Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 8/1 kur. 27-31
  • Je! Mtoto Wako Mdogo ‘Anakua Kuelekea Wokovu’?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Mtoto Wako Mdogo ‘Anakua Kuelekea Wokovu’?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uhusiano wa Karibu sana Pamoja na Yehova
  • Liwe Lenye Kufurahika
  • Jamaa Yenye Furaha Yenye Usawaziko
  • Wasaidie Wajiwekee Miradi Inayofaa
  • Sala Upate Msaada
  • Usikate Tamaa
  • Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga Sana
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Kulea Watoto tangu Uchanga
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Wazazi, Fikieni Moyo wa Mtoto Wenu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Wazazi—Wafundisheni Watoto Wenu Tangu Utotoni
    Huduma Yetu ya Ufalme—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 8/1 kur. 27-31

Je! Mtoto Wako Mdogo ‘Anakua Kuelekea Wokovu’?

WAZAZI wote Wakristo wanataka kuona watoto wao wakikua wawe watu wazima waliokomaa ambao ni Wakristo. Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba haiwi hivyo sikuzote. Kwa vyo vyote haijitokezi tu kwamba mtoto wa mzazi Mkristo atajikulia mwenyewe awe Mkristo. Sababu ni nini?

Tunaweza kuona sababu moja kutokana na maneno ya Petro: “Kama vitoto vichanga vilivyozaliwa karibuni, fanyizeni nia ya kutamani sana maziwa yasiyochanganywa kitu ambayo ni ya lile neno, ili kupitia kwalo mpate kukua kwenye wokovu.” (1 Petro 2:2, 3, NW ) Kitia-moyo cha ‘kufanyiza nia ya kutamani sana’ kinadokeza kwamba watoto wetu hawatazaliwa wakiwa wanatamani sana mambo ya kiroho. Huenda tukalazimika kufanyiza au kukuza tamaa nyingi hiyo ndani yao. Hata hivyo, kama vile andiko linavyoonyesha pia, wokovu unahusika. Sawa na vile inavyolazimu watoto wajifunze kupenda chakula chenye afya ndipo waweze kukua wafikie utu mzima wenye afya, ndivyo ilivyo lazima wao wajifunze kufurahia chakula cha kiroho ili waweze “kukua kwenye wokovu.”

Wazazi—je! ninyi mna watoto ambao bado hawajawa vijana—matineja? Je! programu yenu ya kulea watoto na kuwatia nidhamu imekuwa yenye mafaa kwenu kufikia hapo? Ikiwa ndivyo, ni vizuri sana. Lakini, huenda mambo yakabadilika wakati wa miaka ya utineja. Kwa kweli, ingawa nyakati nyingine matatizo yanayotokea wakati wa kubalehe yanakaziwa kupita kiasi, wazazi wenye ujuzi wanaonya kwamba inakupasa utazamie nyakati fulani za mahangaiko katika kipindi hicho. Je! mnaweza kujitayarishia nyakati hizo sasa, mtoto wenu anapokuwa angali mdogo? Ndiyo, kuna hatua fulani za wazi mnazoweza kuchukua. Kwa mfano, inatupasa tuwasaidie kukuza . . .

Uhusiano wa Karibu sana Pamoja na Yehova

Samweli mdogo, ambaye kuzaliwa kwake kulikuwa jibu kwa sala ya Hana, mama yake, ‘alikua pamoja na Yehova.’ (1 Samweli 2:20, 21, NW ) Lo! malezi mazuri kama nini! Kumbuka, pia, jinsi katika pindi moja wazazi walivyoletea Yesu watoto wao wadogo. Kwanza, wanafunzi waliwakemea, lakini “Yesu alipoona alichukizwa sana, akawaambia, Waacheni watoto wadogo waje kwangu, msiwazuie; kwa maana watoto kama hawa ufalme wa Mungu ni wao.” Yesu alilikubali jambo la kwamba wazazi walimletea yeye watoto wao. Aliwakumbatia watoto hao akawabariki.—Marko 10:13-16.

Je! leo wazazi wanaweza kusaidia watoto wao ‘wakue pamoja na Yehova’ na kuwaleta kwa Yesu Kristo, hivyo kuwasaidia wakuze uhusiano pamoja na Yehova na Yesu? Wanaweza, lakini inachukua muda. Yesu alikuwa na nia ya kutumia wakati akiwa pamoja na watoto wa watu wengine, kwa hiyo hakika sisi tunaweza kutumia wakati tukiwa pamoja na watoto wetu wenyewe. Ikiwezekana, inatupasa tuanze jambo hilo tangu utoto mchanga, kama alivyofanya mama ya Timotheo. (2 Timotheo 3:15) Inatupasa tuongee juu ya Yehova na Yesu kama watu halisi, tukifundisha wadogo wetu wathamini baadhi ya kazi zao za ajabu za uumbaji. Tunapowapeleka katika bustani ya starehe, kwenye sehemu walikofungiwa wanyama, au nje sehemu za mashambani, tunaweza kuwasaidia wauone mkono wa Yehova katika maajabu wanayoona. Kwa maongezi yetu, tunaweza kukuza ndani yao tamaa ya kutenda yaliyo mema kwa sababu jambo hilo linafurahisha Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 6:7.) Usiahirishe kufanya jambo hilo. Muda ambao watoto wetu wanakuwa wadogo ni mfupi mno. Wao wanakua haraka, kwa hiyo wakati unaotumiwa pamoja nao ni wa thamani kubwa.—Mathayo 19:13-15.

Bila shaka, njia ya msingi ambayo tunatumiwa kufundisha watoto wetu ukweli na kuwasaidia wapate uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova ni kupitia funzo la Biblia la kijamaa. Lakini, litakuwa na mafanikio makubwa zaidi ikiwa tutalifanya . . .

Liwe Lenye Kufurahika

Mama anayetaka mtoto wake afurahie chakula kinachofaa halazimishi mtoto huyo ameze kiasi kingi. Bali, atakitayarisha kiwe na ladha nzuri na kumtia moyo ale visehemu vidogo-vidogo kwa wakati mmoja, pole kwa pole akiongeza tamaa yake ya kutaka kukila, Jambo kama hilo linahitajiwa kwa chakula cha kiroho. Kama sasa ndipo unapoanza programu ya funzo kwa mara ya kwanza au unataka kufanya rekebisho fulani katika programu yako kwa sababu mtoto wako hapendezwi sana nayo, takwa ni lile lile moja. Jitahidi kuifanya programu iwe yenye kupendeza.

Kwa habari ya watoto wadogo si lazima ushike sana njia rasmi ya maulizo kwa majibu, wala si lazima ufanye kila funzo liwe la saa nzima. Lilinganishe na mtoto wako. Msimulie hadithi juu ya watu wanaotajwa katika Biblia. Mwache yeye achore picha za tamasha za Biblia. Waache watoto waige kwa vitendo matukio ya Biblia na michezo ya kuigiza iliomo. Wape mambo watakayobaki wakijitahidia mpaka wakati ule mwingine. Yafanye mambo hayo yawe ya kuchangamsha na ya ladha mbalimbali. Unataka mtoto wako ‘afanyize nia ya kutamani sana neno,’ kwa hiyo mfanyie liwe na ladha nzuri kama iwezekanavyo.—1 Petro 2:2, 3, NW.

Matokeo yanafanya jitihada hiyo istahili kufanywa kwa sababu yanaendelea muda mrefu. Ikiwa mtoto wako anafurahia mambo ya kiroho anapokuwa mdogo, anaweza kusaidiwa akuze uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova utakaodumu muda wote wa maisha yake. “Mwanzishe mvulana katika barabara inayofaa, na hata katika umri wa uzee yeye hataiacha.” (Mithali 22:6, The New English Bible) Lakini kuna jambo jingine litakalosaidia mtoto wako akuze upendo wa mambo ya kiroho. Ni jambo gani hilo?

Jamaa Yenye Furaha Yenye Usawaziko

Ndiyo, sawa na mmea unavyokua vizuri zaidi wakati udongo ni wenye rutuba na hali ya anga inaufaa Kabisa, ndivyo mtoto atakavyositawi kiroho katika hali yenye furaha katika jamaa. Lakini, Ili kuwe na hali hiyo, washiriki wa jamaa wanahitaji kutumia wakati wakiwa pamoja. Wazazi, je! mnahakikisha kwamba washiriki wa jamaa yenu wanatumia wakati wakiwa pamoja na kusemezana? Je! ninyi mna miongozo ya kijamaa juu ya utazamaji televisheni? Juu ya tafrija? juu ya uchaguzi wa muziki? juu ya funzo la jamaa? juu ya utendaji wa kiroho mwingine? Hali ya kijamaa inakuwaje wakati wa chakula cha jioni? Katika nyumba nyingi, chakula cha jioni ndio wakati ulio mzuri zaidi wa jamaa kuwa pamoja. Unawapa nafasi ya kuzungumza mambo ambayo yametukia mchana ya kushirikiana kidogo mambo ya kuchekesha na kupiga mdomo kwa njia yenye starehe. Jambo hilo linaweza kufaidi kila mtu.

Kumbuka, pia, kwamba ingawa watoto wanahitaji utendaji wa kiroho na ni lazima watimize madaraka yao nyumbani, wanahitaji pia wakati wa kucheza. Charles R. Foster, katika kitabu chake Psychology for Life Today, alisema: “Wakitambua umaana wa tafrija katika maisha za watoto wao, wazazi wanapaswa wafanyie watoto wao maandalizi ya kuzifurahia. . . . Watoto, wanapoendelea kukua na kusitawi, wanapaswa waone uhusiano ulio kati ya utendaji huo na gharama za kijamaa na pia madaraka ya nyumbani. Ikiwa wao wanatambua uhusiano ulio kati ya mambo hayo, na hawatumii tafrija kama njia ya kuepa wajibu na madaraka mbali-mbali ya nyumbani, kutakuwa na hali yenye furaha zaidi nyumbani.”

Wazazi wanaosaidia mtoto wao akuze mwelekeo uliosawazika kuhusu tafrija, kazi na mambo ya kiroho wanamsaidia sana afurahie mambo ya kiroho na ukaribu wake kwa, Yehova. (Linganisha 2 Timotheo 3:4b; Tito 3:3.) Maendeleo hayo yatawaletea wazazi furaha nyingi. Na kuna jambo jingine wanaloweza kufanya mapema utotoni ili wakuze uthamini wa mtoto wao juu ya mambo ya kiroho:

Wasaidie Wajiwekee Miradi Inayofaa

Mfalme Sulemani mwenye hekima alitoa mashauri mazuri juu ya kulea watoto aliposema hivi: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Maneno “katika njia impasayo” yangeweza kumaanisha ama kulingana na uwezo wake, au, inaelekea zaidi, ni katika namna ya maisha, njia, mradi katika maisha, ambao wewe ungependa ajichagulie. Hivyo, moja ya njia zilizo za maana zaidi ambazo mzazi anaweza kutumia aongezee furaha na hali ya kiroho ya mtoto wake ni kumsaidia ajiwekee miradi yenye maana. Miradi hiyo inapasa kuwa (yenye mafaa na inayoweza kutimizwa, Inapasa pia iwe inayoweza kufikiwa kwa muda usio mwingi kupita kiasi. Halafu, miradi fulani inapotimizwa, jambo hilo litamtia moyo mtoto ajiwekee mingine iliyo ya juu zaidi.

Kosa linafanywa mara nyingi la kungoja mtoto ajiwekee miradi yake mwenyewe maishani. Ujuzi wa mtoto mdogo mno. Wazazi wasipomsaidia kujiwekea miradi, mtu mwingine atafanya hivyo—labda watoto wale wengine shuleni au washauri wa mambo ya shuleni. Wazazi Wakristo wanaweza kusaidia mtoto ajiwekee miradi inayopatana na uthamini wake wa mambo ya kiroho. Watoto wadogo wangeweza kujiwekea mradi wa kustahili kujiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Katika utumishi wa shambani, miradi mizuri inayoweza kutimizwa na mtoto ingeweza kuwa ni kutoa kikaratasi cha ukaribishaji mlangoni, halafu kutoa magazeti na mwishowe, kutoa mahubiri rahisi. Miradi ya kujifunza inaweza kuwekwa. Watoto wangeweza kujifunza hatua kwa hatua kufuatisha majina ya vitabu vya Biblia kama yalivyopangwa na kukariri maandiko fulani makuu. Miradi ya kazi za maisha inapasa izungumzwe mapema. Ingawa washauri wa mambo ya shuleni watatolea mtoto aina fulani ya kazi ya maisha, wazazi Wakristo wanaweza kukazia miradi itakayotosheleza kupendezwa kwake kunakoongezeka kuhusu kutumikia Yehova, kama vile (upainia , utumishi wa Betheli, na umisionari.

Wazazi wanataka pia mtoto wao akuze hali ya kujisikia ina madaraka ya kutimiza. Wanaweza kumsaidia azoeze dhamiri yake kwa kutegemea kanuni za Biblia. Anapoendelea kukua, inawapasa wamjulishe kwamba wao wana tumaini naye kwamba atafanya jambo lililo jema. Wanaweza kumpa uhuru wenye mipaka katika mambo fulani anayojaribu kufanya, na mtoto akifanya kosa, wanaweza kumsaidia ajifunze kutokana nalo, badala ya kumlaumu vikali. Watoto watajivunia kujipatia sifa ya kuwa wenye kutegemeka na jambo hilo litawasaidia ‘wakue kwenye wokovu.’

Mtoto anapoendelea kukua, wazazi wanakuwa macho kuona mabadiliko na kuwa chonjo kurekebisha mazoezi na nidhamu ilingane na hali mpya-mpya. Wao wanamweleza mambo kwa unyofu wa moyo kabisa bila kumficha. Wanapashana habari naye kuhusu maoni yao juu ya vitendo vyake na mabadiliko yanayompata. Kwa kusema mambo kwa unyofu bila kumficha wanatumainia kumsaidia apashane nao habari kwa uhuru—yeye hatakuwa ni kama mgeni katika nyumba yao.

Daudi kijana alisitawisha tamaa nyingi ya mambo ya kiroho. Zaburi alizoandika zinafunua uthamini wa ndani sana kuelekea upendo wa Yehova. (Zaburi 23:1-6) Kumtumaini Yehova kwa uhakika hivyo kulimweka katika hali nzuri alipolazimika kukabiliana na dubu-mwitu, simba, na mwishowe lile jitu la Kifilisti Goliathi lililokuwa limeingiza hofu nyingi katika mioyo ya jeshi lote la Israeli. Wazia jinsi Yese baba ya Daudi alivyoona fahari kwa sababu ya imani ya Daudi! Daudi alikuza uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova ulioendelea muda wote wa maisha yake. (1 Samweli 17:32-37, 45-50; Zaburi 19:9, 10, 14; 15:1, 2; 24:3, 4) Watoto wetu wanaweza kujenga uhusiano kama huo wa kindani na kutufanya sisi pia tuwaonee fahari—kwa msaada wetu. Lakini hatuwezi kufanya hivyo pekee yetu.

Sala Upate Msaada

Manoa alipojua kwamba angekuwa baba, yeye aliomba mwongozo juu ya jinsi ya kulea mtoto ambaye angempata na jinsi ya kumzoeza. Yehova alijibu sala yake. (Waamuzi 13: 8, 12, 24) Wazazi leo, pia, hawapaswi kuacha kupelekea Yehova sala kuhusu watoto wao, wakimsihi sana awape hekima wanapojaribu kuwaongoza katika njia ya uzima. Samweli, nabii wa Yehova, alihesabu kuwa ni ‘kumtenda Yehova dhambi’ kama angeacha kusali kwa ajili ya watu wa Yehova. (1 Samweli 12: 23; Linganisha Mithali 1:24, 25.) Sisi tunapaswa kujisikia vivyo hivyo kuhusu daraka tulilo nalo kuelekea watoto wetu. Tunawataka wakuze mwelekeo wa kiroho. Tunahitajiwa sana tutoe sala ya ukawaida kuomba msaada.

Usikate Tamaa

Je! lo lote la mambo hayo ni rahisi? Bila shaka sivyo. Ni mambo yenye kuthawabisha lakini si rahisi. Mtoto wetu anapokuwa kijana-tineja, matatizo na magumu makubwa yatatokea bila shaka. Yanapoonekana, usibabaike. Yashughulikie moja moja usitazamie miujiza. Uwe imara lakini usitende kupita kiasi; jiepushe na kusema maneno yenye kuchoma bali ushughulikie tatizo kwa subira. Tukidumisha utulivu wetu kwa njia hiyo, kwa ujumla ugumu ule mkubwa uliokuwapo unapita, nasi tunaweza tena kufurahia ukaribu pamoja na mtoto wetu.

Wazazi wote wanaomwogopa Mungu wanatakia watoto wao yalio bora zaidi. Tunawataka ‘wathamini mambo matakatifu,’ wafanyize tamaa nyingi ya kutaka lile neno la Mungu, ili kupitia kwalo wapate “kukua kwenye wokofu.” Ni kweli kwamba nyakati nyingine wazazi Wakristo wanaona watoto wao wakikua kufikia umri mkubwa halafu wanaukataa ukweli, ijapokuwa wazazi walijitahidi sana. Hata hivyo, bidii kwa upande wetu itapunguza uwezekano wa jambo hilo kutokea. Kwa msaada wa Yehova tutajitahidi kuzoeza watoto wetu kulingana na njia inayowapasa. Na tupate thawabu ya kuwaona wakivumilia katika njia ya ukweli muda wote wa maisha zao.—Waebrani 12:16; 1 Petro 2:2; Mithali 22:6.

[Blabu katika ukurasa wa 28]

Yesu alikuwa na nia ya kutumia wakati akiwa pamoja na watoto wa watu wengine. Hakika sisi tunaweza kutumia wakati tukiwa pamoja na watoto wetu wenyewe

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Ikiwa wewe unataka mtoto wako ‘afanyize tamaa ya kutaka sana lile neno,’ mfanyie liwe lenye ladha nzuri iwezekanavyo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki