Sura ya 7
“Mfikirieni Sana Yeye Ambaye Amevumilia
1-3. (a) Yesu ana hisia nyingi kadiri gani anapokuwa katika bustani ya Gethsemane, nazo zinatokana na nini? (b) Ni nini kinachoweza kusemwa kuhusu mfano wa Yesu wa uvumilivu, na ni maswali gani yanayotokea?
YESU ana mikazo mingi. Hajapata kuwa na mambo mengi hivyo yenye kumhangaisha kiakili na kihisia. Anakaribia mwisho wa maisha yake duniani. Akitembea pamoja na mitume wake, anafika katika bustani ya Gethsemane. Amekutana nao hapo mara nyingi. Hata hivyo, usiku huu, anahitaji kuwa peke yake. Anawaacha mitume wake na kuingia ndani zaidi ya bustani, kisha anapiga magoti na kuanza kusali. Anasali kwa bidii sana na kwa hisia nyingi sana hivi kwamba jasho lake linakuwa “kama matone ya damu yakianguka chini.”—Luka 22:39-44.
2 Kwa nini Yesu amefadhaika sana hivyo? Ni kweli anajua kwamba karibuni atateseka sana, lakini si hilo linalomhangaisha. Anafikiria mambo mazito zaidi. Anahangaikia sana jina la Baba yake na anatambua kwamba wakati ujao wa wanadamu unategemea kuendelea kwake kuwa mwaminifu. Yesu anajua lazima avumilie. Akishindwa, atafanya jina la Yehova litukanwe. Lakini, Yesu hakushindwa. Baadaye siku hiyohiyo, muda mfupi kabla ya kukata pumzi, mtu huyo aliyeweka mfano mzuri zaidi wa uvumilivu hapa duniani anapaaza sauti hivi kwa ushindi: “Imetimizwa!”—Yohana 19:30.
3 Biblia inatuhimiza hivi: “Mfikirieni sana yeye [Yesu] ambaye amevumilia.” (Waebrania 12:3) Hivyo, kuna maswali ya maana yanayohitaji kujibiwa: Ni majaribu gani ambayo Yesu alivumilia? Ni nini kilichomwezesha kuvumilia? Tunaweza kuiga mfano wake jinsi gani? Hata hivyo, kabla hatujajibu maswali hayo, acheni tuchunguze maana ya uvumilivu.
Uvumilivu Ni Nini?
4, 5. (a) “Uvumilivu” ni nini? (b) Toa mfano unaoonyesha kwamba uvumilivu unatia ndani mengi zaidi kuliko kupatwa na hali ngumu isiyoweza kuepukwa.
4 Mara kwa mara, sisi sote ‘tunahuzunishwa na majaribu ya namna mbalimbali.’ (1 Petro 1:6) Je, kukabili tu jaribu kunamaanisha kwamba tunalivumilia? Hapana. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “uvumilivu” linamaanisha “uwezo wa kustahimili au kubaki imara mtu anapokabili tatizo.” Mtaalamu fulani anasema hivi kuhusu aina ya uvumilivu unaozungumziwa na waandikaji wa Biblia: ‘Ni mtazamo unaomwezesha mtu kustahimili mambo, si kwa sababu tu hana la kufanya bali kwa sababu ana tumaini thabiti. Ni sifa inayomwezesha mtu kusimama imara huku akiendelea kukabili tatizo fulani. Ni sifa nzuri inayoweza kufanya jaribu kali sana lionekane kuwa jambo linaloleta utukufu kwa sababu ingawa kuna maumivu, bado kuna tumaini.’
5 Kwa hiyo basi, kuvumilia si kupatwa tu na hali ngumu isiyoepukika. Kulingana na Biblia, uvumilivu unatia ndani kusimama imara, kuwa na mtazamo unaofaa na tumaini ingawa kuna majaribu. Fikiria mfano huu: Wanaume wawili wamefungwa katika gereza moja lakini kwa sababu tofauti. Mmoja amevunja sheria naye anatumikia kifungo chake kwa kulazimishwa akiwa bila tumaini lolote. Yule mwingine ni Mkristo wa kweli ambaye amefungwa kwa sababu ya uaminifu wake, naye anasimama imara na kuwa na maoni yanayofaa kwa sababu anaiona hali yake kuwa nafasi ya kuonyesha imani yake. Bila shaka, Mkristo huyo mshikamanifu ni mfano mzuri wa sifa hiyo nzuri ya uvumilivu, lakini, hatuwezi kusema kwamba yule aliyevunja sheria ni mfano mzuri wa sifa hiyo.—Yakobo 1:2-4.
6. Tunakuza uvumilivu jinsi gani?
6 Ili kupata wokovu, lazima tuvumilie. (Mathayo 24:13) Hata hivyo, hatuzaliwi tukiwa na sifa hiyo. Lazima tukuze sifa ya uvumilivu. Jinsi gani? Andiko la Waroma 5:3 linasema: “Dhiki hutokeza uvumilivu.” Ndiyo, ikiwa kwa kweli tunataka kukuza uvumilivu, hatutaepuka majaribu yote ya imani kwa sababu ya woga. Badala yake, lazima tuyakabili. Tunakuza uvumilivu siku baada ya siku tunapokabili na kushinda majaribu makubwa na madogo. Kila jaribu tunaloshinda linatupa nguvu za kukabili linalofuata. Bila shaka, hatukuzi uvumilivu kwa uwezo wetu wenyewe. ‘Tunategemea nguvu ambazo Mungu hutoa.’ (1 Petro 4:11) Ili kutusaidia tuendelee kuwa imara, Yehova ametupa msaada mzuri zaidi, mfano wa Mwana wake. Acheni tuchunguze mfano mkamilifu ambao Yesu alituwekea kwa kuonyesha uvumilivu.
Mambo Ambayo Yesu Alivumilia
7, 8. Yesu alivumilia nini alipokaribia mwisho wa maisha yake duniani?
7 Alipokaribia mwisho wa maisha yake hapa duniani, Yesu alivumilia ukatili mwingi. Mbali na mikazo mingi ya akili aliyokuwa nayo usiku uliotangulia kifo chake, wazia jinsi alivyokatishwa tamaa na kudharauliwa. Alisalitiwa na mtu aliyeshirikiana naye kwa ukaribu, akaachwa na rafiki zake wa karibu, akashtakiwa kinyume cha sheria, nao washiriki wa mahakama kuu zaidi ya kidini nchini wakamdhihaki, wakamtemea mate, na kumpiga ngumi. Hata hivyo, alivumilia yote hayo kwa utulivu na uhodari.—Mathayo 26:46-49, 56, 59-68.
8 Saa za mwisho za maisha yake, Yesu alivumilia mateso mengi sana ya kimwili. Alipigwa mijeledi akawa na ‘michubuko mikubwa inayotoka damu.’ Alitundikwa mtini, adhabu ambayo ingesababisha “kifo cha polepole chenye maumivu na mateso makali sana.” Fikiria maumivu makali aliyopata wakati mikono na miguu yake ilipokuwa ikipigiliwa misumari mikubwa kwenye mti. (Yohana 19:1, 16-18) Wazia uchungu mwingi aliosikia mti huo uliposimamishwa, mwili wake wote ukiwa umeshikiliwa kwa misumari tu na mgongo wake uliojeruhiwa ukisuguliwa na mti huo. Alivumilia mateso mengi sana ya kimwili huku akiwa na mahangaiko mazito yaliyotajwa mwanzoni mwa sura hii.
9. Kuchukua ‘mti wetu wa mateso’ na kumfuata Yesu kunatia ndani nini?
9 Tukiwa wafuasi wa Kristo, huenda tukalazimika kuvumilia nini? Yesu alisema: ‘Mtu yeyote akitaka kunifuata, na achukue mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote.’ (Mathayo 16:24) Katika andiko hilo, maneno ‘mti wa mateso’ yanawakilisha kuteseka, aibu, au hata kifo. Si rahisi kumfuata Kristo. Kanuni zetu za Kikristo zinatufanya tuwe tofauti. Ulimwengu huu unatuchukia kwa sababu sisi si sehemu yake. (Yohana 15:18-20; 1 Petro 4:4) Hata hivyo, tuko tayari kuchukua mti wetu wa mateso, ndiyo, tuko tayari kuteseka, hata kufa, kuliko kuacha kumfuata Yesu, Kielelezo chetu.—2 Timotheo 3:12.
10-12. (a) Kwa nini kutokamilika kwa watu walioshirikiana na Yesu kulijaribu uvumilivu wake? (b) Ni hali gani zenye kujaribu ambazo Yesu alivumilia?
10 Wakati wa huduma yake, Yesu alikabili majaribu mengine yaliyotokana na kutokamilika kwa watu walioshirikiana naye. Kumbuka kwamba yeye ndiye “stadi wa kazi,” ambaye Yehova alimtumia kuumba dunia na vitu vyote vyenye uhai vilivyomo. (Methali 8:22-31) Kwa hiyo Yesu alijua kusudi la Yehova kwa wanadamu; walipaswa kuiga sifa Zake na kufurahia maisha wakiwa na afya kamilifu. (Mwanzo 1:26-28) Alipokuwa duniani, Yesu aliona matokeo yenye kuhuzunisha ya dhambi akiwa katika hali tofauti. Yeye mwenyewe alikuwa mwanadamu ambaye angeweza kuhisi na kuona mambo kama wanadamu wengine. Alipojionea mwenyewe jinsi wanadamu walivyokuwa mbali na ukamilifu wa Adamu na Hawa, jambo hilo lilimuumiza sana! Hivyo basi, Yesu alikabili jaribu la uvumilivu. Je, alivunjika moyo au kukata tamaa, na kuona kwamba wanadamu wenye dhambi hawana tumaini lolote? Acheni tuone.
11 Kutopendezwa kwa Wayahudi kulimfadhaisha Yesu sana hivi kwamba alilia hadharani. Je, aliruhusu kutopendezwa kwao kumfanye apunguze bidii yake au aache kuhubiri? Hapana! Badala yake aliendelea ‘kufundisha kila siku katika hekalu.’ (Luka 19:41-44, 47) Kutojali kwa Mafarisayo waliokuwa wakichunguza sana waone ikiwa atamponya mtu fulani siku ya Sabato, ‘kulimhuzunisha.’ Je, aliwaogopa watu hao waliokuwa wakimpinga, ambao walijiona kuwa waadilifu? Sivyo hata kidogo! Hakuwa na wasiwasi, bali alimponya mtu huyo, tena katikati ya sinagogi!—Marko 3:1-5.
12 Lazima Yesu alijaribiwa pia na udhaifu wa wanafunzi wake wa karibu. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 3, walionyesha tena na tena tamaa ya kujitakia makuu. (Mathayo 20:20-24; Luka 9:46) Zaidi ya mara moja, Yesu aliwashauri kwamba wanahitaji kuwa wanyenyekevu. (Mathayo 18:1-6; 20:25-28) Hata hivyo iliwachukua muda mrefu kusitawisha sifa hiyo. Wazia kwamba hata usiku wa mwisho aliokuwa pamoja nao, bado walikuwa na “bishano kali” kuhusu ni nani kati yao aliye mkuu zaidi ya wote! (Luka 22:24) Je, Yesu aliona kwamba hawawezi kubadilika, naye akaacha kujaribu kuwasaidia? Hapana. Akiwa mwenye subira kama kawaida yake, aliendelea kuwa na tumaini na maoni yanayofaa, akiendelea kuona sifa nzuri walizokuwa nazo. Alijua kwamba walimpenda Yehova kutoka moyoni na kwa kweli walitaka kufanya mapenzi Yake.—Luka 22:25-27.
Tutaruhusu upinzani upunguze bidii yetu, au tutaendelea kuhubiri kwa bidii?
13. Kama Yesu, huenda tukakabili majaribu gani?
13 Tunaweza kupatwa na majaribu kama yale ambayo Yesu alivumilia. Kwa mfano, tunaweza kupata watu wasiopendezwa au hata watu wanaopinga ujumbe wa Ufalme. Je, tutaruhusu hali hiyo ituvunje moyo, au tutaendelea kuhubiri kwa bidii? (Tito 2:14) Hali ya kutokamilika ya ndugu zetu Wakristo inaweza kujaribu imani yetu. Wanaweza kusema au kutenda bila kufikiri na hivyo kuumiza hisia zetu. (Methali 12:18) Je, tutaacha udhaifu wa waamini wenzetu utufanye tuone kwamba hawafai, au tutaendelea kuvumilia udhaifu wao na kukazia fikira sifa zao nzuri?—Wakolosai 3:13.
Kilichomwezesha Yesu Kuvumilia
14. Ni mambo gani mawili yaliyomsaidia Yesu kusimama imara?
14 Ni nini kilimchomsaidia Yesu kusimama imara na kuendelea kuwa mtimilifu alipovunjiwa heshima, kukatishwa tamaa, na kuteswa? Kuna mambo mawili yaliyomsaidia Yesu. Kwanza, alitazama juu, kwa kuomba msaada wa “Mungu anayetoa uvumilivu.” (Waroma 15:5) Pili, Yesu alitazama mbele, kwa kukazia fikira matokeo ya uvumilivu wake. Acheni tuchunguze mambo hayo.
15, 16. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu hakutegemea nguvu zake mwenyewe ili kuvumilia? (b) Yesu alikuwa na uhakika gani kuhusu Baba yake, na kwa nini?
15 Ingawa Yesu alikuwa Mwana mkamilifu wa Mungu, hakutegemea nguvu zake mwenyewe ili kuvumilia. Badala yake, alimtegemea Baba yake wa mbinguni na kumwomba msaada. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kristo alitoa dua na pia maombi kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa kutoka katika kifo, pamoja na vilio vyenye nguvu na machozi.” (Waebrania 5:7) Ona kwamba mbali na maombi, Yesu “alitoa” dua pia. Neno “dua” linamaanisha ombi la kutoka moyoni linalotolewa kwa bidii, ndiyo, kuomba msaada kwa kusihi. Katika lugha ya awali, neno linalotafsiriwa “dua” liko katika hali ya wingi kuonyesha kwamba Yesu alimsihi Yehova zaidi ya mara moja. Kwa kweli, katika bustani ya Gethsemane, Yesu alisali tena na tena na kwa bidii.—Mathayo 26:36-44.
16 Yesu alikuwa na hakika kabisa kwamba Yehova angejibu dua zake, kwa maana alijua kwamba Baba yake ni “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Kabla ya kuja duniani, Mwana huyo mzaliwa wa kwanza aliona jinsi Baba yake anavyojibu sala za waabudu washikamanifu. Kwa mfano, Mwana huyo alipokuwa mbinguni alijionea mwenyewe Yehova alipomtuma malaika aende kujibu sala ya kutoka moyoni ya nabii Danieli, hata kabla Danieli hajamaliza kusali. (Danieli 9:20, 21) Basi je, kweli Baba huyo angekosa kujibu wakati Mwana wake mzaliwa-pekee alipomimina moyo wake wote kwa “vilio vyenye nguvu na machozi”? Yehova alijibu maombi hayo ya kusihi ya Mwana wake na kumtuma malaika ili ampe nguvu za kuvumilia jaribu hilo.—Luka 22:43.
17. Ili tuvumilie, kwa nini tunapaswa kutazama juu, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?
17 Ili tuvumilie, sisi pia lazima tutazame juu, kwa kuomba msaada wa Mungu ‘anayetupa nguvu.’ (Wafilipi 4:13) Ikiwa Mwana mkamilifu wa Mungu aliona uhitaji wa kuomba dua ili kupata msaada wa Yehova, sisi tunapaswa kufanya hivyo hata zaidi! Kama alivyofanya Yesu, huenda tukahitaji kumsihi Yehova tena na tena. (Mathayo 7:7) Ingawa hatutazamii kutembelewa na malaika, tunaweza kuwa na uhakika kuhusu jambo hili: Mungu wetu mwenye upendo atajibu maombi ya kusihi ya Mkristo mshikamanifu ‘anayedumu katika dua na sala usiku na mchana.’ (1 Timotheo 5:5) Hata tupatwe na majaribu gani, iwe ni ugonjwa, kifo cha mpendwa, au kuteswa na wanaotupinga, Yehova atajibu sala zetu za bidii za kuomba hekima, uhodari, na nguvu za kuvumilia.—2 Wakorintho 4:7-11; Yakobo 1:5.
Yehova atajibu sala zetu za bidii za kuomba msaada wa kuvumilia
18. Ni kwa njia gani Yesu alitazama mbele badala ya kukazia fikira mateso aliyokabili?
18 Jambo la pili lililomsaidia Yesu kuvumilia ni kwamba alitazama mbele, hakukazia fikira mateso aliyokabili bali mambo yaliyokuwa mbele yake. Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake, yeye alivumilia mti wa mateso.” (Waebrania 12:2) Mfano wa Yesu unaonyesha jinsi tumaini, shangwe, na uvumilivu zinavyofanya kazi pamoja. Kwa ufupi, tunaweza kusema kwamba: Tumaini huleta shangwe, nayo shangwe inatuwezesha kuvumilia. (Waroma 15:13; Wakolosai 1:11) Yesu alikuwa na matazamio mazuri. Alijua kwamba uaminifu wake ungesaidia kutetea enzi kuu ya Baba yake na kumwezesha kuwakomboa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo. Pia, Yesu alikuwa na tumaini la kutawala akiwa Mfalme na kuwa Kuhani Mkuu, na hivyo kuwaletea wanadamu watiifu baraka zaidi. (Mathayo 20:28; Waebrania 7:23-26) Kwa kukazia fikira matazamio na tumaini lililokuwa mbele yake, Yesu alipata shangwe isiyo na kifani, nayo shangwe ikamsaidia kuvumilia.
19. Tunapokabili majaribu ya imani, tunaweza kufanya nini ili kuruhusu tumaini, shangwe, na uvumilivu zifanye kazi pamoja kwa faida yetu?
19 Kama Yesu, tunahitaji kuruhusu tumaini, shangwe, na uvumilivu zifanye kazi pamoja kwa faida yetu. Mtume Paulo alisema hivi: “Shangilieni katika tumaini.” Kisha akaongeza: “Vumilieni chini ya dhiki.” (Waroma 12:12) Je, unakabili jaribu kali la imani sasa? Basi, tazama mbele. Usisahau kwamba uvumilivu wako utaletea jina la Yehova sifa. Endelea kukazia fikira tumaini la Ufalme lenye thamani. Jiwazie ukiwa katika ulimwengu mpya wa Mungu huku ukifurahia baraka za Paradiso. Kutazamia mambo mazuri ambayo Yehova ameahidi, kutia ndani kutetewa kwa enzi kuu yake, kuondolewa kwa uovu duniani, na kuondolewa kwa magonjwa na kifo, kutakupa shangwe nyingi sana, na shangwe hiyo inaweza kukusaidia kuvumilia jaribu lolote utakalokabili. Yanapolinganishwa na utimizo wa tumaini la Ufalme, mateso yoyote katika mfumo huu wa mambo ni ‘ya dakika na mepesi.’—2 Wakorintho 4:17.
‘Fuata Hatua Zake kwa Ukaribu’
20, 21. Yehova anatutazamia tufanye nini kuhusiana na uvumilivu, na azimio letu linapaswa kuwa nini?
20 Yesu alijua kwamba haingekuwa rahisi kuwa mfuasi wake, na kwamba uvumilivu ungehitajiwa. (Yohana 15:20) Alikuwa tayari kuweka mfano, akijua kwamba mfano wake ungewatia wengine nguvu. (Yohana 16:33) Ni kweli kwamba Yesu aliweka kielelezo kikamilifu cha uvumilivu, lakini sisi si wakamilifu. Yehova anatazamia tufanye nini? Petro anaeleza: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Yesu alituwekea “kielelezo,” au mfano wa kufuata, tunapokuwa katika majaribu.a Uvumilivu wake chini ya hali tofauti-tofauti unaweza kulinganishwa na “hatua,” au nyayo. Hatuwezi kufuata hatua hizo kikamilifu, lakini tunaweza kuzifuata “kwa ukaribu.”
21 Basi, acheni tuazimie kufuata mfano wa Yesu kwa kadiri tuwezavyo. Na tusisahau kwamba kadiri tunavyofuata hatua za Yesu kwa ukaribu, ndivyo tutakavyoweza kuvumilia “mpaka mwisho,” yaani, mwisho wa mfumo huu wa mambo au mwisho wa maisha yetu ya sasa. Hatujui ni nini kitakachokuja kwanza, lakini tunajua jambo hili: Yehova atatupa thawabu milele na milele kwa uvumilivu wetu.—Mathayo 24:13.
a Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kielelezo,” linamaanisha “kuandika chini ya maandishi.” Mtume Petro ndiye mwandikaji pekee wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo aliyetumia neno hilo ambalo inasemwa kwamba linamaanisha “‘maandishi ya kuiga’ yaliyoandikwa ifaavyo katika kitabu cha kuandikia cha mtoto, ili mtoto afuatishe kwa kadiri awezavyo.”