Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 8/15 kur. 8-13
  • Wenye Furaha ni Wale Wanaotumia Uwezo kwa Njia Inayofaa!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wenye Furaha ni Wale Wanaotumia Uwezo kwa Njia Inayofaa!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova—Mwenye Uwezo Mwingi, Lakini Pia Mwenye Hekima na wa Haki.
  • Mfano wa Yesu Kristo
  • Wengine Ambao Hawakutumia Vibaya Uwezo
  • “Mwenyezi-Mungu . . . Amejaa Nguvu”
    Mkaribie Yehova
  • Jilinde Usitumie Vibaya Uwezo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Yehova—Mungu Aliye Hodari kwa Nguvu Zake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • “Tafuteni Bwana na Nguvu Yake”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 8/15 kur. 8-13

Wenye Furaha ni Wale Wanaotumia Uwezo kwa Njia Inayofaa!

“Yehova ni wa polepole kukasirika na ni mkuu katika uwezo, na kwa vyo vyote Yehova hatasita kuadhibu.”​—NAHUMU 1:3, NW.

1. Kwa sababu gani kuwa na aina fulani ya uwezo si msingi wa mtu kujivuna?

KUNA aina nyingi za uwezo ambazo watu wenye akili wanaweza kutumia kwa njia inayofaa. Kwa sababu ya kipawa tulichozaliwa nacho au kwa sababu ya hali mbali mbali, huenda tukawa tuna uwezo wa aina fulani. Lakini je! huo ni msingi wa kujisifu? Hata kidogo. Tunasoma nini kwenye Yeremia 9:23? “Acheni mtu mwenye hekima asijivunie hekima yake wala mtu mwenye nguvu asijivunie nguvu zake wala mtu tajiri asijisifu juu ya utajiri wake.” (New International Version) Kwa sababu gani? Mtume Paulo anatoa jibu zuri kwenye 1 Wakorintho 4:7, NW: “Ni nani anayekufanya uwe tofauti na mwingine? Ndiyo, una nini ambacho hukupokea? Ikiwa, sasa, ulikipokea, sababu gani unajivuna kana kwamba hukukipokea?”

2. Kwa sababu gani tunahitaji kujihadhari katika habari ya kutumia uwezo?

2 Kwa sababu gani tunahitaji kujihadhari tusitumie vibaya uwezo wo wote ambao huenda tukawa nao? Kwa sababu “elekeo la moyo wa mwanadamu ni baya tangu ujana wake” (Mwanzo 8:21, NW) Kwa kuwa sisi sote tuna elekeo hilo tulilorithi la kuwa na uchoyo tunahitaji sikuzote kujihadhari tutumie kwa njia inayofaa uwezo wo wote tulio nao. Wakati mmoja mshairi alieleza wazo hili: “Hakuna hazina isiyoambatana na wasiwasi fulani. Hakuna uwezo usioandamwa na mtego fulani.” Ndiyo, kwa sababu ya hali ya kutokamilika iliyorithiwa, sikuzote kuna elekeo la kutumia uwezo kwa uchoyo.

Yehova—Mwenye Uwezo Mwingi, Lakini Pia Mwenye Hekima na wa Haki.

3. Ni aina zipi za uwezo zinazokaa katika Yehova?

3 Hakuna mwingine ila ni Muumba, Yehova Mungu, anatuwekea mfano mzuri sana, ndiyo, ulio mkamilifu wa matumizi ya uwezo. Yeye si mwenye haraka-haraka bali ni wa polepole katika kukasirika hata kunapokuwa na uhitaji wa kuonyesha uwezo wake kwa njia kali. (Nahumu 1:3) Hakuna mtu aliye na uwezo mkubwa kuliko Mungu, hiyo ikiwa ndiyo sababu inayotufanya tumtaje kuwa Mwenye uwezo wote au mwenye nguvu zote. Kwa kufaa yeye anatumia neno la cheo “Mwenye nguvu zote” kwa habari yake mwenyewe, (Mwanzo 17:1, NW) Si kwamba yeye ana uwezo kamili tu katika maana ya kuwa na nguvu zisizo na mipaka bali pia yeye ana uwezo kwa kuwa ana mamlaka yote kwa sababu ya cheo chake akiwa ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote aliouumba yeye. Ndiyo sababu hakuna mtu anayeweza kufanya kimbelembele ‘auzuie mkono wake, wala kumwuliza, Unafanya nini wewe?’​—Danieli 4:35.

4. Kwa sababu gani kuogopa Yehova ndio mwendo wa hekima?

4 Kwa sababu ya uhakika wa kwamba Yehova Mungu ni mwenye nguvu zote, mwendo wa hekima kwetu sisi ni kuogopa kumchukiza. Ndiyo, “[Kumwogopa Yehova] ni mwanzo wa hekima; na kumjua Mtakatifu ni ufahamu.” (Mithali 9:10) Paulo anatuonya tusimchochee Yehova Mungu aone wivu kwa kujitia katika namna yo yote ya kuabudu sanamu, kwani ‘je! sisi tuna nguvu zaidi ya yeye?’ Hata kidogo! (1 Wakorintho 10:22) Hata hivyo, wote wanaovunja kwa makusudi amri za Mungu za uadilifu wanatenda kana kwamba wao ni wenye nguvu kuliko Yehova! Maneno ya Paulo yanayofuata yanakazia jambo hili: “Mungu wetu ni moto ulao.”​—Waebrania 12:29.

5. Kwa sababu gani hatuhitaji kuwa na woga mbaya sana juu ya Yehova kwa sababu ya uweza-yote alio nao?

5 Mambo hayo yangeweza kutufanya tujawe na woga mbaya sana au hofu nyingi kama isingekuwa kwamba Yehova Mungu anasawazisha kwa ukamilifu nguvu zake za uwezo wote na sifa zake zile nyingine tatu zilizo kuu zaidi: hekima, haki, na upendo. Matumizi yake ya uwezo kwa njia kali yanapatana sikuzote na sifa hizo. Kwa mfano, Gharika ya siku za Noa ilikuwa udhihirisho mkubwa kweli kweli wa uwezo wa Yehova. Lakini je! matumizi ya Mungu ya uwezo yalikuwa ya udhalimu au yasiyo ya upendo? Hata kidogo! Wanadamu walikuwa wamepoteza sana njia yao hata Mungu akaona Uchungu moyoni mwake kwa sababu ya mambo aliyoona. (Mwanzo 6:5-11) Kwa kuwa waovu hao wa kabla ya gharika walikuwa wakitumia vibaya baraka za Mungu, yeye alichukua hatua inayofaa kwa kuwafagia watoke duniani, hasa kwa kuwa wao waliyapuuza maonyo ya yule “mhubiri wa uadilifu,” Noa.​—2 Petro 2:5, NW.

6. Mambo ambayo Yehova alifanya kushughulikia Sodoma na Gomora yanaonyesha nini?

6 Wakati wakaaji wa Sodoma na Gomora walipojionyesha kuwa watenda dhambi walioshuka sana tabia, kwa kutumia vibaya baraka ambazo wao wakiwa sehemu moja ya wanadamu, walikuwa wakifurahia kwa kupewa na Yehova, yeye aliagiza kwamba wakaaji hao wapaswa kuharibiwa. Kwa sababu ya kumfikiria Abrahamu rafiki yake, Yehova alimwambia mwanamume huyo mwenye imani juu ya kusudi Lake kuhusu Sodoma na Gomora. Abrahamu alielekea kufikiri kwamba hayo yangekuwa matumizi mabaya sana ya uwezo, kwa hiyo akamwuliza Yehova: “Je! Hakimu wa dunia yote hatafanya yanayofaa?” Ingawa hivyo Abrahamu alijihangaisha sana na jambo hilo kwa sababu ya kuelewa vibaya. Mwishoni alilazimika kukubali kwamba agizo la Yehova lilikuwa la uadilifu kikweli, kwa maana hakukuweza kupatikana hata nafsi kumi zenye uadilifu katika miji hiyo miwili. Hakika hiyo inaonyesha jinsi Yehova Mungu alivyo mwangalifu sana kutumia uwezo wake kwa haki.​—Mwanzo 18:17-33 NW; Isaya 41:8.

7. Kwa sababu gani Farao alistahili kupokea wonyesho mkali wa uwezo wa Yehova?

7 Baadaye, ulipofika wakati wa kukomboa watu wake kutoka utumwa wao wa udhalimu katika Misri, Yehova alimpa Farao nafasi ya kufanya ushirikiano naye asijiumize mwenyewe na watu wake. Lakini Farao alikataa kwa ugumu wa moyo na shingo kulikubali ombi la Yehova. Kwa hiyo Mungu akampa Farao wonyesho mmoja baada ya mwingine wa uwezo wake katika yale mapigo kumi juu ya Misri. (Kutoka 9:16) Farao alipokwisha kuwaacha Waisraeli waende, aliendelea kwa ugumu wa shingo kumkaidi Yehova kwa kuwafuatia Waisraeli. Kwa hiyo, Yehova alitumia kwa haki uwezo wake hodari kufagilia mbali Farao na jeshi lake lenye nguvu katika Bahari Nyekundu. (Zaburi 136:15) Katika kila kimoja cha visa hivyo, na iangaliwe kwamba, Yehova alitumia pia uwezo wake mkuu kuhifadhi watumishi wake waaminifu: Noa na jamaa yake: Loti na binti zake wawili, na taifa Israeli.​—Mwanzo 19:16.

8. Ni kwa sababu gani nzuri Yehova alishughulika na Senakeribu kwa jinsi alivyofanya?

8 Karne nyingi baadaye, katika wakati wa Mfalme Hezekia, Yehova alidhihirisha uwezo wake mkuu kwa njia ya kustaajabisha sana na yenye uadilifu mwingi wakati Mfalme Mwashuri Senakeribu alipoutisha Yerusalemu Kwa kuongozwa na Mfalme Hezekia mcha-Mungu na mshikamanifu, watu wa Yehova walimwomba sana Yeye awasaidie. Wao walikuwa wakimtumikia kwa uaminifu, kwa hiyo Mungu alichukua hatua kwa ajili yao. Kwa upande mwingine, mjumbe wa Mfalme Senakeribu alikuwa amejivuna hivi: ‘Msimsikilize Hezekia, msimwache awashawishi kwa kuahidi kwamba Yehova atawakomboa ninyi. Je! iyo yote ya ile miungu ya mataifa yale mengine imeweza kukomboa watu wayo katika mkono wa Senakeribu? Kwa kuwa hakuna ye yote ya miungu hiyo iliyoweza kufanya hivyo mbona ninyi mnawazia kwamba Yehova ataweza kuwakomboa ninyi?’ (Isaya 36:13-20 NW) Kwa sababu ya kujivuna hivyo, Mungu hakuwa na jambo jingine la kufanya isipokuwa kutokeza uwezo wake mkuu, akafanya askari 185,000 waanguke katika usiku mmoja, akithibitisha kwamba kwa kweli kulikuwa na tofauti kati ya miungu ya mataifa na Yehova.

9. Ni mifano gani mingine inayoweza kutajwa kuonyesha kwamba Yehova ni mwangalifu juu ya jinsi anavyotumia uwezo wake?

9 Fikiria mifano mingine michache kati ya mingi ambayo ingeweza kutolewa. Wakati Yehova alipompiga Miriamu kwa ukoma, huo ulikuwa wonyesho wenye haki na hekima kabisa wa uwezo wake. Miriamu alistahili adhabu hiyo kwa kunena akijitanguliza sana dhidi ya Musa ndugu yake, mwekwa-rasmi wa Mungu. (Hesabu 12:1-15) Ndivyo ilivyokuwa pia wakati mfalme Uzia alipovamia patakatifu pa hekalu bila hata kuona haya na kujitanguliza afukize ubani juu ya madhabahu ile ya dhahabu, akakataa kwa majivuno ya moyo kuwachishwa kitendo hicho na makuhani Walawi. Yehova alionyesha uwezo Wake kwa kumpiga kwa haki mfalme huyo kwa ukoma. (2 Mambo ya Nyakati 26:16-21) Sawa na vile dhambi zao zilivyotofautiana, ndivyo na adhabu aliyowapa Yehova ilivyotofautiana pia: ukoma wa Miriamu ulikuwa wa muda, lakini Uzia alikufa akiwa mwenye ukoma. Hivyo tunaweza kuona kwamba nyakati zote Yehova anakuwa mwangalifu kutumia uwezo wake kwa njia yenye hekima na haki, hivyo akiwa na uwezo wa kuhifadhi waaminifu wanaompenda na kuharibu waovu.​—Zaburi 145:20.

Mfano wa Yesu Kristo

10, 11. Ni visa gani vinavyoonyesha kwamba Yesu alijali kutumia uwezo kwa njia inayofaa?

10 Mwana wa Mungu alikuwa mfuata-mfano mzuri kweli kweli wa Baba yake katika matumizi ya uwezo. Kati ya visa vya kwanza-kwanza ni wakati Shetani alipogombana naye kuhusu mwili wa Musa. Yule Logosi (neno) angaliweza kumkemea vikali Shetani. Badala ya hivyo, Logosi ni kama alijirudisha nyuma ili aache kemeo litoke kwa Yehova Mungu mwenyewe.​—Yuda 8, 9.

11 Kile kishawishi chenyewe cha kwanza ambacho Shetani alimtokezea Yesu jangwani kilihusiana na jambo hili la kutumia vibaya uwezo. Shetani alimshawishi Yesu atumie uwezo wake unaozidi ule wa kawaida kwa kusudi la kichoyo, ageuze mawe yawe mkate. Hicho kilikuwa kishawishi kweli kweli kwa sababu Yesu hakuwa amekula kwa siku 40 na ‘aliona njaa.’ Shetani alitokeza kishawishi hicho kwa njia ya kumtega Yesu afuate mwendo wa kichoyo, kwa maana alianza kwa kusema, “UKIWA Mwana wa Mungu amuru kwamba mawe haya yawe mikate.” Bila shaka alitumainia kwamba Yesu angejibu, ‘Hakika mimi ni Mwana wa Mungu, na ili kuthibitisha hivyo nitageuza mawe yale yawe mkate.’ Badala ya kushawishwa au kutegwa atende kwa uchoyo au upumbavu, Yesu alijibu: “Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” (Mathayo 4:1-4) Yeye alipuuza kidokezo juu ya kama alikuwa Mwana wa Mungu, na akakataa kutumia vibaya uwezo aliokuwa amepewa na Mungu.

12. Yesu alionyeshaje zaidi kwamba yeye hakuwa na pupa ya uwezo?

12 Baadaye, Yesu Kristo alipokwisha kulisha wanaume 5,000 bila kuhesabu wanawake na watoto wengi, Wayahudi walitaka kumfanya mfalme. Kama yeye angalikubali toleo lao, hayo yangalikuwa matumizi mabaya ya uwezo aliokuwa nao wa kuvuta watu kupitia miujiza yake. Alifahamu kwamba ilimpasa aendelee kutokuwamo katika siasa za kilimwengu na kumngojea Yehova Mungu ampe umaliki. (Yohana 6:1-15) Hata muda fulani baadaye, wakati kundi la watu wenye ghasia lilipokuja kumchukua akafungwe, yeye angaliweza kuomba majeshi 12 ya malaika na kwa njia hiyo azuie kufungwa kwake. Lakini, hayo yangalikuwa matumizi mabaya ya uwezo, kwa maana yalikuwa mapenzi ya Baba yake atii.​—Mathayo 26:39, 53.

Wengine Ambao Hawakutumia Vibaya Uwezo

13, 14. (a) Ni mfano gani mzuri sana alioutoa Gideoni kuonyesha kwamba hakuwa na pupa ya uwezo? (b) Sauli aliwekaje mfano mwema alipokuwa mfalme pale mwanzoni?

13 Kati ya wanadamu wasio wakamilifu ambao walipinga sana kishawishi cha kutumia vibaya uwezo, ni lazima atajwe Mwamuzi Gideoni. Baada ya yeye kukomboa Israeli mkononi mwa Midiani, watu walitaka kumfanya mfalme wao. Gideoni alikataa, kwa kufaa akasema: “Mimi sitatawala juu yenu, wala mwanangu hatatawala juu yenu; yeye [Yehova] atatawala juu yenu.” Ndiyo kiasi ambacho yeye alionyesha palepale mwanzoni mwa kazi yake ya maisha ya uamuzi kilikuwa kingali kiko. Na itikio la Gideoni lilionyesha jinsi Yehova Mungu mwenyewe alivyohisi juu ya Waisraeli kuwa na mfalme wa kibidanamu. Tunaweza kuona jambo hili kutokana na vile yeye alivyojibu wakati Israeli walipotaka mfalme katika wakati wa nabii Samweli.​—Waamuzi 8:23; 6:12-16; 1 Samweli 8:7.

14 Hata hivyo, wakati mfalme alipochaguliwa, kwanza Sauli aliweka mfano mzuri sana wa kujizuia katika matumizi ya uwezo. Watu fulani wasiofaa kitu walisema: “‘Ni jinsi gani huyo atatuokoa?’ Kwa hiyo wao wakamdharau . . . Lakini yeye akaendelea kama mtu ambaye amekua ivyo hivyo bila kusema.” Angaliweza kutenda haraka-haraka, kwa kutumia uwezo wake wa kifalme, lakini hakufanya hivyo. Vilevile, baada ya Sauli kupata ushindi juu ya Waamoni, wengine wa watu wake walifikiri huo ungekuwa wakati mzuri sana wa kuwalipa wale waliokuwa wamedharau Sauli. Kwa hiyo wao walimwambia hivi: “Ni nani anayesema, ‘Sauli​—je! huyo atakuwa mfalme juu yetu’? Tupe sisi watu hao tupate kuwaua.” Ingawa hivyo, Sauli hakuwa mtu wa akili hiyo hata kidogo. Yeye alipinga hivi: “Hakuna mtu anayepaswa kuuawa siku hii, kwa sababu leo Yehova amefanya wokovu katika Israeli.” Tunaweza kuona kwamba Sauli kwa kweli alianza vizuri na akiwa mwenye kiasi. (1 Samweli 9:21; 10:20-23, 27; 11:12, 13, NW.) Ni jambo la kusitikisha kama nini kwamba yeye alianza kutumia vibaya uwezo wake wa kifalme na hivyo akafikia mwisho mbaya!—1 Samweli 28:6; 31:3-6.

15, 16. (a) Ni ushahidi gani ambao Mwamuzi Samweli aliweza kutoa juu ya matumizi ya uwezo wake wa kuhukumu? (b) Ni mfano gani kama huo aliouweka Mfalme Daudi?

15 Samweli, yule nabii ambaye pia alihukumu Israeli, aliweka mfano mzuri sana. Mungu alimtumia sana tangu utoto wake. Samweli alihukumu kwa haki watu wake na kuwaletea ukombozi. Je! wakati wo wote yeye alitumia cheo chake ili kupata faida ya kichoyo? Hata kidogo! Yeye alisema hivi katika hotuba yake ya kuwaaga watu hao: “Angalieni, nimesikiliza sauti katika hayo yote mliyoniambia, nami nimemtawaza mfalme juu yenu . . . Nami nipo hapa; basi mnishuhudie mbele za [Yehova], na mbele ya masihi wake, nalitwaa ng’ombe wa nani? au nalitwaa punda wa nani? au ni nani niliyemdhulumu? ni nani niliyemwonea? au kwa mkono wa nani nimepokea rushwa inipofushe macho?” Watu wake walilazimika kukiri kwamba mwendo wa Samweli haukuwa na lawama katika mambo yote hayo. Yeye hakuwa ametumia vibaya uwezo wa cheo chake cha kuhukumu.​—1 Samweli 12:1-5.

16 Wala haitupasi kusahau mfano mzuri sana aliouweka Daudi. Mara mbili yeye alimpata Mfalme Sauli katika uwezo wake na angaliweza kumwua. Daudi angaliweza kuwaza hivi: ‘Sauli anajitahidi sana aupate uhai wangu, kwa hiyo mambo ni mawili, mimi nimumalize au yeye animalize.’ Au angaliweza kuwaza hivi kwa uchoyo: ‘Kwa kuwa Samweli amenipaka mafuta mimi niwe mfalme anayekuja wa Israeli, mwishowe ni lazima iwe hivyo. Mbona basi isiwe hivyo sasa?’ Hapana, Daudi alingoja kwa subira mpaka wakati wa Yehova ukafika wa kumpa ule ufalme. (1 Samweli 24:1-22; 26:1-25) Lakini, jambo la kusikitisha ni kwamba, baada ya Daudi kuwa mfalme, yeye alitumia vibaya uwezo wake katika pindi mbili: katika kusababisha kifo cha Uria na katika kuhesabu jeshi la Israeli.​—2 Samweli 11:15; 24:2-4, 12-14.

17. Paulo alionyeshaje kwamba hakuwa kamwe na pupa wala hakutumia vibaya uwezo wake?

17 Kati ya wafuasi wa Yesu Kristo, mtume Paulo aliweka mfano mzuri sana kwa habari hii. Yeye angaliweza kudai riziki kutoka makundi aliyotumikia. Lakini, yeye hakutumia hilo kwa faida yake. Aliwaambia wazee wa Efeso: “Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu. Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami.” (Matendo 20:33, 34) Alipokuwa akiandikia kundi katika Korintho, mtume alijieleza kwa uthabiti mwingi zaidi juu ya jambo hilo. (1 Wakorintho 9:1-18) Yeye alikuwa na mamlaka ya kujiepusha na kazi ya kimwili, kwa maana ni mtu yupi anayetumikia akiwa askari kwa gharama yake mwenyewe? Je! Musa hakusema ng’ombe anayepura nafaka asifungwe kinywa? “Lakini,” Paulo anaeleza, “Mimi sikutumia mambo hayo hata moja.” Thawabu yake ilikuwa nini? “Ya kuwa nihubiripo, nitaitoa Injili bila gharama, bila kutumia [vibaya] uwezo nilio nao katika Injili.”

18. (a) Inatupasa tuwe na maoni gani juu ya jinsi Yehova anavyotumia uwezo vizuri sana? (b) Kwa sababu gani wale wanaomwiga yeye katika habari hii wanaweza kusemwa kuwa wenye furaha?

18 Inaweza kusemwa kikweli kwamba, ‘Ni wenye furaha wale wote wasiotumia vibaya uwezo wao.’ Yehova Mungu ana jina lililo bora kama nini kwa sababu ya kuweka mfano mzuri sana wa namna hiyo, kwa kuacha uweza wote alio nao usawazishwe sikuzote na sifa zake nyingine za hekima, haki, na upendo! Hivyo, tunaweza kusema hivi pamoja na mtunga zaburi Daudi: “Ee nafsi yangu, umhimidi [Yehova]. Naam, vyote vilivyo ndani yangu vilihimidi jina lake takatifu.” (Zaburi 103:1) Wote ambao wamefuata mfano wa Yehova katika matumizi yanayofaa ya uwezo ni wenye furaha kweli kweli. Mifano ambayo tumefikiria kutokana na Maandiko inathibitisha kwamba, ingawa sisi ni wanadamu wasio wakamilifu, sisi, pia, tunaweza kutumia kwa njia inayofaa uwezo wa namna nyingi tulio nao. Kwa kufanya hivyo, tunaweza kuwa si na dhamiri safi tu, bali pia na kibali cha Mungu na heshima ya wanadamu wenzetu.

Wewe Unakumbuka?

◻ Kwa sababu gani mashauri kuhusu matumizi mabaya ya uwezo yanahitajiwa kabisa?

◻ Ni mifano gani inayoonyesha kwamba Yehova Mungu anatumia uwezo kwa halali?

◻ Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba Yesu alikuwa mwangalifu asitumie uwezo vibaya?

◻ Ni watu gani wanaotajwa katika Maandiko ya Kiebrania walioonyesha kwamba hawakutumia uwezo vibaya?

◻ Mtume Paulo alijionyeshaje kuwa mfano mwema katika matumizi ya uwezo?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Sifa zile kubwa-kubwa za Yehova zimesawazika kwa ukamilifu

Upendo Uwezo Haki Hekima

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mungu alionyesha uwezo wake kwa haki:

kwa kutumia Gharika

katika Sodoma

katika Bahari Nyekundu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki