Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 4/1 kur. 15-20
  • Kitabu Kutoka kwa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu Kutoka kwa Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kitabu Ambacho Chakubaliana na Sayansi
  • Kitabu Chenye Kutumika kwa Maisha ya Kisasa
  • Kitabu cha Unabii wa Kweli
  • Je, Kitabu Hiki Chaafikiana Na Sayansi?
    Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
  • Kitabu Cha Unabii
    Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
  • Biblia—Kitabu Kutoka kwa Mungu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Kitabu Chenye Kutumika Kwa Maisha Ya Kisasa
    Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 4/1 kur. 15-20

Kitabu Kutoka kwa Mungu

“Unabii haukuletwa wakati wowote kamwe kwa mapenzi ya binadamu, bali wanadamu walisema kutoka kwa Mungu walipokuwa wakichukuliwa na roho takatifu.”—2 PETRO 1:21.

1, 2. (a) Kwa nini watu fulani hushuku kama Biblia yahusu maisha ya kisasa? (b) Twaweza kutumia ithibati gani tatu ili kuonyesha kwamba Biblia ilitoka kwa Mungu?

JE, BIBLIA yawahusu watu wanaoishi kwenye ukingo wa karne ya 21? Watu fulani hufikiri haiwahusu. “Hakuna mtu awezaye kutetea matumizi ya chapa ya mwaka wa 1924 ya [kitabu] cha mafundisho ya kemia, katika darasa la kisasa la kemia—mengi mno yamejulikana juu ya kemia tangu wakati huo,” akaandika Dakt. Eli S. Chesen, akieleza ni kwa nini alihisi kwamba Biblia imepitwa na wakati. Kijuujuu, hoja hiyo yaonekana yenye maana. Hata hivyo, tangu nyakati za Biblia mwanadamu amejua mengi juu ya sayansi, afya ya kiakili, na tabia ya kibinadamu. Kwa hiyo, watu fulani huuliza hivi: ‘Kitabu hicho cha kale kingewezaje kuwa bila makosa ya kisayansi? Je, kingeweza kuwa na shauri liwezalo kutumika katika maisha ya kisasa?’

2 Biblia yenyewe yatoa jibu. Kwenye 2 Petro 1:21, twaambiwa kwamba manabii wa Biblia “walisema kutoka kwa Mungu walipokuwa wakichukuliwa na roho takatifu.” Hivyo Biblia yaonyesha kwamba imetoka kwa Mungu. Ingawa hivyo, twaweza kusadikishaje wengine kwamba ndivyo ilivyo? Acheni tufikirie ithibati tatu zinazoonyesha kwamba Biblia ni Neno la Mungu: (1) Ni sahihi kisayansi, (2) ina kanuni zenye kudumu ambazo ni zenye kutumika katika maisha ya kisasa, na (3) ina unabii mahususi ambao umetimizwa, kama ithibitishwavyo na mambo ya hakika ya kihistoria.

Kitabu Ambacho Chakubaliana na Sayansi

3. Kwa nini mavumbuzi ya kisayansi hayaitishi Biblia?

3 Biblia si kitabu cha mafundisho ya sayansi. Hata hivyo, ni kitabu juu ya kweli, na kweli yaweza kustahimili kwa muda wote. (Yohana 17:17) Hakuna mavumbuzi ya kisayansi ambayo yameitisha Biblia. Itajapo mambo yahusianayo na sayansi, Biblia haina dhana zozote za kale za “kisayansi” zilizothibitika kuwa ngano tu. Kwa hakika, Biblia ina taarifa zipinganazo kabisa na maoni yaliyokubaliwa ya siku yake, ambazo pia ni sahihi kisayansi. Kwa kielelezo, fikiria mwafaka uliopo kati ya Biblia na sayansi ya kitiba.

4, 5. (a) Matabibu wa kale walikosa kuelewa nini juu ya maradhi? (b) Kwa nini hakuna shaka kwamba Musa alijua sana mazoea ya kitiba ya matabibu Wamisri?

4 Matabibu wa kale hawakuelewa kabisa jinsi maradhi yaeneavyo, wala hawakung’amua umaana wa usafi wa kutunza afya katika kuzuia ugonjwa. Mazoea mengi ya kale ya kitiba yangeonekana ya kishenzi kwa kulinganishwa na viwango vya kisasa. Mojawapo ya maandishi ya kitiba ya zamani zaidi yawezayo kupatikana ni yale yaitwayo Funjo la Ebers, ambayo ni mkusanyo wa ujuzi wa kitiba wa Wamisri, wa tangu mwaka wa 1550 K.W.K. Yana tiba 700 za maumivu mbalimbali, “kuanzia yale ya kuumwa na mamba hadi maumivu ya kidole.” Tiba nyingi zilikuwa bila matokeo yoyote, lakini baadhi yazo zilikuwa hatari sana. Ili kutibu jeraha, maagizo yaliyopendekezwa yalikuwa kulipaka mchanganyiko wa kinyesi cha binadamu na vitu vingine.

5 Maandishi hayo ya tiba za Wamisri yaliandikwa yapata wakati uleule vitabu vya kwanza vya Biblia vilipoandikwa, ambavyo vyatia ndani Sheria ya Kimusa. Musa, aliyezaliwa mwaka wa 1593 K.W.K., alikulia Misri. (Kutoka 2:1-10) Akiwa amelelewa nyumbani mwa Farao, Musa “[ali]funzwa katika hekima yote ya Wamisri.” (Matendo 7:22) Alijuana sana na “madaktari” wa Misri. (Mwanzo 50:1-3, NW) Je, maandishi yake yaliathiriwa na mazoea yao ya kitiba yaliyokuwa bila matokeo au yenye hatari?

6. Sayansi ya kisasa ya kitiba huiona kanuni gani ya usafi wa kutunza afya katika Sheria ya Kimusa kuwa ya akili?

6 Kinyume cha hilo, Sheria ya Kimusa ilitia ndani kanuni za usafi wa kutunza afya ambazo zingeonwa na sayansi ya kitiba ya kisasa kuwa za akili. Kwa kielelezo, sheria kuhusu kambi za kijeshi ilihitaji kwamba kinyesi kifunikwe kwa ardhi nje ya kambi. (Kumbukumbu la Torati 23:13) Hiyo ilikuwa hatua ya kujikinga ya hali ya juu sana. Ilisaidia kutunza vyanzo vya maji vikiwa bila uchafu na iliandaa kinga dhidi ya ugonjwa wa kuhara damu uletwao na nzi na magonjwa mengine ya kuhara ambayo huua mamilioni ya watu kila mwaka, hasa katika nchi zinazositawi.

7. Katika Sheria ya Kimusa, ni kanuni gani ya usafi wa kutunza afya iliyosaidia kuzuia kuenea kwa magonjwa ya kuambukiza?

7 Sheria ya Kimusa ilikuwa na kanuni nyingine za usafi wa kutunza afya ambazo zilisaidia kuzuia kuenea kwa maradhi yenye kuambukiza. Mtu aliyekuwa na maradhi ya kuambukiza au aliyeshukiwa kuwa nayo, alitengwa na wengine. (Mambo ya Walawi 13:1-5) Mavazi na vyombo vilivyogusa mnyama aliyekufa mwenyewe (labda kutokana na maradhi) zilipasa ama kuoshwa kabla ya kutumiwa tena ama kuharibiwa. (Mambo ya Walawi 11:27, 28, 32, 33) Mtu yeyote aliyegusa maiti alionwa kuwa asiye safi na alilazimika kufuata utaratibu wa kutakaswa uliotia ndani kuosha mavazi na kuoga. Wakati wa kile kipindi cha siku saba cha ukosefu wa usafi, alilazimika kuepuka kugusana kimwili na wengine.—Hesabu 19:1-13.

8, 9. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba ule mfumo wa sheria ya usafi wa kutunza afya katika Sheria ya Kimusa, ulikuwa wa hali ya juu?

8 Mfumo huo wa sheria wa usafi wa kutunza afya hufunua hekima ya hali ya juu. Sayansi ya kitiba ya kisasa imejua mengi juu ya kuenea na kuzuia maradhi. Kwa kielelezo, hatua za kitiba katika karne ya 19 ziliongoza kwenye kuanzishwa kwa uzuiaji wa kukua kwa bakteria, yaani, usafi ili kupunguza maambukizo. Tokeo lilikuwa kupungua kwa kiwango kikubwa kwa maambukizo na vifo vya kabla ya wakati. Mwaka wa 1900, matarajio ya muda wa kuishi tangu kuzaliwa yalikuwa chini ya miaka 50 katika nchi nyingi za Ulaya na Marekani. Tangu wakati huo, yameongezeka kwa kutazamisha kwa sababu ya maendeleo ya kitiba katika kudhibiti maradhi, na pia kwa sababu ya hali bora za usafi wa kutunza afya na za kuishi.

9 Hata hivyo, maelfu ya miaka kabla sayansi ya kitiba haijajua jinsi maradhi yaeneavyo, Biblia iliagiza juu ya hatua za akili za uzuiaji zikiwa kinga dhidi ya maradhi. Haishangazi kwamba, Musa angeweza kusema juu ya Waisraeli wa siku yake ambao kwa ujumla waliishi kufikia umri wa miaka 70 au 80. (Zaburi 90:10) Musa angeweza kujuaje juu ya kanuni hizo za usafi wa kutunza afya? Biblia yenyewe yaeleza hivi: Mfumo wa Sheria “[u]lipitishwa kupitia kwao malaika.” (Wagalatia 3:19) Ndiyo, Biblia si kitabu cha hekima ya kibinadamu; ni kitabu kutoka kwa Mungu.

Kitabu Chenye Kutumika kwa Maisha ya Kisasa

10. Ingawa Biblia ilikamilishwa karibu miaka 2,000 iliyopita, ni jambo gani lililo kweli kuhusu shauri lake?

10 Vitabu vyenye kutoa maagizo huelekea kupitwa na wakati navyo punde si punde hurekebishwa au vingine hutengenezwa badala yake. Lakini Biblia ni ya pekee kwa kweli. “Shuhuda zako ni amini sana,” yasema Zaburi 93:5. Ingawa Biblia ilikamilishwa karibu miaka 2,000 iliyopita, maneno yake bado yaweza kutumika. Na hutumika kukiwa na matokeo sawa hata rangi yetu ya ngozi iwe gani au tuwe twaishi nchi gani. Fikiria vielelezo kadhaa vya shauri la Biblia lenye kudumu na “lenye kutumainika sana.”

11. Miongo kadhaa iliyopita, wazazi wengi waliongozwa kuamini nini juu ya kuwatia nidhamu watoto?

11 Miongo kadhaa iliyopita wazazi wengi—wakichochewa na “uvumbuzi wa mawazo mapya” juu ya kulea watoto—walifikiri kwamba “mtu hapaswi kuwatia watoto nidhamu.” Walihofu kwamba kuwawekea watoto vizuizi, kungesababisha vurugu na kukata tamaa. Washauri wenye makusudi mazuri walikuwa wakisisitiza kwamba wazazi wapaswa kuwatolea watoto wao sahihisho lisilo kali sana. Wengi wa wataalamu hao sasa “wanawahimiza wazazi wawe wakali zaidi, ili kuwatia nidhamu watoto wao,” laripoti gazeti The New York Times.

12. Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “nidhamu” lamaanisha nini, na ni kwa nini watoto wahitaji nidhamu hiyo?

12 Hata hivyo, sikuzote Biblia imetoa shauri mahususi na lenye usawaziko juu ya kuzoeza mtoto. Hiyo yatoa shauri hili: “Akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Nomino ya Kigiriki ambayo imetafsiriwa “nidhamu” humaanisha “kulea, kuzoeza, kufundisha.” Biblia husema kwamba nidhamu, au fundisho, ni uthibitisho wa upendo wa mzazi. (Mithali 13:24) Watoto husitawi chini ya miongozo dhahiri ambayo huwasaidia kusitawisha utambuzi wa mema na mabaya. Nidhamu ambayo imetolewa ifaavyo huwasaidia kuhisi salama; huwaambia kwamba wazazi wao huwajali na hujali juu ya aina ya mtu ambaye wanakuwa.—Linganisha Mithali 4:10-13.

13. (a) Biblia huwatolea wazazi hadhari gani kuhusu nidhamu? (b) Biblia hupendekeza nidhamu ya aina gani?

13 Lakini Biblia yatolea wazazi hadhari juu ya nidhamu. Mamlaka ya mzazi haipaswi kutumiwa vibaya. (Mithali 22:15) Mtoto yeyote hapaswi kamwe kutiwa adhabu kikatili. Jeuri ya kimwili hairuhusiwi katika familia ambayo huishi kupatana na Biblia. (Zaburi 11:5) Wala jeuri ya kihisia-moyo—maneno makali, uchambuzi wa daima, na kejeli yenye kuumiza, zote ambazo zaweza kuponda roho ya mtoto. (Linganisha Mithali 12:18.) Kwa hekima, Biblia yaonya hivi: “Msiwe mkichochea watoto wenu wakasirike, ili wasishuke moyo [au, “mtawavunja moyo kabisa,” Phillips].” (Wakolosai 3:21) Biblia hupendekeza hatua za kinga. Kwenye Kumbukumbu la Torati 11:19, wazazi wahimizwa watumie kwa manufaa wasaa wa mapumziko ili kukaza katika watoto wao kanuni za kiadili na za kiroho. Shauri hilo lililo wazi na la akili juu ya kulea mtoto, ni lenye kutumika leo kama lilivyotumika nyakati za Biblia.

14, 15. (a) Biblia huandaa mengi zaidi ya shauri lenye hekima katika njia gani? (b) Ni mafundisho gani ya Biblia yawezayo kuwasaidia wanaume na wanawake wa jamii na mataifa tofauti waone mmoja na mwenzake kuwa sawa?

14 Biblia huandaa mengi zaidi ya shauri lenye hekima tu. Ujumbe wake huvutia moyo. Waebrania 4:12 lasema hivi: “Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na hudunga hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na uloto wavyo, na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” Fikiria kielelezo kimoja cha nguvu ya Biblia yenye kuchochea.

15 Watu leo wamegawanywa na vizuizi vya kijamii, kitaifa, na kikabila. Vizuizi hivyo bandia vimechangia kuchinjwa kijumla kwa wanadamu wasio na hatia katika vita ulimwenguni pote. Kwa upande mwingine, Biblia ina mafundisho ambayo husaidia wanaume na wanawake wa jamii na mataifa tofauti waonane kuwa sawa. Kwa mfano, Matendo 17:26 lasema kwamba Mungu “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu.” Hilo laonyesha kwamba kwa kweli kuna jamii moja tu—ile ya kibinadamu! Biblia yaendelea kututia moyo “[tuwe] waigaji wa Mungu,” ambaye juu yake yasema hivi: “[Yeye] si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Waefeso 5:1; Matendo 10:34, 35) Ujuzi huo ni wenye matokeo kwa wale watafutao kwa kweli kuishi kupatana na mafundisho ya Biblia. Huo hugusa hisi ya ndani kabisa—moyo—ukiharibu vizuizi vyenye kutengenezwa na watu ambavyo hugawanya watu. Je, ujuzi huo kwa kweli hufanya kazi katika ulimwengu wa leo?

16. Simulia ono moja linaloonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova ni udugu wa kimataifa.

16 Bila shaka hufanya hivyo! Mashahidi wa Yehova wajulikana vizuri kwa sababu ya udugu wao wa kimataifa, ambao huunganisha watu wa malezi tofauti ambao kwa kawaida hawangekuwa na amani wao kwa wao. Kwa kielelezo, wakati wa mapigano ya kikabila huko Rwanda, Mashahidi wa Yehova wa kila kabila waliwalinda ndugu na dada zao Wakristo wa kabila lile jingine, wakihatarisha maisha zao wenyewe katika kufanya hivyo. Katika kisa kimoja, Shahidi Mhutu aliificha nyumbani mwake familia ya Watutsi sita wa kutaniko lake. Kwa kusikitisha, hiyo familia ya Watutsi iligunduliwa mwishowe na kuuawa. Huyo ndugu Mhutu na familia yake sasa walikabili hasira ya kisasi ya hao wauaji, wakalazimika kukimbilia Tanzania. Vielelezo sawa na hivyo viliripotiwa. Mashahidi wa Yehova hukiri kwa utayari kwamba muungano huo huwezekana kwa sababu mioyo yao imeguswa sana na nguvu yenye kuchochea ya ujumbe wa Biblia. Uhakika wa kwamba Biblia yaweza kuunganisha watu katika ulimwengu huu uliojaa chuki ni uthibitisho wenye nguvu kwamba imetoka kwa Mungu.

Kitabu cha Unabii wa Kweli

17. Unabii mbalimbali wa Biblia uko tofauti jinsi gani na matabiri bandia yafanywayo na watu?

17 “Hakuna unabii wa Andiko uchipukao kutokana na fasiri yoyote ya faragha,” lasema andiko la 2 Petro 1:20. Manabii wa Biblia hawakuchanganua mielekeo ya mambo yaliyokuwako ulimwenguni, kisha wakafanya matabiri yaliyotegemea ufasiri wao wa kibinafsi juu ya mambo hayo. Wala hawakutamka matabiri ambayo yangeweza kupotoshwa yafae tukio lolote tu la wakati ujao. Kwa kielelezo, acheni tuchunguze unabii wa Biblia ambao kwa kutokeza ulikuwa mahususi na ambao ulitabiri kinyume kabisa cha yale ambayo watu walioishi wakati huo, huenda wakawa walitarajia.

18. Kwa nini bila shaka wakaaji wa Babiloni walihisi kuwa salama sana, hata hivyo Isaya alikuwa ametabiri nini juu ya Babiloni?

18 Kufikia karne ya saba K.W.K., Babiloni lilionekana kuwa jiji kuu la Milki ya Babiloni lisiloweza kushindwa. Hilo jiji lilitagaa juu ya Mto Eufrati, na maji yake yalitumiwa kufanyiza handaki la maji lililokuwa pana na lenye kina, na mfumo wa mifereji. Hilo jiji pia lilikuwa limelindwa na mfumo wa kuta maradufu, zilizotegemezwa kwa minara ya ulinzi. Bila shaka wakaaji wa Babiloni walihisi wakiwa salama sana. Hata hivyo, katika karne ya nane K.W.K., hata kabla ya Babiloni kuinuka kufikia upeo wa utukufu wake, nabii Isaya alitabiri hivi: ‘Babiloni litakuwa kama Sodoma na Gomora hapo Mungu alipoiangamiza. Halitakaliwa na watu tena kabisa, wala watu hawatakaa ndani yake tangu kizazi hadi kizazi. Mwarabu hatapiga hema yake huko, wala wachungaji hawatalaza makundi yao huko.’ (Isaya 13:19, 20) Ona kwamba huo unabii ulitabiri kwamba Babiloni lingeharibiwa na pia lingekuwa bila wakaaji milele. Ni utabiri wenye ujasiri kama nini kuutoa! Je, yawezekana kuwa Isaya aliandika unabii wake baada ya kuona Babiloni lililokuwa ukiwa? Historia yajibu la!

19. Kwa nini unabii wa Isaya haukutimizwa kabisa Oktoba 5, 539 K.W.K.?

19 Usiku wa Oktoba 5, 539 K.W.K., Babiloni lilishindwa na majeshi ya Umedi na Uajemi chini ya Koreshi Mkubwa. Hata hivyo, unabii wa Isaya haukutimizwa kabisa wakati huo. Kufuatia kutwaliwa na Koreshi, Babiloni lenye wakaaji—lijapokuwa hafifu—liliendelea kwa karne nyingi. Katika karne ya pili K.W.K., yapata wakati ule Hati-Kunjo ya Baharifu ya Isaya iliponakiliwa, Waparthi walikuwa na mamlaka juu ya Babiloni, lililoonekana wakati huo kuwa jiji lisilo na kifani ambalo mataifa yaliyolizunguka yalilipigania. Mwanahistoria Myahudi, Josephus, aripoti kwamba “idadi kubwa” ya Wayahudi walikuwa wakiishi huko katika karne ya kwanza K.W.K. Kulingana na kitabu The Cambridge Ancient History, wafanya-biashara kutoka kisiwa cha Palmyra walianzisha koloni huko Babiloni mwaka wa 24 W.K. Kwa hiyo, mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., Babiloni lilikuwa bado halijawa ukiwa kabisa; hata hivyo kitabu cha Isaya kilikuwa kimekamilika muda mrefu kabla ya wakati huo.—1 Petro 5:13.

20. Kuna ithibati gani kwamba mwishowe Babiloni lilipata kuwa “magofu”?

20 Isaya hakuishi kuona Babiloni likiwa bila wakaaji. Lakini kwa utimizo wa unabii, mwishowe Babiloni lilipata kuwa “magofu.” (Yeremia 51:37) Kulingana na Jerome, msomi Myahudi (aliyezaliwa karne ya nne W.K.), kufikia siku yake Babiloni lilikuwa eneo la uwindaji ambalo ndani yake “hayawani wa kila aina” walizurura, na laendelea kuwa ukiwa hadi siku hii. Kurudishwa kokote kwa Babiloni kuwa uvutio wa watalii huenda kukavuta wageni, lakini “mwana na mjukuu” wa Babiloni wametoweka milele, kama vile Isaya alivyotabiri.—Isaya 14:22.

21. Kwa nini manabii waaminifu waliweza kutabiri juu ya wakati ujao kwa usahihi usioweza kukosea?

21 Nabii Isaya hakufanya kisio lenye kutegemea mambo aliyoona. Wala hakuandika tena historia ili kuifanya ionekane kuwa unabii. Isaya alikuwa nabii wa kweli. Na ndivyo walivyokuwa manabii wengine wote wa Biblia waliokuwa waaminifu. Kwa nini wanaume hao waliweza kufanya jambo ambalo hakuna wanadamu wengine wowote wawezao kulifanya—kutabiri wakati ujao kwa usahihi usioweza kukosea? Jibu ni wazi. Huo unabii ulitokana na Mungu wa unabii, Yehova, ‘atangazaye mwisho tangu mwanzo.’—Isaya 46:10.

22. Kwa nini twapaswa kufanya yote tuwezayo ili kuwahimiza wenye mioyo ya haki wajichunguzie Biblia?

22 Je, Biblia yastahili kuchunguzwa? Twajua kwamba yastahili! Lakini watu wengi hawasadikishwi. Wamefanyiza maoni juu ya Biblia hata ingawa huenda ikawa hawajaisoma. Kumbuka yule profesa aliyetajwa mwanzoni mwa makala iliyotangulia. Alikubali kuisoma Biblia, na baada ya kuichunguza Biblia kwa uangalifu, alifikia mkataa kwamba hiyo ni kitabu kutoka kwa Mungu. Mwishowe alibatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na leo hutumikia akiwa mzee! Acheni tufanye yote tuwezayo kuwahimiza watu wenye mioyo ya haki wajichunguzie Biblia, kisha wapate maoni fulani kuihusu. Tuna uhakika kwamba wakijifanyia uchunguzi wa moyo mweupe na wa moja kwa moja, watakuja kung’amua kwamba Biblia ni kitabu cha pekee kwa ajili ya watu wote!

Je, Waweza Kueleza?

◻ Je, waweza kutumiaje Sheria ya Kimusa ili kuonyesha kwamba chanzo cha Biblia si cha kibinadamu?

◻ Ni kanuni zipi za Biblia zenye kudumu ambazo ni zenye kutumika kwa maisha ya kisasa?

◻ Kwa nini unabii kwenye Isaya 13:19, 20 haungeweza kuwa uliandikwa baada ya tukio hilo?

◻ Twapaswa kuwatia moyo watu wenye mioyo ya haki wafanye nini, na kwa nini?

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

Vipi Mambo Ambayo Hayawezi Kuthibitishwa?

Biblia ina taarifa mbalimbali ambazo hazina uthibitisho wa kiasili kando na Biblia. Kwa kielelezo, yale isemayo juu ya milki isiyoonekana ikaliwayo na viumbe wa roho hayawezi kuthibitishwa—au kutothibitishwa—kisayansi. Je, lazima marejezo hayo yasiyoweza kuthibitishwa yaifanye Biblia ihitilafiane na Sayansi?

Hilo ndilo lililokuwa swali lililomkabili mtaalamu wa jiolojia ya sayari aliyeanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova miaka kadhaa iliyopita. “Lazima nikiri kwamba kuikubali Biblia kulikuwa jambo gumu kwangu mwanzoni kwa sababu singeweza kuthibitisha kisayansi taarifa fulani za Biblia,” yeye akumbuka. Mwanamume huyu mwenye moyo mweupe aliendelea kujifunza Biblia na mwishowe akasadikishwa kwamba uthibitisho wenye kupatikana waonyesha kwamba hilo ni Neno la Mungu. “Hilo lilipunguza tamaa nyingi ya kutaka kila jambo katika Biblia lithibitishwe likiwa peke yake,” yeye aeleza. “Mtu mwenye mwelekeo wa kisayansi lazima awe tayari kuichunguza Biblia kwa maoni ya kiroho, au hataweza kamwe kukubali kweli. Sayansi haiwezi kutarajiwa ithibitishe kila taarifa katika Biblia. Lakini kwa sababu taarifa nyingine haziwezi kuthibitishwa, hilo halimaanishi kwamba si za kweli. Jambo la maana ni kwamba iwezekanapo usahihi wa Biblia huthibitishwa.”

[Picha katika ukurasa wa 17]

Musa alirekodi kanuni za usafi wa kutunza afya zilizo kuwa za hali ya juu sana

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki