Uzuri wa Utu wa Kikristo
“Mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.”—WAEFES0 4:24.
1. Ni uzuri gani tunaotamani kueleza hapa?
KUNA usemi wa kwamba ‘uzuri wa kitu unategemea macho ya mwonaji.’ Maana yake ni kwamba uzuri (urembo) unakadirika tofauti tofauti. Uzuri wa mwanamume au mwanamke Mkristo ni nini? Hilo ndilo tunalotaka kuzungumza sasa.
Kufafanua Uzuri Katika Mwanamume Mkristo
2. Kwa sababu gani sifa za kimwili zikiwa peke yazo zinashindwa kufanya mwanamume awe mtu wa Mungu?
2 Na tuanze kwa kufikiria sifa zinazompa mwanamume Mkristo sura ya kupendeza inayofanya wengine wafurahie kuwa pamoja naye. Sifa za kimwili sizo peke yazo zinazofanya mmoja awe “mtu wa Mungu.” (1 Timotheo 6:11) Sura ya nje ya mwanamume, hata kama ni ya kuvutia namna gani, haina ubora ikiwa yeye ni kichwa-maji katika kuwaza kwake. Ikiwa ni mwenye kiburi, fidhuli, mkosa-adabu, na mpumbavu, havutii watu—anawasukumia mbali. Adabu zake zikimwonyesha kuwa mtu asiyethamini anayotendewa, hakika anaweza kuwa kikwazo kwa wengine. Ikiwa anajali mambo yake mwenyewe tu na jinsi sura yake ilivyo au vile anavyotazamisha wengine, hatakuwa aina ya mtu ambaye wengine watataka kushirikiana naye.
3, 4. (a) Ni nini baadhi ya sifa za mwanamume aliye mtu wa Mungu kama zilivyoonyeshwa na mfano uliowekwa na Yesu Kristo? (b) Wewe ungeelezaje baadhi ya tabia za mwanamume aliye mtu wa Mungu?
3 Bali, mwanamume aliye mtu wa Mungu atakuwa amesitawisha sifa za haki, rehema, upendo, na fadhili. Yesu Kristo hakujulikana kwa sababu ya mwili wake mkamilifu bali kwa sababu alikuwa mshikamanifu kwa kanuni na ukweli. Njia yake ya kufundisha ilimtambulisha kuwa mtu aliyenena kwa mamlaka iliyotoka kwa Mungu. (Mathayo 7:28, 29; Yohana 7:46) Mwanamume aliye mtu wa Mungu hatachafuliwa na tamaa ya kutaka mamlaka au umashuhuri. Yeye hawezi kujiuza ili tu apate faida zinazopatikana kwa kuwa na cheo fulani. Ni mwanamume mwenye nguvu za kusimamia hiari yake. Anapenda unyenyekevu na hatasema uwongo. Anaonyesha woga unaofaa kuelekea Yehova. (Mithali 22:4) Hizo ni baadhi ya sifa zinazopatikana katika mwanamume aliye mtu wa Mungu.
4 Mwanamume aliye mtu wa Mungu ana dhamiri, moyo mwema, na kusudio linalofaa. (1 Timotheo 1:5; Mithali 4:23) Hatafanya mambo yanayochafua dhamiri yake, akipuuza kanuni za uadilifu. Kwa sababu ya kuwa na moyo mwema na kusudio linalofaa, yeye hatatumia mbinu za kichinichini anaposhughulika na wengine. (Waebrania 13:18) Hataruhusu mwenendo na vitendo vibaya vibomoe makusudio yake mema. (Hosea 4:11) Anajitia nidhamu daima ili azuie moyo wake usiwe na hila. Kwa maneno na matendo anaonekana wazi kuwa mwanamume mwenye kufuata kanuni.—Zaburi 15:1, 2.
5. Huruma ina sehemu gani katika maisha ya mwanamume aliye mtu wa Mungu?
5 Mwanamume aliye mtu wa Mungu anaonyesha wengine huruma, ni mwenye kusamehe na mfadhili. Mwanamume mwenye huruma ni mwanamume mwenye kusikitikia. Anaweza kujitia katika shida za wengine na kufahamu hali yao wanapokuwa na mambo yanayowatatiza na yenye kuwahangaisha. Zaidi ya hilo, anaweza kusamehe anapokosewa na mtu fulani. Anaweza kuishinda ile tamaa ya silika ya kutaka kulipa dhara kwa dhara na tusi kwa tusi. Kwa kweli maneno ya 1 Petro 3:8, 9 yanamfaa mwanamume huyo. Kwa kumpa mtu baraka wala si laana anajionyesha kuwa mfadhili, tena mwenye kuzuia tamaa zile nyonge za mwanamume dhaifu asiye na uwezo wa kuhurumia, kusamehe, na kufadhili wengine.—Waefeso 4:31, 32.
6. (a) Ni sifa gani nyingine za kutokeza alizo nazo mwanamume aliye mtu wa Mungu, nazo zinamaanisha nini? (b) Mke na watoto wa mwanamume wa namna hiyo watakuwa na maoni gani juu yake?
6 Sifa nyingine za kutokeza zinazoonyesha mwanamume aliye mtu wa Mungu ni kwamba yeye ni mkarimu. Na ikiwa ameoa, ni mume kweli kweli na baba mnyofu. Katika cheo chake cha kuwa mtu aliyeoa, mwanamume aliye mtu wa Mungu ana nafasi kubwa sana ya kutolea mkeye na watoto wake uvutano na kiolezo cha kutenda mema. (Wakolosai 3:19, 21) Katika lile jambo la kuwa mkarimu, mwanamume wa namna hiyo anafuata shauri zuri la Bwana Yesu Kristo, aliyesema: “Wapeni watu vitu [“zoeeni kutoa,”NW] nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa,na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.” (Luka 6:38) Katika uhusiano wake wa kijamaa, mwanamume wa namna hiyo atawatunza kweli kweli wale walio wa nyumba yake. Lakini pia atalifuata onyo zuri la upole lililo katika Waefeso 4:28, kutenda ‘kazi iliyo nzuri apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji.’ Akiwa mume wa kweli, mwanamume aliye mtu wa Mungu ataendeleza uaminifu katika mpango wa ndoa. Mke wake ataweza kuwa na utumainifu na uhakika kamili juu yake kwamba kweli yeye ni mwanamume aliye kitu kimoja naye katika kifungo cha ndoa. (Mithali 5:18, 19) Tena, ikiwa wana watoto, atajionyesha kuwa baba mnyofu, si mpunjaji au mdanganyifu katika shughuli zake na wengine. Hivyo, atakaza kikiki kanuni za unyofu katika watoto wake. (Mithali 4:1-5) Mwanamume wa namna hiyo ni mfano mwema kama nini katika akili changa za watoto wake! Wataweza kumtegemea kuwa mwanamume mshikamanifu, mshika-ukamilifu.—Mithali 11:3, 4.
7. Mwanamume aliye mtu wa Mungu atakuwa na maoni gani yaliyosawazika juu ya kutokuwa na madeni?
7 Katika jambo hilo, pia, mwanamume aliye mtu wa Mungu atachunga ili yeye na jamaa yake wasijiletee madeni yenye kuwalemea, akijua kwamba yanaweza kutokeza matatizo makubwa. Bila shaka, inamaanisha kwamba hatajiruhusu yeye mwenyewe na jamaa yake waishi maisha ya juu na kumbe mapato yao ni ya chini. Yeye ni mtu atakayehesabu gharama kabla ya kuanza jambo fulani. (Luka 14:28-30) Anaweza kujinyima wakati wa sasa kwa ajili ya wakati ujao na, kwa usemi wa mfano, anaweza kuacha vinavyoonekana kwa ajili ya visivyoonekana. (Linganisha Waebrania 11:8-10.) Kuishi kwa njia hiyo kutamsaidia mwanamume aliye mtu wa Mungu aendeleze uaminifu wa Kikristo katika maisha yake ya kila siku.
8. Mwanamume wa namna hiyo atakabilije hali zisizopendeza maishani mwake?
8 Katika maisha za wanadamu wote, nyakati nyingine kuna uhitaji wa kukubali kukabili hali ambazo hazipendezi kwa sababu ya dhambi na kutokukamilika. Lakini mwanamume aliye mtu wa Mungu atakuwa shujaa na mwenye kufuata kanuni katika hali za namna hiyo, kulingana na kiolezo kilichowekwa na Yesu. (Yohana 16:33) Kwa nguvu za Mungu wake, Yehova, atayakabili mambo yenye kutatiza sana kwa ushujaa, akimtegemea Yehova kwa msaada na uongozi Wake—Mithali 18:10.
9. Wewe ungeelezaje juu ya maisha ya kiadili ya mwanamume anayetafuta kumpendeza Yehova?
9 Mwanamume wa kweli aliye mtu wa Mungu ndiye bwana-mkubwa wa mwili wake. Ndiyo kusema, yeye ndiye anayesimamia tamaa na nyege zake, akijua kwamba mwili unapokuwa mtumishi kunakuwa na mafaa, lakini ukiwa ndio bwana-mkubwa matokeo yanakuwa mabaya sana. Yeye anayakumbuka wakati wote maneno ya mtume Paulo: “Mimi naupiga-piga ngumi mwili wangu na kuufanya kama mtumwa.” (1 Wakorintho 9:27, NW) Basi, anatafuta sikuzote kusitawisha tunda lile la “roho . . . kujiweza,” akiepuka mambo ambayo yangemchafua. (Wagalatia 5:22, 23, NW) Yeye ni mwenye hekima kwa kujua kwamba kujiachilia afuate mawazo ya uasherati kunaweza kumwongoza kwenye mwenendo usio wa adili. Tena, tegemeo lake ni juu ya Mungu wake, Yehova na nguvu ambazo Yeye anatoa.—Wafilipi 4:13.
10, 11. (a) Ni sifa gani yenye kuleta upatano inayoonyeshwa na mwanamume aliye mtu wa Mungu anapofanya makosa katika uamuzi? (b) Ni kiolezo gani kitakachofuatwa na vichwa vya jamaa kwa habari ya funzo la jamaa?
10 Na mwisho, mwanamume aliye mtu wa Mungu anaweza kukubali makosa yake, kuwapa watu pole anapokosa, kuonyesha mwenzi wake wa ndoa na wengine sikitiko ikiwa amewaudhi au kuwakasirisha kwa njia fulani kwa sababu ya hali zake za kutokamilika. Anaweza kumwendea Yehova kisha kwa moyo safi amwombe msamaha wa dhambi zake kwa sababu yeye amekwisha kuomba mke wake, mwanadamu mwenzake, watoto wake, wamsamehe. Hakika kuweza kusema “Pole, mimi nilikosa” ni alama ya kuonyesha mtu aliye mwanamume kweli kweli, hasa mwanamume aliye mtu wa Mungu.—Mathayo 18:21, 22; Marko 11:25.
11 Je! wewe hungesema kwamba mwanamume aliyeoa aliye baba wa namna hiyo angepata msaada wa Yehova? (Zaburi 54:4) Hakika angekuwa amejiandaa kushughulika na matatizo ambayo ulimwengu huu wa kisasa unaleta juu yetu sote kwa sababu ya mbinu za Shetani na kusudi alilo nalo la kuvunjavunja kila lililo jema, kutia na ndoa na muungo wa jamaa yenye furaha. Mwanamume huyo angeangalia vizuri hali ya kiroho ya washiriki wa jamaa, kuwaongoza katika funzo la ukawaida la Neno la Mungu na katika sala, kwa kufuata kiolezo cha watumishi waaminifu wa Mungu katika nyakati za Biblia.—Kumbukumbu la Torati 11:18-21; Mithali 7:1-3.
12. Ni jukumu gani la maana ambalo sasa tutafikiria?
12 Lakini kuna zaidi ya kufikiriwa. Pia kuna jukumu la mke la kushughulika na matatizo katika jamaa. Sasa na tuweke fikira zetu kwenye sifa zile ambazo yeye atataka kusitawisha maishani mwake.—Mithali 19:14.
Kufafanua Uzuri Katika Mwanamke Mkristo
13, 14. Mwanamke anaweza kuchukua hatua zipi apate upendeleo wa Yehova na ikiwa ameolewa, wa jamaa yake, naye mtume Petro alitolea jamia ya wanawake shauri gani kwenye 1 Petro 3:1-5?
13 Kitabu cha Mithali kinatuambia jambo fulani juu ya mwanamke aliye mtu wa Mungu: “Madaha huenda yakawa ya uwongo, na uzuri wa umbo huenda ukawa ni ubatili; lakini mwanamke anayeogopa Yehova atajipatia sifa.” (Mithali 31:30, NW) Basi je, mwanamke anapata jinsi gani sifa hizo zinazomfanya apendwe sana na mumeye na watoto au na wengine ikiwa yeye ni mseja, na kumfanya awe mtu ambaye wengine wanaweza kufurahia kumkaribia? Kwanza, mwanamke aliye mtu wa Mungu ni mwenye moyo uliofunguka, maana yake mtu mkarimu, anayetamani kusaidia wengine kwa njia zo zote anazoweza, kimwili au kiroho. Kunapokuwa na watu wenye uhitaji, anakuwa kati ya walio wa kwanza kutaka kusaidia, akipendezwa kikweli na mahitaji ya wengine lakini, bila shaka, akisawazisha upendezi huo na utunzaji na uangalizi anaopaswa kuipa jamaa yake mwenyewe, ikiwa ameolewa.—Tito 2:3-5.
14 Zaidi ya hilo, mwanamke wa namna hiyo ana akili ya unyenyekevu wala si ya kiburi, ni mwenye fadhili wala si mwenye kisirani, vitu vyake vinakuwa nadhifu si shaghala-baghala, ni mwenye hisani wala si mtaka vita. Na ikiwa ameolewa anajitahidi kufuata shauri analotoa mtume kwenye 1 Petro 3:1-5.
15. (a) Mwanamke aliye mtu wa Mungu anapaswa kuwa na mradi gani, na anaweza kuufikiaje? (b) Anamuungaje mkono mume wake? (c) Kwa sababu gani anaendelea kupendwa katika jamaa?
15 Tena, mwanamke aliye mtu wa Mungu si mwenye hekima ya kilimwengu, bali anajitahidi kusitawisha hali ya kiroho. Yeye ni msomaji wa Biblia mwenye bidii na anapendezwa kutumia kanuni zayo maishani mwake. (Zaburi 119:66) Huo si upendezi wa kujifikiria binafsi tu, kutaka yeye mwenyewe tu awe na maarifa, bali anafikiria kugawia wengine mambo mema anayojifunza, katika huduma ya Kikristo na pia anapoonana kila siku na majirani, watu wa ukoo, na marafiki. Mume Mkristo anafurahia mke ambaye anaweza kuongea naye mambo ya kiroho, akiwa kikamilisho chake, mtu anayethamini pia mambo ya kiroho na kutaka kushiriki naye katika kumjua Yehova vizuri zaidi. (Mithali 9:9, 10) Kwa hiyo mwanamke aliye mtu wa Mungu ni mwenye utambuzi na ufahamu. Ikiwa ameolewa anajua jukumu lake la kuwa kikamilisho cha mume wake. Anamuunga mkono mume wake katika kuwapa watoto mafundisho ya kiroho, hasa mume asipokuwapo nyumbani. (Linganisha 2 Timotheo 1:2, 5; 2 Yohana 1, 2.) Ataendelea kupenda na kupendwa katika jamaa muda mrefu hata ikiwa uzuri wa ujana wake utakuwa umefifia. Mume wake anaweza kumtegemea kwa maoni mema na ya haki, mawazo timamu na kitia-moyo chenye unyofu, kwa sababu ni mwanamke mwenye urafiki, mwenye kutumia akili. (Mithali 25:11) Abigaili alipotenda kwa utambuzi na wepesi wa kuchukua hatua, hapo ndipo Daudi aliposema: “Akili yako ibarikiwe.”—1 Samweli 25:32, 33, ZSB.
16. Ni maneno na vitendo vya aina gani vinavyotambulisha mwanamke aliye mtu wa Mungu?
16 Kiasi anachoonyesha mke ili kutokeza mema anapounga mkono mume wake hakitakuwa na maneno yanayochoma, yenye kutia au uchungu au ya dharau. Mtu anapata upendeleo wa mwingine kwa kumpa matazamo yenye neema, maneno yenye kusemwa ifaavyo, vitendo vyororo vya upendo, bidii ya kazi, kwa fadhili zenye uanana na kwa ufahamu wa kindani. (Linganisha Mithali 25:11; 31:10-28; 1 Wathesalonike 2:7.) Upole, imani, kiasi, hayo ndiyo mambo yanayofanya mwanamke aliye mtu wa Mungu apendwe sana daima.—Zaburi 37:11; Waebrania 11:11, 31, 35; Mithali 11:2.
17. Sifa ya upendo ina ubora gani kwa mwanamke aliye mtu wa Mungu?
17 Sifa nyingine ya kutokeza ya mwanamke aliye mtu wa Mungu ni uwezo wa kuonyesha hisani na shauku ya upendo. (Warumi 12:10) Pambo lake lililo maridadi zaidi ni upendo, ambao utamzuia kuwa asiyesikilizana na watu katika mambo madogo-madogo. Upendo huo unasimuliwa vizuri kama nini katika 1 Wakorintho 13:4-7. Kulingana na The New English Bible andiko hilo linasomwa hivi: “Upendo ni wenye subira: upendo ni wenye fadhili na hauonei mtu ye yote kijicho. Upendo si wenye kujisifu kamwe, wala hauna majivuno, wala hauna ufidhuli; si wenye uchoyo kamwe, si wenye haraka kuudhika. Upendo hauweki hesabu yo yote ya makosa uliyotendwa; hausimangi dhambi za watu wale wengine, bali unapendezwa na ukweli. Hakuna jambo ambalo upendo hauwezi kukabili; hakuna mpaka wa imani yao, tumaini lao, na uvumilivu wao.”
Sisi Ni Nini?
18. Kila mmoja wetu anakabili maulizo gani binafsi, na kujichunguza wenyewe kutakuwa na matokeo gani?
18 Sasa ulizo kubwa ni hili: Je! sisi tunaweza kutambuliwa kuwa mtu aliye Mkristo, tuwe tumefunga ndoa au tu waseja? Je! kuna pande ambazo tunaweza kuona uhitaji wa kufanya marekebisho zaidi tunapotafuta kumpendeza Yehova na mwanadamu mwenzetu? Inaelekea sana kwamba, kujichunguza wenyewe kutafunua pande ambazo tunaweza kufanyia maendeleo, lakini itakuwa furaha kama nini wakati sisi tuonapo maendeleo hayo ndani yetu wenyewe na, zaidi ya hilo, wakati wengine waonapo na kusema tumefanya mabadiliko kwa sababu ya kufuata kwa ukaribu Neno la Mungu na mafundisho yalo!—2 Wakorintho 13:5; 1 Timotheo 4:15, 16.
19. Tunapaswa kutatuaje matatizo tunayokabili tunapofuatia maisha yenye amani, ya kumcha Mungu?
19 Katika kufuatia maisha ya useja, kila mtu anaweza kujitahidi asitawishe sifa hizo. (1 Wakorintho 7:32) Halafu ikifika siku ambayo mtu anaamua kufunga ndoa, hakika sifa hizo zitamfaa sana yule ambaye amezisitawisha. Kati ya wale waliofunga ndoa, kuendelea kusitawisha mema ya Kikristo kutatokeza furaha na shangwe kubwa. (Wafilipi 4:8, 9) Kutatua matatizo kunahitaji wenzi wote wawili katika mpango wa ndoa wafanye jitihada. Nia ya mtu kukubali kwamba ana tabia zisizofaa kisha kuzibadili inaweza kumsaidia sana avae utu wa Kikristo unaopendeza. (Wakolosai 3:8-10) Kumbuka, pia, alama inayoonyesha mtu ni mwanamume au mwanamke Mkristo ni ule uwezo wa kusema, “Pole, tafadhali nisamehe.” Sisi sote tunafanya makosa. Tunapoyakiri, tunaonyesha ushuhuda wa kwamba tunasitawisha sifa bora za kiasi na unyenyekevu.—Mika 6:8; Yakobo 3:2.
20. Ni maneno gani yanayofaa ya mtume Paulo kwenye Wakolosai 3:12-17 yanayotusaidia na kutufaa sisi sote?
20 Yanafaa kama nini maneno haya ambayo Paulo aliambia kundi katika Kolosai: “Halafu vaeni mavazi yanayowafaa watu wachaguliwa wa Mungu, wake mwenyewe, wapendwa wake: huruma, fadhili, unyenyekevu, uanana, subira. Mwe wenye kuchukulia mtu na mwenzake, na wenye kusamehe, mahali ambapo ye yote wenu ana kisababishi cha lalamiko: lazima ninyi msamehe kama Bwana alivyosamehe ninyi. Kwa kumalizia, lazima kuwe na upendo, kufunganisha wote pamoja na kukamilisha ujumla wote. Acheni amani ya Kristo iwe mkata-maneno katika mioyo yenu; kwenye amani hii ninyi mliitwa mwe washiriki wa mwili mmoja. Na mjawe na shukrani. Acheni ujumbe wa Kristo ukae miongoni mwenu ukiwa na utajiri wao wote. Fundishaneni na mwonyane kwa upole mtu na mwenzake kwa hekima ile ya juu kabisa. Imbieni Mungu kwa kupiga asante katika mioyo yenu, kwa zaburi na tenzi za sifa na nyimbo za kiroho. Lo lote mnalofanya, iwe mnanena au mnatenda, fanyeni kila jambo katika jina la Bwana Yesu, mkimpa asante Mungu aliye Baba kupitia kwake.”—Wakolosai 3:12-17, New English Bible.
21. Mwenendo na utendaji wetu unaweza kuwatiaje wengine moyo?
21 Mifano myema iliyo katika Biblia, na pia katika kundi la Kikristo katika karne hii ya 20, inapasa kuwatia wote moyo waendelee kuuvaa utu mpya. (Waefeso 4:22-24) Kwa kufanya hivyo, tutakuwa baraka kwa wote wale tunaoshirikiana nao. Kuongezea hilo, wengi tunaopelekea ujumbe wa Ufalme watavutiwa kisha watiwe moyo, si na maneno yetu tu, bali pia na bidii na mwenendo mwema watakaouona katika jamaa ya duniani pote ya Mashahidi wa Yehova.—Yohana 13:34, 35.
Kwa kufanya muhtasari wa yaliyotangulia, ungesemaje?
◻ Ni sifa zipi zinazopasa kusitawishwa na mwanamume aliye mtu wa Mungu?
◻ Mwanamume Mkristo atatunza mke na jamaa yake namna gani?
◻ Mwanamke Mkristo anapambanuliwa na mema gani?
◻ Ni kwa njia gani ya hekima waseja wanaweza kujengea wakati ujao?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Mwanamume wa kiroho anaonyesha sifa zinazovuta wengine waje kwake
[Picha katika ukurasa wa 20]
Mke anayemcha Mungu anapenda, na anapendwa
[Picha katika ukurasa wa 22]
Wakristo waseja wanaweza kuusitawisha utu mpya ili wawe na maisha yenye faida kamili na furaha