Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Baada ya Daudi na Bath-sheba kutenda dhambi, kwa sababu gani mwana wao akapaswa kufa, kwa kuwa maandiko ya Kumbukumbu la Torati 24:16 na Ezekieli 18:20 yanasema kwamba mwana hapaswi kufa kwa kosa la baba yake?
Daudi alikuwa ameoa na pia Bath-sheba alikuwa ameolewa wakati walipofanya uzinzi kisha Bath-sheba akawa mja mzito. Uzinzi wao ulikuwa dhambi kubwa iliyostahili adhabu ya kifo chini ya sheria ya Mungu. (2 Samweli 11:1-5; Kumbukumbu la Torati 5:18; 22:22) Kwa hiyo kama Mungu angaliruhusu kwamba washughulikiwe na wanadamu chini ya Torati, mwana huyo aliyekuwa akikua ndani ya tumbo la uzazi la Bath-sheba angalikufa pamoja na mama yake. Lakini Yehova alichagua kushughulikia kisa chao kwa njia tofauti, naye kwa hakika alikuwa na haki ya kufanya hivyo kwa maana ndiye “Mhukumu ulimwengu wote.”—Mwanzo 18:25.
Alipokabilishwa hatia yake, Daudi alikiri hivi: “Nimemfanyia [Yehova] dhambi.” Halafu mnenaji wa Mungu akamwambia Daudi: “[Yehova] naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa.” (2 Samweli 12:13) Daudi alionyeshwa rehema kwa sababu ya agano la Ufalme. Zaidi ya hilo, kwa kuwa Mungu anaweza kusoma mioyo, bila shaka aliupima ukweli wa toba ya Daudi na kukata shauri kwamba kulikuwako msingi wa kuwaonyesha rehema. Hata hivyo Daudi na Bath-sheba hawangeepuka adhabu zote ambazo kosa lao lilistahili. Waliambiwa hivi: “Ijapokuwa hivyo, kwa sababu pasipo shaka wewe umemtenda Yehova bila heshima kwa jambo hilo, pia mwana mwenyewe, uliyetoka kuzaliliwa, atakufa hakika.—2 Samweli 12:14, NW.
Mungu ‘alimpiga dharuba’ mtoto wao ambaye hawakumstahili; kivulana huyo akawa mgonjwa na kufa. HUenda leo mtu akaelekea kukaza fikira juu ya kifo cha mtoto huyo na kuwa na maoni ya kwamba hukumu ya ukatili ilifikilizwa. Lakini, ni vizuri kuzingatia kwamba kama uzinzi huo ungalishughulikiwa na kuthibitishwa mbele ya mahakimu wa kibinadamu chini ya Torati, wote watatu (Daudi, Bath-sheba, na mwana ambaye angekuwa ndani ya tumbo lake la uzazi) wangalipoteza uhai wao. Mambo yakionwa kwa njia hiyo, ruhusa ya Mungu kwamba wawili kati yao waendelee kuwa hai ilikuwa jambo la rehema. Tena, kwa kuwa umepita muda mwingi tangu jambo hilo litokee, sisi hatujui mambo yote ya hakika, kama vile kujua afya ambayo kitoto hicho kilikuwa nayo mara tu baada ya kuzaliwa. Hata hivyo, tunaweza kuikubali njia iliyotumiwa na Mungu kushughulikia jambo hilo, tukiwa na uhakika kwamba alilofanya halikuwa na upendeleo, lilikuwa la hekima, na la uadilifu. Hata Daudi alikiri hivi baadaye: “Kwa habari ya Mungu wa kweli, njia yake ni kamilifu.”—2 Samweli 22:31, NW; linganisha Ayubu 34:12; Isaya 55:11, UV.
Kukiri hivyo kunapatana na vile Daudi alivyotenda alipokwisha kuisikia hukumu ya Mungu. Mtoto alipokuwa mgonjwa, Daudi alipatwa na kihoro na kufunga kula. Lakini kifo kilipokwisha kutokea, Daudi alifahamu kwamba jambo hilo lilikuwa limefikia mwisho. (2 Samweli 12:22, 23) Basi, Daudi aliitumaini hukumu ya Mungu na kumfariji Bath-sheba (ambaye sasa alikuwa mke wake wa halali), akamhakikishia kwamba uhusiano wao wa ndoa ungeendelea. Baadaye walimzaa Sulemani kisha yeye akawa mwandamizi wa Daudi.
Njia ya Mungu ya kushughulika na kisa hicho isionwe kuwa inahitilafiana na Kumbukumbu la Torati 24:16 au Ezekieli 18:20.
Mungu alielekeza hivi, hii ikiwa ni sehemu ya Torati: “Mababa wasiuawe kwa ajili ya watoto wao, wala watoto wasiuawe kwa ajili ya baba zao; kila mtu na auawe kwa ajili ya dhambi yake mwenyewe.” (Kumbukumbu la Torati 24:16) Miongozo hiyo ilitolewa kwa ajili ya mahakimu Waisraeli wenye kushughulikia kesi za kisheria. Mahakimu hawangeweza kusoma mioyo ya watu. Walipaswa kushughulika na kila mtu kwa kutegemea mwenendo wake mwenyewe kama ulivyothibitishwa na mambo ya hakika.
Vivyo hivyo, andiko la Ezekieli 18:20 linatoa maoni haya: “Mwana hatauchukua uovu wa baba yake, wala baba hatauchukua uovu wa mwanawe; haki yake mwenye haki itakuwa juu yake, na uovu wake mwenye uovu utakuwa juu yake.” Maneno hayo yalimaanisha watu wazima hasa. Habari zinazozunguka zinasema juu ya mwana aliyeshuhudia uovu wa babaye lakini akakataa kuushiriki; bali, mwana huyo alitenda kulingana na maamuzi ya hukumu ya Yehova na kutembea katika sheria zake. Mwana wa namna hiyo angehifadhiwa hai wakati baba yake angekufa.—Ezekieli 18:14-17.
Ingawa hivyo, haiwezi kukanwa kwamba watoto wanaweza kuumia kwa sababu ya matendo ya wazazi wao. Wazazi wanaotapanya vitu ovyo au walio wapumbavu huenda wakaleta umaskini juu ya jamaa nzima. Au fikiria matokeo yanayokuwa juu ya watoto ikiwa mzazi anahukumiwa kufungwa gerezani kwa kutenda uhalifu. Hata mabaya ambayo Mungu kwa haki alileta juu ya Israeli kwa sababu ya uovu wao yaliwapata watoto wa wakati huo. (Kumbukumbu la Torati 28:15, 20-32; Ezekieli 8:6-18; 9:5-10) Tofauti na hivyo, Mungu aliwahimiza hivi watu wake: “Chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako; kumpenda [Yehova], Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uzima wako, na wingi wa siku zako.”—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.
Kwa hiyo, yaliyowapata Daudi na Bath-sheba yanapasa kuwakazia wazazi kwamba mwenendo wao unaweza kuumiza sana watoto wao. Wazazi wakiwa ‘wanalicha jina la Mungu, jua la haki linaweza kuwazukia’ liwe baraka kwa jamaa nzima.—Malaki 4:2.