Kung’ang’ania Mamlaka ya Duniani Pote Ni Nani Atakayeshinda?
“SHABAHA iliyo kubwa ya Urusi ilikuwa kutulazimisha sisi tuache mipango ya kujitayarisha kujikinga katika Vita ya Anga za Juu. Mimi nafikiri . . . Bw. Gorbachev anaelewa kwamba hatukusudii kuacha.” Hivyo ndivyo alivyosema Reagan Rais wa United States baada ya ule mkutano wa Geneva katika Novemba 1985.
Kama wewe unavyojua, katika kipindi cha mwaka mmoja tangu wakati huo ushindani kati ya serikali hizo mbili zilizo kubwa zaidi ulimwenguni umeendelea. Lakini kuna mataifa mengi yaliyofungamana upande wa hizo au yanayoziunga mkono, nayo yanajumlika kuwa Mashariki (ambayo hasa ni kile kikundi cha mataifa ya kikomunisti) na Magharibi (ambayo kwa kawaida ni kile kikundi cha mataifa ya kibepari). Hali hiyo inalifanya jambo hilo liwe ni kung’ang’ania mamlaka duniani pote. Kwa hiyo wewe unahusika. Zaidi ya hilo, yale mashindano ya kutengeneza silaha zaidi yanaendeleza daima lile tisho la kutokea kwa vita kubwa sana, yenye kuleta shaka juu ya kama wewe utakuwako wakati ujao—hata kama unaishi katika nchi isiyofungamana upande wo wote.
Basi, inakupasa utake kujua matokeo ya jambo hili la kung’ang’ania mamlaka. Je! kutamalizwa kwa njia yenye amani? Ikiwa sivyo, ni nani atakayeshinda? Kujua jambo hilo kunaweza kuhusu wakati ujao wako.
Jinsi Kulivyoanza
Vitabu vingi vya historia ya kisasa vinadokeza kwamba ushindani uliopo kati ya Mashariki na Magharibi ulianza muda mfupi baada ya kumalizika Vita ya Ulimwengu ya Pili. Lakini, historia ya Biblia inaonyesha kwamba huo ni mwendelezo wa kung’ang’ania uongozi wa ulimwengu kulikoanza karibu miaka 2,300 iliyopita.
Ikiwa wewe umesoma historia ya Ugiriki ya Kale, unajua kwamba Aleksanda Mkuu alilifanya taifa hilo likawa milki ya kifalme. Jambo hilo lilitabiriwa na Danieli nabii wa Biblia. Kulingana na ilivyokuwa imetabiriwa na unabii huo, baada ya huyo ‘mfalme hodari’ kufa mwaka 323 K.W.K., mwishowe milki hiyo ‘iligawanyika kuzielekea zile pepo nne’—kati ya wanne wa majenerali wake. (Danieli 11:2-4) Kati ya hao, Seleuko Niketa wa Kwanza alianza kutawala Siria na Mesopotamia—maeneo yaliyo kaskazini na mashariki mwa nchi ya nyumbani kwa Danieli, yaani, Yuda. Tolemi Lago, jenerali mwingine Mgiriki, alianza kutawala Misri na Palestina, na hivyo akawa kusini na magharibi mwa eneo la utawala wa Seleuko Niketa. Upande ambao kila mmoja wao alikuwa ndio uliowafanya wakawa “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini.”—Danieli 11:5, 6.
“Kaskazini” na “kusini” zikaja kufananisha mataifa yenye nguvu nyingi yaliyojazia vyeo fulani vya kiunabii.a Katika muda wa karne zilizofuata, mataifa tofauti-tofauti yamejazia vyeo vya “wafalme” hao wawili; lakini sikuzote mataifa hayo yamefanana na maelezo ya kiunabii yanayoyahusu. Sikuzote yametambuliwa kwa sababu ya ushindani yalio nao, hali kwa kawaida yamekuwa yakitawala maeneo yaliyo kaskazini na kusini mwa taifa lile jingine.
Leo vyeo hivyo vinalingana na yale majina “Mashariki” na “Magharibi.” Hiyo, pia, ni mitajo ya mfano, kwa sababu maeneo yanayohusika yamepitana-pitana. Mitajo hii ya Kibiblia “kaskazini” na “kusini” ni mifano inayofaa pia ijapokuwa hiyo vilevile imepitana-pitana.
Mungu wa “Mfalme wa Kaskazini”
Akitazama mbele kwenye “wakati wa mwisho,” Danieli alisema kwamba “mfalme wa kaskazini” ‘angejitukuza mwenyewe juu ya kila mungu,’ ‘asifikirie hata kidogo’ “Mungu wa baba zake.” Badala yake, yeye angempa utukufu “mungu wa ngome . . . kwa njia ya dhahabu . . . fedha . . . jiwe lenye thamani na . . . vitu vya kutamanika” kabla hajaja “njia yote hiyo afikie mwisho wake.—Danieli 11:35-39, 45, NW.
“Akiwa kwa msingi haamini Mungu, mfalme wa kaskazini” wa leo anasema anakana kuwako kwa Mungu na mara nyingi amegandamiza dini. Yeye anategemea zaidi silaha na nguvu za kivita kuliko vile anavyotegemea njia nyinginezo ili apanue uvutano wake kati ya mataifa. Kwa hiyo yeye anatumia fedha ili ‘ampe utukufu’ yule “mungu wa ngome.” Kwa kulinganisha, ingawa yule “mfalme wa kusini” wa kisasa anatukuza pia silaha na nguvu za kivita, yeye anatambua miungu mingine, na wengi wa watu wake wanajihusisha sana katika mambo ya kidini.
Kung’ang’ania Mamlaka kwa Kisasa
Ukitaja matukio ya siku zetu hasa, unabii unasema: “Katika wakati wa mwisho mfalme wa kusini atashikana na [mfalme wa kaskazini] katika msukumano, na dhidi yake mfalme wa kaskazini atakuja kwa fujo nyingi akiwa na [vifaa vya kivita]; na kwa hakika [mfalme wa kaskazini] ataingia katika nchi nyingi na kuzigharikisha na kupita.—Danieli 11:40, NW.
Labda wewe unajua kwamba tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili siasa na uongozi wa “mfalme wa kaskazini” imeenezwa katika nchi nyingi, ijapokuwa kumekuwa na vita vya kuzuia jambo hilo. Bado tutangoja tuone ni kwa kadiri gani yeye atafanikiwa ‘kuingia katika nchi nyingi na kuzigharikisha na kupita’; lakini yule “mfalme wa kusini” wa kisasa amejaribu kumzuia asipenye-penye ndani ya ule unaoitwa ulimwengu ulio huru. Hivyo wapinzani hao wenye kung’ang’ana wanashikana katika “msukumano” ambao sasa umeendelea ukawa wa kuongeza silaha kwa haraka na kushindania anga za juu. Na wakati wanapofanya hivyo, kila mmoja anashtaki mwenzake juu ya kutaka kuutawala ulimwengu.
Danieli anaendelea kusema: “Yeye [mfalme wa kaskazini] kwa kweli atazitawala hazina zilizofichwa . . . na vitu vyote vinavyotamanika vya Misri. Na Walibia na Waethiopia watafuata hatua yake.” (Danieli 11:43, NW) Huenda jambo hilo likawa linamaanisha mali za asili; naye “mfalme wa kaskazini” wa kisasa anatawala maeneo yaliyo na wingi wa mali zinazochimbuliwa katika ardhi, kutia na mafuta. Yeye ana uvutano wenye nguvu pia katika maeneo yaliyo nje ya milki yake yaliyo na mali nyingi za asili. Sisi sote tuna sababu ya kutazama tukitaka kuona kama yeye atapata utawala mkubwa zaidi wa maeneo hayo na uvutano wake wa kiuchumi utafika wapi.
Ni Nani Atakayeshinda?
Ingawa hivyo, ni nini kinachowazuia ‘wafalme’ hao wasifanye vitakomesha ya kupigana papo hapo? Jambo moja kubwa ni kwamba wao wanaogopa sana nguvu za kuangamizana wao kwa wao zilizo katika silaha zao za nyukilia. Wanaona ni afadhali wazugumze njia za kufanya mapatano, ingawa ni mara chache njia hizo zinapoheshimiwa. Ni kama vile Danieli alivyotabiri: “Penye meza moja uwongo ndio wataendelea kunena. Lakini hakuna jambo litakalofaulu, kwa sababu ule mwisho ungali bado ni kwa ajili ya wakati uliowekwa.—Danieli 11:27, NW.
Kwa hiyo inaelekea wewe unataka kujua, Ni jambo gani litakalotukia mwishowe? Je! hatimaye wao watazungumza wapate njia ya kuleta amani ya kudumu? Au mmoja atamshinda mwenzake? Kulingana na unabii ulio katika Neno la Mungu, jibu kwa maulizo yote mawili ni La. Kwa sababu gani? Kwa sababu mfalme wa tatu atawashinda kisha awapokonye utawala wa ulimwengu. Kwa hiyo kutakuwa na badiliko la utawala—karibuni!
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mfano, yale maneno yanayosema “ndipo badala yake atasimama mmoja” yanamaanisha kuchukua cheo cha “mfalme wa kaskazini.”—Danieli 11:20, 21
[Picha katika ukurasa wa 4]
NGUVU ZA KIVITA ZA MATAIFA MAKUBWA-MAKUBWA NA VIKUNDI-VIKUNDI
Silaha za nyukilia
50,000
Wanajeshi
11,913,000
Meli za vita
1,350
Ndege 20,100 za kuangusha makombora na za kupinga mashambulizi
Vifaru
95,800