Unavyoweza Kuonyesha Shukrani kwa Aliyoyafanya Yesu
VITENDO vina sauti ya kusema “Asante” kuliko maneno matupu. Basi, ikiwa wewe unathamini yale aliyokufanyia Yesu, utataka kujizoeza imani katika yeye kuwa Mwokozi wako. Kwa kweli, ni kwa kufanya hivyo tu kwamba unaweza kutumainia kufaidika na dhabihu ya Yesu. Kumbuka yale maneno yanayopatikana kwenye Yohana 3:16 (NW), ‘kujizoeza imani’? Kusema hivyo hakumaanishi kuamini tu na kuingiza akilini wazo la kwamba alikufa kwa ajili yako. Kunatia ndani kutenda pia kupatana na imani hiyo.
Yatii maagizo ambayo Petro aliwapa wasikilizaji wake wa Kiyahudi muda mfupi tu baada ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K.: “Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe.” (Matendo 3:19) Hiyo inaonyesha tendo la namna mbili. Kwa upande mmoja, tunayapinga kwa weupe wa moyo maelekeo yenye dhambi ya akili na miili yetu. Kwa upande mwingine, tunamsihi sana Mungu atusamehe dhambi zetu kwa msingi wa dhabihu ya Yesu.—1 Yohana 2:1, 2.
Fuata Mfano wa Yesu
Colin, ambaye amekuwa Mkristo aliyebatizwa kwa muda wa miaka 24 iliyopita, aliulizwa ni sababu gani inayomfanya ashukuru kwa yale aliyoyafanya Yesu. Yeye alijibu hivi: “Mimi naithamini dhabihu yake ya ukombozi, lakini mfano aliouweka ndio unaonisaidia mimi zaidi. Maisha yake yanakuwa kwangu kielelezo cha kufuata.”
Ikiwa sisi tunashukuru kweli kweli, je, hatungetaka kufuata mfano wa Yesu wa unyenyekevu, kujitiisha, na wa upendo wa kujinyima? Midomo yako ikijibu “ndivyo!,” nao mwelekeo na vitendo vyako vinajibuje? Kwa mfano, watu walio wengi wangeitikiaje wakikabiliwa na mgawo utakaoendeleza ibada ya kweli lakini wenye kuwataka wawe na unyenyekevu na kujinyima, kama vile kusafisha sakafu katika mahali pa mikutano ya Kikristo? Wewe ungeitikiaje? Je, kwa kuthamini Yesu na Baba yake wa kimbingu, ungekuwa na nia ya kukubali mgawo ambao wangi wangeuona kuwa usiokistahili cheo chao na usiompa mtu starehe nyingi? Yesu alijinyenyekeza akawafanyia wengine utumishi unaolingana na huo.—Yohana 13:2-17; Wafilipi 2:7, 8.
Na tufikirie mfano mwingine. Mara nyingi hali za kutokuelewana kati ya watu zinawafanya waseme maneno makali na kuoneana uchungu. Watu walio wengi wangefanya nini wakiwa katika chumba kilichojawa na watu, kutia na mtu fulani aliyewakosea sana? Wewe ungefanya nini? Kwa sababu ya kuwaonyesha shukrani Yesu na Yehova, je, wewe ungekuwa na nia ya kuchukua hatua ya kwanza usuluhishe tofauti zako na yule aliyekukosea, ufanye hivyo kwa roho ya utulivu na upole? Hivyo ndivyo Yesu na Baba yake wa kimbingu walivyofanyia wanadamu wenye dhambi.—Warumi 5:6-10; 1 Yohana 4:9-11.
Zaidi ya kuacha utukufu wake wa kimbingu awe mwanadamu kisha atoe uhai wake wa kidunia akiwa mkombozi wa wanadamu, kwa mafundisho yake Yesu alifanyia jamii ya kibinadamu utumishi usiohesabika thamani. Hakuna mwanadamu mwingine aliyewafaidi sana wanadamu kama Yesu Kristo. Yeye alikuwa mwalimu asiye na kifani. Alifundisha wanadamu juu ya jina la Mungu, utu wake, makusudi yake, na mapenzi yake kwa viumbe wa kibinadamu.—Yohana 7:45, 46.
Kati ya mifano yenye kutokeza ya mafundisho yake ni yale Mahubiri ya Mlimani. Katika hayo Yesu aliitaja ile ambayo imekuja kujulikana kuwa kanuni ya kanuni bora zaidi: “Sikuzote tendea wengine kama vile wewe ungependa wao wakutendee wewe.” (Mathayo 7:12, The New English Bible) Pia alionyesha amri mbili zilizo kubwa kupita zote katika Torati: ‘Kupenda Yehova Mungu kwa moyo wako wote, nafsi yote, akili zote, na nguvu zako zote, na kupenda jirani yako kama wewe mwenyewe.’ (Marko 12:29-31, NW) Usio wa kusahauliwa pia ni unabii mbalimbali alioutoa, na utimizo wa unabii huo unaoonyesha wazi sana mahali tulipofika katika orodha ya wakati ya Mungu.—Mathayo, sura 24 na 25.
Yesu aliunga mkono mafundisho yake kwa matendo yake, akatupa sisi mfano bora na ulio mkamilifu wa kufuata. Alianza kazi yake ya maisha kwa kujitoa ili afanye mapenzi ya Baba yake muda wote kisha akaonyesha amejitoa kwa kubatizwa katika maji. Mungu alimtuma duniani, hasa atoe ushuhuda kuhusu ukweli. Muda mfupi tu kabla Yesu hajafa, aliweza kumwambia Baba yake hivi: “Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye,” tena “jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu.”—Yohana 17:4, 6.
Yesu alikusudia kwamba wengine wafuate mfano wake. Hilo linaonekana kutokana na maneno yake mwenyewe na yale ya wengine. “Nifuateni,” na “Njoo unifuate,” akasema Yesu kwenye Mathayo 4:19 na 19:21. “Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake,” na “Mnifuate mimi kama mimi ninavyomfuata Kristo,” ndivyo walivyoandika mitume Petro na Paulo.—1 Petro 2:21; 1 Wakorintho 11:1.
Ili uonyeshe shukrani kwa yale Yesu Kristo aliyokufanyia akiwa ndiye Mwalimu na Mfano Mkuu, endelea kujifahamisha vizuri na mafundisho yake. Jambo hilo linakutaka ujifunze kwa ukawaida Neno la Mungu, hasa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambamo mafundisho ya Yesu yanapatikana. Kwa kuwa uhitaji msaada uelewe na kuthamini unayosoma, lingekuwa jambo la hekima ujifaidi kutokana na misaada iliyochapishwa ya kujifunzia Biblia ili utimize kusudi hilo.a Pia, dhamiria sana ujitahidi kuyatumia katika maisha yako ya kila siku mambo utakayojifunza. Ndiyo, unatakwa uchukue hatua inayofaa. Yesu alitoa maoni haya: “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.”—Mathayo 7:21; 4:17; Luka 4:17-21.
Tanguliza Ibada ya Yehova
Leo watu zaidi ya 1,056,000,000 wanadai kuwa ni Wakristo. Lakini lo, walio wengi kati yao wanaonyesha shukrani kidogo kama nini kwa yale Yesu aliyowafanyia! Inaonekana kwamba wengi wanaona wako sawa tu wakienda kanisani mara mbili kwa mwaka, katika zile sikukuu kubwa-kubwa za Jumuiya ya Wakristo. Au wengine watasema hivi: ‘Mimi nampenda Mungu kwa sababu naziamini Amri Kumi.’ Lakini ni wangapi wanaozitii? Hiyo orodha kamilifu ya sheria, ambazo wakati mmoja zilipasa kushikwa na taifa la Israeli wa kale, iliiweka ibada inayofaa ya Yehova Mungu katika nafasi ya kwanza, ikataja hivyo waziwazi kupitia zile amri nne za kwanza.—Kutoka 20:1-11, NW.
Ni watu wangapi wanaodai kuwa ni Wakristo wanaoufuata kweli kweli mfano wa Yesu kwa kuzitumia kanuni za Amri Kumi katika maisha yao ya kila siku? Je! wao wanampa Mungu “ibada ya pekee,” kama inavyotakwa katika amri ya pili? Kama Yesu, je! wanadhihirisha jina la Mungu kwa njia inayofaa, njia iliyokaziwa na amri ya tatu? Wakristo wa kweli hawafanyi yaliyo mema tu, bali pia wanatanguliza kwanza kabisa ibada ya Yehova katika maisha zao.—Mathayo 6:33.
Wakristo wengi wa namna hiyo wanajua kwamba kukusanyika pamoja ni sehemu ya ibada ya Mungu. Lakini je, wewe umepata kufikiria kwamba kuhudhuria mikutano ya Kikristo ni ishara ya kuonyesha shukrani? Mtume Paulo alifikiria hivyo. Yeye anawaza kwa njia hiyo katika sura ya 10 ya barua aliyowaandikia Waebrania. Pia anaifunua hatari ya kuonyesha ubaridi kuelekea mikutano ya Kikristo. Mwelekeo wa namna hiyo ungeweza kufanya Mkristo avunjike moyo na kuwa asiye mtendaji wa matendo mema ya imani. Halafu huenda uthamini wa wengine ukawa unapungua juu ya njia aliyoitumia Mungu kutoa wokovu kupitia Kristo. Ikiwa ndivyo ilivyo, kisha imani yao yenye kufifia isirekebishwe, huenda jambo hilo likaongoza kwenye dhambi ya makusudi, hata uasi-imani. Hiyo ingekuwa ni sawa na kuichukua zawadi ya Mungu kama “kitu ovyo,” au cha kikawaida tu—hiyo ikiwa ni kumwonyesha Yehova na Yesu ufidhuli.—Waebrania 10:23-31.
Angalia onyo la Paulo kuhusu wale wanaoipita hatua ya kudharau mikutano na kuikataa kikweli zawadi ya Mungu ya wokovu. “Mtu aliyeidharau sheria ya Musa hufa pasipo huruma, kwa neno la mashahidi wawili au watatu. Mwaonaje? Haikumpasa adhabu iliyo kubwa zaidi mtu yule aliyemkanyaga Mwana wa Mungu, na kuihesabu damu ya agano aliyotakaswa kwayo kuwa ni kitu ovyo, na [kuifanyia jeuri roho ya neema]?”—Waebrania 10:28, 29.
Torati ni zawadi iliyotolewa na Mungu kupitia Musa. Kwa hiyo Paulo anawakumbusha wasomaji wake kwamba ikiwa wavunjaji wasiotubu wa Torati hiyo ya kimungu walipokea adhabu ya kifo, wale wanaoipuuza kwa madharau zawadi kubwa zaidi aliyoitoa Mungu kupitia Yesu Kristo, yule Musa Mkubwa Zaidi, wanastahili adhabu kubwa zaidi ya hiyo. Wale wanaopuuza ubora wa Mwana wa Mungu kuwa Mwokozi wao na kudharau dhabihu yake watakuja kupatwa na “mauti ya pili”—adhabu kali isiyo na tumaini la ufufuo.—Ufunuo 21:8; Kumbukumbu la Torati 13:6-10; 17:2-7.
Paulo anaonyesha pia namna mtenda dhambi huyo wa kukusudia au mwasi-imani amekosa sana shukrani. Mtu huyo ametenda ufidhuli ulio mbaya kabisa kwa njia tatu. Kwanza, ‘amemkanyaga Mwana wa Mungu.’ Sasa ama anamwona Yesu kuwa adui yake, kwa maana washindi wa kale walikanyaga shingo za adui waliowashinda, ama anamchukua Yesu kwa madharau, kwa sababu watu wanakanyaga-kanyaga kitu wanachodharau. (Linganisha Mathayo 7:6.) Pili, ‘ameihesabu damu ya agano aliyotakaswa kwayo kuwa ni kitu ovyo.’ Njia ile iliyotumiwa ili atangazwe kuwa safi (nayo ni damu ya Kristo), anaidharau dhihaka. Anaihesabu damu hiyo, inayolihalalisha agano jipya, kuwa ya thamani moja tu na damu ya wanadamu wasio wakamilifu, kuwa kitu kisicho kitakatifu. Tatu, yeye ‘ameifanyia jeuri roho ya neema kwa madharau.’ Ameikufuru kani ya utendaji wa Mungu, akapinga kwa makusudi maongozi ya Yehova, akisema ni ya bure tu na basi hayamfai kitu yeye.—Waefeso 4:30.
Madharau hayo ya wazi yanaweza kuepukwa ikiwa sikuzote tutaithamini sana zawadi ya wokovu tuliyopewa na Mungu. Mikutano ya Kikristo ni njia ambayo kwayo tunaweza kuendeleza heshima inayofaa. Kwa kuwa Yehova na Yesu wanakuwapo bila kuonekana kwenye mikusanyiko hiyo, Wakristo wenye shukrani hawataibeza (hawataidharau), kama wanavyofanya waasi-imani, bali watafanya jitihada za kadiri wanayoweza ili waihudhurie kwa ukawaida.—Linganisha Malaki 3:16; Mathayo 18:20.
Basi, uwe na shukrani kwa yale aliyokufanyia Yesu. Jizoeze imani ya kweli katika dhabihu ya ukombozi. Fuata mfano wake katika shughuli zako na wengine. Tanguliza maishani mwako ibada ya Babaye, Yehova Mungu. Kwa njia hiyo unaweza kusema: “Tumshukuru Mungu kwa ajili ya zawadi yake isiyo na kifano” ya fadhili zisizostahilika kupitia Yesu.—2 Wakorintho 9:15, HNWW.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mfano, tunakipendekeza kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichochapishwa na Sosaiti yetu.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Njia ambazo unaweza kuonyesha una shukrani kwa Yesu