Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme
Upendo, “Kifungo Kikamilifu cha Muungano”
UPENDO kati ya Wakristo ni “kifungo kikamilifu cha muungano,” nao unapozoewa unaleta udugu wa ulimwenguni pote. (Wakolosai 3:14, NW) Hicho “kifungo kikamilifu cha muungano” kinadhihirishwa na ndugu zetu katika Afrika wanapoonyeshana upendo wao kwa wao na kwa Yehova, aliye Mpaji na Mwendelezaji wa Uhai.—Zaburi 36:9; Matendo 17:28.
Kwa sababu ya ukame wa miaka mitatu uliotokea Zimbabwe hivi majuzi, maeneo mengi yalikuwa katika hali yenye shida nyingi. Bila shaka, jambo hilo liliwapata ndugu zetu wanaoishi katika maeneo hayo. Lakini, Mashahidi wenzao waliitikia vizuri sana mwito wa kusaidia. Kwa kweli, mavazi yalitolewa mengi sana mpaka ikawa lazima kuwajulisha akina ndugu wasiendelee kuchanga mpaka watakapojulishwa. Jambo hilo, kuongeza na msaada uliotolewa na serikali, lilifanya wengi wa ndugu zetu wapokee msaada waliouhitaji. “Wale ambao wangali wanahitaji msaada wanatunzwa,” inaripoti afisi ya tawi ya Sosaiti.
Msaada huo wenye upendo uliotolewa na ndugu zetu haukupita bila kuonekana. Mume mmoja asiyeamini alimwambia hivi mke wake, ambaye ni Shahidi: “Wakati wengine wanapokamua watu mali zao zote, ninyi [Mashahidi] mnawapa chakula na mavazi.” Maneno mazuri yamesemwa na wengine pia.
Upendo kati ya Mashahidi wa Yehova unatumika kama “kifungo kikamilifu cha muungano,” na kuwatambulisha kuwa Wakristo wa kweli.—Yohana 13:35.
◻ Mfano mwingine wa upendo na umoja kati ya watu wa Yehova ulionekana kwenye “Umoja wa Ufalme” Mkusanyiko wa Wilaya uliofanywa katika Freetown, Sierra Leone. Wajumbe walikuja kwenye mkusanyiko huo kutoka Guinea na Liberia, na pia kutoka sehemu mbalimbali za Sierra Leone. Vipindi viwili vilifanywa kwa wakati ule ule mmoja: Kimoja kwa Kiingereza na Krio, kile kingine kwa Kisi na Kifaransa. Ripoti ya tawi inaeleza upendo na umoja uliodhihirika katika pindi hiyo. Inasema:
“Ulikuwa wasaa wenye kusisimua wakati ndugu wanaosema lugha ya Kisi na wale wanaosema ya Kifaransa walipojiunga na kipindi cha Kiingereza kwa wimbo na sala ya mwisho. Wengi walitokwa na machozi ya shangwe walipotazama na kuona wajumbe zaidi ya 400 wakipita kati ya uwanja wakajiunge nao kumwabudu Yehova kwa umoja katika wimbo na sala.” Ripoti inamtaja mtazamaji mmoja kuwa alisema: “Yehova anajua jinsi ya kupanga watu wake kitengenezo. Huo ulikuwa wonyesho ulio wazi kama nini wa umoja!”
Umoja huo unaonekana wazi zaidi tunapofikiria kwamba wakusanyikaji walikuwa wa makabila mbalimbali, na hali walikutana pamoja kwa amani. Roho ya Yehova inahitajiwa ili kutimiza jambo hilo. Umoja huo ulitabiriwa katika Ufunuo 7:9: “Baada ya hayo nikaona, na tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao.” Mstari wa 10 wa sura iyo hiyo unaonyesha siri ya umoja huo: “Wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.”