Unabii wa Danieli Ndoto Zinazokuhusu Wewe
“Mwajua, mimi narudia kuangalia manabii wenu wa kale katika Agano la Kale na ishara zinazotabiri Har–Magedoni, kisha najikuta nikijiuliza kama—kama sisi ndicho kizazi kitakachoona mambo hayo yakitokea. Mimi sijui kama ninyi mmeona wo wote wa unabii mbalimbali hivi majuzi, lakini aminini ninayosema, mambo hayo kwa uhakika yanazieleza nyakati ambazo sisi tunazipitia sasa.”—Rais Ronald Reagan wa United States.
RAIS REAGAN siye peke yake amejiuliza kama nyakati tunamoishi ndizo zinazotabiriwa katika unabii wa Biblia. Mamilioni ya watu wengine wameshangazwa sana pia na jinsi hali za sasa za ulimwengu zinavyolingana na unabii wa Kimaandiko. Lakini, huu hautabiri wakati wa taabu tu ambao haujapata kuwa na kifani, bali unatabiri pia mfumo mpya wa mambo wenye uadilifu utakaokuja mara tu baada ya taabu hiyo.
Makala hii inaanzisha mfululizo, wenye matoleo manne yanayofuatana ya Mnara wa Mlinzi, yanakusudiwa kukuzoeza wewe na habari za mmoja wa manabii hawa wa kale, ambaye jina lake ni Danieli. Huenda wewe ukawa unajua mambo yanayomhusu. Yeye alikuwa Myahudi aliyezaliwa katika jamaa yenye cheo. Alipokuwa angali kijana, Danieli alihamishwa akapelekwa Babuloni, ambako alielimishwa katika jumba la Nebukadreza, mfalme wa pili wa Milki ya Babuloni Mpya. Jambo hilo lilifanyika mwishoni mwa karne ya saba K.W.K., kabla ya uharibifu wa Yerusalemu. Danieli alibaki akiwa mateka mpaka Babuloni ilipoanguka mwaka 539 K.W.K., na baada ya hapo akatumikia katika jumba la watawala wa kwanza-kwanza wa Milki ya Wamedi na Waajemi. Wakati wa uhamisho wake alifasiri ndoto kadhaa na kupata njozi zilizoongozwa na Mungu ambazo zinahusu siku zetu. Ndiyo, wewe na jamaa yako mnahusika katika mambo aliyoyatabiri Danieli.
Ndoto na Njozi za Kiunabii
Kwa kweli, ndoto na njozi za kitabu cha Danieli ni unabii wa mambo ambayo yangetukia baada ya muda mfupi na baada ya muda mrefu pia. Ni historia ya ulimwengu iliyoandikwa mapema. Ndoto na njozi hizo zilitangulia kuonyesha jinsi mamlaka ingeng’ang’niwa na wanaume, ukoo mbalimbali wa kifalme, na milki za kisiasa tangu wakati wa Danieli na kuendelea katika historia yote mpaka “wakati wa mwisho.”—Danieli 8:17, 19.
Kutimizwa kwa ule unabii uliohusu mambo yaliyotukia baada ya muda mfupi kunapasa kutia nguvu uhakika wetu katika matabiri ya mambo ambayo yangetukia baadaye sana, yenye kuufikia wakati wetu. Mengine ni gani ya matabiri hayo ambayo yangetukia baada ya muda mfupi?
Moja ilikuwa ndoto iliyohusu mti mkubwa uliokatwa ukaangushwa, na kufungwa pingu kwa “nyakati saba” au miaka saba, kabla ya kuruhusiwa uchipuke tena. (Danieli 4:10-17) Katika utimizo wenye kutukia baada ya muda mfupi, unabii huo ulihusu Mfalme Nebukadreza, aliyeipata ndoto hiyo. Mwaka mmoja baadaye, mtawala huyo ‘alikatwa akaangushwa,’ na inaonekana ilikuwa kupatwa na ugonjwa wa akili. Kwa miaka saba yeye alijiendesha kama mnyama wa uwanjani. Halafu, “mwishoni mwa zile siku” zilizotabiriwa, Nebukadreza alirudiwa na fahamu zake na kiti chake cha kifalme. (Danieli 4:28-37, NW) Kulingana na The International Standard Bible Encyclopedia, vyanzo vya kale vinaonyesha kwamba, Nebukadreza alikuwa mgonjwa kuelekea mwisho wa utawala wake. Lakini ndoto hiyo ilikuwa na utimizo ambao ungetukia pia baada ya muda mrefu, kama vile makala ya baadaye katika mfululizo huu itakavyoonyesha.
Unabii mwingine ambao ungetukia baada ya muda mfupi katika kitabu cha Danieli unatolewa na ule mwandiko wa kimwujiza katika ukuta wa jumba la karamu ambamo Belshaza mjukuu wa Nebukadreza na wakuu wake wa kifalme walikuwa wakila karamu. (Danieli, sura ya 5) Walikuwa wakinajisi vyombo vitakatifu vilivyochukuliwa kutoka hekalu la Yehova katika Yerusalemu. Chini ya uongozi wa Mungu, Danieli aliufasiri ujumbe huu wa hukumu ya kimungu. Na kwa utimizo, “usiku uo huo” Babuloni ilianguka na “Belshaza, mfalme wa Kaldayo, akauawa,” kama inavyothibitishwa na Xenophon mwanahistoria Mgiriki. (Danieli 5:30) Lakini leo kuna mwandiko ukutani kwa ajili ya mfumo mbovu wa mambo wa sasa. Mwandiko huo, pia, utaeleza katika makala moja ya mfululizo huu.
Muhuri Unaondolewa katika “wakati wa mwisho”
Kuelekea mwisho wa kitabu chake cha unabii, Danieli aliandika ujumbe huu alioupokea kutoka kwa malaika: “Lakini wewe, Ee Danieli, yafunge maneno haya, ukakitia muhuri kitabu, hata wakati wa mwisho; wengi wataenda mbio huko na huko, na maarifa [ya kweli] yataongezeka.”—Danieli 12:4.
Leo ‘maarifa ya kweli’ juu ya utimizo wa unabii wa Biblia yameongezeka kweli kweli. Ufahamu huo ulioongezeka umesadikisha mamilioni ya watu wenye kujifunza Biblia kwa uzito kwamba kweli kweli tunaishi katika “wakati wa mwisho” na kwamba Ufalme wa Mungu wa uadilifu uko karibu. (Danieli 2:44) Vikionyesha kufaa kwa kitabu cha Danieli katika habari hii, vichapo vinavyoitwa Soncino Books of the Bible vinasema: “Mshindi wa uadilifu baadaye, ambao utafikia kilele kwa kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu, unaonyeshwa kwa msingi katika Danieli.”
Je! wewe unatumainia “ushindi wa baadaye wa uadilifu”? Ikiwa ndivyo, unahitaji sana utake kuzijua ndoto na njozi za kiunabii za Danieli. Makala inayofuata itakupasha habari juu ya baadhi yazo na kukupa ushuhuda unaothibitisha kwamba Danieli ni kitabu kilichohakikishwa kuwa cha unabii.