi uchangamfu na msisimuko tunapokuwa chini ya jaribu. (Linganisha Waebrania 12:11.) Hata hivyo, kwa kutazama mbele kwenye thawabu, huenda tukaweza ‘kuhesabu ya kuwa ni furaha tupu’ hata tunapokabili hali zenye kujaribu zaidi. (Yakobo 1:2-4; Matendo 5:41) Jambo la maana ni kwamba tuendelee kuwa thabiti—hata ikiwa ni lazima iwe kwa machozi. Kwa vyovyote vile, Yesu hakusema, ‘Mwenye kulia machozi machache zaidi, ndiye atakayeokoka’ bali, “Mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.”—Mathayo 24:13.

21. (a) Kwenye 2 Petro 1:5, 6, tunahimizwa kutia nini katika uvumilivu wetu? (b) Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika makala inayofuata?

21 Hivyo uvumilivu ni wa muhimu ili kupata wokovu. Hata hivyo, kwenye 2 Petro 1:5, 6, tunahimizwa kutia ujitoaji kimungu katika uvumilivu wetu. Ujitoaji kimungu ni nini? Unahusianaje na uvumilivu, na wewe unaweza kuupataje? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

a Kule kuteseka kwingi ambako Yesu alivumilia kwaweza labda kuonwa kutokana na jambo la kwamba mwili wake mkamilifu ulikufa baada ya muda wa saa chache tu ukiwa mtini, ilihali wale watenda maovu waliotundikwa kando yake walilazimika kuvunjwa miguu ili kuharakisha kifo. (Yohana 19:31-33) Hawakuwa wamepatwa na kule kuteseka kiakili na kimwili kulikompata Yesu katika lile jaribu la usiku kucha bila usingizi kabla ya kutundikwa, labda kufikia hatua ambayo hangeweza hata kuchukua mti wake mwenyewe wa mateso.—Marko 15:15, 21.

Ungejibuje?

◻ Kuvumilia kunamaanisha nini?

◻ Kwa nini watu wa Yehova wana uhitaji wa pekee wa uvumilivu?

◻ Ni nini kilichomwezesha Ayubu avumilie?

◻ Kielelezo cha Yesu kinatusaidiaje kuwa na maoni halisi juu ya uvumilivu?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Shule za Ufalme zilianzishwa ili kuwafundisha watoto Wakristo waliofukuzwa shuleni kwa sababu ya kuelekeza ibada yao kwa Yehova pekee

[Picha katika ukurasa wa 12]

Akiwa ameazimia kumheshimu Baba yake, Yesu alisali ili kupata nguvu za kuvumilia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki