Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme
Kupata Kusudi Katika Maisha
KATIKA ulimwengu huu uliozorota adili na kupinduka juu-chini watu kadha wanatafuta maana na kusudi la maisha. Wanauliza: ‘Sababu gani tupo hapa? Tulitoka wapi? Wakati ujao una mambo gani?’ Wengi wanamwelekea Mungu wakitafuta majibu naye hawakatishi tumaini. (Mathayo 7:7, 8) Ndivyo alivyoona mwanamke mmoja katika Ugiriki. Anasema:
◻ “Mimi nilikuwa na umri wa miaka 14 nilipoanza kujiuliza-uliza juu ya mwanadamu na kusudi lake maishani. Baada ya kujifunza shuleni elimu ya asili ya mwanadamu na hali za maisha yake kwa ujumla, nilifikiri elimu ya tiba ingejibu maulizo yangu, lakini nikaondoa mawazo hayo iliposhindikana kunieleza asili ya mwanadamu.” Anaendelea kusema: “Nikageuza mawazo kwenye unajimu, na nikajifunza dini za huko Esia, kama vile Uislamu na dini ya Tibet. Nikaanza kufuata fundisho la dini ya Lama maishani mwangu, halafu imani ya kupashana habari na ulimwengu wa roho. Nilipowasiliana na roho, nilihisi nimeupata ukweli. Dini za Uzunguni zilidai kwamba msingi wa imani zao ulikuwa Biblia, lakini kwa kuwa mwalimu wangu wa kidini shuleni hakuweza kujibu maulizo yangu kutokana na Biblia, niliendelea na mazoea yangu ya kupashana habari na roho, kuchunguza miendo ya nyota, na kufanyia watu viini-macho kwa kuwaingiza katika hali ya usingizi wakiwa macho.
Mwaka 1982 mwanamke huyo alikutana na Mashahidi wa Yehova, lakini yeye anasimulia hivi: “Uelezaji wao juu ya Biblia ulikuwa rahisi kupita kiasi ukilinganishwa na yale mafundisho yasiyoeleweka vizuri niliyokuwa nimejifunza. Lakini kitu fulani kikaendelea kunihimiza nijaribu kuichunguza Biblia. Kwa hiyo kwa kuongozwa na ubinafsi nilikubali funzo la Biblia ili niwathibitishie Mashahidi kuwa wanakosea.”
Baada ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova kwa karibu mwaka mmoja, mwanamke huyo anaeleza hivi: “Sasa namshukuru Yehova kwa moyo wangu wote kwa kunisaidia niujue ule ambao hakika ndio ukweli. Hatimaye nimekwisha kuwa huru na makisio yote ya uongo na mawazo ya ushirikina. Ukweli ni rahisi sana tena ni mwepesi kupatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Hatimaye nimeyapata majibu kwa maulizo yangu; sasa najua asili ya mwanadamu na kusudi la maisha.”
◻ Mwanamume Mgiriki mwenye umri wa miaka 27 ambaye hapo kwanza alihusika na ukomunisti alipata pia kusudi katika maisha. Alijifunza uhandisi (uinjinia) katika Ujeremani, kisha akarudi Ugiriki na kujiandikisha jeshini. Yaliyompata yalimsadikisha pole kwa pole kwamba mwanadamu amekwisha kuwa asiyeweza kutatua matatizo yake na kufanya maisha yake yawe afadhali. Kabla ya mwanamume huyo kwenda Ujeremani, jirani Shahidi alikuwa amesema naye juu ya Biblia, na sasa yeye aliyakumbuka maongezi hayo. Kwa hiyo, miezi michache tu kabla ya kupewa ruhusa ya kuacha jeshi, alimwambia afisa wake mkuu hivi: “Sijifikirii tena kuwa askari!” Jamaa yao walidhani alikuwa amerukwa na akili wakamlazimisha akaone madaktari wa magonjwa ya akili. Madaktari walimpa dawa nyingi za namna mbalimbali, zikawa na matokeo mabaya katika mwili na akili yake hata mwishowe akaacha kuzitumia.
Alikutwa na Mashahidi wawili katika huduma ya mlango kwa mlango kisha akaanza kujifunza Biblia pamoja nao. Baada ya kupatanisha maisha yake na matakwa ya Yehova, akawa mtangazaji mwenye bidii wa zile habari njema. Mwaka 1984 alihudhuria Ukumbusho pamoja na watu kumi wa ukoo aliokuwa amewaalika.
Ndiyo, alikuwa amepata kusudi katika maisha, na sasa anataka kumtumikia Yehova akiwa painia wa pekee. Tumaini lake ni kupata uzima wa milele katika Utaratibu Mpya wa Mungu wenye uadilifu.—Isaya 65:17, 18.