Kupata Furaha Katika Zawadi ya Ndoa
“Kitu ambacho Mungu amefungia nira pamoja mtu asikitenganishe.”—MATHAYO 19:6, Biblia ya New World Translation.
1. Ni maneno gani ya Yesu yanayojulikana sana katika Jumuiya ya Wakristo, lakini kuna maulizo gani kuhusiana nayo?
JE! HAYO ni maneno unayojua? Bila shaka yanajulikana sana na mamilioni ya watu katika Jumuiya ya Wakristo, ambao ndio sehemu kubwa ya idadi ya watu wa ulimwengu, kwa maana yalinenwa na Bwana Yesu alipokuwa akisema na Wafarisayo wa kidini wa siku zake. Ingawa huenda ikawa maneno hayo yanajulikana, namna gani maana ya uneni huo wa Yesu? Je! umaana wa mashauri hayo unafuatwa na wanadamu kwa ujumla? Ebu tuone.
2-4. (a) Hali ikoje leo katika nchi nyingi juu ya kuyatii maneno ya Yesu katika Mathayo 19:6? (b) Ni nia gani inayoonyeshwa wazi na wale wanaopuuza mashauri ya Biblia juu ya kudumu kwa noda?
2 Katika nchi nyingi leo, watu hawaheshimu sana mpango wa ndoa wala hawakiendelezi kile ambacho Mungu amekifungia nira pamoja. Talaka zimepanda zikawa kama ugonjwa wa kipuku katika nchi baada ya nchi. Hata katika nchi ambako talaka hairuhusiwi kisheria na serikali mambo si mazuri, kwa maana katika nchi hizo watu mara nyingi wanaacha wenzi wa ndoa na kuanza kuishi na mtu mwingine. Kwa hiyo mashauri yanayofaa ya Yesu katika Mathayo 19:6 hayafuatwi na mamilioni ya watu katika Jumuiya ya Wakristo na kwingineko pia. Je! hiyo ni kwa sababu mashauri hayo aliyotoa Yesu ni mabaya, au ni kwa sababu watu hawasikilizi Yesu anaposema, na hawajali sana mashauri ya Yesu katika jambo hilo?
3 Ushuhuda unaonyesha kwamba asilimia kubwa ya watu hawaioni ndoa kuwa mkataba wa maisha yote ikiwa inavuruga mitindo yao wenyewe ya maisha na tamaa zao. Kwa watu wa namna hiyo, ndoa inaonwa kuwa mpango wa muda tu ikiwa inavuruga shughuli wanazofuatia, mapendezi yao au machukio yao. Kwa hiyo inaelekea kuwa ni kama kwamba watu wengine wanabwaga chini mwenzi wa ndoa sawa na vile lilivyo jambo rahisi kubwaga koti au kofia chini, bila kufikiria hata kidogo mashauri ambayo Yesu aliwapa wale wanaoingia katika uhusiano wa ndoa.
4 Kwa kuwa umeenea sana ule mwelekeo wa kusema kila mtu anafanya hivyo, wale wanaotaka kuyafuata mashauri salama ya Biblia wanaweza kuvutwa waingie katika njia inayowaondoa kwenye fundisho zuri la Neno la Mungu. Mashauri mazuri yanayotolewa kupitia vichapo na kwa mdomo, lakini kutofuata mashauri ya Biblia kunaweza kuwa na matatizo katika ndoa. (Linganisha Zaburi 19:7-11.) Ikiwa tunaufuata mwelekeo wa kwamba tunaweza kuacha mielekezo ya Mungu kuhusu ndoa ili tugeuze jambo lo lote linalovuruga mtindo wa maisha yetu, anasa zetu, tamaa zetu, basi sisi tumo hatarini. Kuwa na mwelekeo wa namna hiyo kunatukutanisha uso kwa uso na moja la matatizo makubwa zaidi ya wanadamu, lile la uchoyo. Kwani kwa ujumla uchoyo ndio chanzo cha matatizo ya ndoa. Kwa sababu gani tunasema hivyo?
Kazi ya Dhambi
5. Mtume Paulo katika Warumi 7:15-20 anaelezaje tatizo tulilo nalo kwa sababu ya kuzaliwa katika dhambi?
5 Wanaume na wanawake, wazao wa Adamu na Hawa, wanazaliwa katika dhambi na hali ya kutokamilika. Maana yake ni kwamba, kwa sababu ya urithi wa dhambi, mwanadamu anaikosa shabaha yake na ni mvunja sheria kwa kadiri moja au nyingine. (1 Yohana 3:4) Mtume Paulo alisema juu ya mzigo mkubwa sana ambao dhambi inawekea wanadamu, kwa maana alijikuta mwenyewe akitenda asilotaka kutenda na akikosa kutenda alilopaswa kutenda. (Warumi 7:15-20) Mtu ye yote anayevunja sheria ya Mungu kwa makusudi ni mchoyo. Huenda kwa watu fulani mmoja mmoja ikawa uchoyo wa kadiri ndogo, lakini kwa wengine inakuwa ndiyo kawaida ya maisha yao, na uchoyo wao unakuwa mkubwa.
6, 7. Ni matatizo gani mawili yanayosababishwa na uchoyo katika ndoa, yakituongoza kwenye ulizo gani lililowazwa vizuri?
6 Katika mpango wa ndoa ulioanzishwa na Mungu, mara nyingi uchoyo ndio chanzo cha tatizo kati ya wenzi wa ndoa. Mwanamke anayetaka kutumikiwa, huku yeye mwenyewe akiwa anakula raha tu, kama vile watu wanavyosema, akitenda kulingana na alivyoendekezwa na mama au baba yake, ni mchoyo hasa. Naye mwanamume anayetaka aendeleze mtindo wa maisha ya useja, ule wa kuwa sikuzote pamoja na “wavulana” baada ya ndoa yake, ni mchoyo hasa. Fikiria njia zote ambazo mume na mke wanakuwa na hali za kutokuelewana, nawe utaona kwamba uchoyo wa mtu mwenyewe ndio chanzo cha matatizo mengi sana.
7 Mtu anapojitahidi kushughulika na matatizo yanayotukia katika ndoa, analishindaje elekeo hilo la uchoyo alilorithi? Kuna mambo kadha yanayoweza kufanywa ambayo yakitumiwa yanaweza kusaidia ndoa inayoyumbayumba. Lakini kila mwenzi katika mpango wa ndoa anapaswa awe na moyo wa kupenda kutimiza fungu lake. Si jambo la kufanywa na mtu mmoja tu. Acheni tuchunguze chache kati ya sababu zinazohusika.
Kutokuwa na Uchoyo Katika Ndoa
8. Ni jinsi gani ndoa ilivyo kugawana vitu?
8 Ndoa ni kugawana vitu, hiyo ikiwa na maana ya kwamba ye yote wa wenzi wa ndoa hawezi kumtendea mwenzake kwa kuwa na maoni ya kwamba mambo yatakuwa sawa mradi mwenzi mmoja anampa mwenzake na huyo mwingine anakuwa wa kupokea tu. Kufanya hivyo hakutamletea baraka ye yote wa hao wawili. Kwa mfano, ni lazima watu wa ukoo wa pande zote mbili wafikiriwe. Jambo hilo halipasi liachwe liwe likitokeza-tokeza matata katika mpango wa ndoa hata mtu awe akifikiria wazazi wake mwenyewe au watu wa ukoo wake bila kuwafikiria wale wa mwenzi wake. Maamuzi yanayohusu mahali ambapo jamaa itaenda kutembelea au katika vipindi vya kujistarehesha hayapasi sikuzote yawe yakifanywa na upande mmoja tu. Ndoa itakuwa na mafanikio ikiwa yule mwingine atafikiriwa. Usiwe kamwe ukimtendea mwenzako hivi hivi tu bali onyesha kwamba huna uchoyo.—Wafilipi 2:4.
Umri
9. Maoni ya kupuuza umaana wa ndoa yanaleta matokeo gani ya kusikitisha?
9 Kwa sababu ya maoni yaliyopo sana kati ya watu wengi wa kizazi hiki kwamba ikiwa ndoa haiwi na matokeo mazuri inaweza kukomeshwa kwa talaka, vijana wengi wanaianza wakiwa na maoni hayo ya kuupuuza mpango wa ndoa. Jambo hilo linaweza kuongoza na linaongoza kwenye mivunjiko ya ndoa nyingi za wasiofika umri wa miaka 20 na zaidi. Pia linafanya wazaliwe ulimwenguni watoto wengi wasiotakwa. Mara nyingi watoto hao wanakua bila kujua kamwe maana ya kuwa na mama na baba wanaowapenda na kuwajali sana.
10. Ni kwa njia zipi andiko la Wagalatia 5:22, 23 linavyoweza kusaidia wale wanaofikiria ndoa?
10 Mtu anapaswa kuwa wa umri gani kabla ya kufikiria ndoa? Haungekuwa mwendo wa hekima kufanya sheria juu ya jambo hili. Hata hivyo Maandiko yanatoa mashauri mazuri juu ya mambo yanayoonyesha ukomavu wa kiakili na wa kiroho—aina ya ukomavu unaohitajiwa na wale wanaoingia katika maisha ya ndoa. Tafadhali soma Wagalatia 5:22, 23, ambamo utaona orodha ya matunda ya roho. Chunguza kwa uangalifu kila moja la matunda yaliyotajwa humo. Hizo ndizo sifa ambazo mtu anahitaji kusitawisha maishani. Mtu hapaswi kuanza kuzionyesha baada ya ndoa, bali azionyeshe kila siku muda mrefu kabla ya hapo katika maisha yake ya kuwa Mkristo.
11. Wale wanaofikiria kufunga ndoa wanaweza kujichunguzaje?
11 Kwa mfano, je, wewe ni mtu mwenye kujawa na shangwe maishani, mwenye furaha kwa sababu uko hai, mwenye kutumikia faida za Ufalme wa Kristo? Je! wewe unakaa kwa amani pamoja na wengine, ukiendeleza uhusiano wenye amani pamoja nao? Au wewe ni mtu mwenye kutaka ugomvi, mtu wa vishindo vya hasira-hasira na matusi? Je! wewe ni mstahimilivu, mtu anayeweza kuchukuliana na udhaifu mbalimbali wa ndungu au dada yake, mama au baba yake? Au wewe ni mtu wa kuhamaki upesi na kukasirika-kasirika ikiwa wengine hawakubaliani upesi na yale unayotaka? Je! unaona kwamba unawafadhili wengine unaposhughulika nao, ukiwa mwanana na kuwatendea mema? Au wewe ni mchoyo, mwenye ubinafsi, mtu mwenye kukosa kujiweza, mwenye haraka ya kurukia wengine unapotendwa kijambo kidogo kinachokuudhi? Je! una upendo wa kweli kwa wengine, kutaka kuwasaidia, ukihiari ufanye hivyo, kujitoa wewe mwenyewe hata mali na nguvu zako ili uwafurahishe wengine? Au unataka wengine ndio wakuonyeshe wewe upendo, sikuzote wawe ndio wanaokupa wewe mali na nguvu zao?
12. Mwanamume au mwanamke ambaye amejionea mengi kwa sababu ya kuishi miaka mingi kabla ndoa anakuwaje afadhali?
12 Ni jambo sahihi kusema kwamba hakuna wo wote kati yetu walio na sifa hizo kwa ukamilifu. Lakini, mwanamume au mwanamke ambaye amejionea mengi kwa sababu ya miaka kadha ya maisha, na ambaye amekuwa na nafasi ya kusitawisha sifa hizo za kiroho, yumo katika msimamo mzuri wa kufanikisha ndoa—msimamo ambao ni afadhali kuliko wa mtu ambaye ndiyo sasa tu anaanza kujaribu kuyaweza matunda hayo ya roho akiisha kufunga ndoa.—Linganisha 2 Petro 1:5-8.
13, 14. (a) Kupita kwa wakati kunaandaa nini kwa habari ya kusitawisha maoni ya kiroho? (b) Wazazi wanaweza kufanya nini wasaidie watoto wao?
13 Sababu gani usijichunguze mwenyewe kwa unyofu, na pia mapendezi na machukio yako? Je! huoni kwamba njia yako ya kuthamini maisha imekuwa bora kwa sababu ya wakati kupita? Je! ulipokuwa na umri wa miaka 13 uliyachukua mambo jinsi ulivyoyachukua ulipokuwa na miaka 5, au je, ulipokuwa na miaka 20 uliyachukua kama ulivyoyachukua ukiwa na miaka 13? Je! Ufahamu na uthamini wako kuhusu maisha umeongeze au umepungua muda wa miaka iliyopita ulipoendelea kupata ujuzi mkubwa zaidi? Wakati huu ambao wewe ni mtu mzima, je, unatazamia watu wawe na sifa zile zile ulizotaka kuona ndani yao ulipokuwa mtoto? Je! si kweli kwamba msichana anapokuwa mwanamke mzima anatia umaana mkubwa zaidi kwa tabia na utu wa kumwogopa Mungu wa mwanamume kisha anamsahau kabisa yule aliyeona kuwa ndiye mvulana “pekee na hakuna mwingine” alipokuwa na umri wa miaka 16 au 17? Inaelekea kuwa afikapo umri wa miaka 22 au 23 maoni yake yatategemea zaidi tabia za mwanamume za kiroho, za kiakili, na za kimoyoni kuliko maumbo ya kimwili. Ndivyo inavyoweza kusemwa juu ya kivulana anayekua akawe mwanamume mzima. Matumaini na tamaa zake kuhusu mke anayetaka zinakomaa anapoendelea kuwa mtu mzima. Katika miaka yake ya baadaye, njia yake ya kuona mambo inapobadilika, atatafuta mwenzi wa ndoa mwenye ufahamu na fadhili, anayeweza kuwa mtunza nyumba na mama, ambaye moyoni ana tamaa imara ya kumfurahisha Muumba wake, Yehova, na kufanya mapenzi Yake.—Mithali 31:10, 26, 27.
14 Linalosemwa ni kwamba kupita kwa wakati kunabadili maoni ya mtu juu ya ubora wa mambo. Basi, kufanya haraka haraka ya kuingia katika ndoa katika umri mdogo kuna hatari nyingi. Huenda isiwezekane kuwasadikisha watu wawili walio na umri mdogo sana wangoje kidogo kabla ya kufunga ndoa. Lakini wazazi wanaweza kuwatia moyo watoto wao, hasa katika miaka ile ya mwanzo-mwanzo wa maisha zao, wafikiri kwa uzito juu ya maisha, juu ya kujitayarishia ndoa katika hali ya kiroho, ya kimoyoni, na ya kiakili kabla ya kuingia pamoja na mtu katika mkataba wa maisha yote utakaofanya waone mema au waone mabaya.
15. Kwa kuwa si sikuzote ndoa ya watu wenye umri mkubwa inapokuwa jawabu kwa matatizo yote, ni shauri gani limetolewa juu ya kuendeleza maoni yanayofaa?
15 Wala hiyo si kusema kwamba kufunga ndoa ukiwa na umri mkubwa zaidi ndilo jawabu kamili. Hata wakati huo yanaweza kuwako matatizo, hasa ikiwa nia ya uchoyo inaruhusiwa ijipenyeze na kuingiza mwanya kati ya watu wawili. Ni lazima mahitaji ya kiakili, kimoyoni, na kiroho ya kila mtu aliye katika kifungo cha ndoa yafikiriwe. Wakristo wengine wamejiruhusu wahusike sana katika kazi ya kimwili, wakaachilia utendaji wa kundi, kutia na kuhudhuria mikutano na kushiriki katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Halafu, wanajaribu kulijaza pengo wanalojisikia wakiwa nalo maishani kwa kujiingiza katika tafrija nyingi. Wanaelekea kufikiri kwamba mradi wanajishughulisha na mambo fulani, kwa sasa matatizo yao yatatatuliwa kidogo, halafu katika Utaratibu Mpya wa mambo ndipo kila mmoja wao ataanza kuangalia aone mwenzake ana mahitaji gani ya kimoyoni, ya kiakili, na ya kiroho. Lakini mambo hayaendi hivyo maishani. Paulo alitoa shauri kwamba mwanamume atunze mke wake kama anavyoutunza mwili wake mwenyewe. (Waefeso 5:28) Maana yake ni kuelekeza fikira sasa kwenye mahitaji ya mwenzi wake wa ndoa, sawa na vile anavyoelekeza fikira kwenye mahitaji yake mwenyewe. Ndivyo inavyoweza kusemwa juu ya mwanamke pia.
Maoni Yaliyosawazika Kuhusu Maisha ya Ndoa
16-18. (a) Kwa sababu gani maoni yaliyosawazika juu ya maisha na ndoa yanahitajiwa kabisa, na ni hadhari gani tunazopewa kuhusiana na matakwa yetu na mahitaji ya wengine? (b) Kwa sababu gani ni vizuri kuwaza sana juu ya mambo hayo kabla ya ndoa?
16 Maoni yaliyosawazika kuhusu maisha yatasaidia kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu ndoa. Mtu mwenye usawaziko atatambua kwamba kwa sababu ya maelekeo ya kichoyo aliyorithi ni lazima ajitahidi nyakati zote kushinda mawaa hayo. Ni rahisi sana kutofikiria kamwe kutanguliza mahitaji ya wengine mbele ya matakwa ya mtu binafsi. Kitoto kinataka vidude vyote vya kuchezea viwe mali yacho, na kwa ujumla kinakataa kuvishiriki pamoja na wengine kisipozoezwa vizuri na wazazi. Katika miaka ya baadaye, uchoyo wa kitoto hicho utapanuka uingie katika mambo mengine. Hivyo mara nyingi tunakuta vijana wadogo na wakubwa wakitaka mambo yafanywe kivyao tu, na wanapojitahidi kutosheleza matakwa yao hawajali kama wengine wataumia au wataabike. Katika miaka ya baadaye ya utu mzima, watu wa namna hiyo wanatamani sikuzote yale ambayo wao wanapenda, wasijali hata chembe moja juu ya mahitaji ya wengine.
17 Mtu mwenye usawaziko hatajinyima mambo yote kabisa, lakini atasimamia maisha yake mwenyewe kwa njia itakayomwezesha awafikirie wengine pia. Atauliza anaweza kufanya nini awasaidie wengine,ajitoe yeye mwenyewe na mali zake kufaidi wengine.Hatasisitiza sikuzote mambo yafanywe kivyake tu,hivi kwamba yeye akisema jambo ni basi. Mithali inasema: “Nafsi ya mwenye ukarimu itanenepa, naye anayenyweshwa, atanyweshwa mwenyewe.”—Mithali 11:25, ZSB.
18 Kufuata mwendo wa namna hiyo katika maisha ya useja kutamfaidi sana mtu katika maisha ya ndoa. Atamfikiria sikuzote mwenzi wake wa ndoa katika maamuzi yo yote anayofanya. Badala ya kuwaza kwamba ndoa ni kitu cha kujaribia au mpango wa muda tu, mtu wa namna hiyo ataiona ndoa kuwa mpango uliokusudiwa na Yehova Mungu uwe wa kudumu alipowaunganisha watu wawili wa kwanza katika Edeni. (Mwanzo 2:22-24) Wakati wote, jitihada zitafanywa za kuendeleza ndoa ibaki ikiwa imeungana, za kumsaidia mwenzi wa ndoa, huku wote wawili wakiongeza uthamini wao kwa Mungu na kwa mmoja na mwenzake.
Kwa Muhtasari
19-21. (a) Tunaweza kuhakikishaje kwamba hatutaiona ndoa kuwa mpango wa kujaribia tu? (b) Ni mambo gani yanayopasa kuzingatiwa na watu wote, wenye umri mdogo na mkubwa pia, wanaotafuta furaha ya kweli katika ndoa?
19 “Kitu ambacho Mungu amefungia nira pamoja mtu asikitenganishe.” Ndiyo, shauri hilo la Yesu limejawa na maana kwa Mkristo wa kweli. Ndoa si mpango wa kujaribia tu unaoweza kuachwa mtu akiona mambo yamekuwa magumu. Ni lazima tupigane daima na mwili usiokamilika kuchunga elekeo la kibinadamu la kufanya uchoyo, na hivyo tupate ukubali wa Mungu. (Linganisha Warumi 7:21-25.) Ili kuufanikisha mkataba wa ndoa, ni lazima wenzi wote wawili wajifunze kupa na kupewa, kuandalia na kuandaliwa, na mmoja wao asimtendee mwenzake kamwe kwa njia ya hivi hivi.—Waefeso 5:21-23, 28, 33.
20 Na ingawa hakuna umri uliowekwa unaoweza kusisitizwa kama sheria ili mtu aufikie kwanza anapotaka kufunga ndoa, isipokuwa ule uliowekwa na serikali kuwa umri halali, kila mmoja anaweza kuzingatia uhitaji wa kukua kiroho kupatana na Wagalatia 5:22, 23, ili awe mwenzi wa ndoa anayestahili sana. Kwa kweli kupita kwa wakati kunageuza maoni ya mtu. Kwa hiyo, mtu ye yote asifanye haraka haraka ya kufunga ndoa. Kwanza, kila mmoja na asitawishe utu wa Kikristo ili awe amejitayarishia vizuri nira ya ndoa. Tena usisahau kamwe kwamba, hakuna mtu anayepaswa kukitenganisha kitu ambacho Mungu ameunganisha pamoja.—Mathayo 19:4-6.
21 Mtu akiwa na maoni yaliyosawazika juu ya maisha halafu juu ya ndoa, anaweza kupata shangwe na furaha ya kweli katika mpango ulioagizwa rasmi na Yehova Mungu mwenyewe kwa ajili ya mwanamume na mwanamke, kama ilivyoonyeshwa na ndoa ya kwanza katika Edeni. (Mithali 5:18) Lakini kila mmoja anaweza kufanya mambo gani zaidi ajithibitishe kuwa mwanamume au mwanamke aliyejitayarisha kuchukua jukumu la mume au mke? Tafadhali soma habari inayofuata juu ya utu wa mwanamume na mwanamke Mkristo.
Kwa kurudia, wewe ungejibuje yanayofuata?
◻ Ni mielekeo gani kuhusu ndoa inayopasa kuepukwa?
◻ Wenzi wa ndoa wanaweza kushughulikaje na maelekeo waliyorithi ya kutenda dhambi?
◻ Kwa sababu gani Wakristo wenye tabia za ujana hawapaswi kufanya haraka haraka ya kufunga ndoa?
◻ Ni maoni gani yaliyosawazika kuhusu maisha ya ndoa yanayopendekezwa?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kujichunguza kwa unyofu kunaweza kuonyesha wazi makosa yanayotupasa kuondoa