Biblia—Je, Inazifaa Siku Zetu?
ULIMWENGU huu umebadilika kwa njia ya kutazamisha katika muda wa karne iliyopita. Badiliko la kuziacha zile siku za kukokota gari kwa kutumia farasi na kuingia kwenye kizazi cha kisasa cha anga za juu limesonga mbele haraka sana hivi kwamba vitabu vya elimu ya kiufundi vinakuwa vikuu-kuu baada ya muda mfupi vikiisha kuchapwa. Yenye kusonga mbele zaidi yamekuwa ni mambo ya kisayansi na elimu ya ufundi. Ingawa mawazo ya kutumia tarakimu za kuandikwa kwa mikono yalifuatwa mara ya kwanza yapata miaka 150 iliyopita, ni katika miaka ya majuzi tu kompyuta zimeanza kutumiwa ulimwenguni pote, zikiongoza kila kitu kuanzia kurusha satelaiti na vyombo vya anga za juu mpaka kupangia matumizi ya kifedha ndani ya nyumba. Limekuwa jambo la kustaajabisha kweli kweli! Ni vigumu kufuatana na mambo yote ambayo yametokana na jambo hilo.
Mengi ya mabadiliko ambayo yametokea yamekuwa yenye faida. Kati ya hayo kumekuwa na maendeleo katika mambo ya upashanaji habari, usafirishaji, vifaa vya kuokoa wakati katika kazi, na tiba. Kwa mfano, mkono au kidole, ambacho hapo zamani kilikuwa kikifikiriwa hakina kazi baada kukatika na kutoka, sasa mara nyingi kinaweza kurudishwa kitumiwe tena kwa kufanyiwa upasuaji wa kuunganisha hata visehemu vile vidogo vidogo. Tunaweza kuruka kwa ndege kwenda ng’ambo ile nyingine ya dunia katika kisehemu kimoja tu cha siku, hivyo tukiokoa miezi ya wakati wa kusafiri. Kwa kulinganishwa na miaka mia moja tu iliyopita—wakati ambao hakukuwa na magari, redio, mashine za barafu, za kufulia nguo, sinema, vitamini, dawa za kushambulia viini vya magonjwa, za kuchanjia, na mamia ya vitu vingine vinavyokubaliwa sana leo—sisi kweli kweli tunaishi katika kipindi kipya.
Lakini si mambo yote yamekuwa ya kutufaidi sana. Kwa mfano, matumizi ya nishati za nyukilia yametokeza tisho kubwa kwa wanadamu kupitia vita au kwa munururisho. Uchafuzi ulioenea sana wa kemikali, unaotokana na ufundi wa viwandani, unaongezea tisho hilo. Dawa za kulevya zilizo haramu na utamaduni wa kisasa wenye kutumia dawa hizo unaingiza uharibifu mkubwa katika maisha za wengi.
Lenye kuonekana zaidi ni badiliko ambalo limepata maisha za watu. Ongezeko la viwanda na badiliko la kutoka mashambani kwenda mijini ili kuishi huko limegawanya-gawanya jamaa. Zaidi ya wakati mwinginewo wote—na hasa kati ya wanawake na watoto—watu wanajiona wakiwa huru na wenye kujitegemea. Kupata uhuru wa vizuizi vya desturi zilizokuwa zikishikiliwa hapo kwanza kumetokeza mitindo mipya ya maisha na kubadili maadili ya kijamii hivi kwamba sasa yako tofauti na yalivyokuwa ulimwenguni kwa maelfu ya miaka.
Biblia Haijabadilika
Basi, je, ni wapi mtu atageukia apate mwongozo? Ni shauri gani linalotumika leo? Waelimishaji wa kisasa wanasahihisha-sahihisha njia zao za kufundisha na vitabu vya masomo ili wasiachwe nyuma na ulimwengu wetu wenye kubadilika. Viongozi wa kidini na wataalamu wengine wanarekebisha shauri lao mambo litegemee mambo yanayokubaliwa na watu kwa ujumla.
Kwa upande mwingine, Biblia imebaki bila kubadilika maelfu na maelfu ya miaka. Kwa kweli, hiyo ina maonyo thabiti kwamba lisiongezwe wala lisiondolewe lo lote la maneno yaliyoandikwa humo. (Mithali 30:5, 6 Ufunuo 22:18, 19) Je! Biblia inaweza kukubaliwa kuwa mwongozo wenye mafaa kwa siku zetu za kisasa?
Wengine wanasema hapana. “Hakuna mtu ambaye angeunga mkono matumizi ya chapa ya mwaka 1924 ya kitabu cha masomo ya kemia katika darasa la kisasa la somo la kemia—mambo mengi mno yamekwisha kujulikana juu ya kemia tangu hapo,” ndivyo anavyoandika Dakt. Eli S. Chesen katika kitabu chake Religion May Be Hazardous to Your Health. Anaendelea kusema: “Kwa njia hiyo hiyo, mengi yamekwisha kujulikana juu ya elimu ya tabia za kijamii, falsafa, na saikolojia katika muda wa miaka elfu kadha iliyopita; hata hivyo, Biblia (ambayo inasema mengi juu ya habari hizo) inatumiwa kuwa mamlaka ya kuthibitishia mambo na hali haisahihishwi mara nyingi.”
Yeye anaongeza hivi: “Mimi nashangaa sana siku zote ninaposikia mtu akizungumza ‘muujiza’ wa jinsi Biblia isivyokuwa na mipaka ya wakati na jinsi ilivyo ya maana leo kama ilivyokuwa wakati ilipoandikwa. Jambo hilo linafanana kidogo na vile mtu anavyoweza kushangaa kwa sababu ya ‘usahihi’ wa unajimu, Biblia imekuwa na mamlaka yenye nguvu sana hivyo kwamba ni watu wachache tu wanaofikiria kuifanya iwe ya kisasa au kuitupilia mbali.”
Lakini, je, kweli Biblia imekuwa ya kizamani katika ulimwengu wetu wa kisasa? Au, shauri ambalo inatoa lingali na mafaa na lenye maana kwa wakati wetu?