Je! Sisi Tunaishi Katika “Wakati wa Mwisho”?
“Lakini wewe, Ee Danieli, yafunge maneno haya, ukakitie muhuri kitabu, hata wakati wa mwisho.”—Danieli 12:4.
MTU mwenye kula chakula alivurugika. Alipokuwa akitazama nje ya dirisha la mkahawa mmoja katikati ya mji wa Manhattan wenye kuelekeana na Times Square, Mji wa New York, aligeuza-geuza macho yake kutazama pale na pale kati ya vipima-saa vitatu mbalimbali vya ukutani, huku zile herufi kubwa za vipima-saa hivyo zikiwaka-waka kuonyesha wakati. Kipima-saa kimoja kilionyesha ni saa 5:28. Kingine kikawa kimebaki nyuma kilionyesha ni saa 5:26 kana kwamba kilikuwa kikitia shaka juu ya kuchelewa kwa wakati, lakini hali kile cha tatu kikaonekana kilikosa subira kwa kukimbia mbele kikionyesha ni saa 5:29.
‘Kuchelewa dakika moja au mbili tu si kitu sana,’ huenda wewe ukasema. Hata hivyo, jaribu kusadikisha hivyo mtu ambaye sasa hivi tu ameachwa na basi gari-moshi, au ndege, si kwa dakika nyingi, bali kwa sekunde chache tu! Kuujua wakati sahihi ni kwa maana. Kujua mahali tulipo katika ratiba ya wakati wa Mungu ni kwa maana hata zaidi.
Uwezekano wa Kutokea kwa Siku ya Maangamizi
Bila shaka, kama vile huenda wewe ukawa unajua, watu wamekuwa wakiongea juu ya “wakati wa mwisho”—wengine wanasema ‘mwisho wa ulimwengu’ au ‘siku ya maangamizi’—kwa muda wa karne nyingi. Nabii Danieli alinena juu ya jambo hilo karne 25 zilizopita. (Danieli 12:4) Lakini siku hizi, kulingana na James David Besser aliye mwandikaji wa kujitegemea, “si lazima tena mtu awe na imani ya kidini wala yenye nguvu nyingi kuliko zile za kibinadamu ndipo aweze kukubali kwamba kuna uwezekano wa kutokea kwa siku ya maangamizi; analohitaji kufanya tu ni kuweza kusikiliza habari za televisheni.” Je! wewe hukubaliani na hilo?
Bila shaka, televisheni inafanya habari za ulimwengu ziweze kutufikia kwa kadiri kubwa zaidi kwa kuyaleta matukio ndani ya vyumba vyetu wenyewe. Inafanya matatizo yaelekee zaidi kuonekana kuwa yametendeka sasa hivi na yanatuhusu zaidi sisi binafsi. Inatukumbusha kwamba hata sisi tungeweza kupatwa na mambo yote yanayotukia jiji au mji wenye kubomolewa na silaha za nyukilia, mwana au binti kutendwa kinyama katika fujo fulani za uhalifu, mama au baba kutekwa nyara katika shambulio la kiharamia. Hata hivyo, mambo hayo yanayoweza kutukia hayatoshi kuthibitisha kwamba siku ya maangamizi itatufikia hivi karibuni. Lakini yanafanya ielekee zaidi kuonekana kwamba siku hiyo inaweza kutokea. Na hiyo inafanya ulizo hili, Je! sisi tunaishi katika “wakati wa mwisho”? lihitaji kujibiwa kwa uharaka mkubwa zaidi.
Yesu, Danieli, na Mwisho wa Ulimwengu
Zaidi ya karne 19 zilizopita, wanafunzi wa Yesu walimwuliza hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo [“Mwisho wa ulimwengu,” King James Version]?” (Mathayo 24:3, NW) Alipokuwa akiwapa ishara Yesu alinena juu ya mambo mengi yenye kushuhudia jambo hilo, na yote yangejumlika kuonyesha kwamba tumefikia “umalizio wa mfumo wa mambo.” Fungua Biblia yako kwenye Mathayo sura 24 na 25, Marko sura 13 na Luka sura 21, ujisomee mwenyewe.
Huenda ukashangaa kuona kwamba mambo unayosoma yanasikika yakikaribia sana kufanana na habari zinazoletwa na televisheni leo. Utasoma juu ya vita, matetemeko makubwa ya ardhi, magonjwa ya kipuku, na upungufu wa chakula, yote hayo yakiwa yanatukia duniani pote. Utasoma pia juu ya “huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea” na juu ya mataifa ‘yakizimia kwa sababu ya hofu na kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na ‘watu.’ Je! wewe ungeweza kupata maneno yanayofaa kuliko hayo yaieleze hali iliyomo ulimwenguni, tunayoelezwa kwa wingi sana leo na vipindi vya televisheni?—Luka 21:10, 11, 25, 26, NW.
Ushuhuda huo wa hali ambao unatosha kuthibitisha kwamba tunaishi katika “wakati wa mwisho” sio tu tulio nao. Kama vile ambavyo tumetangulia kuona, tunapata ushuhuda wa kuongezea huo kwa kurudi nyuma miaka mingine 500 kwenye siku za Danieli yule nabii Myahudi. Yesu alimtaja kwa jina, na akaelekeza kwenye utimizo wa unabii. (Linganisha Mathayo 24:3,15, 21 na Danieli 11:31; 12:1.) Kwa kufanya hivyo, Yesu alionyesha kwamba yeye hakuyaona maneno ya Danieli ya “Agano la Kale” kuwa yasiyofaa kutumiwa siku hizi wala kuwa hayana maana. Wala haitupasi sisi kuwa na maoni hayo.
Angalia ufanani ulio kati ya maneno ya Danieli na yale ya Yesu kama yalivyoandikwa hapa juu. Halafu jiulize, ‘Je! wao hawakuwa wakitaja jambo lile lile moja.’
Ni wazi kwamba Danieli na Yesu walitabiri jambo lile lile moja, “wakati wa mwisho,” ambapo Kristo angekuwapo katika mamlaka ya Ufalme. Mwishoni mwa kipindi hicho, yeye angeangamiza adui zake wote hapa duniani katika dhiki kubwa. Lakini watu wa Mungu wangeokolewa.
Je! wewe unataka uwe kati ya waokokaji hao? Basi fikiria ushuhuda ambao Danieli anatoa juu ya “wakati wa mwisho.” Ushuhuda huo unatusaidia tujue barabara tumefika wapi katika ratiba ya wakati wa Mungu.
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
DANIELI
“Wakati wa mwisho . . . Mikaeli [Yesu Kristo] atasimama,. . . na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa . . . Na wakati huo watu wako wataokolewa.”—Danieli 11:40; 12:1.
YESU
“Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo . . .
Kutakuwako dhiki kubwa ya namna ambayo haijatukia tangu mwanzo wa ulimwengu . . .
Kama siku hizo zisingekatwa ziwe fupi, hakuna mwili ambao ungeokolewa; lakini . . . siku hizo zitakatwa ziwe fupi.”—Mathayo 24:3, 21,22, NW.